Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 49

“Kuna Wakati Uliowekwa” wa Kufanya Kazi na Kupumzika

“Kuna Wakati Uliowekwa” wa Kufanya Kazi na Kupumzika

“Twendeni faraghani mahali pasipo na watu ili mpumzike kidogo.”—MARKO 6:31.

WIMBO 143 Endeleeni Kufanya Kazi, Kukesha, na Kusubiri

MUHTASARI *

1. Watu wengi wana maoni gani kuhusu kazi?

WATU wengi wana maoni gani kuhusu kazi katika eneo unaloishi? Katika nchi nyingi, leo kuliko wakati mwingine wowote, watu hufanya kazi kwa bidii zaidi na kwa saa nyingi zaidi. Watu wanaofanya kazi kupita kiasi hawana muda wa kupumzika, kuwa pamoja na familia zao, au kutosheleza uhitaji wao wa kiroho. (Mhu. 2:23) Kwa upande mwingine, baadhi ya watu hawapendi kufanya kazi na wanatafuta visingizio vya kutofanya kazi.—Met. 26:13, 14.

2-3. Yehova na Yesu wanatuwekea mfano gani inapohusu kazi?

2 Tofauti na mitazamo isiyofaa ya watu leo, fikiria mtazamo wa Yehova na Yesu kuhusu kazi. Hatuna shaka kwamba Yehova anapenda kufanya kazi. Yesu alionyesha hilo wazi aliposema hivi: “Baba yangu anaendelea kufanya kazi mpaka sasa, nami ninaendelea kufanya kazi.” (Yoh. 5:17) Wazia kazi kubwa aliyofanya Mungu alipoumba viumbe wengi wa roho na ulimwengu huu mkubwa. Pia, tunajionea uthibitisho mwingi wa kazi za Mungu za uumbaji katika dunia maridadi tunayoishi. Mtunga-zaburi alisema hivi kwa usahihi: “Jinsi kazi zako zilivyo nyingi sana, Ee Yehova! Umezifanya zote kwa hekima. Dunia imejaa vitu ulivyoumba.”—Zab. 104:24.

3 Yesu alimwiga Baba yake. Akirejelewa kama hekima, Mwana alihusika Mungu “alipozitayarisha mbingu.” (Met. 8:27-31) Baadaye, Yesu alipokuwa duniani, alifanya kazi bora sana. Kazi hiyo ilikuwa kama chakula kwake, na kazi zote alizofanya zilithibitisha kwamba alitumwa na Mungu.— Yoh. 4:34; 5:36; 14:10.

4. Tunajifunza nini kuhusu kupumzika kutoka kwa Yehova na Yesu?

4 Je, mfano wanaotuwekea Yehova na Yesu katika kufanya kazi kwa bidii unamaanisha kwamba hatuhitaji kupumzika? Hapana. Yehova hachoki kamwe hivyo hahitaji kupumzika baada ya kufanya kazi. Hata hivyo, Biblia inasema kwamba baada ya Yehova kuumba mbingu na dunia, ‘alipumzika na kustarehe.’ (Kut. 31:17) Inaelekea hilo lilimaanisha kwamba Yehova alitua na kufurahia mambo aliyoumba. Na ingawa Yesu alifanya kazi kwa bidii alipokuwa duniani, bado alitenga wakati wa kupumzika na kufurahia kula chakula pamoja na rafiki zake.—Mt. 14:13; Luka 7:34.

5. Watu wengi hukabili changamoto gani?

5 Biblia inawatia moyo watu wa Mungu wafurahie kufanya kazi. Watumishi wake wanapaswa kuwa wenye bidii badala ya kuwa wavivu. (Met. 15:19) Huenda unafanya kazi ya kimwili ili kutunza familia yako. Kwa kuongezea, wanafunzi wote wa Kristo wana jukumu la kushiriki katika kazi ya kuhubiri habari njema. Lakini, unahitaji pia kupumzika vya kutosha. Je, nyakati nyingine ni vigumu kwako kuwa na usawaziko inapohusu kazi ya kimwili, huduma, na kupumzika? Tunaweza kujuaje tunapaswa kufanya kazi kwa muda gani na kupumzika kwa muda gani?

