Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana, Muumba Wenu Anataka Muwe na Furaha

Vijana, Muumba Wenu Anataka Muwe na Furaha

“Hukushibisha kwa vitu vyema maisha yako yote.”​—ZAB. 103:5.

NYIMBO: 135, 39

1, 2. Tunapochagua malengo tutakayofuatia maishani, kwa nini ni jambo la hekima kumsikiliza Muumba wetu? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

IKIWA wewe ni kijana, huenda umepokea ushauri mwingi kuhusu wakati wako ujao. Huenda walimu, washauri, na watu wengine wamekutia moyo ufuatie elimu ya juu na kazi nzuri yenye mshahara mnono. Hata hivyo, Yehova anakushauri ufuate mkondo tofauti. Ukweli ni kwamba anataka utie bidii shuleni ili uweze kujiruzuku utakapomaliza masomo. (Kol. 3:23) Lakini unapofanya uamuzi kuhusu mambo utakayotanguliza maishani, anakutia moyo uongozwe na kanuni zake ambazo huchangia katika kutimizwa kwa kusudi na mapenzi yake kutuhusu katika kipindi hiki cha mwisho.—Mt. 24:14.

2 Pia, zingatia akilini kwamba Yehova ana picha kamili ya mambo kwa sababu anajua kile kitakachoupata ulimwengu huu na anajua kwamba mwisho wake uko karibu sana. (Isa. 46:10; Mt. 24:3, 36) Zaidi ya hilo, anatujua vizuri—anajua mambo yanayotufanya turidhike kikweli na kutuletea furaha na pia mambo yanayoweza kufanya tukate tamaa na kutufanya tukose furaha. Hivyo, hata ushauri wa wanadamu uonekane kuwa mzuri kadiri gani, ikiwa hautegemei Neno la Mungu, ushauri huo si wa hekima hata kidogo.—Met. 19:21.

“HAKUNA HEKIMA . . . KATIKA KUMPINGA YEHOVA”

3, 4. Adamu na Hawa pamoja na watoto wao walipata matokeo gani kwa sababu ya kufuata ushauri mbaya?

3 Ushauri mbaya ulianza kutolewa mapema sana katika historia ya wanadamu Shetani alipotokea. Mshauri huyo mwenye kimbelembele aliyejipatia cheo cha kuwapa wengine ushauri, alimwambia Hawa kwamba yeye na mume wake wangekuwa na furaha zaidi ikiwa wangejiamulia wenyewe njia watakayofuata maishani. (Mwa. 3:1-6) Hata hivyo, ukweli wa mambo ni kwamba nia ya Shetani ilikuwa ya ubinafsi. Alitaka Adamu na Hawa, na baadaye watoto wao, wajitiishe kwake na kumwabudu yeye badala ya kumwabudu Yehova. Lakini je, kuna jambo lolote ambalo alikuwa amewatendea? Yehova ndiye aliyekuwa amewapa vitu vyote walivyokuwa navyo—mwenzi wa ndoa, bustani maridadi iwe makao yao, na miili mikamilifu ambayo ingewasaidia kuishi milele.

4 Kwa kusikitisha, Adamu na Hawa hawakumtii Mungu, nao wakajiondoa kutoka kwake. Kama ujuavyo, matokeo yalikuwa mabaya sana. Kama maua yaliyokatwa kutoka kwenye mmea, pole kwa pole walidhoofika na mwishowe wakafa. Watoto wao pia waliathiriwa na laana ya dhambi. (Rom. 5:12) Licha ya hilo, bado watu wengi leo huchagua kwamba hawatajitiisha kwa Mungu. Wao hutaka kuishi wapendavyo. (Efe. 2:1-3) Matokeo ya kufanya hivyo yanaonyesha wazi kwamba “hakuna hekima . . . katika kumpinga Yehova.”—Met. 21:30.

