Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 52

Wazazi—Wafundisheni Watoto Wenu Kumpenda Yehova

Wazazi—Wafundisheni Watoto Wenu Kumpenda Yehova

“Watoto ni urithi kutoka kwa Yehova.”ZAB. 127:3.

WIMBO 134 Watoto—Amana Kutoka kwa Mungu

MUHTASARI *

1. Yehova amewapa wazazi jukumu gani?

YEHOVA aliumba wenzi wa ndoa wa kwanza wakiwa na tamaa ya kuwa na watoto. Biblia inasema hivi: “Watoto ni urithi kutoka kwa Yehova.” (Zab. 127:3) Hilo linamaanisha nini? Tuseme kwamba rafiki yako wa karibu anakuomba umtunzie kiasi kikubwa cha pesa. Ungehisije? Huenda, ungehisi anakuheshimu kwa kuwa anakutumaini. Lakini huenda ukawa na wasiwasi kuhusu usalama wa pesa hizo nyingi. Rafiki yetu wa karibu, Yehova, amewapa wazazi kitu cha kutunza chenye thamani kubwa kuliko pesa. Amewapa jukumu la kuhakikisha kwamba watoto wao wanatunzwa vizuri na wana furaha.

2. Tutazungumzia maswali gani?

2 Ni nani anayepaswa kuamua ikiwa wenzi wa ndoa wanapaswa kuzaa watoto na ni wakati gani wafanye hivyo? Na wazazi wanaweza kufanya nini ili watoto wao wawe na furaha maishani? Fikiria baadhi ya kanuni zinazopatikana katika Neno la Mungu ambazo zitawasaidia wenzi wa ndoa Wakristo kufanya maamuzi ya hekima.

HESHIMU UAMUZI WA WENZI WA NDOA

3. (a) Ni nani anayepaswa kuamua ikiwa wenzi wa ndoa watapata watoto? (b) Ni kanuni gani ya Biblia ambayo marafiki na watu wa familia wanapaswa kukumbuka?

3 Katika tamaduni fulani, wenzi wapya wa ndoa wanatarajiwa kuanza kuzaa watoto mapema iwezekanavyo. Huenda wakahisi kwamba familia zao na wengine wanawashinikiza kufuata desturi hiyo. Jethro, ndugu kutoka bara la Asia anasema hivi: “Baadhi ya wenzi wa ndoa wenye watoto kutanikoni, huwashinikiza wale ambao hawana watoto kuanzisha familia.” Jeffrey, ndugu mwingine kutoka Asia, anasema hivi: “Wengine huwaambia wenzi wa ndoa ambao hawana watoto kwamba watakapozeeka watakosa mtu wa kuwatunza.” Hata hivyo, wenzi wa ndoa wanapaswa kuamua wenyewe ikiwa watakuwa na watoto au la. Wao ndio wanaopaswa kufanya uamuzi huo; ni wajibu wao. (Gal. 6:5, maelezo ya chini) Ni kweli kwamba marafiki na watu wa familia wangependa wenzi hao wapya wawe na furaha. Hata hivyo, wanahitaji kukumbuka kwamba uamuzi wa kuwa na watoto au la ni wa wenzi hao.—1 The. 4:11.

4-5. Wenzi wa ndoa wanahitaji kuzungumzia mambo gani mawili na ni wakati gani unaofaa zaidi kufanya hivyo? Eleza.

4 Ingefaa kwa wenzi wa ndoa wanaoamua kuwa na watoto kujadili maswali haya mawili muhimu: Kwanza, ni wakati gani wangependa kuanzisha familia? Pili, wangependa kuwa na watoto wangapi? Ni wakati gani unaofaa kwa wenzi hao wa ndoa kuzungumzia mambo hayo? Na kwa nini maswali hayo mawili ni muhimu sana?

