Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Tutaonana Paradiso!”

“Tutaonana Paradiso!”

“Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.”LUKA 23:43.

NYIMBO: 145, 139

1, 2. Watu wana maoni gani yanayotofautiana kuhusu paradiso?

ILIKUWA pindi iliyojaa hisia nyingi. Wajumbe kutoka nchi mbalimbali walipokuwa wakiondoka uwanjani baada ya kusanyiko jijini Seoul, Korea, Mashahidi wenyeji walikusanyika karibu nao. Wengi wao waliwapungia mkono na kuwaambia hivi kwa sauti kubwa: “Tutaonana Paradiso!” Unafikiri walikuwa wakizungumzia paradiso gani?

2 Watu wana maoni mbalimbali kuhusu paradiso. Baadhi ya watu husema kwamba paradiso ni jambo la kuwaziwa tu. Wengine husema kwamba paradiso ni mahali popote wanapoweza kupata shangwe na furaha. Mtu mwenye njaa kali akiwa ameketi mbele ya meza yenye vyakula vingi anaweza kuhisi kwamba yuko paradisoni. Katika karne ya 19, mgeni fulani alisema hivi kwa msisimko alipoona bonde lililojaa maua ya mwituni, “Oh, paradiso maridadi sana!” Eneo hilo bado linaitwa Paradiso, ingawa theluji yenye kina cha mita 15 huanguka kila mwaka katika eneo hilo. Wewe unafikiri Paradiso ni nini? Je, unaitarajia?

3. Paradiso inatajwa kwa mara ya kwanza wapi katika Biblia?

3 Biblia huzungumza kuhusu paradiso ambayo ilikuwepo hapo awali na nyingine itakayokuja. Tunasoma kuhusu Paradiso kwa mara ya kwanza kwenye kitabu cha kwanza kabisa cha Biblia. Katika tafsiri ya Biblia inayoitwa Catholic Douay Version iliyotafsiriwa kutoka Kilatini, andiko la Mwanzo 2:8 linasema: “Tangu mwanzo Bwana Mungu alikuwa amepanda paradiso ya raha: ambapo alimweka [Adamu] aliyekuwa amemuumba.” (Tumelaza maneno ili kukazia maana.) Maandiko ya Kiebrania huzungumza kuhusu bustani ya Edeni. Neno Edeni linamaanisha “Raha,” na kwa kweli bustani hiyo ilikuwa maridadi sana. Ilikuwa na chakula tele, mandhari yenye kuvutia, na wanadamu walifurahia kuishi pamoja na wanyama wengi wa aina tofauti-tofauti.—Mwa. 1:29-31.

4. Kwa nini tafsiri ya Kigiriki ilirejelea bustani ya Edeni kuwa paradiso, na kwa nini neno hilo linafaa?

4 Neno la Kiebrania “bustani,” linapotafsiriwa katika Kigiriki ni pa·raʹdei·sos. Kitabu kimoja cha utafiti cha M’Clintock na Strong kinasema hivi kuhusu pa·raʹdei·sos: “Ni bustani kubwa, iliyo wazi na salama, ambayo umaridadi wake wa asili haujaharibiwa, iliyo na msitu wenye miti mirefu na yenye kuvutia, na idadi kubwa ya miti hiyo ina matunda, nayo ina mito yenye maji safi, na kuna makundi makubwa ya swala au kondoo yanayotembea huku na huku kwenye kingo za mito hiyo—hiyo ndiyo picha ambayo Mgiriki anayesafiri alikuwa nayo akilini kuhusu paradiso.”—Linganisha Mwanzo 2:15, 16.

5, 6. Paradiso ilipoteaje, na huenda watu wakajiuliza swali gani?

5 Mungu aliwaweka Adamu na Hawa katika paradiso ya aina hiyo, lakini hawakuendelea kuishi humo. Kwa nini? Walikosa kumtii Mungu, hivyo hawakustahili kuendelea kuishi humo. Kwa sababu hiyo, wao pamoja na wazao wao walipoteza fursa ya kuendelea kuishi katika Paradiso. (Mwa. 3:23, 24) Ingawa wanadamu hawakuendelea kuishi katika Paradiso, inaonekana kwamba bustani hiyo iliendelea kuwepo hadi wakati wa Gharika ya siku za Noa.