5. Mungu alikuwa na uhakika gani kuhusu wanadamu aliowaumba, na je, alikuwa na msingi wa kuwa na uhakika huo?

5 Hata hivyo, Yehova alijua kwamba baadhi ya wanadamu, kutia ndani vijana wengi wenye sifa nzuri, wangemtafuta na kumtumikia yeye. (Zab. 103:17, 18; 110:3) Anawapenda sana vijana kama hao! Je, unajihesabu kuwa miongoni mwao? Ikiwa ndivyo, bila shaka unafurahia “vitu [vingi] vyema” kutoka kwa Mungu vinavyokufanya uwe na furaha. (Soma Zaburi 103:5; Met. 10:22) Kama tutakavyoona sasa, ‘vitu hivyo vyema’ vinatia ndani chakula kingi kizuri cha kiroho, marafiki bora, malengo yatakayokunufaisha, na uhuru wa kweli.

YEHOVA HUTOSHELEZA UHITAJI WAKO WA KIROHO

6. Kwa nini unapaswa kushughulikia uhitaji wako wa kiroho, na Yehova anakuandaliaje chakula cha kiroho?

6 Tofauti na wanyama, wewe una uhitaji wa kiroho, na ni Muumba wako pekee anayeweza kuutosheleza. (Mt. 4:4) Unapomsikiliza kwa makini, utapata ufahamu, hekima, na furaha. Yesu alisema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.” (Mt. 5:3) Mungu hutosheleza uhitaji wako wa kiroho kupitia Neno lake na chakula kingi cha kiroho anachoandaa kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45) Chakula hicho ni cha aina mbalimbali na chenye lishe kwelikweli!—Isa. 65:13, 14.

7. Taja baadhi ya manufaa utakayopata kwa kujilisha chakula cha kiroho.

7 Chakula cha kiroho ambacho Mungu huandaa kitakusaidia upate hekima na uwezo wa kufikiri utakaokulinda katika njia mbalimbali. (Soma Methali 2:10-14.) Kwa mfano, sifa hizo zitakusaidia utambue mafundisho ya uwongo kama vile fundisho la kwamba hakuna Muumba. Zitakulinda usiathiriwe na uwongo wa kwamba pesa na mali ndiyo siri ya kupata furaha. Pia, zitakusaidia utambue na kupinga tamaa zisizofaa na mazoea yatakayokusababishia madhara. Hivyo, endelea kutafuta hekima inayotoka kwa Mungu na uwezo wa kufikiri, na uendelee kuziona sifa hizo kuwa kama hazina! Kadiri unavyoendelea kusitawisha sifa hizo zenye thamani ndivyo utakavyojionea kibinafsi kwamba Yehova anakupenda na anataka ufurahie mambo mema kabisa maishani.—Zab. 34:8; Isa. 48:17, 18.

8. Kwa nini unapaswa kumkaribia Mungu sasa, nawe utanufaikaje wakati ujao kwa kufanya hivyo?

8 Hivi karibuni, mfumo wote wa ulimwengu wa Shetani utaporomoka, na Yehova pekee ndiye atakayekuwa kimbilio letu. Kwa kweli, huenda wakati utafika ambapo tutahitaji kumtegemea Yehova ili kupata chakula tunachohitaji siku hiyo! (Hab. 3:2, 12-19) Naam, sasa ndio wakati wa kumkaribia Baba yako wa mbinguni na kuendelea kumtumaini hata zaidi. (2 Pet. 2:9) Hata upatwe na jambo gani, ukifanya hivyo, utahisi kama mtunga zaburi, Daudi, aliyeandika hivi: “Ninamweka Yehova mbele yangu daima. Kwa sababu yuko mkono wangu wa kulia, sitatikiswa kamwe.”—Zab. 16:8.

YEHOVA HUKUPATIA MARAFIKI BORA KABISA

9. (a) Kulingana na andiko la Yohana 6:44, Yehova hufanya nini? (b) Ni hali gani ya pekee ambayo huwa miongoni mwa Mashahidi wa Yehova wanapokutana kwa mara ya kwanza?

