Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana, Mnaweza Kuwa na Maisha Yenye Kuridhisha

Vijana, Mnaweza Kuwa na Maisha Yenye Kuridhisha

“Unanijulisha njia ya uzima.”​—ZAB. 16:11.

NYIMBO: 133, 89

1, 2. Kama tulivyoona katika kisa cha mwanafunzi mmoja wa sekondari, mtu anaweza kufanya mabadiliko gani?

MWANAFUNZI wa sekondari anayeitwa Tony, alikuwa karibu kuacha shule. Hakuwa na baba na hakupenda masomo, hivyo alitumia siku za mwisho juma pamoja na marafiki au akitazama sinema. Hakupenda fujo wala hakuwa mraibu wa dawa za kulevya. Kwa ufupi, hakuwa na kusudi maishani. Na alitilia shaka ikiwa kuna Mungu. Kisha alikutana na wenzi fulani wa ndoa waliokuwa Mashahidi na akawauliza maswali na kuwaeleza kuhusu mambo aliyokuwa akitilia shaka. Walimpa broshua mbili​—Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai na Uhai—Ulitokana na Muumba?

2 Wenzi hao wa ndoa walipokutana tena na Tony, mtazamo wake ulikuwa umebadilika. Alikuwa amesoma broshua hizo tena na tena hivi kwamba kurasa zake zilikuwa zimejikunja na kuchakaa. Tony aliwaambia hivi: “Lazima kuwe kuna Mungu.” Alikubali kujifunza Biblia, na hatua kwa hatua mtazamo wake kuhusu maisha ukabadilika. Pia, aliacha kuanguka mitihani na akawa miongoni mwa wanafunzi bora zaidi shuleni. Hata mwalimu mkuu, ambaye alijua kwamba Tony alikuwa ameanza kujifunza Biblia, alishangaa. Alimwambia hivi: “Mtazamo wako umebadilika sana na sasa maksi zako ni nzuri. Je, ni kwa sababu umeanza kushirikiana na Mashahidi wa Yehova?” Tony alijibu “ndiyo,” na kisha akamtolea ushahidi mzuri sana. Alimaliza masomo yake ya sekondari na leo yeye ni mtumishi wa huduma na anatumikia akiwa painia wa kawaida. Pia, yeye ni mwenye furaha kwa sababu sasa amepata Baba mzuri sana, Yehova.—Zab. 68:5.

MTII YEHOVA, NAWE UTAFANIKIWA

3. Yehova anawapendekezea vijana wafuate njia gani?

3 Kisa cha Tony kinatukumbusha jinsi Yehova anavyopendezwa sana nanyi vijana mlio miongoni mwetu. Anataka mfanikiwe kikweli na muwe na maisha yenye kuridhisha. Hivyo, anawapa ushauri huu: “Mkumbuke Muumba wako Mkuu katika siku za ujana wako.” (Mhu. 12:1) Si rahisi kufanya hivyo katika ulimwengu wa leo. Hata hivyo, inawezekana. Kwa msaada wa Mungu, unaweza kufanikiwa, si tu ukiwa kijana, bali pia katika maisha yako yote. Kwa mfano, fikiria somo tunalojifunza kutokana na jinsi Waisraeli walivyoyashinda mataifa yaliyokuwa katika Nchi ya Ahadi na kisa cha Daudi alipokabiliana na Goliathi.

4, 5. Tunaweza kujifunza somo gani muhimu kutokana na jinsi Waisraeli walivyoyashinda mataifa yaliyokuwa Kanaani na jinsi Daudi alivyokabiliana na Goliathi? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

4 Waisraeli walipokaribia kuingia katika Nchi ya Ahadi, Mungu hakuwaamuru wanoe ustadi wao wa kupigana au wajizoeze kwa ajili ya vita. (Kum. 28:1, 2) Badala yake, aliwaambia kwamba walipaswa kutii amri zake na kumtumaini. (Yos. 1:7-9) Kwa maoni ya kibinadamu, ushauri huo ungeonekana kuwa wa kipumbavu! Lakini huo ndio uliokuwa ushauri bora kabisa, kwani Yehova aliwasaidia watu wake tena na tena kupata ushindi mkubwa dhidi ya Wakanaani. (Yos. 24:11-13) Naam, tunahitaji imani ili kumtii Mungu, na sikuzote imani hiyo hutuletea mafanikio. Ukweli wa jambo hilo haubadiliki hata baada ya muda kupita. Na haujabadilika hadi leo.

