Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Biblia inasema kwamba angalau mashahidi wawili wanahitajika ili kuthibitisha jambo. (Hes. 35:30; Kum. 17:6; 19:15; Mt. 18:16; 1 Tim. 5:19) Lakini chini ya Sheria, ikiwa mwanamume angembaka “uwanjani” msichana aliyechumbiwa, na msichana akapiga mayowe, msichana hangekuwa na hatia ya uzinzi lakini mwanamume angekuwa na hatia. Kwa kuwa hakuna mashahidi walioshuhudia ubakaji huo, kwa nini msichana huyo hangekuwa na hatia ingawa mwanamume angekuwa na hatia?

Simulizi linalopatikana katika Kumbukumbu la Torati 22:25-27 halikazii tu kuthibitisha ikiwa mwanamume huyo alikuwa na hatia kwa sababu tayari alikuwa na hatia. Sheria ilikazia kuthibitisha kwamba mwanamke hakuwa na hatia. Acheni tuchunguze muktadha.

Mistari inayotangulia inazungumzia mwanamume aliyefanya ngono “jijini” na mwanamke aliyechumbiwa. Kwa kufanya hivyo, mwanamume huyo alikuwa na hatia ya uzinzi kwa kuwa mwanamke aliyechumbiwa alionwa kuwa amefunga ndoa tayari. Vipi kuhusu mwanamke? “Hakupiga mayowe jijini.” Ikiwa angefanya hivyo, ni wazi kwamba watu wangesikia na kumsaidia. Hata hivyo hakupiga mayowe. Hivyo, alishiriki katika kufanya uzinzi na wote wawili walihukumiwa kuwa na hatia.—Kum. 22:23, 24.

Kisha, Sheria inataja hali tofauti: “Hata hivyo, ikiwa mwanamume huyo alimkuta uwanjani msichana huyo aliyechumbiwa na kumkamata kwa nguvu na kufanya naye ngono, mwanamume huyo aliyelala naye atauawa peke yake, lakini msimtendee lolote msichana huyo. Msichana huyo hajatenda dhambi inayostahili kifo. Kisa chake ni sawa na cha mtu anayemshambulia mwenzake na kumuua. Kwa maana mwanamume huyo alimkuta uwanjani, na msichana huyo aliyechumbiwa akapiga mayowe, lakini hakukuwa na mtu wa kumwokoa.”—Kum. 22:25-27.

Katika kisa hicho, waamuzi walimwamini mwanamke huyo. Kwa nini? Kwa kuwa alisema kwamba alipiga “mayowe, lakini hakukuwa na mtu wa kumwokoa.” Hivyo, hakufanya uzinzi. Lakini mwanamume alikuwa na hatia ya kumbaka na kufanya uzinzi kwa sababu ‘alimkamata kwa nguvu na kufanya ngono’ na mwanamke huyo aliyechumbiwa.

Ingawa sheria hii ilikazia fikira kutokuwa na hatia kwa mwanamke, simulizi linaonyesha wazi kwamba mwanamume alikuwa na hatia ya kubaka na kufanya uzinzi. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba waamuzi ‘walichunguza jambo hilo kikamili’ na kutoa uamuzi kulingana na kiwango alichoweka Mungu waziwazi na alichorudia tena na tena.—Kum. 13:14; 17:4; Kut. 20:14.