Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

‘Yehova Ametutendea kwa Fadhili’

‘Yehova Ametutendea kwa Fadhili’

MIMI pamoja na mke wangu, Danièle, tulikuwa tu tumewasili kwenye hoteli ambayo tungekaa mhudumu wa mapokezi aliponiambia, “Tafadhali wapigie simu polisi wanaolinda mipaka ya nchi.” Saa chache mapema tulikuwa tumeingia nchini Gabon, nchi ya Afrika Magharibi ambako kazi yetu ya kuhubiri ilikuwa imepigwa marufuku katika miaka ya 1970.

Danièle, ambaye alikuwa na akili nyingi, alininong’onezea hivi: “Usijishughulishe kuwapigia simu polisi, tayari wamefika!” Papo hapo, gari likaingia na kusimamishwa nje ya hoteli. Dakika chache baadaye, sote wawili tulikamatwa na wanajeshi. Lakini kwa sababu Danièle alikuwa amenitahadharisha mapema, nilipata nafasi ya kumkabidhi ndugu mwingine nyaraka fulani.

Tulipokuwa tukipelekwa kwenye kituo cha polisi, nilifurahi sana kwamba nilikuwa na mke jasiri na aliyehangaikia mambo ya kiroho. Hiyo ni mojawapo ya pindi nyingi ambazo mimi na Danièle tulifanya mambo kwa ushirikiano. Acheni nieleze sababu zilizofanya tutembelee nchi ambazo kazi yetu ya kuhubiri ilikuwa chini ya vizuizi.

KWA FADHILI YEHOVA ALINIFUNGUA MACHO

Nilizaliwa mwaka wa 1930 katika familia iliyofuata sana dini ya Kikatoliki, kwenye mji mdogo uitwao Croix, kaskazini mwa nchi ya Ufaransa. Familia yetu ilihudhuria misa kila juma, na Baba alijihusisha sana na shughuli za kanisa. Hata hivyo, nilipokuwa nikikaribia umri wa miaka 14, tukio fulani lilinifungua macho nami nikaona unafiki wa viongozi wa kanisa.

Nchi ya Ufaransa ilikuwa chini ya jeshi la Ujerumani wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu. Katika mahubiri yake, kasisi wetu alikuwa na kawaida ya kututia moyo tuunge mkono serikali ya Vichy iliyopendelea utawala wa Wanazi. Mahubiri yake yalitushtua sana. Kama watu wengi nchini Ufaransa walivyokuwa wakifanya, tulisikiliza kisiri kituo cha redio cha BBC, ambacho kilipeperusha habari kuhusu Majeshi ya Muungano. Kisha ghafla kasisi akabadili msimamo wake na katika mwezi wa Septemba 1944 akapanga kuwe na ibada ya kutoa shukrani ili kusherehekea Majeshi ya Muungano yaliyokuwa yakiendelea kudhibiti maeneo mbalimbali nchini Ufaransa. Jambo hilo lilinishtua sana. Nikaanza kuwatilia shaka makasisi.

Muda mfupi baada ya vita, Baba alikufa. Dada yangu mkubwa alikuwa tayari ameolewa na alikuwa akiishi nchini Ubelgiji, hivyo nilihisi kwamba nilikuwa na wajibu wa kumtunza Mama. Nilipata kazi katika kiwanda fulani cha nguo. Mwajiri wangu na wanawe walikuwa Wakatoliki walioshika sana dini. Ingawa nilikuwa na fursa za kupata ufanisi katika kampuni hiyo, punde si punde nilikabili jaribu fulani.

Dada yangu mkubwa Simone, ambaye tayari alikuwa Shahidi, alikuja kututembelea mwaka wa 1953. Akitumia Biblia, alifunua kwa ustadi mafundisho ya uwongo ya Kanisa Katoliki kuhusu moto wa mateso, Utatu, na kutokufa kwa nafsi. Mwanzoni, nilibishana naye kwamba hakuwa akitumia Biblia ya Kikatoliki, lakini baada ya muda mfupi nikasadiki kwamba alikuwa akiniambia ukweli. Baadaye aliniletea matoleo ya zamani ya gazeti la Mnara wa Mlinzi, ambayo niliyasoma kwa bidii usiku kwenye chumba changu cha kulala. Mara moja nilitambua kwamba nimepata kweli; ingawa hivyo, niliogopa kwamba nitapoteza kazi yangu ikiwa ningechukua msimamo upande wa Yehova.

