Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mmewekwa Huru kwa Fadhili Zisizostahiliwa

Mmewekwa Huru kwa Fadhili Zisizostahiliwa

“Dhambi haipaswi kuwa bwana juu yenu, kwa kuwa ninyi [mko] . . . chini ya fadhili zisizostahiliwa.”—ROM. 6:14.

NYIMBO: 2, 61

1, 2. Kwa nini Mashahidi wa Yehova wanapendezwa na andiko la Waroma 5:12?

IKIWA ungeambiwa utaje maandiko ambayo Mashahidi wa Yehova wanajua na kuyatumia sana, je, Waroma 5:12 lingekuwa kati ya maandiko ambayo ungetaja kwanza? Fikiria mara ambazo umesoma maneno haya: “Kama vile kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.”

2 Andiko hilo limetumiwa mara nyingi katika kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? Unapojifunza kitabu hicho pamoja na watoto wako au na watu wengine, inaelekea utasoma andiko la Waroma 5:12 unapozungumzia kusudi la Mungu kwa dunia katika sura ya 3, fidia katika 5, na hali ya wafu katika 6. Lakini ni mara ngapi unafikiria andiko hilo kuhusiana na matendo yako, tumaini lako la wakati ujao, na uhusiano wako na Yehova?

3. Tunapaswa kukubali ukweli gani kuhusu dhambi?

3 Ni lazima tukubali kwamba sisi sote ni watenda dhambi. Tunakosea kila siku. Hata hivyo, tuna uhakika kwamba Mungu anakumbuka sisi ni mavumbi na yuko tayari kutuonyesha rehema. (Zab. 103:13, 14) Katika sala ya kielelezo, Yesu alitia ndani ombi hili: “Utusamehe dhambi zetu.” (Luka 11:2-4) Kwa hiyo, hatuna sababu ya kuendelea kufikiria makosa ambayo Mungu ametusamehe. Lakini tunaweza kunufaika kwa kufikiria jinsi ambavyo ametusamehe.

TUMESAMEHEWA KUPITIA FADHILI ZISIZOSTAHILIWA

4, 5. (a) Ni nini kinachotusaidia kuelewa andiko la Waroma 5:12? (b) Andiko la Waroma 3:24 linamaanisha nini linapotaja “fadhili zake zisizostahiliwa?”

4 Tunapata habari muhimu katika muktadha wa maneno ya mtume Paulo kwenye andiko la Waroma 5:12, hasa sura ya 6. Habari hiyo itatusaidia kuelewa jinsi Yehova anavyoweza kutusamehe. Tunasoma hivi katika sura ya 3: “Wote wamefanya dhambi . . . , nayo ni zawadi ya bure kwamba wanatangazwa kuwa waadilifu kwa fadhili zake zisizostahiliwa kupitia kuachiliwa huru kwa njia ya fidia ambayo Kristo Yesu alilipa.” (Rom. 3:23, 24) Paulo alimaanisha nini aliposema “fadhili zake zisizostahiliwa”? Kulingana na kitabu kimoja cha marejeo, alitumia neno la Kigiriki linalomaanisha “kuonyesha fadhili kwa ukarimu bila kudai au kutarajia malipo yoyote.” Hatujafanya lolote kustahili fadhili hizo.

5 Msomi John Parkhurst alisema hivi: “Neno hilo [la Kigiriki] linapotumiwa kumhusu Mungu au Kristo, mara nyingi hurejelea fadhili zisizostahiliwa wanazoonyesha bure au fadhili wanazoonyesha katika kuwakomboa na kuwaokoa wanadamu.” Hivyo, maneno “fadhili zake zisizostahiliwa” kama yanavyotumiwa katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya yanafaa. Lakini Mungu alionyeshaje fadhili hizo zisizostahiliwa? Na sifa hiyo inahusianaje na tumaini lako na vilevile uhusiano wako pamoja na Mungu? Acheni tuone.

