Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 51

Unamjua Yehova Vizuri Kadiri Gani?

Unamjua Yehova Vizuri Kadiri Gani?

“Wale wanaolijua jina lako watakutumaini wewe; hutawaacha kamwe wale wanaokutafuta, Ee Yehova.”—ZAB 9:10.

WIMBO 56 Fanya Kweli Iwe Njia Yako ya Maisha

MUHTASARI *

1-2. Kama mfano wa Angelito unavyoonyesha, kila mmoja wetu anapaswa kufanya nini?

JE, WAZAZI wako ni Mashahidi wa Yehova? Ikiwa ndivyo, kumbuka kwamba huwezi kurithi uhusiano wa karibu na Yehova kutoka kwa wazazi wako. Iwe wazazi wetu wanamtumikia Yehova au la, ni lazima kila mmoja wetu ajenge urafiki wake binafsi pamoja na Yehova.

2 Mfikirie ndugu anayeitwa Angelito. Alilelewa katika familia ya Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, alipokuwa mdogo, hakuhisi akiwa karibu na Mungu. Anakiri hivi: “Nilimtumikia Yehova kwa sababu nilitaka tu kufanya kile ambacho familia yangu ilifanya.” Hata hivyo, Angelito aliamua kutumia wakati mwingi zaidi kusoma na kutafakari Neno la Mungu na akaanza kusali kwa Yehova mara nyingi zaidi. Matokeo yalikuwa nini? Angelito anasema hivi: “Nilijifunza kwamba njia pekee ya kuwa karibu na Baba yangu mpendwa, Yehova, ni mimi binafsi kumjua vizuri zaidi.” Mfano wa Angelito unatokeza maswali fulani muhimu: Kuna tofauti gani kati ya kumfahamu Yehova na kumjua vizuri? Tunaweza kumjua Yehova jinsi gani?

3. Kuna tofauti gani kati ya kujua kumhusu Yehova na kumjua vizuri?

3 Tunaweza kusema kwamba mtu anajua kumhusu Yehova ikiwa analijua jina lake au anafahamu mambo fulani aliyosema au kutenda. Lakini kumjua Yehova vizuri kunahusisha mambo mengi zaidi. Tunahitaji kutumia wakati kujifunza kumhusu Yehova na sifa zake zenye kustaajabisha. Kwa kufanya hivyo tutaanza kuelewa kwa nini anasema na kutenda mambo fulani. Hilo litatusaidia kutambua ikiwa anapendezwa na maoni, maamuzi, na matendo yetu. Tunapotambua mapenzi ya Yehova kutuelekea, tunahitaji kutenda kulingana na mambo tuliyojifunza.

4. Kuchunguza mifano katika Biblia kutatusaidiaje?

4 Huenda baadhi ya watu wakatudhihaki kwa sababu tumeamua kumtumikia Yehova, na huenda wakatupinga hata zaidi tunapoanza kushirikiana na watu wake. Hata hivyo, tukimtumaini Yehova hatatutamausha kamwe. Tutakuwa tukiweka msingi wa urafiki utakaodumu pamoja na Mungu. Je, kweli tunaweza kumjua Yehova vizuri hivyo? Ndiyo tunaweza. Mifano ya wanadamu wasio wakamilifu, kama vile Musa na Mfalme Daudi, inathibitisha kwamba tunaweza kufanya hivyo. Tunapochunguza mambo waliyofanya, tutajibu maswali mawili yafuatayo: Watu hao walimjuaje Yehova? Na tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wao?

MUSA ALIMWONA “YULE ASIYEONEKANA”

5. Musa alichagua kufanya nini?

5 Musa alitenda kulingana na mambo aliyojifunza. Alipokuwa na umri wa miaka 40, Musa alichagua kushirikiana na Waisraeli, watu wa Mungu, badala ya kujulikana kuwa “mwana wa binti ya Farao.” (Ebr. 11:24) Musa aliacha cheo chake cha juu. Kwa kuamua kushirikiana na Waisraeli, ambao walikuwa watumwa nchini Misri, angekabili hasira ya Farao, mtawala mwenye nguvu ambaye alionwa kuwa mungu. Hilo lilikuwa tendo la imani kwelikweli! Musa alimtumaini Yehova. Na hilo ndilo jiwe la msingi katika kujenga urafiki unaodumu.—Met. 3:5.