6 Huenda watu fulani wakajiuliza, ‘Je, kweli kuna mwanamume, mwanamke, au mtoto yeyote atakayeishi katika Paradiso duniani?’ Ukweli wa mambo ni nini? Ikiwa unatamani kuishi katika Paradiso pamoja na watu unaowapenda, je, una sababu za msingi za kuamini kwamba tumaini lako litatimia? Je, unaweza kueleza kwa nini una hakika kwamba kutakuwa na Paradiso wakati ujao?

MAMBO YANAYOONYESHA KUTAKUWA NA PARADISO

7, 8. (a) Mungu alimpa Abrahamu ahadi gani? (b) Baada ya kupokea ahadi kutoka kwa Mungu, Abrahamu angeweza kufikia mkataa gani?

7 Mahali panapofaa zaidi pa kupata majibu ni katika kitabu kilichotungwa na Muumba wa Paradiso ya kwanza. Fikiria jambo ambalo Mungu alimwambia Abrahamu, rafiki yake. Mungu alimwambia kwamba angeufanya uzao wake uwe mwingi “kama chembe za mchanga kwenye ufuo wa bahari.” Na Yehova alimpa ahadi hii muhimu sana: “Kupitia uzao wako mataifa yote ya dunia yatajipatia baraka kwa sababu umeisikiliza sauti yangu.” (Mwa. 22:17, 18) Mungu alirudia ahadi hiyo ya msingi alipozungumza na mwana wa Abrahamu na baadaye mjukuu wake.—Soma Mwanzo 26:4; 28:14.

8 Hakuna jambo lolote katika Biblia linaloonyesha kwamba Abrahamu alifikiri kuwa mwishowe wanadamu wangepata thawabu ya kuishi katika paradiso ambayo ingekuwa mbinguni. Hivyo, Mungu aliposema kwamba “mataifa yote ya dunia” yangebarikiwa, Abrahamu angeweza kufikia mkataa kwamba baraka hizo zingetimia hapa duniani. Ahadi hiyo ilitoka kwa Mungu, na hilo lilionyesha kwamba “mataifa yote ya dunia” yangekuwa na hali nzuri. Je, kuna mambo mengine yanayotajwa katika Biblia yanayounga mkono wazo hilo?

9, 10. Ni ahadi gani nyingine zinazotupatia sababu za kuamini kwamba kutakuwa na paradiso wakati ujao?

9 Daudi, mmoja wa wazao wa Abrahamu, alizungumza kuhusu wakati ujao ambapo “waovu” na “watenda dhambi” wangepitilia mbali. Hilo linamaanisha nini? Kwamba “waovu hawatakuwepo tena.” (Zab. 37:1, 2, 10) Badala yake, “wapole wataimiliki dunia, nao watafurahia kwelikweli wingi wa amani.” Pia, Daudi aliongozwa na roho kutabiri hivi: “Waadilifu wataimiliki dunia, nao wataishi humo milele.” (Zab. 37:11, 29; 2 Sam. 23:2) Unafikiri ahadi hizo ziliwaimarisha jinsi gani watu waliotamani kufanya mapenzi ya Mungu? Ziliwapa sababu ya kuamini kwamba ikiwa watu waadilifu pekee ndio watakaoishi duniani, basi baada ya muda dunia ingekuwa paradiso tena kama bustani ya Edeni ilivyokuwa.

10 Kadiri miaka ilivyopita, Waisraeli wengi waliodai kuwa wanamtumikia Yehova walimwasi na kuacha ibada yake ya kweli. Hivyo, Mungu aliwaruhusu Wababiloni wawashambulie watu wake, waharibu nchi yao, na kuwapeleka wengi wao uhamishoni. (2 Nya. 36:15-21; Yer. 4:22-27) Ingawa hivyo, manabii wa Mungu walitabiri kwamba baada ya miaka 70, watu wa Mungu wangerudi katika nchi yao. Mambo hayo yaliyotabiriwa yalitimia. Lakini yanatuhusu sisi pia. Sasa tunapochunguza baadhi ya unabii huo mbalimbali, zingatia akilini jambo hili—paradiso tunayotarajia duniani wakati ujao.