5 Goliathi alikuwa shujaa hodari mwenye urefu wa mita 2.9, na alikuwa amejihami kwa silaha. (1 Sam. 17:4-7) Lakini Daudi alikuwa na vitu viwili tu: kombeo na imani kwa Mungu wake, Yehova. Kwa watu wasio na imani, kwa hakika Daudi alionekana kuwa mtu mpumbavu. Lakini walikuwa wamekosea sana! Goliathi ndiye aliyekuwa mpumbavu.—1 Sam. 17:48-51.

6. Tutachunguza nini kwa undani zaidi?

6 Katika makala iliyotangulia, tulichunguza mambo manne yanayotuletea furaha na mafanikio maishani. Mambo hayo ni kutosheleza uhitaji wetu wa kiroho, kuthamini marafiki ambao Mungu ametusaidia kupata, kujiwekea malengo yatakayotunufaisha, na kutumia vizuri uhuru tulio nao tukiwa watu wa Mungu. Sasa acheni tuchunguze kwa undani zaidi mambo hayo, na wakati huu tutazungumzia baadhi ya kanuni zinazopatikana katika Zaburi ya 16.

TOSHELEZA UHITAJI WAKO WA KIROHO

7. (a) Ungemfafanuaje mtu wa kiroho? (b) “Fungu” la Daudi lilikuwa nini, nalo lilimfanya ahisije?

7 Mtu wa kiroho ana imani kwa Mungu na anaona mambo kama Mungu anavyoyaona. Anamtegemea Mungu ili kupata mwongozo na ameazimia kumtii. (1 Kor. 2:12, 13) Daudi ni mfano mzuri wa mtu wa kiroho. Aliimba hivi: “Yehova ni fungu langu, sehemu niliyogawiwa, na kikombe changu.” (Zab. 16:5) “Fungu” hilo lilitia ndani uhusiano wake wa karibu pamoja na Mungu, ambaye Daudi alimfanya kuwa kimbilio lake. (Zab. 16:1) Ndiyo sababu Daudi alisema, “Nafsi yangu yote ina shangwe.” Naam, hakuna jambo lililompa Daudi shangwe nyingi kuliko uhusiano wake wa karibu pamoja na Mungu.—Soma Zaburi 16:9, 11.

8. Taja baadhi ya mambo yanayoweza kufanya maisha yako yawe yenye kuridhisha.

8 Wale wanaotanguliza raha na utajiri maishani mwao hawawezi kupata shangwe ambayo Daudi alikuwa nayo. (1 Tim. 6:9, 10) Ndugu mmoja kutoka Kanada anaeleza hivi: “Furaha ya kweli haitokani na vitu tunavyopata maishani, bali hutokana na kile tunachompa Mpaji wa kila zawadi njema, yaani, Yehova Mungu.” (Yak. 1:17) Naam, kusitawisha imani kwa Yehova na kumtumikia kutakufanya uridhike na uwe na kusudi maishani. Unaweza kufanya nini ili imani yako ikue? Ni lazima utumie muda pamoja na Yehova kwa kusoma Neno lake, kutazama uumbaji wake, na kutafakari kuhusu sifa zake, kutia ndani mambo yanayoonyesha kwamba anakupenda.—Rom. 1:20; 5:8.