Kwa miezi kadhaa, niliendelea kujifunza Biblia na makala za gazeti la Mnara wa Mlinzi nikiwa peke yangu. Hatimaye niliamua kwenda kwenye Jumba la Ufalme. Upendo niliojionea katika kutaniko ulinigusa sana. Baada ya kujifunza Biblia kwa miezi sita na ndugu mmoja mzoefu, nilibatizwa mwezi wa Septemba 1954. Muda mrefu haukupita nami nikapata shangwe ya kumwona Mama na dada yangu mdogo wakibatizwa na kuwa Mashahidi.

KUMTEGEMEA YEHOVA KATIKA UTUMISHI WA WAKATI WOTE

Kwa kusikitisha, Mama alikufa majuma machache kabla ya kusanyiko la kimataifa la mwaka wa 1958 lililofanyika jijini New York, ambalo nilipata pendeleo la kuhudhuria. Niliporudi, sikuwa tena na majukumu ya familia, hivyo niliacha kazi na kuanza upainia. Katika kipindi hichohicho, nilianza kumchumbia Danièle Delie, dada painia mwenye bidii, na baadaye akawa mke wangu mwezi wa Mei 1959.

Danièle alikuwa ameanza utumishi wa wakati wote mbali na nyumbani kwao katika eneo la mashambani lililoko Brittany. Alihitaji sifa ya ujasiri ili kuhubiri katika eneo hilo lililojaa watu wenye imani ya Kikatoliki na kusafiri kwa baiskeli ili kufika kwenye maeneo ya mashambani. Kama mimi, yeye pia alichochewa na hisi ya uharaka kwani hatukujua mwisho ulikuwa karibu kadiri gani. (Mt. 25:13) Roho yake ya kujidhabihu ilitusaidia kuendelea na utumishi wa wakati wote kwa uvumilivu.

Siku chache baada ya kufunga ndoa, tulipewa mgawo wa kuzungukia makutaniko. Tulijifunza kuzoea maisha ya hali ya chini. Kutaniko la kwanza tulilotembelea lilikuwa na wahubiri 14, na akina ndugu hawakuwa na uwezo wa kutupatia mahali pa kulala. Hivyo, tulitandaza magodoro yetu kwenye jukwaa la Jumba la Ufalme. Kulala chini hakukustarehesha, lakini kulisaidia sana mgongo!

Tulitembelea makutaniko kwa kutumia gari letu dogo

Licha ya ratiba yetu yenye mambo mengi, Danièle alizoea haraka kazi ya kuzungukia makutaniko. Mara kwa mara alilazimika kunisubiri ndani ya gari letu dogo nilipohitaji kufanya mkutano wa dharura pamoja na wazee, lakini hakuwahi kulalamika. Tulizungukia makutaniko kwa miaka miwili tu, na katika kipindi hicho tulijifunza jinsi ilivyo muhimu kwa wenzi wa ndoa kuwasiliana kwa unyoofu na kufanya mambo kwa ushirikiano.—Mhu. 4:9.

TUNAPOKEA MIGAWO MIPYA YA UTUMISHI

Katika mwaka wa 1962, tulialikwa kuhudhuria mtaala wa miezi kumi wa darasa la 37 la Shule ya Gileadi huko Brooklyn, New York. Kati ya wanafunzi 100 waliohudhuria, kulikuwa na wenzi wa ndoa 13, hivyo tulihisi kwamba lilikuwa pendeleo kubwa kuhudhuria tukiwa wenzi wa ndoa. Ningali na kumbukumbu nzuri za jinsi tulivyoshirikiana na akina ndugu waliokuwa kama nguzo za imani, kama vile Frederick Franz, Ulysses Glass, na Alexander H. Macmillan.

Tulifurahia sana kuhudhuria Shule ya Gileadi tukiwa pamoja!

Tulipokuwa shuleni, tulihimizwa tusitawishe uwezo wetu wa kuchunguza mambo yanayotuzunguka. Katika baadhi ya Jumamosi kipindi cha alasiri baada ya masomo kumalizika, mazoezi yetu yalihusisha kutembelea maeneo ya New York City. Tulijua kwamba itakapofika Jumatatu, tutapewa mtihani kuhusu mambo tuliyojionea. Mara nyingi tulirudi tukiwa tumechoka, lakini Mwanabetheli aliyekuwa akitutembeza angetuuliza maswali ya pitio ili kutusaidia kukumbuka mambo makuu kwa ajili ya mtihani. Jumamosi moja tulitembea alasiri nzima huku na kule jijini. Tulitembelea kituo cha kuchunguza nyota na sayari na tulijifunza mambo mengi kuhusu nyota-mkia na vimondo. Tulipokuwa kwenye Jumba la Makumbusho la Historia ya Asili la Marekani, tulijifunza tofauti kati ya mamba wa Marekani (alligator) na mamba wengine. Tuliporudi Betheli, ndugu aliyekuwa akitutembeza alituuliza, “Haya, niambieni tofauti kati ya nyota-mkia na kimondo.” Danièle alikuwa amechoka, hivyo akajibu, “Vimondo vina meno marefu zaidi!”

