Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Toeni Shukrani Kuhusu Kila Jambo”

“Toeni Shukrani Kuhusu Kila Jambo”

JE, WEWE ni mtu mwenye kutoa shukrani? Ni vizuri kila mmoja wetu ajiulize swali hilo. Biblia ilitabiri kwamba katika siku zetu, watu wengi wangekuwa “wasio na shukrani.” (2 Tim. 3:2) Huenda umekutana na watu ambao wanatarajia wengine wawapatie vitu au wafanye mambo kwa faida yao. Ni kama wanahisi kwamba hawahitaji kuwa wenye shukrani kuelekea vitu walivyopewa. Kwa kweli hatungefurahia kushirikiana na watu wenye mtazamo huo.

Hata hivyo, watumishi wa Yehova wanaambiwa hivi: ‘Jionyesheni kuwa wenye shukrani.’ Na tunapaswa ‘kutoa shukrani kuhusu kila jambo.’ (Kol. 3:15; 1 The. 5:18) Kwa kweli, kusitawisha roho ya shukrani ni jambo zuri kwetu. Kuna sababu kadhaa kwa nini inafaa kufanya hivyo.

KUWA NA SHUKRANI NA MAONI YENYE USAWAZIKO KUJIHUSU

Sababu moja ya msingi ya kusitawisha roho ya kuwa na shukrani ni kwamba itatusaidia kuwa na maoni yenye usawaziko kujihusu. Mtu mwenye shukrani hujihisi vizuri na mtu anayepokea shukrani hujihisi vizuri pia. Kwa nini kuwa na shukrani hutufanya sisi na wengine kuwa na furaha? Kwa mfano, mtu anapokufanyia jambo zuri, hilo linaonyesha kwamba anahisi unastahili jambo hilo, sivyo? Anakujali. Unapoona jinsi anavyokujali, hilo litakufanya ujihisi vizuri. Huenda hivyo ndivyo alivyohisi Ruthu. Boazi alimwonyesha ukarimu. Bila shaka hilo lilimfanya Ruthu afurahi kujua kwamba kuna mtu anayemjali.—Rut. 2:10-13.

Ni muhimu hata zaidi kuwa na shukrani kwa Mungu. Bila shaka, pindi fulani umefikiria kuhusu zawadi nyingi za kiroho na za kimwili ambazo amekupatia na anaendelea kukupatia. (Kum. 8:17, 18; Mdo. 14:17) Badala ya kufikiria kwa ufupi tu mambo mema ambayo Mungu amekufanyia, kwa nini usitumie wakati kutafakari kuhusu baraka nyingi ambazo Mungu amekupatia wewe na wapendwa wako? Kufanya hivyo kutaongeza uthamini wako kumwelekea na utajithibitishia hata zaidi kwamba anakupenda na anakuthamini.—1 Yoh. 4:9.

Lakini unapaswa kufanya mengi zaidi ya kutafakari kuhusu ukarimu na baraka zake; mshukuru Yehova kwa wema wake. (Zab. 100:4, 5) Watu husema kwamba “kuwa mwenye shukrani hufanya mtu awe na furaha.”

KUWA NA SHUKRANI HUBORESHA URAFIKI NA WENGINE

Sababu nyingine ya kuwa na shukrani ni kwamba urafiki wetu na wengine utakuwa bora zaidi. Sote tunapenda kuhisi kwamba tunathaminiwa. Unapotoa shukrani kutoka moyoni kwa jambo fulani la fadhili ambalo mtu amekufanyia, urafiki wenu unaimarika zaidi. (Rom. 16:3, 4) Kwa kuongezea, watu wenye shukrani huwa tayari kuwasaidia wengine. Wanatambua pindi wanazoonyeshwa fadhili nao huchochewa kuonyesha fadhili pia. Kwa kweli, kuwasaidia wengine hutufanya tuwe na furaha. Ni kama tu Yesu alivyosema: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”—Mdo. 20:35.

