Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Mwadilifu Atashangilia kwa Sababu ya Yehova”

“Mwadilifu Atashangilia kwa Sababu ya Yehova”

DIANA ana umri wa zaidi ya miaka 80. Mume wake alipata ugonjwa wa Alzheimer unaoathiri akili, na alikuwa kwenye nyumba ya kuwatunzia wazee kwa miaka kadhaa kabla ya kifo chake. Pia, alifiwa na wanawe wawili na akapatwa na ugonjwa wa kansa ya matiti. Licha ya hayo, ndugu na dada wa kutaniko lake wanapomwona kwenye Jumba la Ufalme au kwenye huduma, yeye huwa mwenye shangwe sikuzote.

John alikuwa mwangalizi wa mzunguko kwa zaidi ya miaka 43. Alipenda sana utumishi huo—ulikuwa sehemu ya maisha yake! Hata hivyo, aliacha mgawo wa kuzungukia makutaniko ili amtunze mtu wake wa ukoo aliyekuwa mgonjwa, na sasa anatumikia katika kutaniko la nyumbani. Wale waliomjua John zamani wanapokutana naye kwenye makusanyiko, wanaona kwamba hajabadilika hata kidogo. Bado ana shangwe nyingi.

Inawezekanaje kwamba Diana na John bado wana shangwe? Mtu anayeteseka kihisia na kimwili anawezaje kuwa na shangwe? Na inawezekanaje kwa mtu aliyepoteza pendeleo la utumishi kuendelea kuwa mwenye furaha? Biblia inatusaidia kuelewa jambo hilo, inaposema: “Mwadilifu atashangilia kwa sababu ya Yehova.” (Zab. 64:10) Tunaweza kuelewa vizuri zaidi ukweli huo muhimu tukitambua mambo yanayoleta shangwe ya moyoni na mambo ambayo hayawezi kuleta shangwe hiyo.

SHANGWE ISIYODUMU

Bila shaka unajua mambo fulani ambayo kwa kawaida humfanya mtu awe na shangwe. Fikiria kuhusu watu wawili wanaopendana wanapofunga ndoa. Au fikiria kuhusu kupata mtoto au pendeleo fulani la utumishi. Mambo hayo huleta shangwe na inafaa kuwa hivyo, kwa sababu yanatoka kwa Yehova. Yeye ndiye Mwanzilishi wa ndoa, ndiye aliyewapa wanadamu uwezo wa kuzaa watoto, na kuwapa migawo kupitia kutaniko la Kikristo.—Mwa. 2:18, 22; Zab. 127:3; 1 Tim. 3:1.

Hata hivyo, baadhi ya mambo yanayomfanya mtu awe na shangwe huenda yasidumu. Kwa kusikitisha, mwenzi wa ndoa anaweza kukosa uaminifu au akafa. (Eze. 24:18; Hos. 3:1) Baadhi ya watoto hukosa kuwatii wazazi wao na pia Mungu, na hata hutengwa na ushirika. Wana wa Samweli hawakumtumikia Yehova kwa njia inayokubalika, na matendo ya Daudi yalimsababishia matatizo makubwa ndani ya nyumba yake mwenyewe. (1 Sam. 8:1-3; 2 Sam. 12:11) Mambo kama hayo huleta huzuni na mikazo. Kwa kweli hayatuletei shangwe.

Vivyo hivyo, mapendeleo ya utumishi yanaweza kuisha labda kwa sababu ya matatizo ya afya, majukumu ya kifamilia, au mabadiliko ya kitengenezo. Wengi wa wale waliopata mabadiliko hayo wanakiri kwamba wanakosa hisia za kuridhika ambazo mgawo wao uliwapa.

Hivyo, tunaweza kuona kwamba shangwe ambayo hutokana na mambo hayo ni ya kadiri fulani tu au ya muda mfupi. Basi je, kuna shangwe ambayo hudumu hata hali zinapobadilika na kuwa ngumu? Lazima iwepo, kwa sababu Samweli, Daudi, na wengine waliendelea kuwa na shangwe hata walipokabili majaribu.

