Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Huwathawabisha Wale Wanaomtafuta kwa Bidii

Yehova Huwathawabisha Wale Wanaomtafuta kwa Bidii

“Yule anayemkaribia Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.”—EBR. 11:6.

NYIMBO: 85, 134

1, 2. (a) Kuna uhusiano gani kati ya upendo na imani? (b) Tutachunguza maswali gani?

TUNAMPENDA Yehova “kwa sababu yeye alitupenda sisi kwanza.” (1 Yoh. 4:19) Yehova amechukua hatua ya kuwabariki watumishi wake waaminifu ikiwa njia moja ya kuonyesha upendo wake mwororo. Kadiri upendo wetu kwa Mungu unavyozidi kuongezeka, ndivyo tunavyokuwa na imani yenye nguvu kwamba yeye yupo na kuwa hakosi kuwathawabisha wale wanaompenda.​—Soma Waebrania 11:6.

2 Yehova ni mthawabishaji wa watumishi wake. Kuwathawabisha ni sehemu muhimu ya utu na matendo yake. Hatuwezi kuwa na imani kamili tusiposadiki kwamba Mungu atawathawabisha wale wanaomtafuta kwa bidii, kwa kuwa “imani ni tarajio lililohakikishwa la mambo yanayotumainiwa.” (Ebr. 11:1) Naam, imani inahusisha tarajio lililohakikishwa la baraka za Mungu zilizoahidiwa. Hata hivyo, kuwa na tumaini la kupata thawabu kunatunufaishaje? Yehova anawathawabishaje watumishi wake leo na alifanyaje hivyo wakati uliopita? Acheni tuone.

YEHOVA ANAAHIDI KUWABARIKI WATUMISHI WAKE

3. Tunapata ahadi gani katika andiko la Malaki 3:10?

3 Yehova Mungu amejipa wajibu wa kuwathawabisha watumishi wake waaminifu, hivyo anatualika tujitahidi kupata baraka zake. Tunasoma hivi: “‘Tafadhali, mnijaribu, . . .’ Yehova wa majeshi amesema, ‘kama sitawafungulia ninyi malango ya mbinguni na kuwamwagia baraka hata kusiwe na uhitaji tena.’” (Mal. 3:10) Tunapokubali mwaliko huo wa Yehova, tunaonyesha kwamba tunauthamini sana.

4. Kwa nini tunaweza kuamini ahadi ya Yesu kwenye Mathayo 6:33?

4 Yesu aliwahakikishia wanafunzi wake kwamba wakitanguliza Ufalme, Mungu atawategemeza. (Soma Mathayo 6:33.) Yesu alipotoa ahadi hiyo, alikuwa na uhakika kwamba ingetimizwa kwa sababu ya historia ya Yehova ya kutimiza ahadi zake. Yesu alijua kuwa ahadi za Mungu hazikosi kamwe kutimia. (Isa. 55:11) Sisi pia tunaweza kuwa na uhakika kwamba tukiwa na imani ya kweli katika Yehova, atatimiza ahadi hii: “Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.” (Ebr. 13:5) Tunaweza kuona uhusiano wa andiko hilo lililoongozwa na roho na kile ambacho Yesu alisema kuhusu kuutafuta kwanza Ufalme wa Mungu na uadilifu wake.

Yesu alionyesha kwamba wanafunzi wake wangebarikiwa kwa sababu ya kujidhabihu (Tazama fungu la 5)

5. Kwa nini jibu ambalo Yesu alimpa Petro linaimarisha imani?

5 Pindi moja, mtume Petro alimwuliza Yesu swali hili: “Tumeacha vitu vyote na kukufuata wewe; kwa kweli kutakuwa na nini kwa ajili yetu?” (Mt. 19:27) Badala ya kumkemea Petro kwa kuuliza swali hilo, Yesu aliwaambia wanafunzi wake kwamba watathawabishwa kwa sababu ya kujidhabihu. Mitume hao waaminifu pamoja na wengine watatawala na Yesu mbinguni. Lakini hata sasa tunathawabishwa. Yesu alisema hivi: “Kila mtu ambaye ameacha nyumba au ndugu au dada au baba au mama au watoto au mashamba kwa ajili ya jina langu atapokea mara nyingi zaidi naye atarithi uzima wa milele.” (Mt. 19:29) Wanafunzi wake wangepata baraka nyingi kuliko mambo yoyote ambayo wangeacha. Je, kuwa na baba, mama, ndugu, dada, na watoto wa kiroho si jambo lenye thamani zaidi kuliko vitu tulivyoacha kwa ajili ya Ufalme?