9 Yehova huwavuta kwake watu anaowakubali kuwa washiriki wa familia yake ya kiroho, naye huwavuta kwa wororo watu wanyoofu kwenye ibada ya kweli. (Soma Yohana 6:44.) Unapokutana kwa mara ya kwanza na mtu ambaye si mwabudu wa Yehova, unajua habari zipi kumhusu? Zaidi ya jina lake na sura yake, huenda unajua mambo machache sana kumhusu. Lakini sivyo ilivyo unapokutana kwa mara ya kwanza na mtu anayemjua Yehova na kumpenda. Hata iwe mtu huyo anatoka katika malezi, nchi, kabila, au tamaduni tofauti na yako, tayari unajua mambo mengi kumhusu, naye pia anajua mambo mengi kukuhusu!

Yehova anataka tuwe na marafiki bora na tujiwekee malengo ya kiroho (Tazama fungu la 9 hadi 12)

10, 11. Watu wa Yehova wanafanana katika njia ipi, na hilo hutunufaishaje?

10 Kwa mfano, unapokutana na Shahidi mwingine, mara moja unatambua kwamba nyote wawili mnazungumza “lugha” moja, yaani, “lugha safi” ya kweli. (Sef. 3:9) Hivyo, kila mmoja wenu anajua mambo ambayo mwenzake anaamini kuhusu Mungu, viwango vya maadili, na tumaini la wakati ujao, miongoni mwa mambo mengine mengi. Isitoshe, hayo ndiyo mambo muhimu zaidi ambayo ungependa kujua kumhusu mtu, mambo ambayo yatakusaidia umwamini. Mambo hayo pia ni msingi wa urafiki mzuri utakaodumu.

11 Hatutilii chumvi kusema kwamba ukiwa mwabudu wa Yehova umezungukwa na marafiki bora zaidi ambao wameenea kotekote ulimwenguni, ingawa hujapata fursa ya kukutana na wengi wao! Ni nani wengine wanaofurahia zawadi hiyo yenye thamani, isipokuwa watu wa Yehova?

YEHOVA HUKUPA MALENGO YATAKAYOKUNUFAISHA

12. Ni malengo gani mazuri ya kiroho unayoweza kujiwekea?

12 Soma Mhubiri 11:9–12:1. Je, una lengo au malengo ya kiroho unayojitahidi kufikia? Huenda unajitahidi kusoma sehemu fulani ya Biblia kila siku. Au labda unajitahidi kuboresha uwezo wako wa kufundisha na kuwa msemaji mzuri. Vyovyote vile, unapoona ukifanya maendeleo au wengine wanapoona maendeleo hayo na kukupongeza, wewe huhisije? Bila shaka unahisi kwamba umetimiza jambo fulani nawe unapata shangwe. Na kwa kweli unapaswa kuhisi hivyo, kwa sababu unamwiga Yesu kwa kutanguliza mapenzi ya Yehova badala ya kutanguliza mambo yako mwenyewe.—Zab. 40:8; Met. 27:11.

13. Tofauti na kufuatia mambo ya ulimwengu huu, kwa nini kumtumikia Mungu ni jambo la pekee lisiloweza kulinganishwa na kitu chochote?

13 Unapojitahidi kufuatia malengo ya kiroho, unatimiza jambo ambalo litakuridhisha kikweli kwa sababu mambo unayotimiza si ya bure. Mtume Paulo aliandika hivi: “Iweni imara, thabiti, sikuzote mkiwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana, mkijua kwamba kazi yenu si ya bure kuhusiana na Bwana.” (1 Kor. 15:58) Tofauti na hilo, maisha ya kufuatia mambo ya ulimwengu huu, hata ikiwa mambo hayo yanatuletea mafanikio makubwa sana, ni maisha yaliyojaa ubatili mtupu. (Luka 9:25) Mfalme Sulemani ni mfano wa mtu aliyejionea ukweli wa jambo hilo, nasi tunajifunza jambo fulani kutoka kwake.—Rom. 15:4.