6. Mfano wa Musa unatufundisha nini?

6 Tunajifunza nini? Kama Musa, sisi sote tunahitaji kufanya uamuzi: Je, tutachagua kumtumikia Mungu na kushirikiana na watu wake? Huenda tukahitaji kujidhabihu ili kumtumikia Mungu, na tukakabili upinzani kutoka kwa wale wasiomjua Yehova. Hata hivyo, tukimtumaini Baba yetu wa mbinguni, tunaweza kuwa na hakika kwamba atatutegemeza!

7-8. Musa aliendelea kujifunza nini?

7 Musa aliendelea kujifunza kuhusu sifa za Yehova na kufanya mapenzi Yake. Kwa mfano, Musa alipoambiwa aliongoze taifa la Israeli kutoka utekwani, alikosa ujasiri hivi kwamba akamwambia Yehova tena na tena kwamba alihisi hastahili. Mungu alimwonyesha Musa huruma na kumpatia msaada. (Kut. 4:10-16) Matokeo ni kwamba Musa aliweza kufikisha jumbe nzito za hukumu kwa Farao. Kisha, Musa alijionea jinsi Yehova alivyotumia nguvu zake alipowaokoa Waisraeli na kumwangamiza Farao na majeshi yake katika Bahari Nyekundu.—Kut. 14:26-31; Zab. 136:15.

8 Baada ya Musa kuwaongoza Waisraeli kutoka Misri, walilalamika tena na tena kuhusu mambo mengi. Hata hivyo, Musa alijionea jinsi ambavyo Yehova alishughulika kwa subira na watu wake aliowakomboa kutoka katika utumwa. (Zab. 78:40-43) Pia, Musa alijionea jinsi Yehova alivyoonyesha unyenyekevu wa pekee alipobadili maoni Yake baada ya Musa kumwomba afanye hivyo.—Kut. 32:9-14.

9. Kulingana na andiko la Waebrania 11:27, uhusiano wa Musa pamoja na Yehova ulikuwa wa karibu kadiri gani?

9 Baada ya Waisraeli kukombolewa kutoka Misri, Musa alikuwa na uhusiano wa karibu sana na Yehova hivi kwamba ni kama alimwona Baba yake wa mbinguni. (Soma Waebrania 11:27.) Inapofafanua jinsi uhusiano huo ulivyokuwa wa karibu sana, Biblia inasema hivi: “Yehova aliongea na Musa uso kwa uso, kama mwanadamu anavyoongea na mwanadamu mwenzake.”—Kut. 33:11.

10. Tunapaswa kufanya nini ili tumjue Yehova vizuri?

10 Tunajifunza nini? Ili tumjue Yehova vizuri, hatupaswi tu kujifunza kuhusu sifa zake, bali pia tunapaswa kufanya mapenzi yake. Leo, mapenzi ya Yehova ni kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Tim. 2:3, 4) Njia moja ya kufanya mapenzi ya Mungu ni kwa kuwafundisha wengine kumhusu Yehova.

11. Tunapowafundisha wengine kumhusu Yehova, tunamjuaje vizuri zaidi?

11 Mara nyingi tunapowafundisha wengine kumhusu Yehova, sisi wenyewe huzidi kumjua vizuri zaidi. Kwa mfano, tunajionea sifa ya Yehova ya huruma anapotuongoza kwa wale wenye mioyo minyoofu. (Yoh. 6:44; Mdo. 13:48) Tunajionea nguvu za Neno la Mungu zikifanya kazi wakati wale ambao tunajifunza nao wanaacha mazoea mabaya na kuanza kuvaa utu mpya. (Kol. 3:9, 10) Na tunaona uthibitisho wa subira ya Mungu anapowapa wengi katika eneo letu fursa ya kujifunza kumhusu na kuokolewa.—Rom. 10:13-15.

12. Kama inavyoonyeshwa kwenye andiko la Kutoka 33:13, Musa aliomba nini, na kwa nini?

12 Musa alithamini sana uhusiano wake na Yehova. Hata baada ya kufanya miujiza yenye nguvu katika jina la Mungu, Musa kwa heshima aliomba ruhusa ya kumjua Yehova vizuri zaidi. (Soma Kutoka 33:13.) Musa alikuwa na umri wa miaka 80 alipotoa ombi hilo, lakini alitambua kwamba bado alikuwa na mengi ya kujifunza kumhusu Baba yake wa mbinguni mwenye upendo.

