Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

Niliacha Vitu Vyote Ili Kumfuata Bwana

Niliacha Vitu Vyote Ili Kumfuata Bwana

“Ukienda kuhubiri usirudi hapa. Ukirudi nitakuvunja miguu.” Niliamua kuondoka nyumbani kwa sababu ya vitisho hivyo vya Baba. Hiyo ndiyo iliyokuwa mara yangu ya kwanza kuacha vitu vyote ili kumfuata Bwana. Nilikuwa na umri wa miaka 16 tu.

HALI hiyo ilisababishwa na nini? Acheni nieleze. Nilizaliwa Julai 29, 1929, katika kijiji fulani kwenye mkoa wa Bulacan nchini Filipino. Maisha katika kijiji hicho yalikuwa ya hali ya chini kwa sababu kilikuwa kipindi cha mshuko wa kiuchumi. Vita vilizuka nilipokuwa kijana. Majeshi ya nchi ya Japani yakavamia nchi ya Filipino. Hata hivyo, kijiji chetu kilikuwa mbali hivyo hatukuathiriwa moja kwa moja na majeshi hayo. Hatukuwa na redio, televisheni, au magazeti; hivyo tulipata habari za vita kutoka kwa watu.

Nilikuwa mtoto wa pili katika familia yenye watoto wanane, na babu na nyanya (bibi) yangu walikuwa wamenichukua niishi nao nilipokuwa na umri wa miaka minane. Ingawa tulikuwa Wakatoliki, Babu alikubali kuwasikiliza watu wa dini nyingine, hivyo alikuwa na vitabu vya kidini ambavyo marafiki wake walimpa. Ninakumbuka alinionyesha vijitabu Protection, Safety, na Uncovered katika Kitagalogi, * na pia Biblia. Nilipenda kusoma Biblia, hasa vile vitabu vinne vya Injili. Hilo lilinifanya nitamani kufuata kielelezo cha Yesu.—Yoh. 10:27.

NAJIFUNZA KUMFUATA BWANA

Majeshi ya Japani yaliondoka nchini Filipino mwaka wa 1945. Wakati huo wazazi wangu waliniomba nirudi nyumbani. Babu alinihimiza nirudi. Hivyo nikarudi.

Muda mfupi baadaye, Desemba 1945, kikundi fulani cha Mashahidi wa Yehova kutoka mji wa Angat kilikuja kuhubiri katika kijiji chetu. Shahidi mmoja mwenye umri mkubwa alifika nyumbani kwetu na kutueleza kile ambacho Biblia inasema kuhusu “siku za mwisho.” (2 Tim. 3:1-5) Alitualika tuhudhurie funzo la Biblia katika kijiji fulani kilichokuwa karibu. Wazazi wangu hawakwenda, lakini mimi nilienda. Kulikuwa na watu 20 hivi, na baadhi yao waliuliza maswali kuhusu Biblia.

Kwa kuwa sikuelewa walichokuwa wakizungumzia, niliamua kuondoka. Lakini kabla ya kuondoka, wakaanza kuimba wimbo fulani wa Ufalme. Wimbo huo ulinivutia sana, hivyo nikaamua kubaki. Baada ya wimbo na sala, wahudhuriaji wote walialikwa wahudhurie mkutano Jumapili iliyofuata katika mji wa Angat.

Wengi wetu tulitembea kilomita nane hivi ili kuhudhuria mkutano huo uliofanyika katika nyumba ya Ndugu Cruz. Nilistaajabu kuona hata watoto wadogo waliokuwa miongoni mwa wahudhuriaji 50 wakitoa maelezo kuhusu mambo mazito ya Biblia. Baada ya kuhudhuria mikutano kadhaa, siku moja Ndugu Damian Santos, painia mwenye umri mkubwa na ambaye zamani alikuwa meya, alinialika nilale nyumbani kwake. Tulizungumzia Biblia kwa muda mrefu usiku huo.

Siku hizo, wengi wetu tulikubali kweli haraka baada ya kujifunza mafundisho ya msingi ya Biblia. Baada ya kuhudhuria mikutano mara kadhaa, akina ndugu walituuliza hivi: “Je, mngependa kubatizwa?” Mimi nilijibu, “Ndiyo.” Nilijua kwamba ninataka ‘kumtumikia Bwana, Kristo.’ (Kol. 3:24) Tulienda kwenye mto uliokuwa karibu, na wawili miongoni mwetu tukabatizwa Februari 15, 1946.