6. Wanadamu wanaweza kunufaika kadiri gani na fadhili zisizostahiliwa za Mungu?

6 Dhambi na kifo “[viliingia] katika ulimwengu” kupitia “mtu mmoja,” Adamu. Kwa hiyo, “kwa kosa la mtu mmoja kifo kilitawala kama mfalme.” Paulo alitaja pia kwamba tulipokea “wingi wa fadhili zisizostahiliwa” za Mungu “kupitia mtu mmoja, Yesu Kristo.” (Rom. 5:12, 15, 17) Fadhili hizo zisizostahiliwa zimewanufaisha wanadamu wote. “Kupitia kutii kwa mtu mmoja [Yesu] wengi watafanywa kuwa waadilifu.” Kwa kweli, kupitia fadhili zisizostahiliwa za Mungu tunaweza kupata “uzima wa milele kupitia Yesu Kristo.”—Rom. 5:19, 21.

7. Kwa nini uandalizi wa Mungu wa fidia ni wonyesho wa fadhili, na kwa nini hatuustahili?

7 Haikuwa lazima Yehova amtume Mwana wake duniani ili kuandaa fidia. Isitoshe, wanadamu wenye dhambi hawakustahili kile ambacho Mungu na Yesu walifanya ili waandae fidia inayowawezesha wanadamu kupokea msamaha. Hivyo, kusamehewa dhambi zetu na kupewa tumaini la kuishi milele ni fadhili tusizostahili. Tunapaswa kuthamini sana zawadi ya fadhili zisizostahiliwa za Mungu na kuonyesha hivyo kupitia matendo yetu ya kila siku.

TUNAONYESHAJE KWAMBA TUNATHAMINI FADHILI ZISIZOSTAHILIWA ZA MUNGU?

8. Huenda watu fulani wakawa na maoni gani yasiyofaa kuhusu dhambi zao?

8 Kwa kuwa sisi ni wazao wasio wakamilifu wa Adamu, tuna mwelekeo wa kukosea au hata kufanya dhambi. Lakini lingekuwa kosa zito kutumia vibaya fadhili zisizostahiliwa za Mungu kwa kufikiri hivi: ‘Hata nikikosea, au kufanya jambo ambalo Mungu analiona kuwa dhambi, sihitaji kuhangaika. Yehova atanisamehe.’ Inasikitisha kwamba Wakristo fulani walihisi hivyo hata mitume walipokuwa hai. (Soma Yuda 4.) Huenda tusiseme hivyo; lakini mawazo hayo yanaweza kuwa yameanza kusitawi moyoni mwetu au huenda watu wengine wametuathiri na kufanya tufikiri hivyo.

9, 10. Paulo na wengine waliwekwa huru jinsi gani kutoka katika dhambi na kifo?

9 Paulo alikazia kwamba tunapaswa kupinga kabisa maoni kama haya: ‘Mungu anaelewa. Atapuuza matendo yangu mabaya.’ Kwa nini tupinge maoni hayo? Kwa sababu Paulo aliandika kwamba Wakristo “[wamekufa] kuhusiana na dhambi.” (Waroma 6:1, 2.) Kwa nini tunaweza kusema kwamba Wakristo hao walikuwa “[wamekufa] kuhusiana na dhambi,” ingawa bado walikuwa hai?

10 Fidia ambayo Mungu aliandaa ilimnufaisha Paulo na wengine walioishi katika siku zake. Hivyo, Yehova aliwasamehe dhambi zao, akawatia mafuta kwa roho takatifu, na kuwafanya kuwa wana wake wa kiroho. Kisha wakapokea tumaini la kwenda mbinguni. Ikiwa wangeendelea kuwa waaminifu, wangeishi mbinguni na kutawala pamoja na Kristo. Lakini Paulo alisema kwamba walikuwa “[wamekufa] kuhusiana na dhambi” ingawa bado walikuwa hai wakimtumikia Mungu duniani. Alitumia mfano wa Yesu, ambaye alikufa akiwa mwanadamu na akafufuliwa akiwa kiumbe wa roho mbinguni asiyeweza kufa. Kifo hakikuwa bwana tena juu ya Yesu. Ilikuwa hivyo pia kwa Wakristo watiwa mafuta, ambao walijihesabu kuwa “wafu kwelikweli kuhusiana na dhambi lakini walio hai kuhusiana na Mungu kwa njia ya Kristo Yesu.” (Rom. 6:9, 11) Maisha yao yalikuwa yamebadilika. Hawakuwa wakiongozwa tena na tamaa zao zenye dhambi. Walikuwa wamekufa kuhusiana na maisha yao ya zamani.