Tulifurahia kuwatembelea ndugu na dada zetu waaminifu barani Afrika

Tulishangaa sana tulipopokea mgawo wa kutumikia katika ofisi ya tawi ya Ufaransa, ambako tulitumikia pamoja kwa zaidi ya miaka 53. Katika mwaka wa 1976, niliwekwa rasmi kuwa mratibu wa Halmashauri ya Tawi na nikapewa pia mgawo wa kutembelea nchi mbalimbali barani Afrika na Mashariki ya Kati ambako kazi yetu ya kuhubiri ilikuwa chini ya vizuizi au kupigwa marufuku. Mgawo huo ulitufikisha nchini Gabon, ambako kisa kilichotajwa mwanzoni mwa makala hii kilitokea. Kusema kweli, nyakati nyingine nilihisi kwamba sikustahili kushughulikia majukumu hayo ambayo nilipokea bila kutarajia. Lakini Danièle, alikuwa msaada mkubwa sana kwangu kwa sababu alinifanya nihisi kwamba ninaweza kushughulikia mgawo wowote ule.

Nikikalimani hotuba ya Ndugu Theodore Jaracz katika Kusanyiko la “Haki ya Kimungu” jijini Paris, mwaka wa 1988

KUKABILIANA NA JARIBU KUBWA TUKIWA PAMOJA

Tangu mwanzo, tulipenda sana maisha ya Betheli. Danièle, ambaye alikuwa amejifunza Kiingereza kwa miezi mitano tu kabla ya kuhudhuria Shule ya Gileadi, alianza kutumikia akiwa mtafsiri stadi wa machapisho yetu. Tulifurahia sana mgawo wetu wa Betheli, lakini tulipata shangwe nyingi hata zaidi tuliposhirikiana na kutaniko letu. Ningali na kumbukumbu nzuri za wakati ambapo mimi pamoja na Danièle tulisafiri usiku sana kwa treni huko Paris, na ingawa tulikuwa tumechoka, tulikuwa na furaha sana baada ya kujifunza Biblia na watu waliokuwa wakifanya maendeleo ya kiroho. Kwa kusikitisha, afya ya Danièle ilibadilika ghafla na jambo hilo likamzuia kufanya mambo yote ambayo alitamani kufanya.

Katika mwaka wa 1993, uchunguzi ulionyesha kwamba alikuwa na kansa ya matiti. Matibabu yaliyohusisha upasuaji na mfululizo wa matibabu ya kemikali yalimdhoofisha sana. Miaka kumi na tano baadaye aligunduliwa tena kwamba ana kansa, aina ya kansa inayoenea haraka sana. Hata hivyo, alipenda sana kazi yake ya utafsiri hivi kwamba hali yake ilipoimarika kidogo alirudi kazini.

Licha ya ugonjwa huo mbaya sana, mimi na Danièle hatukuwahi kamwe kuwazia kuondoka Betheli. Hata hivyo, unapokuwa mgonjwa ukiwa Betheli, unakabili changamoto za pekee hasa ikiwa wengine hawajui vizuri jinsi hali zilivyo. (Met. 14:13) Hata Danièle alipokuwa akikaribia umri wa miaka 80, uso wake wenye shangwe na uchangamfu wake haukuonyesha hali halisi ya afya yake. Hakujisikitikia. Badala yake, alihangaikia zaidi kuwasaidia wengine. Alijua kwamba watu wanaoteseka hunufaika zaidi mtu anapowasikiliza kwa makini. (Met. 17:17) Danièle hakujiona kuwa mshauri; ingawa hivyo, kupitia mambo aliyopitia aliwasaidia dada wengi wasiogope kansa.

Pia, tulilazimika kukabili changamoto nyingine mpya. Danièle aliposhindwa kufanya kazi kwa siku nzima, alijitahidi kunisaidia katika njia nyingine nyingi. Alijitahidi kufanya maisha yangu yawe rahisi, jambo ambalo liliniwezesha kuendelea kutumikia nikiwa mratibu wa Halmashauri ya Tawi kwa miaka 37. Kwa mfano, kila siku alikuwa na kawaida ya kutayarisha au kuandaa chakula cha mchana ili sote wawili tule pamoja na kisha kupumzika kwa muda mfupi.—Met. 18:22.