14. Tunaweza kujifunza nini kutokana na matokeo ambayo Sulemani alipata kwa kufuatia starehe?

14 Kwa kuwa Sulemani alikuwa tajiri kupindukia na alikuwa na mamlaka kubwa, alijiwekea mradi wa ‘kujaribu starehe ili aone ni jambo gani jema litakalokuja.’ (Mhu. 2:1-10) Alijenga nyumba nyingi, akatengeneza mashamba na bustani, na kufuatia chochote ambacho moyo wake ulitamani. Alihisije baada ya kufanya yote hayo? Je, aliridhika? Je, alitosheka? Je, sasa moyo wake ulitulia? Hatuhitaji kukisia. Sulemani mwenyewe anatupatia jibu. Aliandika hivi: “Nilipofikiria kazi zote nilizofanya kwa mikono yangu mwenyewe . . . , niliona kwamba kila kitu kilikuwa ubatili . . . hakukuwa na kitu chochote chenye thamani ya kweli.” (Mhu. 2:11) Hilo ni somo kubwa sana kwetu! Je, utatenda kwa hekima na kulizingatia moyoni mwako?

15. Kwa nini imani ni muhimu, na kuna manufaa gani ya kuwa na imani?

15 Yehova hataki ujifunze kupitia makosa yako mwenyewe na hataki uumie kwa sababu ya kufanya maamuzi yasiyofaa maishani. Ukweli ni kwamba unahitaji kuwa na imani ili umtii Mungu na kutanguliza mapenzi yake maishani. Imani kama hiyo ni yenye thamani sana, nawe hutatamauka kamwe ukiisitawisha. Naam, Yehova hatasahau kamwe “upendo [ulioonyesha] kwa ajili ya jina lake.” (Ebr. 6:10) Hivyo, jitahidi kabisa kujenga imani yenye nguvu, na utajionea mwenyewe kwamba Baba yako wa mbinguni anakujali sana.—Soma Zaburi 32:8.

MUNGU HUKUPA UHURU WA KWELI

16. Kwa nini tunapaswa kuuona uhuru tulio nao kuwa wenye thamani na kuutumia kwa hekima?

16 Paulo aliandika hivi: “Mahali palipo na roho ya Yehova, pana uhuru.” (2 Kor. 3:17) Naam, Yehova ni Mungu anayependa uhuru, nawe pia unapenda uhuru kwa sababu alikuumba hivyo. Hata hivyo, anataka utumie uhuru wako vizuri, na jambo hilo litakulinda. Huenda unajua baadhi ya vijana wanaotazama ponografia au kufanya uasherati, wanaojihusisha na michezo hatari, au wanaotumia dawa za kulevya na kunywa pombe kupita kiasi. Huenda wanapata msisimko au raha ya muda mfupi. Lakini mara nyingi mambo hayo huwagharimu sana kwa sababu huenda wakapata magonjwa, wakawa waraibu, au hata kufa. (Gal. 6:7, 8) Ni wazi kwamba wanajidanganya kuwa wana “uhuru,” lakini uhuru huo huwaletea madhara.—Tito 3:3.

17, 18. (a) Kwa nini kumtii Mungu ni jambo linalotupatia uhuru? (b) Kuna tofauti gani kati ya uhuru ambao Adamu na Hawa walikuwa nao mwanzoni na uhuru ambao wanadamu wanao leo?