11. Ni katika maana gani sisi tulio na tumaini la kuishi milele katika Paradiso “[tumekufa] kuhusiana na dhambi”?

11 Namna gani sisi? Ni kweli kwamba kabla hatujawa Wakristo, tulifanya dhambi mara nyingi na labda hatukutambua uzito wa matendo yetu machoni pa Mungu. Tulikuwa kama “watumwa wa ukosefu wa usafi na uasi-sheria.” Tunaweza kusema kwamba tulikuwa “watumwa wa dhambi.” (Rom. 6:19, 20) Kisha tukajifunza kweli ya Biblia, tukafanya mabadiliko maishani, tukajiweka wakfu kwa Mungu na kubatizwa. Tangu wakati huo, tumetamani “kutoka moyoni [kuwa] wenye kutii” mafundisho na viwango vya Mungu. Ingawa hatusemi kwamba tumekufa kihalisi, “[tuliwekwa] huru kutoka katika dhambi,” na “[tukawa] watumwa wa uadilifu.” (Rom. 6:17, 18) Hiyo ndiyo sababu Biblia inasema kwamba sisi pia “[tumekufa] kuhusiana na dhambi.”

12. Kila mmoja wetu anahitaji kufanya uamuzi gani?

12 Sasa fikiria jinsi maneno haya ya Paulo yanavyokuhusu: “Msiache dhambi iendelee kutawala kama mfalme katika miili yenu inayoweza kufa hivi kwamba mzitii tamaa zake.” (Rom. 6:12) Huenda “[tukaacha] dhambi iendelee kutawala” kwa kufanya mambo ambayo mwili wetu usio mkamilifu unatusukuma kufanya. Kwa kuwa tuna uhuru wa kuamua ikiwa ‘tutaacha’ dhambi itutawale au la, swali ni, Tunatamani kufanya nini hasa kutoka moyoni? Jiulize hivi: ‘Je, nyakati nyingine ninaruhusu mwili au akili yangu isiyo kamilifu iniongoze vibaya, na hivyo kutenda dhambi? Au je, nimekufa kuhusiana na dhambi? Je, niko hai kuhusiana na Mungu kwa njia ya Kristo Yesu?’ Maamuzi yetu yanategemea tunathamini kadiri gani fadhili zisizostahiliwa ambazo Mungu ametuonyesha kwa kutusamehe.

UNAWEZA KUSHINDA!

13. Kuna uthibitisho gani kwamba tunaweza kuacha kutenda dhambi?

13 Watu wa Yehova wameacha ‘tunda ambalo kwa kawaida walikuwa nalo’ kabla wamjue, wampende, na waanze kumtumikia Mungu. Huenda ikawa maisha yao ya zamani yalihusisha “mambo ambayo sasa [wanayaonea] aibu” na ambayo yangefanya wastahili kufa. (Rom. 6:21) Lakini walibadilika. Wakristo wengi Wakorintho ambao Paulo aliwaandikia walifanya hivyo pia. Baadhi yao walikuwa waabudu sanamu, wazinzi, wanaume wanaolala na wanaume, wezi, walevi, na wengine kama hao. Lakini, ‘walioshwa wakawa safi’ na ‘kutakaswa.’ (1 Kor. 6:9-11) Inaelekea wengine katika kutaniko la Roma walikuwa hivyo pia. Paulo aliongozwa na roho kuwaandikia hivi: “Wala msiendelee kuvitoa viungo vyenu kwa dhambi kuwa silaha za ukosefu wa uadilifu, bali jitoeni wenyewe kwa Mungu kama walio hai kutoka kwa wafu, pia viungo vyenu kwa Mungu kuwa silaha za uadilifu.” (Rom. 6:13) Paulo alikuwa na uhakika kwamba wangebaki safi kiroho na hivyo kuendelea kunufaika na fadhili zisizostahiliwa za Mungu.