Robert Emmons, msimamizi msaidizi katika Chuo Kikuu cha California katika kitengo cha utafiti kuhusu sifa ya shukrani, alisema hivi: “Ili tuwe wenye shukrani, tunapaswa kuelewa kwamba tunategemeana. Wakati mwingine sisi hutoa na wakati mwingine hupokea.” Ukweli ni kwamba maisha yetu hutegemezwa na watu wengine katika njia nyingi. Kwa mfano, huenda wakatupatia chakula au msaada wa matibabu. (1 Kor. 12:21) Ni wazi kwamba mtu mwenye shukrani huthamini mambo anayofanyiwa na wengine. Hivyo, je, wewe huonyesha shukrani kuelekea mambo ambayo wengine wanakufanyia?

KUONYESHA SHUKRANI NA MTAZAMO WAKO KUHUSU MAISHA

Sababu nyingine ya kusitawisha sifa ya shukrani ni kwamba kuwa na shukrani hutusaidia kukazia fikira mambo mazuri maishani. Kwa njia fulani, akili yako inafanya kazi kama chujio. Inakuruhusu kukazia fikira mambo fulani hususa yanayokuzunguka na wakati uleule kuzuia mambo yasiyofaa. Unaanza kuona mambo yanayofaa na kutokazia fikira matatizo. Kadiri unavyozidi kuwa mwenye shukrani, ndivyo unavyoona mambo kwa njia nzuri zaidi na hilo linakufanya kuwa mwenye shukrani hata zaidi. Kuwa na mtazamo wenye shukrani maishani kutakusaidia kufanya kama vile mtume Paulo aliyesema hivi: “Shangilieni sikuzote katika Bwana.”—Flp. 4:4.

Kuwa mwenye shukrani kutakusaidia kuwa na mtazamo chanya. Ni vigumu sana kuwa mwenye shukrani na wakati uleule kuwa na wivu, huzuni, au hasira. Pia, mara nyingi watu wenye shukrani hawafuatilii vitu vya kimwili. Wanaridhika na vitu walivyo navyo na hawakazii fikira kupata vitu zaidi.—Flp. 4:12.

HESABU BARAKA ZAKO!

Ukiwa Mkristo, unajua kwamba Shetani angependa kukuona ukiwa mwenye huzuni na umevunjwa moyo na matatizo unayokabili katika siku hizi za mwisho. Angependa kukuona ukiwa na mtazamo mbaya na mwenye kulalamika kuhusu kila kitu. Ukiwa na mtazamo kama huo itakuwa vigumu kwa watu kukusikiliza unapohubiri habari njema. Sifa ya shukrani ina uhusiano wa moja kwa moja na tunda la roho ya Mungu kama vile, shangwe inayotokana na mambo mema ambayo Mungu amekupatia na kuwa na imani katika ahadi zake zote.—Gal. 5:22, 23.

Ukiwa mwabudu wa Yehova, unakubaliana na kilichosemwa katika makala hii kuhusu sifa ya shukrani. Hata hivyo, unajua kwamba si rahisi kuwa na mtazamo mzuri na kuonyesha shukrani. Lakini usiruhusu hilo likuvunje moyo. Unaweza kusitawisha na kudumisha mtazamo wenye shukrani. Jinsi gani? Tumia muda kila siku kufikiria mambo fulani maishani mwako yanayokupa sababu ya kuwa na shukrani. Kadiri unavyofanya hivyo ndivyo itakavyokuwa rahisi zaidi kuwa na mtazamo wa kuonyesha shukrani. Kufanya hivyo kutakufanya uwe na furaha zaidi ya wale wanaokazia matatizo yao maishani. Tafakari mambo mazuri ambayo Mungu na wengine wamekufanyia ili kukutia moyo, mambo yanayokufanya uwe na furaha. Unaweza hata kuandika mambo hayo katika kitabu. Andika mambo mawili au matatu yanayofanya uwe na shukrani katika siku hiyo.

Watafiti fulani wanasema kwamba “kuwa na kawaida ya kuonyesha shukrani, huboresha uwezo wa ubongo wa kuwa na mtazamo mzuri kuhusu maisha.” Mtu mwenye shukrani ana furaha zaidi. Hivyo, hesabu baraka zako, furahia mambo mazuri maishani mwako na sikuzote onyesha shukrani! Badala ya kupuuzia mambo mazuri, ‘mshukuru Yehova, kwa maana yeye ni mwema.’ Ndiyo, ‘toa shukrani kuhusu kila jambo.’—1 Nya. 16:34; 1 The. 5:18.