KUKABILIANA NA MAHANGAIKO KILA SIKU

Siku zote Danièle alikuwa na mtazamo mzuri sana na alitamani kuendelea kuishi. Kisha akapata kansa kwa mara ya tatu. Tulihisi tumeishiwa na nguvu. Matibabu ya kemikali na ya mionzi yalimlemea sana hivi kwamba nyakati nyingine alishindwa kutembea. Niliumia sana moyoni wakati mke wangu mpendwa, ambaye alikuwa mtafsiri stadi, aliposhindwa kuzungumza vizuri.

Ingawa hatukujua la kufanya, tulidumu katika sala, tukiwa tumesadiki kwamba Yehova hangeruhusu kamwe tuteseke kuliko tunavyoweza kuhimili. (1 Kor. 10:13) Sikuzote tulijitahidi kuthamini msaada ambao Yehova alituandalia kupitia Neno lake, madaktari na wauguzi wa Betheli, na msaada wenye upendo wa ndugu na dada zetu.

Tulimwomba Yehova mara nyingi atupatie mwongozo kuhusu aina ya matibabu tuliyopaswa kukubali. Pindi moja, madaktari hawakujua la kufanya. Daktari aliyekuwa amemsaidia Danièle kwa miaka 23 alishindwa kujua kwa nini Danièle alipoteza fahamu kila baada ya kupokea matibabu ya kemikali. Daktari hakuwa na mapendekezo mengine ya matibabu. Tulihisi tukiwa tumeachwa na hatukujua mambo yatakuwaje. Kisha daktari tofauti wa kansa alikubali kushughulika na hali ya Danièle. Ni kana kwamba Yehova alikuwa ametokeza njia ya kutusaidia kukabiliana na mahangaiko yetu.

Tulijifunza kushughulika na mahangaiko ya leo. Kama Yesu alivyosema, “kila siku ina matatizo yake ya kutosha.” (Mt. 6:34) Pia, mtazamo mzuri na kuwa wacheshi kulitusaidia. Kwa mfano, Danièle alipokaa bila matibabu ya kemikali kwa miezi miwili, aliniambia hivi huku akitabasamu, “Sijawahi kuhisi vizuri kama ninavyohisi sasa!” (Met. 17:22) Licha ya maumivu makali aliyokuwa akipitia, alifurahia sana kujizoeza nyimbo mpya za Ufalme kwa sauti kubwa na yenye nguvu.

Mtazamo wake mzuri ulinisaidia nikabiliane na changamoto mpya nilizopata. Kusema kweli, kwa miaka 57 ambayo tuliishi pamoja, Danièle alishughulikia mahitaji yangu mbalimbali. Hata hakunifundisha jinsi ya kukaanga yai! Hivyo, hali yake ilipomdhoofisha sana, nililazimika kujifunza jinsi ya kuosha vyombo na kufua nguo na vilevile jinsi ya kutayarisha vyakula vyepesi. Tayari nimevunja glasi kadhaa, lakini nilifurahia sana kufanya mambo yaliyomfurahisha. *

TUNAMSHUKURU YEHOVA KWA FADHILI ZAKE ZENYE UPENDO

Ninapotafakari, ninatambua kwamba nimejifunza mambo mengi muhimu kwa sababu ya hali ngumu tulizokabili kutokana na matatizo ya afya na umri kusonga. Kwanza, hatupaswi kuwa wenye shughuli nyingi sana hivi kwamba tunakosa wakati wa kuwa pamoja na mwenzi wetu mpendwa. Tunapaswa kutumia vizuri kabisa miaka ambayo tuna nguvu nyingi kuwatunza watu tunaowapenda. (Mhu. 9:9) Pili, hatupaswi kuwa na wasiwasi kupita kiasi kuhusu mambo madogo; la sivyo, huenda tukashindwa kuona baraka nyingi tunazofurahia kila siku.—Met. 15:15.

Ninapotafakari kuhusu maisha yangu ya utumishi wa wakati wote, sina shaka hata kidogo kwamba Yehova ametubariki kuliko jinsi ambavyo tungeweza kuwazia. Ninahisi kama mtunga zaburi alivyosema: “Yehova amenitendea kwa fadhili.”—Zab. 116:7.

^ fu. 32 Dada Danièle Bockaert alikufa makala hii ilipokuwa ikitayarishwa. Alikuwa na umri wa miaka 78.