Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mtupie Yehova Mahangaiko Yako Yote

Mtupie Yehova Mahangaiko Yako Yote

“[Tupeni] mahangaiko yenu yote juu yake [Yehova], kwa sababu yeye anawajali ninyi.”—1 PET. 5:7.

NYIMBO: 60, 23

1, 2. (a) Kwa nini hatupaswi kushangaa tunapokuwa na mahangaiko? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.) (b) Tutachunguza nini katika makala hii?

TUNAISHI katika nyakati zenye mikazo mingi sana. Shetani Ibilisi ana hasira kali na “anatembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta kummeza mtu.” (1 Pet. 5:8; Ufu. 12:17) Kwa hiyo, haishangazi kwamba nyakati nyingine hata watumishi wa Mungu wanakuwa na mahangaiko. Pindi fulani, hata watumishi wa kale waliomwogopa Yehova, kama vile Mfalme Daudi, walikuwa na “wasiwasi rohoni.” (Zab. 13:2, Biblia Habari Njema) Kumbuka pia kwamba mtume Paulo alikuwa na “[mahangaiko] kwa ajili ya makutaniko yote.” (2 Kor. 11:28) Lakini tunaweza kufanya nini tunapolemewa na mahangaiko?

2 Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo aliwasaidia watumishi wake zamani, naye hutusaidia kupata kitulizo kutokana na mahangaiko hata sasa. Biblia inatuhimiza hivi: “[Tupeni] mahangaiko [wasiwasi] yenu yote juu yake, kwa sababu yeye anawajali ninyi.” (1 Pet. 5:7) Lakini unaweza kufanya hivyo jinsi gani? Acheni tuzungumzie njia nne. Unaweza (1) kusali kutoka moyoni, (2) kusoma na kutafakari Neno la Mungu, (3) kumwomba Yehova akupe roho yake takatifu, na (4) kumweleza rafiki unayemtumaini hisia zako. Tunapochunguza mambo hayo manne, jaribu kuona mambo unayoweza kufanya ili upunguze mahangaiko.

“MTUPIE YEHOVA MZIGO WAKO”

3. Unaweza ‘kumtupia Yehova mzigo wako’ kupitia sala jinsi gani?

3 Jambo la kwanza tunaloweza kufanya ni kusali kwa Yehova kwa bidii. Unapokabili hali zinazoweza kufanya uwe na wasiwasi, mahangaiko, au ukose utulivu, mmiminie Baba yako wa mbinguni moyo wako. Mtunga zaburi Daudi alimsihi Yehova hivi: “Utege sikio, Ee Mungu, kwa sala yangu.” Kisha akasema hivi katika zaburi hiyohiyo: “Mtupie Yehova mzigo wako, naye mwenyewe atakutegemeza.” (Zab. 55:1, 22) Baada ya kufanya yote uwezayo ili kusuluhisha tatizo, utapata matokeo mazuri zaidi kwa kusali kutoka moyoni badala ya kuwa na wasiwasi. Lakini sala inaweza kukusaidiaje usilemewe na fikira zinazofadhaisha na maumivu ya kihisia?—Zab. 94:18, 19.

4. Kwa nini sala ni muhimu tunapokuwa na mahangaiko?

4 Soma Wafilipi 4:6, 7Yehova anaweza kujibu dua zetu za kutoka moyoni tunazotoa kwa bidii. Jinsi gani? Kwa kutupatia utulivu utakaofanya tuache kusumbuka akilini na moyoni. Watu wengi wamejionea jambo hilo maishani. Badala ya kuwa na wasiwasi na woga, Mungu aliwasaidia wapate amani na utulivu ambao hakuna mwanadamu anayeweza kuuelewa. Wewe pia unaweza kupata utulivu huo. Hivyo, “amani ya Mungu” inaweza kushinda hali zozote ngumu ambazo huenda ukakabili. Unaweza kutegemea ahadi hii inayoonyesha huruma za Yehova: “Usifadhaike, mimi ni Mungu wako. Nitakuimarisha na kukusaidia.”—Isa. 41:10, BHN.