Tulitambua kwamba tukiwa Wakristo waliobatizwa, tulipaswa kumwiga Yesu kwa kuhubiri kwa ukawaida. Baba hakufurahishwa na jambo hilo, hivyo akasema, “Wewe ni mdogo sana, hujafikia umri wa kuanza kuhubiri. Isitoshe, kuzamishwa mtoni hakukufanyi uwe mhubiri.” Nilimweleza kwamba ni mapenzi ya Mungu tuhubiri habari njema ya Ufalme. (Mt. 24:14) Kisha nikamwambia, “Ninahitaji kutimiza nadhiri yangu kwa Mungu.” Hapo ndipo baba alipotoa vitisho nilivyosimulia mwanzoni. Naam, alikuwa ameazimia kunizuia nisihubiri. Na hilo ndilo lililonifanya niache vitu vyote kwa mara ya kwanza maishani ili kufuatia malengo ya kiroho.

Familia ya Ndugu Cruz ilinikaribisha niishi nao katika mji wa Angat. Pia, walinitia moyo mimi na binti yao wa mwisho, Nora, kuwa mapainia. Sote tukaanza upainia Novemba 1, 1947. Nora alifanya upainia katika mji mwingine, nami nikaendelea kusaidia kazi ya kuhubiri kwenye mji wa Angat.

FURSA NYINGINE YA KUACHA VITU VYOTE

Baada ya kufanya upainia kwa miaka mitatu, Ndugu Earl Stewart kutoka ofisi ya tawi, alitoa hotuba kwa wahudhuriaji 500 waliokusanyika katika jengo la umma katika mji wa Angat. Alitoa hotuba hiyo katika Kiingereza, na baadaye nikatoa muhtasari wa hotuba hiyo katika Kitagalogi. Nilikuwa na elimu ya shule ya msingi tu, lakini kwa kawaida walimu wetu walitumia Kiingereza. Jambo lingine lililonisaidia kuboresha ujuzi wangu wa lugha ya Kiingereza ni kwamba machapisho ya Kitagalogi yalikuwa machache sana. Kwa hiyo, nilisoma machapisho mengi ya Kiingereza. Hivyo, Kiingereza nilichokuwa nimejifunza kilinisaidia kutafsiri hotuba hiyo na hotuba nyingine zilizotolewa baadaye.

Siku niliyotafsiri hotuba hiyo, Ndugu Stewart aliwaambia washiriki wa kutaniko kwamba ofisi ya tawi ingependa kuwaalika ndugu wawili mapainia waje kusaidia kazi Betheli. Ndugu hao wangesaidia wakati ambapo wamishonari wangeenda kuhudhuria kusanyiko la mwaka 1950 la Ongezeko la Kitheokrasi huko New York, Marekani. Mimi na ndugu mwingine ndio tulioalikwa. Kwa mara nyingine tena, niliacha mazingira niliyokuwa nimezoea ili nikatumikie Betheli.

Niliwasili Betheli Juni 19, 1950 na kuanza mgawo wangu mpya. Ofisi ya Betheli ilikuwa kwenye nyumba kubwa ya zamani, iliyozungukwa na miti mikubwa kwenye eneo lenye ukubwa wa ekari mbili na nusu. Ndugu waseja 12 hivi walikuwa wakitumikia huko. Asubuhi na mapema nilisaidia kazi jikoni. Kisha, kuanzia saa tatu hivi asubuhi nilienda dobi kufanya kazi ya kupiga pasi. Nilifanya vivyo hivyo tena alasiri. Wamishonari waliporudi kutoka katika kusanyiko la kimataifa, bado niliendelea kufanya kazi Betheli. Nilifunga magazeti ili yatumwe kwa njia ya posta, nilishughulikia maandikisho ya magazeti, na nilifanya kazi kwenye mapokezi; nilifanya chochote nilichoombwa nifanye.

NAONDOKA FILIPINO KWENDA SHULE YA GILEADI

Mwaka wa 1952, mimi pamoja na ndugu wengine sita kutoka Filipino, tulisisimka tulipopokea mwaliko wa kuhudhuria darasa la 20 la Shule ya Gileadi. Mambo mengi tuliyojionea nchini Marekani yalikuwa mapya. Kwa kweli, yalikuwa tofauti sana na mambo niliyojua katika kijiji chetu kidogo..

