Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 19

Tunawezaje Kuimarisha Imani Yetu Katika Ahadi ya Yehova ya Ulimwengu Mpya?

Tunawezaje Kuimarisha Imani Yetu Katika Ahadi ya Yehova ya Ulimwengu Mpya?

“[Yehova] akisema jambo, je, hatalitenda?”—HES. 23:19.

WIMBO 142 Kushikilia Tumaini Letu

MUHTASARI a

1-2. Tunahitaji kufanya nini tunaposubiri ulimwengu mpya?

 TUNATHAMINI ahadi ya Yehova ya kuondoa mfumo huu wa mambo na kuleta ulimwengu mpya wenye uadilifu. (2 Pet. 3:13) Ingawa hatujui wakati hususa ambao ulimwengu mpya utafika, mambo yanayotokea katika ulimwengu huu yanaonyesha kwamba ulimwengu huo utafika hivi karibuni.—Mt. 24:32-34, 36; Mdo. 1:7.

2 Kwa sasa, hata iwe tumekuwa katika kweli kwa muda gani, sisi sote tunahitaji kuimarisha imani yetu katika ahadi hiyo. Kwa nini? Kwa sababu hata imani yenye nguvu inaweza kudhoofika. Kwa kweli, mtume Paulo alisema kwamba kukosa imani ni “dhambi inayotutatanisha kwa urahisi.” (Ebr. 12:1) Ili kulinda imani yetu isidhoofike, tunapaswa kuchunguza kwa ukawaida uthibitisho unaoonyesha kwamba ulimwengu mpya utafika hivi karibuni.—Ebr. 11:1.

3. Tutazungumzia nini katika makala hii?

3 Katika makala hii, tutazungumzia njia tatu ambazo zitatusaidia kuimarisha imani yetu katika ahadi ya Yehova ya ulimwengu mpya: (1) kwa kutafakari kuhusu fidia, (2) kwa kutafakari kuhusu nguvu za Yehova, na (3) kwa kushiriki katika utendaji wa kiroho. Kisha tutazungumzia jinsi ujumbe wa Yehova kwa Habakuki unavyoimarisha imani yetu leo. Hata hivyo, acheni kwanza tuchunguze baadhi ya hali ambazo huenda tunakabili sasa ambazo zinahitaji tuwe na imani yenye nguvu katika ahadi ya ulimwengu mpya unaokuja.

HALI ZINAZOHITAJI IMANI YENYE NGUVU

4. Ni maamuzi gani ambayo yanahitaji imani yenye nguvu?

4 Kila siku, tunafanya maamuzi ambayo yanahitaji imani yenye nguvu. Kwa mfano, tunafanya maamuzi kuhusu watu tunaoshirikiana nao, burudani, elimu, ndoa, watoto, na kazi ya kimwili. Ni vizuri tujiulize hivi: ‘Je, maamuzi yangu yanaonyesha nina uhakika kwamba mfumo huu hautaendelea kuwepo sikuzote, na hivi karibuni Mungu ataleta ulimwengu mpya? Au je, maamuzi yangu yanaongozwa na watu ambao wanaishi kana kwamba kifo ndio mwisho wa mambo yote?’ (Mt. 6:19, 20; Luka 12:16-21) Tutafanya maamuzi bora ikiwa tutaimarisha imani yetu kwamba ulimwengu mpya utafika hivi karibuni.

5-6. Kwa nini tunahitaji imani yenye nguvu tunapokabili hali ngumu? Toa mfano.

5 Pia, tunakabili majaribu ambayo yanahitaji imani yenye nguvu. Huenda tukapatwa na mateso, ugonjwa mbaya, au mambo mengine yanayoweza kutuvunja moyo. Huenda mwanzoni tukahisi kwamba tutaweza kuvumilia majaribu hayo. Lakini ikiwa yataendelea kwa muda mrefu—kama inavyokuwa mara nyingi inapohusu majaribu—tutahitaji kuwa na imani yenye nguvu ili tuvumilie na tuendelee kumtumikia Yehova kwa shangwe.—Rom. 12:12; 1 Pet. 1:6, 7.