14, 15. Tunapaswa kujiuliza nini kuhusu kuwa wenye kutii “kutoka moyoni”?

14 Ndivyo ilivyo leo. Huenda baadhi ya ndugu na dada walikuwa kama Wakristo huko Korintho. Lakini wao pia walibadilika. Waliacha maisha yao ya zamani ya dhambi na ‘wakaoshwa wakawa safi.’ Hata iwe hali yako ilikuwaje, msimamo wako mbele za Mungu ukoje sasa? Kwa kuwa umepokea fadhili zisizostahiliwa za Mungu na vilevile msamaha wa dhambi, je, umeazimia kuacha kabisa ‘kuvitoa viungo vyako kwa dhambi’? Na je, ‘utajitoa mwenyewe kwa Mungu kama uliye hai kutoka kwa wafu’?

15 Ili tufanye hivyo, ni lazima tuamue kuepuka mazoea ya kufanya dhambi nzito ambazo baadhi ya Wakristo huko Korintho walikuwa wamefanya. Hilo ni muhimu ili tuonyeshe kuwa tumekubali fadhili zisizostahiliwa za Mungu na kwamba ‘dhambi si bwana juu yetu.’ Lakini je, sisi pia tumeazimia “kutoka moyoni [kuwa] wenye kutii” kwa kufanya yote tuwezayo ili kuepuka dhambi ambazo wengine huona kuwa si nzito?—Rom. 6:14, 17.

16. Tunajuaje kwamba kuwa Mkristo kunahusisha mengi zaidi ya kuacha mazoea ya kufanya dhambi nzito?

16 Mfikirie mtume Paulo. Tuna uhakika kwamba hakuwa akifanya dhambi nzito kama zile zinazotajwa katika 1 Wakorintho 6:9-11. Hata hivyo, alikiri kwamba bado alikuwa na hatia ya dhambi. Aliandika hivi: “Mimi ni wa kimwili, nimeuzwa chini ya dhambi. Kwa maana lile ninalofanya silijui. Kwa maana lile ninalolitaka, hilo sizoei kulifanya; bali lile ninalochukia ndilo ninalofanya.” (Rom. 7:14, 15) Hilo linaonyesha kwamba kulikuwa na mambo mengine ambayo Paulo aliyaona kuwa dhambi, na alikuwa akipambana dhidi ya mambo hayo pia. (Soma Waroma 7:21-23.) Kama Paulo, sisi pia na tuendelee kufanya hivyo tunapojitahidi kutii “kutoka moyoni.”

17. Kwa nini ungependa kuwa mnyoofu?

17 Kwa mfano, fikiria suala la kuwa mnyoofu. Mkristo anapaswa kuwa mnyoofu. (Soma Methali 14:5; Waefeso 4:25.) Shetani ndiye “baba ya uwongo.” Anania na mke wake walikufa kwa sababu ya kusema uwongo. Tunaepuka kusema uwongo kwa kuwa hatungependa kuiga watu kama hao. (Yoh. 8:44; Mdo. 5:1-11) Je, kuwa wanyoofu kunamaanisha tu kuepuka kusema uwongo? Kwa kweli, tukiwa wanyoofu tutaonyesha kwamba tunathamini sana fadhili zisizostahiliwa za Mungu.

18, 19. Kwa nini kuwa mnyoofu kunahusisha mengi zaidi ya kuepuka tu kusema uwongo?

18 Kusema uwongo ni kusema habari zisizo za kweli. Hata hivyo, Yehova anataka watu wake wafanye mengi zaidi ya kuepuka tu kusema uwongo. Aliwahimiza hivi Waisraeli wa kale: “Muwe watakatifu, kwa sababu mimi Yehova Mungu wenu ni mtakatifu.” Kisha akawapa mifano ya jinsi wanavyoweza kuwa watakatifu. Kwa mfano, Mungu alisema: “Msiibe, wala msidanganye, wala msitendeane kwa uwongo mtu yeyote na mwenzake.” (Law. 19:2, 11) Inasikitisha kwamba mtu ambaye ameazimia kutosema uwongo anaweza kudanganya wengine au kuwatendea kwa uwongo kwa kuwapa habari zisizo za kweli.