11. Andiko la Isaya 11:6-9 lilitimizwaje, lakini huenda bado tukajiuliza swali gani?

11 Soma Isaya 11:6-9. Kupitia nabii Isaya, Mungu alitabiri kwamba baada ya watu Wake kurudi katika nchi yao, hawangelazimika kupambana na hali ngumu zilizo hatari; wala hawangehitaji kuogopa kwamba wangeshambuliwa na wanyama au wanadamu wenye tabia za kinyama. Vijana kwa wazee wangekuwa salama. Je, hilo halikukumbushi kuhusu mazingira ambayo Mungu alikuwa ameandaa katika bustani ya Edeni? (Isa. 51:3) Unabii huo wa Isaya ulisema pia kwamba dunia nzima—si taifa la Israeli peke yake—“[ingejaa] ujuzi kumhusu Yehova kama maji yanavyoifunika bahari.” Hilo litatendeka lini?

12. (a) Watu waliorudi kutoka uhamishoni Babiloni walifurahia baraka gani? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba andiko la Isaya 35:5-10 lina utimizo mwingine?

12 Soma Isaya 35:5-10. Isaya alirudia tena kutabiri kwamba wale ambao wangerudi katika nchi yao hawangeshambuliwa na wanyama au wanadamu. Nchi yao ingetokeza mazao tele kwa sababu kungekuwa na maji ya kutosha, kama bustani ya Edeni ilivyokuwa na maji mengi. (Mwa. 2:10-14; Yer. 31:12) Je, huo ndio utimizo pekee wa unabii huo? Hakuna uthibitisho wowote unaoonyesha kwamba wale waliorudi kutoka uhamishoni waliponywa kimuujiza. Kwa mfano, vipofu hawakurudishiwa uwezo wao wa kuona. Hivyo, Mungu alikuwa akionyesha kwamba kungekuwa na uponyaji halisi wakati ujao.

13, 14. Watu waliorudi kutoka uhamishoni walijioneaje andiko la Isaya 65:21-23 likitimia, lakini ni sehemu gani ya unabii huo ambayo bado haijatimia? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

13 Soma Isaya 65:21-23. Wayahudi waliporudi hakukuwa na nyumba nzuri; mashamba hayakuwa yamelimwa wala hakukuwa na mashamba ya mizabibu. Lakini hali ingebadilika kadiri Mungu alivyowabariki. Wangefurahia kwelikweli kujenga nyumba na kuishi humo! Wangepanda mimea na kufurahia mazao tele.

14 Ona jambo fulani muhimu kuhusu unabii huo. Je, wakati utafika ambapo siku zetu za kuishi “zitakuwa kama siku za mti”? Miti fulani huishi kwa maelfu ya miaka. Hivyo, ili wanadamu waishi kwa kipindi kirefu hivyo wanahitaji kuwa na afya nzuri. Na ikiwa wangepata fursa ya kuishi chini ya mazingira ambayo Isaya alitabiri, basi kwa kweli huo ungekuwa utimizo halisi wa ahadi waliyokuwa wakisubiri kwa hamu, paradiso yenyewe! Na unabii huo utatimia!

Ahadi ambayo Yesu alitoa kuhusu Paradiso itatimizwaje? (Tazama fungu 15 na 16)

15. Taja baadhi ya baraka zilizotabiriwa katika kitabu cha Isaya.

15 Tafakari jinsi ahadi tulizozungumzia zinavyoonyesha kwamba kutakuwa na paradiso wakati ujao: Watu duniani kote watabarikiwa na Mungu. Hakuna yeyote atakayeshambuliwa na wanyama au wanadamu wenye tabia za kinyama. Vipofu, viziwi, na vilema wataponywa. Watu watajenga nyumba zao wenyewe na kufurahia kupanda vyakula vyenye lishe. Wataishi miaka mingi kuliko miti. Naam, Biblia inaonyesha kwamba mambo hayo yatatimia wakati ujao. Hata hivyo, huenda baadhi ya watu wakadai kwamba tunaelewa unabii huo kwa njia isiyo sahihi. Wewe ungesemaje? Una sababu gani ya msingi ya kutazamia kwa hamu paradiso halisi hapa duniani? Mtu mkuu zaidi aliyewahi kuishi alitupatia sababu ya msingi ya kutazamia jambo hilo.