JINSI YA KUWA NA USAWAZIKO

6. Andiko la Marko 6:30-34 linaonyeshaje kwamba Yesu alikuwa na usawaziko kuhusu kazi na kupumzika?

6 Ni muhimu sana kuwa na usawaziko inapohusu kazi. Mfalme Sulemani aliongozwa na roho kuandika hivi: “Kuna wakati uliowekwa wa . . . kila shughuli.” Alitaja mambo kama kupanda, kujenga, kulia, kucheka, kucheza dansi, na shughuli nyingine. (Mhu. 3:1-8) Ni wazi kwamba mambo mawili ya msingi katika maisha ni kufanya kazi na kupumzika. Yesu alikuwa na usawaziko ilipohusu kazi na kupumzika. Pindi moja, mitume walikuwa wametoka kuhubiri kwa bidii hivi kwamba “hawakuwa na wakati hata wa kula.” Yesu akawaambia hivi: “Twendeni faraghani mahali pasipo na watu ili mpumzike kidogo.” (Soma Marko 6:30-34.) Ingawa si nyakati zote Yesu na mitume wake waliweza kupumzika vya kutosha, alijua kwamba yeye na mitume wake walihitaji kupumzika.

7. Kuchunguza sheria ya Sabato kutatusaidia jinsi gani?

7 Nyakati nyingine, kwa kweli tunahitaji kupumzika au kubadili ratiba yetu ya kila siku. Tunaelewa hilo kupitia mpango aliofanya Mungu kwa ajili ya watu wake wa kale, yaani, Sabato ya kila juma. Ingawa hatuko chini ya Sheria ya Musa, tunaweza kunufaika kwa kujifunza yale inayosema kuhusu Sabato. Tutakachojifunza kitatusaidia kuchunguza mtazamo wetu kuhusu kazi na kupumzika.

SIKU YA SABATO—WAKATI WA KUPUMZIKA NA KUABUDU

8. Kulingana na Kutoka 31:12-15, siku ya Sabato ilikuwa kwa ajili ya nini?

8 Neno la Mungu linasema kwamba baada ya “siku” sita za uumbaji, Mungu alipumzika kutoka katika kazi yake ya kuumba vitu vilivyomo duniani. (Mwa. 2:2) Yehova anapenda kufanya kazi, naye “anaendelea kufanya kazi” katika njia nyingine. (Yoh. 5:17) Mpango wa Sabato ya kila juma unafuata kielelezo kinachofanana na siku aliyopumzika Yehova inayotajwa katika kitabu cha Mwanzo. Mungu alisema kwamba Sabato ingekuwa ishara kati yake na Waisraeli. Ilikuwa siku ya “pumziko kamili . . . , takatifu kwa Yehova.” (Soma Kutoka 31:12-15.) Amri ya kutofanya kazi ilimhusu kila mtu, kutia ndani watoto, watumwa, na hata wanyama wa kufugwa. (Kut. 20:10) Iliwaruhusu watu kukazia fikira zaidi mambo ya kiroho.

9. Ni mtazamo gani usiofaa uliokuwepo katika siku za Yesu?

9 Siku ya Sabato iliwafaa sana watu wa Mungu; lakini, viongozi wengi wa kidini katika siku za Yesu walikuwa na msimamo mkali, usiobadilika kuhusu siku hiyo. Walidai kwamba katika siku ya Sabato haikuwa halali kuchuma hata masuke ya nafaka au kumponya mgonjwa. (Marko 2:23-27; 3:2-5) Maoni kama hayo hayakupatana na njia ya Mungu ya kufikiri, na Yesu aliwaeleza waziwazi jambo hilo wale waliomsikiliza.

Familia ya Yesu ilitumia siku ya Sabato kukazia fikira mambo ya kiroho (Tazama fungu la 10) *

10. Tunaweza kujifunza nini kuhusu mtazamo wa Yesu kuelekea Sabato katika andiko la Mathayo 12:9-12?

10 Yesu na wafuasi wake Wayahudi walishika Sabato kwa sababu walikuwa chini ya Sheria ya Musa. * Hata hivyo, Yesu alionyesha kwa maneno na matendo yake kwamba walipaswa kushika Sabato kwa njia yenye usawaziko na kwamba matendo yenye fadhili na yaliyowasaidia wengine yaliruhusiwa. Alisema hivi waziwazi: “Ni halali kutenda mema siku ya Sabato.” (Soma Mathayo 12:9-12.) Hakuona kwamba kuonyesha fadhili na kusaidia watu siku ya Sabato kuwa kosa. Matendo ya Yesu yalikazia jambo muhimu kuhusu siku ya Sabato. Kwa kuwa watu wa Mungu walipumzika kutokana na kazi zao za kila siku, waliweza kukazia fikira mambo ya kiroho. Yesu alilelewa katika familia ambayo bila shaka ilitumia siku ya Sabato kujinufaisha kiroho. Hilo linaonekana tunaposoma hivi kumhusu Yesu alipokuwa katika mji wa nyumbani kwao wa Nazareti: “Kulingana na desturi [ya Yesu] siku ya Sabato, akaingia katika sinagogi naye akasimama ili kusoma.”—Luka 4:15-19.