9. Unaweza kufanya nini ili uruhusu Neno la Mungu likufinyange kama lilivyomfinyanga Daudi?

9 Nyakati nyingine, Mungu hutuonyesha kwamba anatupenda kwa kuturekebisha kama Baba. Daudi alikuwa tayari kupokea shauri kama hilo lililotolewa kwa fadhili. Alisema hivi: “Nitamsifu Yehova, ambaye amenipa ushauri. Hata wakati wa usiku, mawazo yangu ya ndani kabisa hunirekebisha.” (Zab. 16:7) Naam, Daudi alitafakari mawazo ya Mungu, akayafanya mawazo hayo yawe mawazo yake na kuyaruhusu yamfinyange au kumwongoza. Ikiwa utachochewa na imani kufanya mambo hayo, upendo wako na tamaa yako ya kumtii Mungu itaongezeka. Pia, ukomavu wako wa kiroho utaongezeka na kuwa wenye kina zaidi. Dada Mkristo anayeitwa Christin anasema hivi: “Ninapofanya utafiti na kutafakari mambo ninayosoma, ninahisi kwamba Yehova aliongoza mambo hayo yaandikwe hasa kwa ajili yangu!”

10. Kama inavyoonyeshwa kwenye andiko la Isaya 26:3, tunapata faida gani tunapokuwa na mtazamo wa kiroho maishani?

10 Hatutilii chumvi kusema kwamba kuwa na mtazamo wa kiroho maishani hutusaidia pia kupata ujuzi wa pekee na ufahamu ambao hutuwezesha kuwa na maoni ya Mungu kuhusu ulimwengu na mambo yatakayoukumba wakati ujao. Kwa nini Mungu anakupatia ujuzi na ufahamu huo? Anataka utangulize mambo yanayofaa maishani mwako, ufanye maamuzi ya hekima, na utazamie wakati ujao ukiwa na uhakika! (Soma Isaya 26:3.) Joshua, ndugu anayeishi nchini Marekani, anasema hivi: “Kukaa karibu na Yehova hutusaidia tujue mambo tunayopaswa kutanguliza.” Maneno hayo ni ya kweli kabisa, na kufanya hivyo huturidhisha kwelikweli!

TAFUTA MARAFIKI WA KWELI

11. Daudi alisema siri ya kupata marafiki wa kweli ni nini?

11 Soma Zaburi 16:3. Daudi alifahamu siri ya kupata marafiki wa kweli. ‘Alipendezwa sana’ na ushirika wa wale waliompenda Yehova. Watu hao wanaofafanuliwa kuwa “watakatifu,” walikuwa safi kiadili na wanyoofu. Mtunga zaburi mwingine alihisi vivyo hivyo pia kuhusu marafiki aliochagua. Aliandika hivi: “Mimi ni rafiki ya wote wanaokuogopa wewe na ya wale wanaoyatii maagizo yako.” (Zab. 119:63) Kama tulivyoona katika makala iliyotangulia, wewe pia unaweza kupata marafiki wengi wazuri miongoni mwa wale wanaomwogopa na kumtii Yehova. Bila shaka marafiki hao wanatia ndani watu wa umri mbalimbali.

12. Urafiki wa Daudi na Yonathani ulikuwa na msingi gani?

12 Mtunga zaburi Daudi hakushirikiana tu na watu wa rika lake. Je, unakumbuka jina la mtu fulani “mtukufu” ambaye alikuwa rafiki yake wa karibu? Aliitwa Yonathani. Kwa kweli, uhusiano wao ni miongoni mwa urafiki maridadi sana ulioandikwa katika Maandiko. Je, ulijua kwamba Yonathani alimzidi Daudi umri kwa miaka 30 hivi? Basi, msingi wa urafiki wao ulikuwa nini? Walikuwa na imani kwa Mungu, waliheshimiana, na kila mmoja aliona jinsi mwenzake alivyoonyesha ujasiri alipopigana dhidi ya maadui wa Mungu.—1 Sam. 13:3; 14:13; 17:48-50; 18:1.

13. Unaweza kufanya nini ili upate marafiki wengi zaidi? Toa mfano.

13 Kama Daudi na Yonathani, sisi pia ‘tunapendezwa sana’ na watu wanaompenda Yehova na wanaoonyesha kwamba wana imani kwake. Kiera, dada ambaye amemtumikia Mungu kwa miaka mingi, anaeleza hivi: “Nimepata marafiki kutoka kila sehemu ya ulimwengu, watu wa malezi na utamaduni mbalimbali.” Wewe pia ukifanya vivyo hivyo, utajionea uthibitisho ulio wazi wa jinsi ambavyo nguvu za Neno la Mungu na roho takatifu hutusaidia tuwe na umoja.