UTAKUWA KATIKA PARADISO!

16, 17. Yesu alikuwa katika hali gani alipozungumza kuhusu Paradiso?

16 Ingawa Yesu hakuwa na hatia, alihukumiwa kifo kwa kutundikwa mtini pamoja na Wayahudi wawili wahalifu waliotundikwa kando yake, upande wa kushoto na wa kulia. Kabla ya Yesu kufa, mmoja wa wahalifu hao alitambua kwamba Yesu alikuwa mfalme na akamsihi hivi: “Yesu, unikumbuke utakapoingia katika Ufalme wako.” (Luka 23:39-42) Jibu ambalo Yesu alimpa kwenye Luka 23:43, linahusu hali yako ya wakati ujao. Wasomi fulani wa nyakati zetu wanatoa tafsiri hii ya neno kwa neno kuhusu andiko hilo: “Amin, nakuambia, leo hii utakuwa pamoja nami Paradiso.” Zingatia neno “leo.” Yesu alipotumia neno “leo” alikuwa akimaanisha nini? Watu wana maoni mbalimbali kuhusu andiko hilo.

17 Katika lugha nyingi, alama ya mkato hutumiwa ili kufanya maana ieleweke au iwe wazi katika sentensi. Lakini katika hati za awali kabisa za Kigiriki alama kama hizo hazikutumiwa kwa ukawaida. Hivyo, swali linazuka: Je, Yesu alikuwa akisema, “Nakuambia, leo hii utakuwa pamoja nami Paradiso”? Au alikuwa akisema, “Ninakuambia leo, utakuwa pamoja nami katika Paradiso”? Watafsiri huweka alama ya mkato kwenye maneno hayo ya Yesu ikitegemea jinsi walivyoyaelewa, hivyo baadhi ya tafsiri za Biblia huwa na alama ya mkato kabla ya neno “leo,” na nyingine baada ya neno hilo.

18, 19. Ni hoja zipi zinazoweza kutusaidia kuelewa kile ambacho Yesu alimaanisha?

18 Hata hivyo, kumbuka kwamba Yesu alikuwa amewaambia hivi wafuasi wake: “Mwana wa binadamu [atakuwa] katika moyo wa ardhi siku tatu mchana na usiku.” Pia, alisema hivi: “Mwana wa binadamu atasalitiwa mikononi mwa watu, nao watamuua, na siku ya tatu atafufuliwa.” (Mt. 12:40; 16:21; 17:22, 23; Marko 10:34) Mtume Petro anataja kwamba jambo hilo lilitukia. (Mdo. 10:39, 40) Hivyo, Yesu hakuenda katika Paradiso siku ambayo yeye na mhalifu huyo walikufa. Yesu alikuwa “katika Kaburi [au ‘Hadesi’]” kwa siku kadhaa, hadi Mungu alipomfufua.—Mdo. 2:31, 32; maelezo ya chini. *

19 Hiyo ndiyo sababu Yesu alipokuwa akimpa ahadi mhalifu huyo alianza kwa kusema: “Kwa kweli ninakuambia leo.” Njia hiyo ya mazungumzo ilikuwa ya kawaida hata katika siku za Musa. Musa alisema hivi: “Maneno haya ninayokuamuru leo lazima yawe moyoni mwako.”—Kum. 6:6; 7:11; 8:1, 19; 30:15.

20. Ni mambo gani yanayounga mkono uelewaji wetu kuhusu maneno ya Yesu?

20 Mtafsiri mmoja wa Biblia kutoka Mashariki ya Kati alisema hivi kuhusu jibu la Yesu: “Neno linalokaziwa katika mstari huo ni ‘leo’ na hivyo mstari huo unapaswa kusomeka, ‘Kwa kweli ninakuambia leo, utakuwa pamoja nami katika Paradiso.’ Ahadi hiyo ilitolewa siku hiyo lakini ilipaswa kutimia wakati ujao. Watu wa Mashariki walizoea kuzungumza hivyo wakimaanisha kwamba ahadi ingetolewa siku fulani na hakungekuwa na shaka kwamba ingetimizwa.” Hivyo, tafsiri ya Kisiria ya karne ya tano ya maandishi matakatifu inasema hivi kuhusu jibu la Yesu: “Kwa hakika, leo hii nakuambia kwamba utakuwa pamoja nami katika Bustani ya Edeni.” Ahadi hiyo inapaswa kututia moyo sisi sote.