Je, tumeazimia kuepuka kusema uwongo na kudanganya?

19 Kwa mfano, mtu anaweza kumwambia mwajiri wake au wafanyakazi wenzake kwamba siku inayofuata hatakuja kazini au ataondoka mapema kwa sababu anahitaji ‘kumwona daktari.’ Ukweli ni kwamba anaposema anahitaji ‘kumwona daktari,’ anamaanisha kwenda kununua dawa au kupitia hospitalini kifupi ili kulipia gharama za matibabu. Kumbe sababu yake kuu ni kwamba alikuwa amepanga kusafiri na alitaka kuanza safari hiyo mapema au alitaka kupeleka familia yake tafrija ufuoni. Ingawa mambo fulani aliyofanya yalihusiana na ‘kumwona daktari,’ je, ungesema kwamba alikuwa mnyoofu, au alikuwa mdanganyifu? Huenda ikawa unajua visa vingine vya watu waliowapotosha wenzao kimakusudi. Labda walifanya hivyo ili kuepuka adhabu au kujifaidi kwa kuwaumiza wengine. Hata ikiwa hawakusema uwongo moja kwa moja, je, walitii amri ya Mungu inayosema, “Msidanganye”? Pia fikiria andiko la Waroma 6:19 linalosema: “Vitoeni viungo vyenu viwe watumwa wa uadilifu kwa kutazamia utakatifu.”

20, 21. Mbali na kuepuka dhambi nzito, fadhili zisizostahiliwa za Mungu zinapaswa kutuchochea kuepuka mambo gani mengine?

20 Wazo kuu ni kwamba kuthamini fadhili zisizostahiliwa za Mungu kunahusisha mengi zaidi ya kuepuka uzinzi, ulevi, au dhambi nyingine ambazo Wakorintho walifanya. Kukubali fadhili zisizostahiliwa za Mungu hakumaanishi kuepuka tu mwenendo mpotovu wa kingono bali pia kupinga kabisa mwelekeo wowote wa kufurahia burudani zisizo safi. Kutoa viungo vyetu viwe watumwa wa uadilifu kutatuzuia tusilewe au kunywa pombe kufikia hatua ya kukaribia kulewa. Jitihada nyingi zinahitajiwa ili kupambana na mazoea hayo mabaya; hata hivyo, tunaweza kushinda.

21 Lengo letu halipaswi kuwa kuepuka tu dhambi nzito, bali pia kuepuka makosa yasiyo dhahiri. Ingawa hatutaweza kufanya hivyo kikamili, tunahitaji kujitahidi kwa kadiri ya uwezo wetu kama Paulo alivyofanya. Aliwahimiza hivi ndugu zake: “Msiache dhambi iendelee kutawala kama mfalme katika miili yenu inayoweza kufa hivi kwamba mzitii tamaa zake.” (Rom. 6:12; 7:18-20) Tunapojitahidi kupinga dhambi za aina zote, tunaonyesha kwamba tunathamini kikweli fadhili zisizostahiliwa za Mungu kupitia Kristo.

22. Wale wanaothamini fadhili zisizostahiliwa za Mungu watapata thawabu gani?

22 Kupitia fadhili zisizostahiliwa za Mungu, tumesamehewa dhambi zetu na Yehova anaweza kuendelea kutusamehe. Acheni tuendelee kuonyesha uthamini kwa kushinda mwelekeo wowote wa kukubali kutenda dhambi ambazo wengine huziona kuwa si nzito. Paulo alikazia thawabu tutakayopata kwa kufanya hivyo: “Sasa, kwa sababu mliwekwa huru kutoka katika dhambi lakini mkawa watumwa kwa Mungu, mnapata tunda lenu katika utakatifu, na mwisho ni uzima wa milele.”—Rom. 6:22.