Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Ni katika maana gani mtume Paulo “alinyakuliwa mpaka kwenye mbingu ya tatu” na “kuingia katika paradiso”?—2 Kor. 12:2-4.

Mtu huyo alikuwa nani? Paulo alipoliandikia kutaniko la Korintho, alikazia kwamba Mungu alikuwa akimtumia yeye kama mtume. (2 Kor. 11:5, 23) Kisha alitaja kuhusu ‘maono na ufunuo wa Bwana.’ Katika muktadha huo Paulo hakutaja ndugu wengine. Hivyo, tunaweza kufikia mkataa kwamba alikuwa akijirejelea yeye mwenyewe kuwa ndiye mwanamume aliyepokea maono na ufunuo.—2 Kor. 12:1, 5.

Hivyo Paulo ndiye aliyenyakuliwa “mpaka kwenye mbingu ya tatu” na “kuingia katika paradiso.” (2 Kor. 12:2-4) Alitumia neno “ufunuo,” ambalo linadokeza kufunuliwa kwa mambo ambayo yatatukia wakati ujao.

“Mbingu ya tatu” ambayo Paulo aliona ni nini?

Katika Biblia, neno “mbingu” linaweza kurejelea mbingu halisi. (Mwa. 11:4; 27:28; Mt. 6:26) Lakini neno “mbingu” hutumiwa pia katika maana nyingine. Nyakati nyingine linarejelea utawala wa wanadamu. (Dan. 4:20-22) Au linaweza kurejelea utawala wa Mungu, akitumia Ufalme wake.—Ufu. 21:1.

Paulo aliona “mbingu ya tatu.Alimaanisha nini? Pindi fulani, katika Biblia jambo fulani hutajwa mara tatu ili kutilia mkazo, kuonyesha msisitizo, au kuongeza uzito wa jambo hilo. (Isa. 6:3; Eze. 21:27; Ufu. 4:8) Inaonekana kwamba Paulo alipozungumza kuhusu “mbingu ya tatu,” alikuwa akikazia utawala wenye ubora wa hali ya juu na uliokwezwa sana, yaani, Ufalme wa Kimasihi, Yesu Kristo akiwa mfalme pamoja na watawala wenzake 144,000. (Tazama Insight on the Scriptures, Buku la 1, uku. 1059, 1062.) Kama mtume Petro alivyoandika, tunatarajia “mbingu mpya” kulingana na ahadi ya Mungu.—2 Pet. 3:13.

Namna gani kuhusu “paradiso” ambayo Paulo alitaja?

Vilevile, neno “paradiso” linaweza pia kurejelea mambo mbalimbali: (1) Kwa kuwa wanadamu walikusudiwa waishi duniani, tunaweza kufikia mkataa kwamba neno “paradiso” linaweza kurejelea Paradiso halisi itakayokuwa hapa duniani. (2) Linaweza kurejelea hali nzuri ya kiroho ambayo watu wa Mungu watafurahia katika ulimwengu mpya. (3) Linaweza kumaanisha hali nzuri katika “paradiso ya Mungu” mbinguni inayotajwa kwenye andiko la Ufunuo 2:7.—Tazama gazeti la Mnara wa Mlinzi la Julai 15, 2015, uku. 8, fu. 8.

Inawezekana kwamba Paulo alikuwa akirejelea maana zote tatu za neno “paradiso” kwenye andiko la 2 Wakorintho 12:4 alipokuwa akifafanua maono aliyopata.

Kwa muhtasari:

Inaonekana kwamba “mbingu ya tatu” inayotajwa kwenye andiko la 2 Wakorintho 12:2 ni Ufalme wa Kimasihi, Yesu Kristo akiwa mfalme pamoja na watawala wenzake 144,000, yaani, “mbingu mpya.”​—2 Pet. 3:13.

Inatajwa kuwa “mbingu ya tatu” kwa sababu Ufalme huo ni utawala wenye ubora wa hali ya juu na uliokwezwa sana.

Inaelekea “paradiso” ambayo Paulo aliona ‘aliponyakuliwa’ katika maono inarejelea (1) Paradiso halisi itakayokuwa hapa duniani, (2) paradiso ya kiroho itakayokuwepo wakati huo, itakayozidi paradiso ya kiroho iliyopo sasa, na (3) “paradiso ya Mungu” mbinguni, na paradiso hizo zote zitakuwepo wakati uleule katika ulimwengu mpya.

Hivyo, ulimwengu mpya ni mbingu mpya na dunia mpya kwa pamoja. Utakuwa mpango mpya, unaotia ndani serikali ya Ufalme wa mbinguni na wanadamu wanaomtumikia Yehova katika paradiso duniani.