SHANGWE INAYODUMU

Yesu alijua maana hasa ya kuwa na shangwe. Alipokuwa mbinguni kabla ya kuzaliwa kama mwanadamu, ambapo hali zilikuwa nzuri, ‘alishangilia mbele za Yehova wakati wote.’ (Met. 8:30) Hata hivyo, alipokuja duniani, nyakati nyingine alikabili hali ngumu sana. Lakini bado Yesu alifurahia kufanya mapenzi ya Baba yake. (Yoh. 4:34) Vipi kuhusu saa zake za mwisho-mwisho kabla ya kufa? Tunasoma hivi: “Kwa sababu ya shangwe iliyowekwa mbele yake, alivumilia mti wa mateso.” (Ebr. 12:2) Kwa msingi huo, tuna sababu nzuri ya kuchunguza mambo mawili ambayo Yesu alisema kuhusu shangwe halisi.

Siku moja, wanafunzi 70 walirudi kwa Yesu baada ya kumaliza kazi ya kuhubiri. Walikuwa na shangwe kwa sababu walikuwa wamefanya kazi zenye nguvu, kutia ndani kuwafukuza roho waovu. Kisha Yesu akawaambia: “Msishangilie kwa sababu mnawatiisha roho waovu, bali shangilieni kwa sababu majina yenu yameandikwa mbinguni.” (Luka 10:1-9, 17, 20) Naam, kuwa na kibali cha Yehova ndilo jambo muhimu zaidi kuliko kufurahia pendeleo fulani la pekee la utumishi. Yehova hangewasahau kamwe wanafunzi hao waaminifu—jambo ambalo lingewaletea shangwe nyingi sana.

Katika pindi nyingine, Yesu alikuwa akizungumza na umati. Mwanamke fulani Myahudi alieleza hisia zake kwamba mama aliyemzaa Yesu, mwalimu stadi, alikuwa mama mwenye furaha sana. Lakini Yesu alimrekebisha na kumwambia hivi: “Hapana, badala yake, wenye furaha ni wale wanaolisikia neno la Mungu na kulishika!” (Luka 11:27, 28) Kuwaonea fahari watoto wetu ni jambo linalofurahisha sana; hata hivyo, kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova kwa sababu tunamtii ndiyo sababu kubwa zaidi ya kuwa na shangwe.

Kwa hakika, kujua kwamba tuna kibali cha Yehova ndiyo siri ya kuwa na shangwe nyingi ya moyoni. Ingawa hatufurahi tunapopitia hali ngumu, majaribu hayawezi kubadili ukweli wa kwamba tuna kibali cha Yehova. Kinyume cha hilo, kuyavumilia kwa utimilifu ni ushindi unaotufanya tuwe na hali nzuri ya moyoni. (Rom. 5:3-5) Isitoshe, Yehova huwapa roho yake wale wanaomtumaini, na sifa ya shangwe ni sehemu ya tunda la roho hiyo. (Gal. 5:22) Jambo hilo linatusaidia kuelewa kwa nini Zaburi 64:10 husema kwa usahihi kwamba “Mwadilifu atashangilia kwa sababu ya Yehova.”

Ni nini ambacho kimemsaidia John kuendelea kuwa na shangwe ya kutoka moyoni?