21. Mhalifu hakupata pendeleo gani, na kwa nini?

21 Mhalifu huyo aliyekuwa amehukumiwa kifo, hakuwa na habari kuwa Yesu alikuwa amefanya agano pamoja na mitume wake waaminifu kwamba watakuwa pamoja naye katika Ufalme wa mbinguni. (Luka 22:29) Isitoshe, mhalifu huyo hakuwa hata amebatizwa. (Yoh. 3:3-6, 12) Kwa msingi huo tunaelewa kwamba Yesu alimwahidi kwamba atakuwa katika paradiso hapa duniani. Miaka mingi baadaye, mtume Paulo alisimulia kuhusu maono ya mtu “[aliyenyakuliwa] kuingia katika paradiso.” (2 Kor. 12:1-4) Tofauti na mhalifu huyo aliyekuwa karibu kufa, Paulo na mitume wengine waaminifu walikuwa wamechaguliwa wakaishi mbinguni ili watawale pamoja na Yesu. Ingawa hivyo, Paulo alikuwa akirejelea kuhusu jambo fulani litakalotukia wakati ujao, yaani, “paradiso.” * Je, paradiso hiyo itakuwa duniani? Na je, wewe utakuwepo?

MAMBO UNAYOWEZA KUTARAJIA

22, 23. Unaweza kutarajia nini?

22 Zingatia akilini kwamba Daudi alitabiri kuhusu wakati ambapo “waadilifu wataimiliki dunia.” (Zab. 37:29; 2 Pet. 3:13) Daudi alikuwa akizungumza kuhusu wakati ambapo watu duniani wangeishi kulingana na njia za Mungu za uadilifu. Unabii ulio kwenye andiko la Isaya 65:22 unasema hivi: “Siku za watu wangu zitakuwa kama siku za mti.” Hilo linaonyesha kwamba watu wataishi kwa maelfu ya miaka. Je, una sababu za kutarajia jambo hilo? Ndiyo, kwa sababu kulingana na andiko la Ufunuo 21:1-4, Mungu atawakazia uangalifu wanadamu, na mojawapo ya baraka anazowaahidi watumishi wake katika ulimwengu wake mpya wenye uadilifu ni kwamba “kifo hakitakuwapo tena.”

23 Hivyo, ukweli wa mambo kuhusu paradiso uko wazi. Adamu na Hawa walipoteza fursa ya kuishi kwenye Paradiso katika bustani ya Edeni, lakini Paradiso itarudishwa tena. Kama Mungu alivyoahidi, wanadamu duniani watapokea baraka zake. Akiongozwa na roho ya Mungu, Daudi alisema kwamba wapole na waadilifu wataimiliki dunia na kuishi humo milele. Unabii mbalimbali wa kitabu cha Isaya unapaswa kutuchochea tutazamie kwa hamu hali zenye kupendeza zitakazoenea kotekote duniani. Wakati gani? Wakati ambapo ahadi ambayo Yesu alimpa yule mhalifu Myahudi itakapotimia. Wewe pia unaweza kuishi katika Paradiso hiyo. Wakati huo, maneno ambayo wale wajumbe nchini Korea waliambiwa yatatimia: “Tutaonana Paradiso!”

^ fu. 18 Profesa C. Marvin Pate aliandika hivi: “Kwa kawaida, watu walielewa neno ‘leo’ kuwa linarejelea kipindi hususa cha saa ishirini na nne. Tatizo la uelewaji huo ni jinsi unavyopingana waziwazi na mistari mingine ya Biblia inayoonyesha kwamba Yesu ‘alishuka’ kwenda hadesi alipokufa (Mt. 12:40; Mdo. 2:31; Rom. 10:7) na baadaye akapanda kwenda mbinguni.”

^ fu. 21 Tazama “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika makala hii.