FUATIA MALENGO YATAKAYOKUNUFAISHA

14. (a) Ni nini kitakachokusaidia ujiwekee malengo yatakayokunufaisha maishani? (b) Baadhi ya vijana wamehisije kuhusu kujiwekea malengo ya kiroho?

14 Soma Zaburi 16:8. Jambo kuu maishani mwa Daudi lilikuwa kumtumikia Yehova. Wewe pia utafurahia maisha yenye kuridhisha kikweli ikiwa utatanguliza utumishi wako kwa Yehova na kujiwekea malengo yanayoonyesha kwamba unamtanguliza maishani. Ndugu anayeitwa Steven anasema hivi: “Kujitahidi kufikia lengo fulani maishani, kulitimiza, na kisha kutafakari maendeleo ambayo nimefanya huniletea furaha.” Ndugu kijana kutoka Ujerumani anayetumikia katika nchi nyingine alisema hivi: “Nitakapozeeka, nisingependa kutafakari jinsi maisha yangu yalivyokuwa na kuona kwamba kila jambo nililofanya lilikuwa kwa faida zangu za kibinafsi.” Tunatumaini wewe pia unahisi vivyo hivyo. Ikiwa ndivyo, tumia zawadi ulizo nazo kumheshimu Mungu na kuwatendea wengine mema. (Gal. 6:10) Jiwekee malengo ya kiroho, na umwombe Yehova katika sala akusaidie uyafikie. Yeye hufurahia sana kujibu sala kama hizo.​—1 Yoh. 3:22; 5:14, 15.

15. Unaweza kujiwekea malengo gani? (Tazama sanduku “ Malengo Unayoweza Kujiwekea.”)

15 Unaweza kujiwekea malengo gani? Unaweza kujiwekea lengo la kutoa maelezo kwa maneno yako mwenyewe katika mikutano ya Kikristo, kushiriki katika utumishi wa upainia, au kwenda Betheli. Unaweza kujifunza lugha nyingine ukiwa na lengo la kutumikia katika eneo linalozungumza lugha ya kigeni. Barak, ndugu kijana anayetumikia akiwa mtumishi wa wakati wote anasema hivi: “Hisia ninazopata ninapoamka kila siku na kujua kwamba ninatumia nguvu zangu zote kumtumikia Yehova ni hisia ambazo hakuna kazi nyingine yoyote inayoweza kunipa.”

TUMIA VIZURI UHURU ULIOPEWA NA MUNGU

16. Daudi alihisije kuhusu viwango vya Yehova vya uadilifu, na kwa nini alihisi hivyo?

16 Soma Zaburi 16:2, 4Kama tulivyoona katika makala iliyotangulia, sheria za Mungu za uadilifu na kanuni zake hutupatia uhuru kwa kutusaidia tujifunze kupenda yaliyo mema na kuchukia yaliyo mabaya. (Amo. 5:15) Mtunga zaburi Daudi alimtambua Yehova kuwa ‘Chanzo chake cha wema.’ Wema ni kuwa na maadili mema, au mwenendo bora. Daudi alijitahidi sana kumwiga Mungu, yaani kuiga wema wa Mungu. Pia, Daudi alijifunza kuchukia mambo yaliyokuwa mabaya machoni pa Mungu. Mambo hayo yalitia ndani ibada ya sanamu, zoea ambalo huwashushia wanadamu heshima na kumwondolea Yehova utukufu anaostahili.—Isa. 2:8, 9; Ufu. 4:11.

17, 18. (a) Daudi alijionea madhara gani ya kujihusisha na ibada ya uwongo? (b) Ni jambo gani ambalo hufanya watu ‘wazidishe huzuni yao’ leo?