Hilo pia linatusaidia kuelewa kwa nini Diana na John waliotajwa mapema, walifanikiwa kuendelea kuwa na shangwe walipokuwa wakikabili hali ngumu. Diana anaeleza hivi: “Nimemfanya Yehova kuwa kimbilio langu, kama ambavyo mtoto humkimbilia mzazi wake.” Anajuaje kwamba ana kibali cha Mungu? Anasema hivi: “Ninahisi kwamba amenibariki kwa kunipa nguvu za kuendelea kuhubiri kwa ukawaida huku nikiwa na tabasamu.” John, ambaye aliendelea kuwa mwenye bidii katika huduma baada ya kuacha mgawo wake wa kuzungukia makutaniko, anaeleza jambo lililomsaidia: “Tangu mwaka wa 1998 nilipopewa mgawo wa kufundisha katika Shule ya Mazoezi ya Kihuduma, nimekuwa nikijifunza kibinafsi mara nyingi zaidi kuliko nilivyowahi kufanya awali.” Akizungumza pia kwa niaba ya mke wake, anasema hivi: “Kwa ujumla mtazamo ambao tumekuwa nao wa kumtumikia Yehova katika mgawo wowote tuliopata umefanya iwe rahisi kwetu kuzoea hali yetu mpya. Hatujawahi kamwe kujutia mgawo wowote tuliopewa.”

Wengine wengi pia wamejionea ukweli wa maneno ya Zaburi 64:10. Fikiria kwa mfano wenzi fulani wa ndoa waliokuwa wametumikia katika Betheli ya Marekani kwa zaidi ya miaka 30. Kisha wakapewa mgawo wa kuwa mapainia wa pekee. Walikiri hivi waziwazi: “Ni jambo la kawaida kuhuzunika unapopoteza kitu unachokipenda,” lakini walisema hivi pia: “Huwezi kuhuzunika milele.” Bila kukawia, walianza kushirikiana na kutaniko katika huduma. Wenzi hao wa ndoa walisema hivi pia: “Tulisali kuhusu mambo hususa sana. Kisha tulipoona sala zetu zikijibiwa tulitiwa moyo sana na hilo lilituletea shangwe. Muda mfupi baada ya kuwasili kutanikoni, baadhi ya ndugu na dada walianza upainia, na tukapata baraka ya kuwa na wanafunzi wawili wa Biblia waliokuwa wakifanya maendeleo ya kiroho.”

“KUSHANGILIA MILELE”

Ukweli ni kwamba si rahisi sikuzote kuwa na shangwe, na maisha yana panda-shuka nyingi. Ingawa hivyo, Mungu aliongoza maneno yenye kufariji ya Zaburi 64:10 yaandikwe. Hata tunapovunjika moyo pindi fulani, tunaweza kuamini kwamba wale watakaojithibitisha wenyewe kuwa ‘waadilifu’ kwa kuendelea kuwa waaminifu licha ya hali zao kubadilika, ‘watashangilia kwa sababu ya Yehova.’ Zaidi ya hilo, tunaweza kutazamia kwamba Yehova atatimiza ahadi yake ya kuleta “mbingu mpya na dunia mpya.” Kisha hali ya kutokamilika itaondolewa kabisa. Watu wote wa Mungu ‘watafurahia na kushangilia milele’ kwa sababu ya vitu ambavyo Mungu ataumba na kuandaa.—Isa. 65:17, 18.

Hebu wazia maana hasa ya maneno hayo: tutafurahia afya kamilifu na tutaamka kila siku tukiwa na nguvu nyingi. Hata iwe tulipitia maumivu makali kadiri gani ya kihisia wakati uliopita, kumbukumbu hizo zenye kuhuzunisha zitatokomea kabisa. Tunahakikishiwa kwamba “mambo ya zamani hayataingia tena akilini, wala hayataingia tena moyoni.” Muujiza wa ufufuo utatuunganisha tena na wapendwa wetu. Mamilioni ya watu watahisi kama wazazi wa msichana mwenye umri wa miaka 12 ambaye alifufuliwa na Yesu. Biblia inasema walikuwa “na shangwe kubwa sana.” (Marko 5:42) Hatimaye kila mtu duniani atakuwa “mwadilifu” katika maana kamili ya neno hilo, na “atashangilia kwa sababu ya Yehova” kwa umilele wote.