KUPATA AMANI YA MOYONI KATIKA NENO LA MUNGU

5. Neno la Mungu linaweza kutusaidiaje kuwa na amani ya moyoni?

5 Jambo la pili tunaloweza kufanya ili tupate amani ya moyoni ni kusoma maandiko mbalimbali katika Biblia na kuyatafakari. Kwa nini ni muhimu kufanya hivyo? Biblia ina mwongozo wa kiroho unaoweza kutusaidia kuepuka, kupunguza, au kushughulika na mahangaiko. Kumbuka kwamba Neno la Mungu hutusaidia na kutuburudisha kwa sababu lina maneno ya hekima kutoka kwa Muumba wetu. Ukitafakari mawazo ya Mungu, iwe ni mchana au usiku, na kufikiria njia bora zaidi ya kutumia mwongozo wa Biblia, utaimarishwa sana. Katika Biblia, Yehova alihusianisha moja kwa moja kusoma Neno lake na kuwa “hodari na mwenye nguvu” bali si ‘kutetemeka na kuwa na hofu.’—Yos. 1:7-9.

6. Maneno ya Yesu yanaweza kukusaidiaje?

6 Katika Neno la Mungu, tunasoma maneno ya Yesu yenye kuburudisha. Maneno na mafundisho yake yaliwaburudisha wasikilizaji wake. Watu wengi walivutiwa naye kwa sababu alituliza mioyo ya watu wenye mahangaiko, akawaimarisha walio dhaifu, na kuwafariji walioshuka moyo. (Soma Mathayo 11:28-30.) Alihangaikia mahitaji ya kiroho, kihisia, na kimwili ya watu wengine kwa upendo. (Marko 6:30-32) Hata leo tunaweza kuamini ahadi yake kwamba atatutegemeza. Anaweza kukutegemeza kama alivyowategemeza mitume waliokuwa wakisafiri pamoja naye. Si lazima iwe uliishi wakati ambapo Yesu alikuwa duniani ili unufaike. Akiwa Mfalme anayetawala mbinguni, Yesu anaelewa hisia za wengine na anaendelea kuwaonyesha huruma. Kwa hiyo, unapokuwa na mahangaiko, kwa huruma anaweza ‘kukusaidia’ na “kuwa msaada kwa wakati unaofaa.” Naam, Yesu anaweza kukusaidia ukabiliane na wasiwasi, na kukufanya uwe na tumaini na ujasiri.—Ebr. 2:17, 18; 4:16.

SIFA ZA ROHO YA MUNGU

7. Utanufaikaje Mungu anapojibu unapomwomba roho takatifu?

7 Yesu aliahidi kwamba Baba yetu wa mbinguni hatakosa kuwapa roho takatifu wale wanaomwomba. (Luka 11:10-13) Jambo la tatu linaloweza kutusaidia sana kuondoa mahangaiko ni sifa za tunda la roho. Sifa hizo nzuri zinazotokezwa na roho takatifu ya Mungu huonyesha jinsi utu wa Mungu mweza yote ulivyo. (Soma Wagalatia 5:22, 23; Kol. 3:10) Kadiri unavyositawisha tunda la roho hiyo, ndivyo utakavyoendelea kuboresha uhusiano wako na watu wengine. Hivyo, hali nyingi zinazoweza kusababisha mahangaiko hazitatokea. Acheni tuchunguze kwa ufupi jinsi sifa za tunda la roho zinavyoweza kukusaidia.

8-12. Sifa za tunda la roho zinaweza kukusaidiaje kuepuka au kushughulika na hali zinazoweza kutokeza mahangaiko?

8 “Upendo, shangwe, amani.” Unapojitahidi kuwaonyesha wengine heshima, inaelekea utagundua kwamba unaweza kushughulika kwa njia bora zaidi na mahangaiko yako mwenyewe. Hilo linawezekanaje? Unapoonyesha upendo wa kindugu, upendo mwororo, na heshima, utaepuka hali zinazoweza kusababisha mahangaiko.—Rom. 12:10.

9 “Ustahimilivu, fadhili, wema.” Unaweza kuishi kwa amani na wengine kwa kutii himizo hili: “Iweni wenye fadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma nyororo, mkisameheana kwa hiari.” (Efe. 4:32) Kwa kufanya hivyo, utaepuka hali ambazo zingeweza kukusababishia mahangaiko. Pia, unaweza kushughulika kwa njia nzuri na hali zinazosababishwa na kutokamilika.

10 “Imani.” Mara nyingi mahangaiko yetu yanahusiana na matatizo ya kifedha na vitu vya kimwili. (Met. 18:11) Kwa sababu hiyo, ukiwa na imani yenye nguvu kwamba Yehova anakupenda na kukujali, unaweza kukabiliana na mahangaiko hayo au hata kuyaepuka. Jinsi gani? Unaweza kuepuka mahangaiko mengi kwa kutii shauri la mtume Paulo lililoongozwa na roho la “[kuridhika] na vitu vya sasa.” Paulo aliongeza hivi: “Kwa maana [Mungu] amesema: ‘Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.’ Hivi kwamba tuwe hodari na kusema: ‘Yehova ni msaidizi wangu; sitaogopa. Mwanadamu anaweza kunitenda nini?’”—Ebr. 13:5, 6.