Nikiwa na wanafunzi wenzangu katika Shule ya Gileadi

Kwa mfano, tulijifunza kutumia vifaa na vyombo ambavyo hatukuwahi kuviona. Na bila shaka hali ya hewa ilikuwa tofauti sana! Asubuhi moja nilitoka nje na kuona ardhi yote ikiwa nyeupe na maridadi sana. Ilikuwa mara yangu ya kwanza kuona theluji. Kisha nikatambua kwamba kulikuwa na baridi—baridi kali sana!

Hata hivyo, mabadiliko niliyohitaji kufanya yalikuwa madogo sana kwa kulinganisha na mazoezi mazuri niliyofurahia katika Shule ya Gileadi. Walimu walitumia mbinu nzuri sana za kufundisha. Tulijifunza kufanya utafiti na kujifunza kwa njia itakayotunufaisha. Kwa kweli mazoezi niliyopata Gileadi yalinisaidia kuboresha hali yangu ya kiroho.

Baada ya kuhitimu, nilipewa mgawo wa muda wa kuwa painia wa pekee katika eneo la Bronx jijini New York City. Hivyo, Julai 1953, nilifaulu kuhudhuria Kusanyiko la New World Society, lililofanyiwa katika eneo hilohilo. Baada ya kusanyiko hilo, nilitumwa kwenye mgawo mwingine nchini Filipino.

NINAONDOKA KATIKA JIJI NILILOZOEA

Akina ndugu katika ofisi ya tawi waliniambia hivi: “Sasa utakuwa mwangalizi wa mzunguko.” Kwa njia halisi, mgawo huo ungenipa fursa ya kufuata hatua za Bwana Yesu ambaye alisafiri katika miji na majiji ya mbali ili kuwasaidia kondoo wa Yehova. (1 Pet. 2:21) Nilipewa mgawo wa kuzungukia makutaniko yaliyokuwa yametawanyika katika eneo lililo katikati ya kisiwa cha Luzon, ambacho ndicho kisiwa kikubwa zaidi nchini Filipino. Mzunguko wangu ulitia ndani mkoa wa Bulacan, Nueva Ecija, Tarlac, na Zambales. Ili kutembelea miji fulani, nilihitaji kupita eneo la Milima ya Sierra Madre lenye miamba mingi. Hakukuwa na magari ya usafiri wa umma yaliyofika maeneo hayo. Hivyo, nilikuwa nikiwaomba madereva wa malori niketi juu ya magogo waliyokuwa wamepakia kwenye malori yao makubwa. Mara nyingi waliniruhusu kupanda, lakini haukuwa usafiri wenye kustarehesha.

Makutaniko mengi yalikuwa madogo na mapya. Hivyo akina ndugu walithamini nilipowasaidia kujua jinsi ya kufanya mikutano na utumishi wa shambani kwa njia bora.

Baadaye nilipewa mgawo wa kuwa mwangalizi wa mzunguko katika eneo lote la Bicol. Mzunguko huo ulikuwa na vikundi vingi vilivyoanzishwa na mapainia wa pekee waliohubiri katika maeneo ambayo hayakuwa yamewahi kuhubiriwa. Katika nyumba moja, choo pekee kilichokuwepo kilikuwa cha shimo na kilikuwa na magogo mawili tu ya kukanyagia. Nilipokanyaga magogo hayo, niliporomoka pamoja nayo na kutumbukia chooni. Nilitumia muda mrefu sana kujisafisha na kujiandaa kwa ajili ya kiamsha kinywa!

Nilipokuwa katika mgawo huo ndipo nilipoanza kumfikiria Nora, ambaye miaka mingi mapema alikuwa ameanza upainia kwenye mkoa wa Bulacan. Sasa alikuwa painia wa pekee katika jiji la Dumaguete City, nami nikaenda kumtembelea huko. Baada ya hapo, tuliendelea kuwasiliana kwa muda fulani na mwaka wa 1956, tukafunga ndoa. Juma la kwanza baada ya harusi yetu tulitembelea kutaniko lililokuwa katika Kisiwa cha Rapu Rapu. Tukiwa huko tulipanda milima na tulitembea kwa muda mrefu, lakini tukiwa wenzi wa ndoa tulifurahia sana kuwatumikia akina ndugu walioishi maeneo hayo ya mbali!

