Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Shetani alipomwambia Hawa kwamba hatakufa ikiwa atakula matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya, je, alikuwa akianzisha wazo la kutokufa kwa nafsi lililoenea leo?

Inaonekana si hivyo. Ibilisi hakumwambia Hawa kwamba akila tunda alilokatazwa na Mungu angeonekana kwamba amekufa lakini sehemu fulani isiyoonekana iliyo ndani yake (sehemu ambayo watu fulani leo huiita nafsi isiyoweza kufa) ingeendelea kuishi mahali pengine. Akizungumza kupitia nyoka, Shetani alidai kwamba ikiwa Hawa angekula matunda ya mti huo, ‘hakika asingekufa’ kabisa. Alikuwa akimaanisha kwamba Hawa angeendelea kuishi, akifurahia maisha bora duniani bila ya kumtegemea Mungu.—Mwa. 2:17; 3:3-5.

Ikiwa fundisho la uwongo la kutokufa kwa nafsi linalofundishwa leo halikuanza katika Edeni, lilianzia wapi? Hatuna uhakika. Tunajua kwamba ibada zote za uwongo zilifutiliwa mbali katika Gharika ya siku za Noa. Hakuna mafundisho yoyote ya uwongo ya kidini yaliyoendelea kufuatwa baada ya Gharika kwa sababu ni Noa na familia yake tu ndio waliokoka, nao walikuwa waabudu wa kweli.

Hivyo basi, fundisho la sasa la kutokufa kwa nafsi ya mwanadamu lazima lilianzishwa mara tu baada ya Gharika. Mungu alipovuruga lugha Babeli na watu wakatawanyika “duniani pote kutoka huko,” ni wazi kwamba waliendeleza wazo la kwamba wanadamu wana nafsi isiyoweza kufa. (Mwa. 11:8, 9) Haidhuru fundisho hilo la uwongo lilianza lini, tunaweza kuwa na hakika kwamba “baba ya uwongo,” Shetani Ibilisi, alihusika na alifurahi sana kuona jinsi lilivyoenea kotekote.—Yoh. 8:44.