6 Tunapokabiliana na jaribu, huenda tukahisi kwamba ulimwengu mpya wa Yehova hautakuja kamwe. Je, hilo linamaanisha kwamba imani yetu ni dhaifu? Si lazima iwe hivyo. Fikiria mfano ufuatao. Katikati ya majira ya baridi kali sana, huenda tukahisi kwamba majira ya joto hayatafika kamwe. Hata hivyo, sikuzote majira ya joto hufika. Vivyo hivyo, tunapokuwa tumevunjika moyo sana, huenda tukahisi kwamba ulimwengu mpya hautakuja kamwe. Hata hivyo, ikiwa tuna imani yenye nguvu tunajua kwamba ahadi za Mungu zitatimia. (Zab. 94:3, 14, 15; Ebr. 6:17-19) Tukiwa na uhakika huo, tunaweza kuendelea kutanguliza ibada ya Yehova maishani mwetu.

7. Tunapaswa kujilinda dhidi ya mtazamo gani?

7 Pia, tunahitaji imani yenye nguvu tunapofanya kazi ya kuhubiri. Watu wengi tunaowahubiria wanafikiri kwamba “habari njema” kuhusu ulimwengu mpya wa Mungu unaokuja ni jambo lisilowezekana. (Mt. 24:14; Eze. 33:32) Hatungependa kamwe mtazamo wao wa kuwa na shaka utuathiri. Ili tusiathiriwe na mtazamo huo, tunapaswa kuendelea kuimarisha imani yetu. Acheni tuchunguze njia tatu zitakazotusaidia kufanya hivyo.

TAFAKARI KUHUSU FIDIA

8-9. Kutafakari kuhusu fidia kunawezaje kuimarisha imani yetu?

8 Njia moja tunayoweza kuimarisha imani yetu ni kwa kutafakari kuhusu fidia. Fidia inatuhakikishia kwamba ahadi za Mungu zitatimia. Tunapotafakari kwa makini kwa nini fidia ilitolewa na mambo yaliyohusika, tunaimarisha imani yetu kwamba ahadi ya Mungu kuhusu kuishi milele katika ulimwengu bora itatimizwa kwa uhakika. Kwa nini tunaweza kusema hivyo?

9 Fidia ilihusisha nini? Yehova alimtuma Mwana wake mpendwa mzaliwa wa kwanza, mwandamani wake wa karibu zaidi, atoke mbinguni na kuzaliwa akiwa mwanadamu mkamilifu. Alipokuwa duniani, Yesu alivumilia hali ngumu mbalimbali. Kisha akateswa na kufa kifo chenye maumivu. Yehova alilipa bei kubwa sana! Mungu wetu mwenye upendo hangeruhusu kamwe Mwana wake ateseke na kufa ili tu kutuandalia maisha bora lakini ya muda mfupi. (Yoh. 3:16; 1 Pet. 1:18, 19) Kwa kuwa alilipa bei kubwa sana, Yehova atahakikisha kwamba tutaishi milele katika ulimwengu mpya.

TAFAKARI KUHUSU NGUVU ZA YEHOVA

10. Kulingana na andiko la Waefeso 3:20, Yehova anaweza kufanya nini?

10 Njia ya pili ya kuimarisha imani yetu ni kwa kutafakari kuhusu nguvu za Yehova. Yeye ana nguvu za kutimiza kila jambo analoahidi kufanya. Huenda watu wengi wakafikiri kwamba kutimizwa kwa ahadi ya kuishi katika ulimwengu mpya ni jambo lisilowezekana. Lakini mara nyingi Yehova huahidi mambo ambayo wanadamu hawawezi kamwe kutimiza. Hiyo ni kwa sababu yeye ni Mungu Mweza-Yote. (Ayu. 42:2; Marko 10:27) Basi haishangazi anapotoa ahadi zenye kustaajabisha.—Soma Waefeso 3:20.

11. Toa mfano mmoja kati ya ahadi zisizo za kawaida ambazo Mungu alitoa? (Tazama sanduku “ Baadhi ya Ahadi Zisizo za Kawaida Zilizotimizwa.”)

11 Fikiria baadhi ya mambo ambayo huenda yalionekana hayawezekani ambayo Yehova aliwaahidi watu wake zamani. Aliwahakikishia Abrahamu na Sara kwamba wangepata mtoto uzeeni. (Mwa. 17:15-17) Pia, alimwambia Abrahamu kwamba wazao wake wangepewa nchi ya Kanaani. Wakati wa kipindi cha miaka mingi ambacho wazao wa Abrahamu, yaani Waisraeli, walikuwa watumwa nchini Misri, huenda ilionekana kwamba ahadi hiyo haingetimia kamwe. Lakini ilitimia. Baadaye, Yehova alitangaza kwamba Elisabeti aliyezeeka angepata mtoto. Pia, alimwambia Maria, aliyekuwa bikira kwamba angemzaa Mwana wa Mungu, ambaye Yehova alikuwa ameahidi angefika, maelfu ya miaka mapema katika bustani ya Edeni, na ahadi hiyo ilitimizwa!—Mwa. 3:15.