NAALIKWA TENA KUTUMIKIA BETHELI

Baada ya kutumikia nikiwa mwangalizi wa mzunguko kwa miaka minne hivi, tulipata mwaliko wa kutumikia katika ofisi ya tawi. Hivyo, Januari 1960 tulianza mgawo huo ambao tumefanya kwa muda mrefu. Kadiri miaka inavyopita, nimejifunza mambo mengi kwa sababu ya kufanya kazi pamoja na ndugu wenye madaraka mazito, naye Nora amefanya kazi mbalimbali hapa Betheli.

Nikitoa hotuba katika kusanyiko nikiwa na mtafsiri wa Kisebuano

Nikiwa hapa Betheli, nimepata baraka ya kushuhudia ukuzi mkubwa sana wa kiroho nchini Filipino. Nilipoanza kutumikia Betheli nikiwa kijana mseja, kulikuwa na wahubiri 10,000 hivi nchini kote. Sasa kuna zaidi ya wahubiri 200,000 nchini Filipino na mamia ya Wanabetheli wanaotegemeza kazi muhimu ya kuhubiri..

Miaka ilivyozidi kupita na kazi ya kuhubiri kuongezeka, majengo ya Betheli hayakuwa na nafasi ya kutosha. Kisha Baraza Linaloongoza likatuomba tutafute eneo ambalo tungeweza kujenga ofisi kubwa zaidi ya tawi. Mimi pamoja na mwangalizi wa Idara ya Uchapishaji tulienda nyumba kwa nyumba katika ujirani wa ofisi ya tawi, ambapo Wachina wengi walikuwa wakiishi, tukiuliza ikiwa kuna yeyote aliyetaka kuuza uwanja wake. Hakuna aliyetaka kuuza uwanja wake, hata mmiliki mmoja alituambia hivi: “Sisi Wachina huwa hatuuzi. Tunanunua tu.”

Nikitafsiri hotuba ya Ndugu Albert Schroeder

Hata hivyo, bila kutarajia siku moja mmiliki fulani alituuliza ikiwa tungependa kununua uwanja wake; alikuwa akihamia Marekani. Huo ulikuwa mwanzo wa mfuatano wa matukio yenye kushangaza. Jirani mwingine aliamua kuuza uwanja wake, na akawatia moyo majirani wenzake wafanye vivyo hivyo. Hata tulifanikiwa kununua uwanja wa mwanamume ambaye alikuwa ametuambia “Sisi Wachina huwa hatuuzi.” Baada ya muda mfupi, eneo la ofisi ya tawi liliongezeka zaidi ya mara tatu. Ninasadiki kwamba Yehova Mungu alitaka iwe hivyo.

Mwaka wa 1950, mimi ndiye niliyekuwa na umri mdogo zaidi katika familia ya Betheli. Lakini sasa mimi na mke wangu ndio wenye umri mkubwa zaidi. Sijutii kamwe kumfuata Bwana popote ambapo amenielekeza. Ni kweli kwamba wazazi wangu walinifukuza nyumbani, lakini Yehova amenipa familia kubwa ya waabudu wenzangu. Sina shaka hata kidogo kwamba Yehova hutuandalia kila kitu tunachohitaji haidhuru tunapokea mgawo gani. Mimi na Nora tunamshukuru sana Yehova kwa kutuandalia kwa fadhili mahitaji yetu, nasi tunawatia moyo wengine wamjaribu Yehova.—Mal. 3:10.

Pindi moja Yesu alimpa mkusanya kodi aliyeitwa Mathayo Lawi mwaliko huu: “Uwe mfuasi wangu.” Aliitikiaje? “Baada ya kuacha kila kitu akaondoka akaanza kumfuata [Yesu].” (Luka 5:27, 28) Mimi pia nimepata fursa kama hizo, nami ninawahimiza wengine kutoka moyoni wafanye vivyo hivyo na kupata baraka nyingi.

Ninafurahia kushiriki katika ukuzi wa kiroho nchini Filipino

^ fu. 6 Vilivyochapishwa na Mashahidi wa Yehova lakini sasa havichapishwi tena.