17 Katika nyakati za Biblia, kwa kawaida ibada ya uwongo ilitia ndani matendo machafu sana ya kingono. (Hos. 4:13, 14) Ukweli ni kwamba wanadamu wenye dhambi walivutiwa na aina hiyo ya ibada. Lakini haikuwaletea furaha ya kudumu. Kinyume chake, kama Daudi alivyosema, ‘Wale waliofuatia miungu mingine walizidisha huzuni yao.’ Pia, waliwasababishia mateso makubwa watoto wengi. (Isa. 57:5) Yehova alichukizwa sana na ukatili huo! (Yer. 7:31) Ikiwa ungekuwepo nyakati hizo, bila shaka ungeshukuru sana kwamba wazazi wako walikuwa na imani kwa Yehova na walimtii.

18 Leo pia, kwa kawaida ibada ya uwongo huunga mkono upotovu wa maadili katika ngono, kutia ndani ngono kati ya watu wa jinsia moja. Lakini matokeo ya kujiingiza bila kujali katika mwenendo uliopotoka kiadili, unaoonwa na watu wengi kuwa ndiyo uhuru, hayajabadilika tangu nyakati za Biblia. (1 Kor. 6:18, 19) Kama ambavyo tayari umejionea, watu “huzidisha huzuni yao.” Hivyo vijana, msikilizeni Baba yenu wa mbinguni. Jisadikishieni kabisa kwamba mnapomtii ninyi ndio mnaofaidika. Kazieni moyoni mwenu kwamba madhara yanayosababishwa na kutenda dhambi yanazidi kwa mbali raha yoyote ya muda mfupi. (Gal. 6:8) Joshua, aliyetajwa awali anasema hivi: “Tunaweza kutumia uhuru wetu vyovyote tupendavyo, lakini kuutumia vibaya hakutaturidhisha.”

19, 20. Vijana walio na imani kwa Yehova na wanaomtii wanatarajia kupata baraka gani wakati ujao?

19 Yesu aliwaambia hivi wafuasi wake: “Mkikaa katika neno langu, ninyi kwa kweli ni wanafunzi wangu, nanyi mtaijua kweli, nayo kweli itawaweka ninyi huru.” (Yoh. 8:31, 32) Uhuru huo unatia ndani kuwa huru kutokana na dini bandia, ukosefu wa ujuzi, na ushirikina. Na unahusisha mambo mengi zaidi. Kama ambavyo tumeona, hatimaye uhuru huo utatia ndani “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.” (Rom. 8:21) Hata sasa, unaweza kufurahia kiwango fulani cha uhuru huo kwa ‘kukaa katika neno la Kristo,’ au mafundisho yake. Kwa njia hiyo, ‘utaijua kweli’ si kwa kujifunza tu kuihusu, bali pia kwa kuishi kulingana nayo.

20 Vijana, tumieni vizuri uhuru ambao Mungu amewapa. Tumieni uhuru huo kwa hekima, na kwa kufanya hivyo mtajiwekea msingi mzuri kwa ajili ya wakati ujao. Ndugu mmoja kijana alisema hivi: “Kutumia uhuru kwa hekima ukiwa kijana ni jambo litakalokunufaisha sana baadaye utakapokabili maamuzi makubwa, kama vile kutafuta kazi inayofaa au kuchagua ikiwa utafunga ndoa au kubaki mseja kwa kipindi fulani.”

21. Ni nini kitakachokusaidia kubaki kwenye njia inayoongoza kwenye “uzima ulio wa kweli”?

21 Katika mfumo huu wa kale wa mambo, hata maisha ambayo watu wengi huyaona kuwa bora, hayatabiriki na ni mafupi. Hatujui mambo yatakayotendeka kesho. (Yak. 4:13, 14) Basi, jambo la hekima ni kubaki katika njia inayoongoza kwenye “uzima ulio wa kweli,” yaani, uzima wa milele. (1 Tim. 6:19) Bila shaka, Mungu hatulazimishi kufuata njia hiyo. Uamuzi ni wetu. Mfanye Yehova kuwa “fungu” lako. Tumia vizuri ‘vitu vingi vyema’ ambavyo amekupatia. (Zab. 103:5) Na uwe na imani kwamba anaweza kukupatia “shangwe tele” na “furaha . . . milele.”—Zab. 16:11.