12. Andiko la Yoshua 23:14 na Isaya 55:10, 11 linatuhakikishia nini kuhusu nguvu za Yehova?

12 Tunaimarisha imani yetu katika nguvu za Yehova za kuleta ulimwengu mpya kwa kutafakari ahadi mbalimbali alizotoa na kuzitimiza. (Soma Yoshua 23:14; Isaya 55:10, 11.) Kufanya hivyo kutatusaidia tuwe tayari zaidi kuwasaidia wengine waelewe kwamba ulimwengu mpya ulioahidiwa si ndoto, au jambo la kuwaziwa. Yehova mwenyewe alisema hivi kuhusu mbingu mpya na dunia mpya: “Maneno haya ni ya uaminifu na ya kweli.”—Ufu. 21:1, 5.

SHIRIKI KATIKA UTENDAJI MBALIMBALI WA KIROHO

MIKUTANO YA KUTANIKO

Utendaji huu wa kiroho unawezaje kuimarisha imani yako? (Tazama fungu la 13)

13. Mikutano ya kutaniko inawezaje kuimarisha imani yetu? Eleza.

13 Njia ya tatu ambayo tunaweza kuimarisha imani yetu ni kwa kushiriki katika utendaji wa kiroho. Kwa mfano, fikiria jinsi tunavyonufaika na mikutano yetu ya kutaniko. Anna, ambaye ameshiriki katika aina mbalimbali za utumishi wa wakati wote kwa miaka mingi, anasema hivi: “Mikutano hunisaidia kuimarisha imani yangu. Hata ikiwa msemaji hana uwezo mkubwa wa kufundisha au hafundishi jambo jipya, mara nyingi mimi husikia jambo ambalo linanisaidia kuelewa vizuri zaidi kweli fulani ya Biblia, na hilo linaimarisha imani yangu.” b Bila shaka, tunathamini pia maelezo yenye kujenga imani ya wahudhuriaji.—Rom. 1:11, 12; 10:17.

HUDUMA YA SHAMBANI

Utendaji huu wa kiroho unawezaje kuimarisha imani yako? (Tazama fungu la 14)

14. Kushiriki katika huduma kunaimarishaje imani yetu?

14 Pia, tunaimarisha imani yetu tunaposhiriki katika huduma ya shambani. (Ebr. 10:23) Barbara, ambaye amekuwa akimtumikia Yehova kwa zaidi ya miaka 70, anasema hivi: “Sikuzote imani yangu imeimarika ninaposhiriki katika kazi ya kuhubiri. Kadiri ninavyozungumza na wengine kuhusu ahadi nzuri za Yehova, ndivyo imani yangu inavyozidi kuimarika.”

FUNZO LA KIBINAFSI

Utendaji huu wa kiroho unawezaje kuimarisha imani yako? (Tazama fungu la 15)

15. Funzo la kibinafsi linaimarishaje imani yetu? (Tazama pia picha.)

15 Fikiria utendaji mwingine wa kiroho ambao unaimarisha imani yetu: funzo la kibinafsi. Susan ananufaika kwa kupanga ratiba ya kujifunza. Anasema hivi: “Jumapili mimi hujifunza makala ya Funzo la Mnara wa Mlinzi la juma linalofuata. Jumatatu na Jumanne, mimi hujitayarisha kwa ajili ya mkutano wa katikati ya juma. Katika siku zinazobaki, ninafanya miradi ya kujifunza kibinafsi.” Kwa kufuata kwa ukawaida ratiba ya kujifunza, Susan anaendelea kujenga imani yake. Irene, ambaye ametumikia kwa miaka mingi katika makao yetu makuu, ametambua kwamba kujifunza unabii wa Biblia kunaimarisha imani yake. Anasema hivi: “Ninastaajabu kuona jinsi unabii wa Yehova unavyotimizwa hata katika mambo madogo sana.” c

“HAKIKA YATATIMIA”