13. Taja njia moja inayothibitisha kwamba tunathamini urafiki wetu na Mungu.

13 Tunajifunza nini? Haijalishi tumemtumikia Yehova kwa muda mrefu kadiri gani, hatupaswi kamwe kuchukulia kivivihivi uhusiano wetu pamoja naye. Njia moja ya kuthibitisha kwamba tunathamini urafiki wetu na Mungu ni kwa kuzungumza naye katika sala.

14. Kwa nini sala ni njia muhimu ya kujifunza mengi zaidi kumhusu Mungu?

14 Mawasiliano mazuri ndio msingi wa uhusiano wenye nguvu. Hivyo, mkaribie Mungu kwa kusali kwa ukawaida, bila kuogopa kumweleza hisia zako za ndani kabisa. (Efe. 6:18) Krista, dada anayeishi Uturuki, anasema hivi: “Upendo na imani yangu kwa Yehova huzidi kukua kila mara ninapomweleza hisia zangu katika sala na kuona jinsi anavyonisaidia. Kujionea jinsi Yehova anavyojibu sala zangu kumenisaidia nimwone Yehova kuwa Baba na Rafiki yangu.”

MTU ALIYEUPENDEZA MOYO WA YEHOVA

15. Yehova alimfafanuaje Mfalme Daudi?

15 Mfalme Daudi alizaliwa katika taifa lililokuwa wakfu kwa Yehova Mungu. Lakini Daudi alifanya mengi zaidi ya kufuata tu mapokeo ya dini ya familia yao. Alijenga uhusiano wake binafsi na Mungu, na Yehova alimpenda sana. Yehova alimfafanua Daudi kuwa ‘mtu aliyeupendeza moyo wake.’ (Mdo. 13:22) Ni nini kilichomsaidia Daudi kuwa na uhusiano wa karibu hivyo na Yehova?

16. Daudi alijifunza nini kumhusu Yehova alipotazama uumbaji?

16 Daudi alijifunza kumhusu Yehova kupitia uumbaji. Daudi alipokuwa kijana, alitumia saa nyingi nje akichunga kondoo za baba yake. Huenda katika pindi hizo alianza kutafakari kuhusu uumbaji wa Yehova. Kwa mfano, Daudi alipotazama angani usiku, hakujionea nyota nyingi tu bali pia alitambua sifa za Yule aliyeziumba. Daudi alichochewa kuandika hivi: “Mbingu zinatangaza utukufu wa Mungu; na anga lililo juu linatangaza kazi ya mikono yake.” (Zab. 19:1, 2) Daudi alipotafakari jinsi wanadamu walivyoumbwa, alijionea hekima yenye kustaajabisha ya Yehova. (Zab. 139:14) Daudi alinyenyekezwa sana alipotafakari kazi za Yehova.—Zab. 139:6.

17. Tunaweza kujifunza nini tunapotafakari kuhusu uumbaji?

17 Tunajifunza nini? Pendezwa na uumbaji. Fanya mengi zaidi ya kuishi tu katika dunia hii nzuri iliyoumbwa na Yehova; staajabishwa na uumbaji! Katika maisha yako ya kila siku, tafakari mambo unayojifunza kumhusu Yehova kupitia uumbaji unaokuzunguka, kama vile mimea, wanyama, na watu. Kisha, kila siku mpya utajifunza mambo mengi kumhusu Baba yako anayekupenda. (Rom. 1:20) Na kila siku utajionea upendo wako kumwelekea ukikua zaidi na zaidi.

18. Kama inavyoonyeshwa kwenye Zaburi ya 18, Daudi alitambua nini?

18 Daudi alitambua kwamba Yehova alikuwa akimsaidia. Kwa mfano, Daudi alipolinda kondoo za baba yake dhidi ya simba na dubu, alitambua kwamba Yehova ndiye aliyemsaidia kukabiliana na wanyama hao wakali. Aliposhinda lile jitu shujaa la vita, Goliathi, Daudi alitambua waziwazi kwamba Yehova ndiye aliyekuwa akimwongoza. (1 Sam. 17:37) Na alipomtoroka Mfalme Sauli mwenye wivu, Daudi alitambua kwamba Yehova ndiye aliyemwokoa. (Zab. 18, utangulizi) Ikiwa Daudi angekuwa mwenye kiburi, angeona kwamba mambo yote aliyotimiza ni kwa uwezo wake. Lakini Daudi alikuwa mnyenyekevu, hivyo aliweza kuutambua mkono wa Yehova katika maisha yake.—Zab. 138:6.

19. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Daudi?

19 Tunajifunza nini? Tunahitaji kufanya mengi zaidi ya kuomba tu msaada wa Yehova. Tunapaswa pia kutambua wakati na njia anayotumia kutupatia msaada. Tukitambua kwa unyenyekevu mipaka yetu, tutaona wazi kwamba Yehova anatupatia kile tunachohitaji. Na kila mara tunapoona Yehova akitusaidia, uhusiano wetu naye unaimarika zaidi. Isaac, ndugu anayeishi Fiji, na ambaye amemtumikia Yehova kwa miaka mingi, alijionea ukweli wa maneno hayo. Anasema hivi: “Ninapokumbuka maisha yangu, ninaona jinsi Yehova alivyonisaidia tangu nilipoanza kujifunza Biblia mpaka sasa. Hivyo, ninamwona Yehova kuwa halisi.”

20. Tunajifunza nini kutokana na uhusiano wa Mungu na Daudi?

20 Daudi aliiga sifa za Yehova. Yehova alituumba tukiwa na uwezo wa kuiga sifa zake. (Mwa. 1:26) Kadiri tunavyojifunza mengi kuhusu sifa za utu wa Yehova, ndivyo tutakavyoweza kumwiga vizuri zaidi. Daudi alimjua Baba yake wa Mbinguni vizuri, hivyo aliweza kumwiga aliposhughulika na wengine. Fikiria mfano mmoja. Daudi alifanya dhambi dhidi ya Yehova alipofanya uzinzi na Bath-sheba na kisha kusababisha kifo cha mume wake. (2 Sam. 11:1-4, 15) Lakini Yehova aliamua kumwonyesha Daudi rehema, mwanamume ambaye alikuwa amewaonyesha wengine rehema. Kwa kuwa Daudi alikuwa na uhusiano mzuri sana na Yehova, alikuja kuwa miongoni mwa wafalme wa Israeli waliopendwa zaidi na watu, na Yehova alimtumia kuwa kielelezo kwa wafalme wengine wa Israeli.—1 Fal. 15:11; 2 Fal. 14:1-3.

21. Kulingana na Waefeso 4:24 na 5:1, tutapata matokeo gani tunapokuwa “waigaji wa Mungu”?

21 Tunajifunza nini? Tunahitaji kuwa “waigaji wa Mungu.” Kufanya hivyo kutatunufaisha na pia kutatusaidia kumjua vizuri. Tunapopatanisha utu wetu na utu wa Mungu, tunathibitisha kwamba sisi ni watoto wake.—Soma Waefeso 4:24; 5:1.

JITAHIDI KUMJUA YEHOVA VIZURI ZAIDI

22-23. Tutapata matokeo gani tunapotumia mambo tunayojifunza kumhusu Yehova?

22 Kama tulivyoona, Yehova hujifunua kwetu kupitia uumbaji na Neno lake, Biblia. Kitabu hicho cha pekee kina mifano mingi ya watumishi waaminifu wa Mungu ambao tunaweza kuwaiga, kama vile Musa na Daudi. Yehova amefanya sehemu yake. Tunahitaji kufungua macho, masikio, na moyo wetu ili tujifunze mengi zaidi kumhusu.

23 Hakuna mwisho wa kujifunza kumhusu Yehova. (Mhu. 3:11) Jambo muhimu si ujuzi tulio nao kumhusu, bali jinsi tunavyotumia ujuzi huo. Ikiwa tutatumia yale tunayojifunza na kujitahidi kumwiga Baba yetu anayetupenda, ataendelea kutukaribia. (Yak. 4:8) Anatuhakikishia kupitia Neno lake kwamba hatawaacha kamwe wale wanaojitahidi kumtafuta.

WIMBO 80 “Onjeni Mwone Kwamba Yehova Ni Mwema”

^ fu. 5 Watu wengi wanaamini kwamba Mungu yupo, lakini hawamjui vizuri. Kumjua Yehova kunamaanisha nini, na tunaweza kujifunza nini kutoka kwa Musa na Mfalme Daudi kuhusu jinsi ya kujenga urafiki wa karibu pamoja na Yehova? Makala hii itajibu maswali hayo.