11 “Upole, kujizuia.” Unaweza kunufaika na kupata matokeo mazuri kwa kuonyesha sifa hizo. Hivyo, yaelekea utaepuka matendo yanayoweza kukusababishia mahangaiko, na utanufaika kwa kuepuka “uchungu wote wenye uovu na hasira na ghadhabu na kupiga kelele na matukano.”—Efe. 4:31.

12 Unahitaji kuwa mnyenyekevu ili ukubali kuongozwa na “mkono wenye nguvu wa Mungu” na ‘kutupa mahangaiko yako yote juu yake.’ (1 Pet. 5:6, 7) Lakini unapositawisha sifa ya unyenyekevu, hatimaye utapata kibali cha Mungu na msaada wake. (Mika 6:8) Ukiwa na usawaziko kuhusu uwezo wako wa kimwili, kiakili, na kihisia inaelekea kwamba hutalemewa na mahangaiko kwa sababu utakuwa ukimtegemea Mungu.

“MSIHANGAIKE KAMWE”

13. Yesu alimaanisha nini aliposema: “Msihangaike kamwe”?

13 Katika andiko la Mathayo 6:34 (soma), tunasoma shauri hili la Yesu: “Msihangaike kamwe.” Hata hivyo, huenda isiwe rahisi kutii shauri hilo. Yesu alimaanisha nini aliposema: “Msihangaike kamwe”? Bila shaka, hakumaanisha kwamba mtumishi wa Mungu hawezi kuwa na mahangaiko kwa sababu tayari tumesoma maneno ya Daudi na Paulo kuhusu jambo hilo. Lakini Yesu alikuwa akiwasaidia wanafunzi wake watambue kwamba kuhangaika isivyo lazima au kuhangaika kupita kiasi hakusuluhishi matatizo. Kila siku ina mahangaiko yake, kwa hiyo Wakristo hawahitaji kujumlisha mahangaiko yao ya sasa na mahangaiko kuhusu mambo yaliyopita au ya wakati ujao. Unaweza kufuata shauri la Yesu jinsi gani, hivyo kupunguza mahangaiko yenye kulemea?

14. Unaweza kushughulikaje na mahangaiko yanayohusu wakati uliopita?

14 Mtu anaweza kuwa na mahangaiko kwa sababu ya makosa yake ya wakati uliopita. Huenda akasumbuliwa na hisia za hatia kuhusu jambo ambalo alifanya zamani. Nyakati nyingine, Mfalme Daudi alihisi kwamba ‘makosa yake yalipita juu ya kichwa chake.’ Alikiri hivi: “Nimenguruma kwa sababu ya kuugua kwa moyo wangu.” (Zab. 38:3, 4, 8, 18) Ni jambo gani la hekima ambalo Daudi alipaswa kufanya katika hali hiyo, naye alifanya nini? Alitumaini kwamba Yehova angemwonyesha rehema na kumsamehe. Alisema hivi akiwa na uhakika: “Mwenye furaha ni mtu ambaye amesamehewa maasi yake.”—Soma Zaburi 32:1-3, 5.

15. (a) Kwa nini hupaswi kuhangaika kuhusu mambo unayokabiliana nayo kwa sasa? (b) Unaweza kuchukua hatua zipi ili kupunguza mahangaiko? (Tazama sanduku lenye kichwa “ Mambo Unayoweza Kufanya Ili Kupunguza Mahangaiko.”)

15 Nyakati nyingine, unaweza kuhangaika kuhusu mambo unayokabiliana nayo kwa sasa. Kwa mfano, Daudi alipoandika Zaburi ya 55 aliogopa kwamba angeweza kuuawa. (Zab. 55:2-5) Hata hivyo, hakuruhusu mahangaiko yake yamzuie kumtegemea Yehova. Daudi alisali kwa bidii kuhusu matatizo yake na pia alielewa umuhimu wa kuchukua hatua zinazofaa ili kushughulika na mahangaiko yake. (2 Sam. 15:30-34) Unaweza kujifunza somo kutoka kwa Daudi. Badala ya kuruhusu ulemewe na mahangaiko, chukua hatua ili ushughulike na hali hiyo. Baada ya kufanya hivyo, mwachie Yehova na uwe na uhakika kwamba atakusaidia.