17 Kwa upande mwingine, unajua watu wangapi ambao wamekuwa wagonjwa kwa sababu walishikamana na viwango vya Biblia? Ni wazi kwamba kumtii Yehova hutufanya tuwe na afya nzuri na hutupatia uhuru. (Zab. 19:7-11) Isitoshe, unapotumia kwa hekima uhuru ulio nao, yaani, kwa kuzingatia mipaka iliyowekwa na sheria kamilifu za Mungu na kanuni zake, unamwonyesha Mungu na pia wazazi wako kwamba unaweza kutegemeka ukipewa uhuru zaidi. Kwa kweli, Mungu amekusudia kwamba hatimaye atawapa watumishi wake waaminifu uhuru mkamilifu, unaofafanuliwa katika Biblia kuwa “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.”—Rom. 8:21.

18 Adamu na Hawa walikuwa na uhuru kama huo. Walipokuwa katika bustani ya Edeni, Mungu aliwakataza mambo mangapi? Jambo moja tu. Hawakupaswa kula matunda ya mti mmoja tu. (Mwa. 2:9, 17) Je, unaweza kusema kwamba amri hiyo iliwabana au kuwakandamiza? Sivyo hata kidogo! Sasa linganisha amri hiyo moja na sheria nyingi sana zilizotungwa na wanadamu ambazo watu hulazimishwa kuzijua na kuzitii.

19. Yehova na Yesu wanatumia nini ili kutufundisha kuwa watu huru?

19 Yehova hushughulika na watumishi wake kwa hekima sana. Badala ya kutupatia sheria nyingi zisizo na kikomo, anatufundisha kwa subira kufuata sheria ya upendo. Yehova anataka tuishi kulingana na kanuni zake na tuchukie yaliyo mabaya. (Rom. 12:9) Mahubiri ya Mlimani ya Yesu ni mfano mzuri wa mafundisho yanayotusaidia kutumia kanuni kwa sababu yanafunua sababu hasa zinazowafanya watu watende mambo mabaya. (Mt. 5:27, 28) Akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu, Kristo ataendelea kutuelimisha katika ulimwengu mpya ili mtazamo wetu kuhusu uadilifu na uasi sheria ufanane na wake kikamilifu. (Ebr. 1:9) Pia, atatusaidia kufikia ukamilifu kimwili na kiakili. Hebu wazia, wakati huo hutaathiriwa tena na dhambi au kupatwa na matokeo yake mabaya. Ndipo hatimaye utafurahia “uhuru wenye utukufu” ambao Yehova amekuahidi.

20. (a) Yehova hutumiaje uhuru wake? (b) Mfano wa Mungu unaweza kukunufaishaje?

20 Bila shaka hatutawahi kuwa na uhuru usio na mipaka. Sikuzote tutahitaji kutumia uhuru wetu kwa njia inayoonyesha kwamba tunampenda Mungu na wanadamu wenzetu. Kimsingi, Yehova anataka tu tumwige. Yeye ana uhuru usio na mipaka; ingawa hivyo, amechagua kuongozwa na sifa ya upendo anaposhughulika na viumbe wake wenye akili. (1 Yoh. 4:7, 8) Hivyo, tunaweza kufikia mkataa kwamba tutakuwa na uhuru kamili ikiwa tu tutaongozwa na upendo kama wa Mungu.

21. (a) Daudi alihisije kumhusu Yehova? (b) Tutachunguza nini katika makala inayofuata?

21 Je, unathamini ‘vitu vingi vyema’ ambavyo Yehova amekupatia, kama vile chakula tele cha kiroho, marafiki wazuri, malengo yatakayokunufaisha, na tumaini la kupata uhuru mkamilifu? (Zab. 103:5) Ikiwa ndivyo, basi unaweza kukubaliana na sala ya mtunga zaburi iliyo kwenye Zaburi 16:11: “Unanijulisha njia ya uzima. Shangwe tele iko mbele zako; kuna furaha kwenye mkono wako wa kuume milele.” Katika makala inayofuata tutachunguza hazina nyingine zaidi za kiroho zinazopatikana kwenye Zaburi ya 16. Hazina hizo zitatusaidia kuelewa vizuri zaidi siri ya kuwa na maisha yenye kuridhisha kikweli.