UNA MTAZAMO GANI KUHUSU KAZI?

11. Yesu alikuwa na kielelezo gani kizuri kuhusu kazi?

11 Ni wazi kwamba Yosefu alikuwa na maoni kama ya Mungu kuhusu kazi kwa kuwa alimfundisha Yesu, mwana wake wa kambo, kuwa seremala. (Mt. 13:55, 56) Yesu alimwona Yosefu akifanya kazi kwa bidii kila siku ili kuitegemeza familia yake kubwa. Pindi moja, Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Mfanyakazi anastahili mshahara wake.” (Luka 10:7) Ni wazi kwamba Yesu alijua jinsi ya kufanya kazi ngumu.

12. Ni Maandiko gani yanayoonyesha mtazamo wa Biblia kuhusu kufanya kazi kwa bidii?

12 Mtume Paulo pia alijua jinsi ya kufanya kazi kwa bidii. Kazi yake kuu ilikuwa kutoa ushahidi kumhusu Yesu na ujumbe aliofundisha. Hata hivyo, Paulo alifanya kazi ili kujitegemeza. Wathesalonike walijua kuhusu “kazi ngumu na yenye kutaabisha,” aliyofanya “usiku na mchana” ili asimpe yeyote “mzigo wenye gharama.” (2 The. 3:8; Mdo. 20:34, 35) Huenda Paulo alikuwa akirejelea kazi yake akiwa mtengeneza mahema. Alipokuwa katika jiji la Korintho, alikaa na Akila na Prisila na “kufanya kazi pamoja nao, kwa maana kazi yao ilikuwa ya kutengeneza mahema.” Andiko linaposema kwamba Paulo alifanya kazi “usiku na mchana” halimaanishi kwamba alifanya kazi bila kupumzika. Kwa mfano, hakufanya kazi ya kutengeneza mahema siku ya Sabato. Siku hiyo ilimpa fursa za kutoa ushahidi kwa Wayahudi, ambao pia hawakuwa wakifanya kazi siku ya Sabato.—Mdo. 13:14-16, 42-44; 16:13; 18:1-4.

13. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Paulo?

13 Mtume Paulo ametuwekea mfano mzuri. Alihitaji kufanya kazi ya kimwili; lakini bado alihakikisha kwamba alishiriki kwa ukawaida katika “kazi takatifu ya habari njema ya Mungu.” (Rom. 15:16; 2 Kor. 11:23) Aliwahimiza wengine wafanye hivyo pia. Akila na Prisila walikuwa ‘wafanyakazi wenzake katika Kristo Yesu.’ (Rom. 12:11; 16:3) Paulo aliwahimiza Wakorintho ‘wawe na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.’ (1 Kor. 15:58; 2 Kor. 9:8) Yehova hata alimwongoza mtume Paulo kuandika hivi: “Mtu yeyote asiyetaka kufanya kazi, asile chakula.”—2 The. 3:10.

14. Yesu alimaanisha nini aliposema maneno yanayopatikana kwenye Yohana 14:12?

14 Katika siku hizi za mwisho, kazi ya muhimu zaidi ni kuhubiri na kufanya wanafunzi. Isitoshe, Yesu alitabiri kwamba wanafunzi wake wangefanya kazi kubwa zaidi ya zile alizofanya! (Soma Yohana 14:12.) Hakumaanisha kwamba tungekuwa na uwezo wa kufanya miujiza kama yeye. Badala yake, wafuasi wake wangehubiri na kufundisha katika eneo kubwa zaidi, kwa watu wengi zaidi, na kwa kipindi kirefu zaidi kuliko yeye.