“NANGA YA NAFSI”

6. Kwa nini Yehova anaahidi kuwathawabisha waabudu wake?

6 Kwa kuwaahidi waabudu wake kwamba atawathawabisha, Yehova anawasaidia waendelee kuwa imara utimilifu wao unapojaribiwa. Watumishi waaminifu wa Yehova wanapata baraka nyingi za kiroho sasa, na pia wanatazamia kwa hamu baraka nyingi zaidi wakati ujao. (1 Tim. 4:8) Naam, kusadiki kabisa kwamba Yehova “huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii,” kutatusaidia tusimame imara katika imani.—Ebr. 11:6.

7. Tumaini ni kama nanga jinsi gani?

7 Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alisema hivi: “Shangilieni na kuruka kwa shangwe, kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni; kwa maana hivyo ndivyo walivyowatesa manabii waliokuwa kabla yenu.” (Mt. 5:12) Mbali na wale watakaopata thawabu ya kwenda mbinguni, pia wale walio na tumaini la kuishi milele katika dunia paradiso wana sababu ya ‘kushangilia na kuruka kwa shangwe.’ (Zab. 37:11; Luka 18:30) Iwe tuna tumaini la kuishi mbinguni au duniani, tumaini hilo linaweza kuwa kama “nanga ya nafsi, likiwa hakika na imara.” (Ebr. 6:17-20) Kama vile nanga huisaidia meli isitikisike wakati wa dhoruba, tumaini hakika la kupata thawabu linaweza kutusaidia tuendelee kuwa imara kihisia, kiakili, na kiroho. Pia, linaweza kutupatia nguvu za kuvumilia hali ngumu.

8. Tumaini lina nguvu za kupunguza mahangaiko jinsi gani?

8 Tumaini letu linalotegemea Biblia lina nguvu za kupunguza mahangaiko yetu ya sasa. Ahadi za Mungu ni kama dawa ya kiroho inayotuliza mioyo yetu inapohangaika. Tunafarijika sana kujua kwamba ‘tunapomtupia Yehova mzigo wetu, atatutegemeza.’ (Zab. 55:22) Tunaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba Mungu anaweza “kufanya kwa wingi zaidi kupita mambo yote tunayoomba au tunayofikiri.” (Efe. 3:20) Wazia hilo, si kwamba atafanya kwa wingi tu, bali “kwa wingi zaidi”!

9. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatubariki?

9 Ili tupate thawabu hiyo, tunahitaji kuwa na imani kamili katika Yehova na kutii miongozo yake. Musa aliwaambia hivi Waisraeli: “Hakika Yehova atakubariki katika nchi ambayo Yehova Mungu wako anakupa iwe urithi, uimiliki, ikiwa tu hutakosa kuisikiliza sauti ya Yehova Mungu wako nawe uwe mwangalifu kufanya amri yote hii ninayokuamuru leo. Kwa maana hakika Yehova Mungu wako atakubariki kama vile alivyokuahidi.” (Kum. 15:4-6) Je, unaamini kabisa kwamba Yehova atakubariki ukiendelea kumtumikia kwa uaminifu? Bila shaka una sababu nzuri za kuamini jambo hilo.

YEHOVA ALIWATHAWABISHA

10, 11. Yehova alimthawabishaje Yosefu?

10 Biblia iliandikwa ili kutunufaisha. Ina masimulizi mengi yanayoonyesha jinsi Mungu alivyowathawabisha watumishi wake waaminifu. (Rom. 15:4) Mfano mmoja wa pekee ni Yosefu. Kwa sababu ya njama ya kaka zake na hila iliyotungwa baadaye na mke wa bwana wake, Yosefu alifungwa gerezani nchini Misri. Je, hilo lilimtenganisha na Mungu wake? La hasha! “Yehova [aliendelea] kuwa pamoja na Yosefu, akazidi kumfanyia fadhili zenye upendo . . . Yehova alikuwa pamoja na Yosefu na yale aliyokuwa akifanya Yehova aliyafanikisha.” (Mwa. 39:21-23) Katika kipindi hicho cha majaribu, Yosefu aliendelea kumngojea Mungu wake kwa subira.