16. Kwa nini uhakikisho ambao Yehova alimpa Habakuki unatuhusu leo? (Waebrania 10:36, 37)

16 Baadhi ya watumishi wa Yehova wamekuwa wakisubiri kwa muda mrefu mwisho wa mfumo huu wa mambo. Kwa maoni ya kibinadamu, huenda ikaonekana kwamba kutimizwa kwa ahadi ya Mungu kunakawia. Yehova anaelewa jambo hilo, na alimhakikishia hivi nabii Habakuki: “Kwa maana maono hayo bado yatatimia kwa wakati wake uliowekwa, nayo yanasonga haraka kuelekea mwisho wake, nayo hayatasema uwongo. Hata yakikawia, endelea kuyatarajia! Kwa maana hakika yatatimia. Hayatachelewa!” (Hab. 2:3) Je, Mungu alitoa uhakikisho huo kwa ajili tu ya Habakuki? Au je, maneno yake yanatuhusu leo? Akiongozwa na roho, mtume Paulo alielekeza maneno hayo kwa Wakristo ambao wanatarajia ulimwengu mpya. (Soma Waebrania 10:36, 37.) Naam, tunaweza kuwa na uhakika kwamba hata ikiwa inaonekana kwamba ahadi ya Mungu ya kutukomboa inachelewa, ‘hakika itatimia. Haitachelewa!’

17. Dada mmoja alitumiaje shauri ambalo Yehova alimpa Habakuki?

17 Watumishi wengi wa Yehova wametii shauri la Yehova la ‘kuendelea kutarajia’—hata kwa miaka mingi sana. Kwa mfano, Dada Louise alianza kumtumikia Yehova mwaka wa 1939. Anasema hivi: “Wakati huo, nilifikiri kwamba Har–Magedoni ingekuja kabla sijamaliza shule ya sekondari. Haikuwa hivyo. Kwa miaka mingi, nimenufaika kwa kusoma maandiko ninayoyaita ‘masimulizi ya kusubiri,’ yaani, masimulizi ya Biblia kumhusu Noa, Abrahamu, Yosefu, na wengine ambao walilazimika kusubiri kwa muda mrefu kabla ya kupokea thawabu waliyoahidiwa na Yehova. Kuendelea kusubiri kumenisaidia mimi na wengine tuendelee kukazia fikira uhakika wa kwamba ulimwengu mpya uko karibu.” Wengine wengi ambao wamemtumikia Yehova kwa miaka mingi wanakubaliana na jambo hilo!

18. Kuchunguza uumbaji kunawezaje kuimarisha imani yetu katika ulimwengu mpya unaokuja?

18 Ni kweli kwamba bado ulimwengu mpya haujafika. Hata hivyo, fikiria baadhi ya mambo tunayoona—nyota, miti, wanyama, na wanadamu wenzetu. Hakuna mtu anayeweza kutilia shaka kwamba vitu hivyo ni halisi hata ingawa kuna wakati ambapo havikuwepo. Vipo sasa kwa sababu tu Yehova aliviumba. (Mwa. 1:1, 26, 27) Pia, Mungu wetu ameahidi kwamba ataleta ulimwengu mpya. Atatimiza ahadi hiyo. Katika ulimwengu mpya, watu watafurahia kuishi milele wakiwa na afya kamilifu. Wakati ambao Mungu ameweka utakapofika, ulimwengu mpya utakuwa halisi kama ulimwengu tunaouona leo.—Isa. 65:17; Ufu. 21:3, 4.

19. Unawezaje kuimarisha imani yako?

19 Kwa wakati huu, fanya yote unayoweza ili kuimarisha imani yako. Sitawisha uthamini kuelekea fidia. Tafakari kuhusu nguvu za Yehova. Shiriki katika utendaji mbalimbali wa kiroho. Ukifanya hivyo, unaweza kuwa kati ya “wale ambao kupitia imani na subira huzirithi ahadi.”—Ebr. 6:11, 12; Rom. 5:5.

WIMBO 139 Wazia Wakati Vitu Vyote Vitakuwa Vipya

a Leo, watu wengi hawaamini ahadi ya Biblia kuhusu ulimwengu mpya. Wanafikiri kwamba ni ndoto, hadithi ya kutungwa, au jambo lisilowezekana. Lakini tuna uhakika kwamba ahadi zote za Yehova zitatimia. Hata hivyo, ili tuendelee kudumisha imani yetu, tunapaswa kuendelea kuiimarisha. Jinsi gani? Makala hii itaeleza.

b Baadhi ya majina yamebadilishwa.

c Unaweza kupata makala nyingi kuhusu unabii wa Biblia ukitazama chini ya kichwa “Unabii” katika Fahirisi. Kwa mfano, ona makala “Yale Anayotabiri Yehova Yanatimia” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 2008.