15. Tunapaswa kujiuliza maswali gani, na kwa nini?

15 Ikiwa unafanya kazi ya kimwili, jiulize maswali haya yafuatayo: ‘Je, ninajulikana kuwa mfanyakazi mwenye bidii mahali ninapofanya kazi? Je, ninakamilisha kazi yangu kwa wakati na kwa uwezo wangu wote?’ Ikiwa jibu lako ni ndiyo, basi kuna uwezekano mkubwa kwamba utatumainiwa na mwajiri wako. Pia, utafanya wale wanaokutazama wavutiwe zaidi na ujumbe wa Ufalme. Jiulize maswali yafuatayo kuhusu kazi yetu ya kuhubiri na kufundisha: ‘Je, ninajulikana kuwa mfanyakazi mwenye bidii katika huduma? Je, ninajitayarisha vizuri kwa ajili ya kufanya ziara ya kwanza? Je, ninarudi bila kukawia ili kuzungumza na watu waliopendezwa? Je, ninashiriki kwa ukawaida katika nyanja mbalimbali za huduma?’ Ikiwa jibu lako ni ndiyo, basi utapata shangwe katika kazi yako.

UNA MTAZAMO GANI KUHUSU KUPUMZIKA?

16. Kuna tofauti gani kati ya mtazamo ambao Yesu na mitume wake walikuwa nao kuhusu kupumzika na mtazamo wa watu wengi leo?

16 Yesu alijua kwamba nyakati nyingine yeye na mitume wake walihitaji kupumzika. Hata hivyo, watu wengi katika siku hizo na wengi leo, wanaweza kufananishwa na yule mwanamume tajiri katika mfano wa Yesu. Mwanamume huyo alijiambia hivi: “Starehe, ule, unywe, na ujifurahishe.” (Luka 12:19; 2 Tim. 3:4) Alifikiri kwamba mambo muhimu zaidi maishani ni kupumzika na kustarehe. Tofauti naye, jambo muhimu zaidi katika maisha ya Yesu na mitume wake halikuwa kujipendeza wenyewe.

Kuwa na usawaziko inapohusu kazi na kupumzika kutatusaidia kufanya kazi njema zinazotuburudisha (Tazama fungu la 17) *

17. Tunatumiaje wakati tulio nao baada ya kazi?

17 Leo, tunamwiga Yesu kwa kutotumia wakati tulio nao baada ya kazi kupumzika tu, bali pia tunawahubiria wengine na kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Kwa kweli, kufanya wanafunzi na kuhudhuria mikutano ni muhimu sana kwetu hivi kwamba tunafanya yote tuwezayo ili kushiriki kwa ukawaida katika utendaji huo mtakatifu. (Ebr. 10:24, 25) Hata tunapokuwa likizo, tunadumisha ratiba yetu ya utendaji wa kiroho kwa kuhudhuria mikutano popote pale tulipo na tunatafuta fursa za kuwahubiria watu tunaokutana nao.—2 Tim. 4:2.

18. Mfalme wetu Kristo Yesu, anataka tufanye nini?

18 Tunathamini sana kwamba Mfalme wetu, Kristo Yesu ni mwenye usawaziko na anatusaidia kuwa na usawaziko inapohusu kazi na kupumzika! (Ebr. 4:15) Anataka tupumzike vya kutosha. Lakini pia anataka tuwe na bidii tunapofanya kazi za kimwili na tunaposhiriki katika kazi inayoburudisha ya kufanya wanafunzi. Katika makala inayofuata, tutazungumzia jukumu la Yesu katika kutuweka huru kutokana na aina fulani ya utumwa ulio mbaya sana.

WIMBO 38 Atakupa Nguvu

^ fu. 5 Maandiko yanatufundisha jinsi ya kuwa na usawaziko inapohusu kazi na kupumzika. Kwenye makala hii tutatumia mfano wa Sabato ya kila juma waliyopewa Waisraeli, itakayotusaidia kuchunguza mtazamo wetu kuhusu kazi na kupumzika.

^ fu. 10 Wanafunzi hao waliheshimu sana sheria ya Sabato hivi kwamba waliahirisha kutayarisha manukato ya kutumia katika mwili wa Yesu mpaka siku ya Sabato ilipoisha.—Luka 23:55, 56.

^ fu. 55 MAELEZO YA PICHA: Yosefu akiipeleka familia yake katika sinagogi siku ya Sabato.

^ fu. 57 MAELEZO YA PICHA: Baba anayefanya kazi ili kuitegemeza familia yake, anatumia wakati alio nao baada ya kazi kushiriki katika utendaji wa kitheokrasi hata anapokuwa likizoni pamoja na familia yake.