11 Miaka kadhaa baadaye, Farao alimtoa Yosefu gerezani na kumfanya mtumwa huyo wa hali ya chini kuwa wa pili katika mamlaka nchini Misri. (Mwa. 41:1, 37-43) Mke wake alipomzalia wana wawili, “Yosefu [alimwita] jina lake mzaliwa wa kwanza Manase, kwa sababu, kama alivyosema, ‘Mungu amenifanya nisahau taabu yangu yote na nyumba yote ya baba yangu.’ Naye yule wa pili akamwita jina lake Efraimu, kwa sababu, kama alivyosema, ‘Mungu ameniwezesha kuwa na uzao katika nchi ya taabu yangu.’” (Mwa. 41:51, 52) Kwa sababu Yosefu aliendelea kuwa mshikamanifu kwa Mungu, Yehova alimthawabisha na kumbariki kwa kumtumia kuhifadhi uhai wa Waisraeli na Wamisri. Wazo kuu ni kwamba Yosefu alitambua kuwa Yehova ndiye aliyemthawabisha na kumbariki.—Mwa. 45:5-9.

12. Yesu alidumishaje uaminifu alipojaribiwa?

12 Yesu Kristo vilevile aliendelea kumtii Mungu licha ya majaribu mbalimbali ya imani, naye akathawabishwa. Ni nini kilichomsaidia kukabiliana na majaribu hayo? Neno la Mungu linaeleza hivi: “Kwa ajili ya shangwe iliyowekwa mbele yake, yeye alivumilia mti wa mateso, akaidharau aibu.” (Ebr. 12:2) Ni wazi kwamba Yesu alipata shangwe katika kulitakasa jina la Mungu. Isitoshe, alithawabishwa kwa kupata kibali cha Baba yake na kupewa migawo mingine ya pekee. Biblia inasema kwamba “ameketi kwenye mkono wa kuume wa kiti cha ufalme cha Mungu.” Na mstari mwingine wa Biblia unasema hivi: “Mungu alimpandisha kwenye cheo cha juu zaidi na kumpa kwa fadhili jina lililo juu ya kila jina lingine.”—Flp. 2:9.

YEHOVA HASAHAU KAZI YETU

13, 14. Yehova huhisije kuhusu mambo tunayofanya kwa ajili yake?

13 Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anathamini jitihada zetu zote za kumtumikia. Anatuelewa tunapohisi kwamba hatustahili kibali chake na tunapotilia shaka uwezo wetu. Yeye hutuonyesha huruma tunapolemewa na matatizo ya kifedha au hali yetu ya kiafya au ya kihisia inapotuzuia kufanya yale tunayotaka katika utumishi mtakatifu. Na tunaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba Yehova anathamini sana mambo ambayo watumishi wake wanafanya ili wadumishe uaminifu wao.—Soma Waebrania 6:10, 11.

14 Kumbuka pia kwamba tunaweza kumfikia “msikiaji wa sala” tukiwa na uhakika kuwa atasikiliza mahangaiko yetu. (Zab. 65:2) “Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote” atatutegemeza kabisa kihisia na kiroho, na huenda akafanya hivyo kupitia waabudu wenzetu. (2 Kor. 1:3) Tunaufurahisha moyo wa Yehova tunapowaonyesha wengine huruma. “Anayemwonyesha kibali mtu wa hali ya chini anamkopesha Yehova, na Yeye atamlipa matendo yake.” (Met. 19:17; Mt. 6:3, 4) Hivyo, tunapowasaidia bila ubinafsi watu wanaokabili hali ngumu, Yehova huona ni kana kwamba tumemkopesha. Na anaahidi kwamba atatuthawabisha kwa tendo hilo la fadhili.

THAWABU ZA SASA NA ZA MILELE

15. Unatazamia kupata thawabu gani wakati ujao? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

15 Wakristo watiwa mafuta wanategemezwa na tumaini la kupokea “taji la uadilifu, ambalo Bwana, aliye mwamuzi mwadilifu, [atawapa] kuwa thawabu katika siku ile.” (2 Tim. 4:7, 8) Hata hivyo, bado Mungu anakuona kuwa mwenye thamani hata kama una tumaini tofauti na hilo. Mamilioni ya “kondoo wengine” wa Yesu wanatazamia kwa hamu kupata thawabu ya uzima wa milele katika paradiso duniani. Wakati huo “watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”—Yoh. 10:16; Zab. 37:11.