16. Kujua maana ya jina la Mungu kunaweza kuimarishaje imani yako?

16 Mara nyingi mahangaiko yasiyo ya lazima hutokea Mkristo anapofikiria matatizo ambayo huenda yakatukia wakati ujao. Hata hivyo, si lazima ulemewe na mahangaiko au kuwa na wasiwasi kuhusu mambo ambayo hujui ikiwa yatatukia. Kwa nini? Kwa sababu mara nyingi mambo hayawi mabaya kama tulivyohofia. Isitoshe, hakuna hali inayomshinda Mungu ambaye unaweza kumtupia mahangaiko yako yote. Jina lake linamaanisha “Nitakuwa Kile Nitakachokuwa.” (Kut. 3:14) Maana halisi ya jina lake inatuhakikishia kwamba Mungu ana uwezo kamili wa kutimiza makusudi yake kuelekea watumishi wake. Unaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu anaweza kuwathawabisha watumishi wake waaminifu na kuwasaidia kukabiliana na mahangaiko ya wakati uliopita, ya sasa, na ya wakati ujao.

ZUNGUMZA KWA UNYOOFU

17, 18. Mawasiliano mazuri yanaweza kukusaidiaje kukabiliana na mahangaiko?

17 Jambo la nne linaloweza kukusaidia ukabiliane na mahangaiko ni kumweleza rafiki wa karibu hisia zako. Mwenzi wako wa ndoa, rafiki wa karibu, au mzee wa kutaniko anaweza kukusaidia uwe na maoni yanayofaa kuhusu mahangaiko yako. “Hangaiko katika moyo wa mtu huufanya uiname, lakini neno jema huufanya ushangilie.” (Met. 12:25) Utaelewa mahangaiko yako na kushughulika nayo vizuri zaidi ukizungumza kwa unyoofu na rafiki wa karibu. Biblia inatuambia hivi: “Mipango huvunjika mahali ambapo hapana mazungumzo ya siri, lakini katika wingi wa washauri mambo hutimizwa.”—Met. 15:22.

18 Yehova pia huwasaidia Wakristo kushughulika na mahangaiko kupitia mikutano ya kutaniko ya kila juma. Ukiwa huko, unaweza kushirikiana na waabudu wenzako wanaokujali na walio tayari kukutia moyo. (Ebr. 10: 24, 25) ‘Ubadilishanaji huo wa kitia-moyo’ utakusaidia kupata tena nguvu za kiroho na kufanya iwe rahisi zaidi kushughulika na mahangaiko.—Rom. 1:12.

UHUSIANO WAKO NA MUNGU UTAKUIMARISHA SANA

19. Kwa nini unaweza kuwa na uhakika kwamba uhusiano wako na Mungu utakuimarisha?

19 Fikiria jinsi mzee mmoja nchini Kanada alivyojifunza umuhimu wa kumtupia Yehova mahangaiko yake. Yeye ni mwalimu na mshauri, kazi ambayo ina mikazo mingi, na vilevile ana ugonjwa wa kuwa na wasiwasi mwingi. Ndugu huyo amekabilianaje na hali hizo? Anaeleza hivi: “Zaidi ya mambo yote, nimeona kwamba ninapojitahidi kuimarisha uhusiano wangu na Yehova, ninapata nguvu za kukabiliana na matatizo yangu ya kihisia. Marafiki wa kweli na ndugu zangu wa kiroho hunisaidia sana ninaposhuka moyo. Mimi humweleza mke wangu hisia zangu kwa unyoofu. Wazee wenzangu na mwangalizi wa mzunguko walinisaidia sana kuwa na maoni yanayofaa kuhusu matatizo yangu. Pia, nilitafuta msaada wa daktari, nikafanya mabadiliko katika ratiba yangu, na kutenga wakati wa kupumzika na kufanya mazoezi. Hatua kwa hatua, nilianza kupata usawaziko maishani. Ninapokabili hali nisizoweza kudhibiti, mimi humwachia Yehova mahangaiko yangu.”

20. (a) Tunaweza kumtupia Mungu mahangaiko yetu jinsi gani? (b) Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

20 Kwa muhtasari, tumeona umuhimu wa kumtupia Mungu mahangaiko yetu kupitia sala za kutoka moyoni, kusoma Neno lake, na kulitafakari. Tumechunguza pia umuhimu wa kusitawisha sifa za tunda la roho, kueleza rafiki wa karibu hisia zetu, na kuimarishwa na ushirika wenye kujenga wa Kikristo. Makala inayofuata itazungumzia jinsi Yehova anavyotutegemeza hata zaidi kwa kutuhakikishia kwamba atatuthawabisha.—Ebr. 11:6.