16. Tunapata faraja gani katika andiko la 1 Yohana 3:19, 20?

16 Nyakati fulani, tunaweza kuhisi hatutimizi mengi, au tukatilia shaka kama Yehova anapendezwa na yale tunayofanya. Huenda hata tukatilia shaka ikiwa tunastahili kupokea thawabu yoyote. Hata hivyo, hatupaswi kamwe kusahau kwamba “Mungu ni mkuu kuliko mioyo yetu naye anajua mambo yote.” (Soma 1 Yohana 3:19, 20.) Mungu hubariki kila namna ya utumishi mtakatifu wa kutoka moyoni ambao unachochewa na imani na upendo, hata iwe anayeutoa anauona kuwa mdogo au usio na thamani.​—Marko 12:41-44.

17. Yehova ametubariki leo katika njia zipi?

17 Hata katika siku hizi za mwisho za mfumo mwovu wa Shetani, Yehova anawabariki watu wake. Anahakikisha kwamba waabudu wake wananawiri katika paradiso ya kiroho, ambayo ina chakula kingi sana cha kiroho. (Isa. 54:13) Kama Yesu alivyotuahidi, Yehova anatubariki sasa kwa kuturuhusu tuwe sehemu ya familia ya kiroho yenye upendo ya ndugu na dada zetu wa ulimwenguni pote. (Marko 10:29, 30) Isitoshe, wale wanaomtafuta Mungu kwa bidii wanathawabishwa kwa kupewa baraka isiyo na kifani ya amani ya akili, uradhi, na furaha.—Flp. 4:4-7.

18, 19. Watumishi wa Yehova wanahisije kuhusu baraka wanazopokea?

18 Watumishi wa Yehova ulimwenguni pote wanaweza kuthibitisha kwamba Yehova anawabariki katika njia mbalimbali. Kwa mfano, Bianca anayeishi Ujerumani anasema hivi: “Ninamshukuru sana Yehova kwa kunisaidia nikabiliane na wasiwasi, na kunitegemeza siku baada ya siku. Ulimwengu umejaa vurugu na hakuna tumaini. Lakini ninapofanya kazi kwa ukaribu pamoja na Yehova, ninajihisi salama. Kila mara ninapojidhabihu katika utumishi wake, ananibariki mara mia.”

19 Au mfikirie Paula, mwenye umri wa miaka 70, anayeishi Kanada ambaye ameathiriwa sana na spina bifida, (ugonjwa unaosababishwa na kutoziba kabisa kwa mrija wa neva katika uti wa mgongo). Anasema hivi: “Sijapunguza utumishi wangu kwa sababu ya kutoweza kutembea sana. Mimi hutumia njia tofauti za kuhubiri kama vile simu na kutoa ushahidi usio rasmi. Nina kitabu ninachoandika maandiko fulani ya Biblia na habari kutoka kwenye machapisho yetu ambacho mimi hukisoma mara kwa mara ili nipate kitia moyo. Mimi hukiita ‘Kitabu Changu cha Kunitia Moyo.’ Tukitafakari ahadi za Yehova hatutavunjika moyo kwa muda mrefu. Sikuzote, Yehova hutusaidia hata hali zetu ziweje.” Huenda hali yako ikawa tofauti na ya Bianca au Paula. Hata hivyo, yaelekea unaweza kutaja njia mbalimbali ambazo Yehova amekubariki wewe pamoja na wapendwa wako. Inafaa sana kutafakari jinsi Yehova anavyokubariki sasa na atakavyokubariki wakati ujao!

20. Tukiendelea kumtumikia Yehova kwa nafsi yote, tunaweza kutazamia nini?

20 Usisahau kamwe kwamba sala zako za kutoka moyoni na uhuru wako wa kusema na Mungu ‘zitathawabishwa.’ Unaweza kuwa na uhakika kwamba “baada ya kufanya mapenzi ya Mungu, [utapokea] utimizo wa ile ahadi.” (Ebr. 10:35, 36) Kwa hiyo, na tuendelee kuimarisha imani yetu na kumtumikia Yehova kwa nafsi yote. Tunaweza kufanya hivyo kwa kuwa tunajua kwamba tutapokea thawabu inayofaa kutoka kwa Yehova.​—Soma Wakolosai 3:23, 24.