5 Kabla ya kufunga ndoa, ingefaa wenzi hao wazungumzie suala la kupata watoto. Kwa nini? Kwa sababu ni jambo la muhimu sana wakubaliane kuhusu jambo hilo. Pia, wanapaswa kuchunguza ikiwa wako tayari kubeba jukumu hilo. Baadhi ya wenzi wa ndoa wameamua kupata watoto mwaka mmoja au miwili baada ya kufunga ndoa. Wanafanya hivyo ili wajipatie muda wa kuzoea maisha ya ndoa. Kufanya hivyo kunawapa nafasi ya kuwa na uhusiano wa karibu zaidi kabla ya kuwa wazazi, daraka linalohitaji muda na nguvu nyingi.—Efe. 5:33.

6. Nyakati tunazoishi zimefanya baadhi ya wenzi wa ndoa wafanye uamuzi gani?

6 Wakristo wengine wameamua kufuata kielelezo cha wana watatu wa Noa na wake zao. Wenzi hao hawakupata watoto mara moja. (Mwa. 6:18; 9:18, 19; 10:1; 2 Pet. 2:5) Yesu alifananisha siku zetu na “siku za Noa,” na hatuna shaka kwamba tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (Mt. 24:37; 2 Tim. 3:1) Kwa sababu hiyo, baadhi ya wenzi wameamua kuahirisha kuwa na watoto ili waweze kutumia muda mwingi zaidi kushiriki katika huduma ya Kikristo.

Wanapoamua ikiwa watakuwa na watoto au la na idadi ya watoto hao, wenzi wa ndoa wenye hekima ‘huhesabu gharama’ kwanza (Tazama fungu la 7) *

7. Kanuni zinazopatikana katika Luka 14:28, 29 na Methali 21:5 zinawezaje kuwasaidia wenzi wa ndoa?

7 Wanapoamua ikiwa watakuwa na watoto au la na idadi ya watoto hao, wenzi wa ndoa wenye hekima ‘huhesabu gharama’ kwanza. (Soma Luka 14:28, 29.) Wazazi wenye uzoefu wanajua kwamba kupata na kulea watoto kunagharimu pesa, wakati na nguvu. Hivyo, ni muhimu kwa wenzi wa ndoa kujiuliza maswali yafuatayo: ‘Je, sote tutahitaji kufanya kazi ili kutimiza mahitaji ya msingi ya familia? Je, tunakubaliana ni mahitaji gani ya msingi ambayo familia yetu inahitaji? Ikiwa sote tutahitaji kufanya kazi, nani atawalea watoto? Nani atawasaidia kufikiri na kutenda katika njia inayofaa?’ Wenzi wanapozungumzia maswali hayo kwa utulivu hutumia maneno ya Methali 21:5.Soma.

Mume mwenye upendo atafanya yote awezayo kumsaidia mke wake (Tazama fungu la 8)

8. Wenzi Wakristo watarajie kukabili changamoto gani, na mume mwenye upendo hufanya nini?

8 Kila mzazi anapaswa kutumia nguvu na wakati wa kutosha pamoja na mtoto. Hivyo, ikiwa wenzi watapata watoto katika kipindi kifupi cha wakati, huenda ikawa changamoto kwao kumlea kila mtoto ipasavyo. Baadhi ya wenzi wa ndoa waliopata watoto ndani ya kipindi kifupi cha wakati walisema kwamba walihisi wamelemewa. Mama anaweza kuhisi kuwa amechoka kimwili na kihisia. Jambo hilo linaweza kuathiri uwezo wake wa kujifunza, kusali, na kushiriki huduma kwa ukawaida. Changamoto nyingine ni kukazia fikira na kunufaika na mikutano ya Kikristo. Ni kweli kwamba mume mwenye upendo atafanya yote awezayo kumsaidia mke wake kulea watoto iwe katika mikutano na hata nyumbani. Kwa mfano, anaweza kumsaidia mke wake kufanya kazi za nyumbani. Atafanya yote awezayo ili kuhakikisha kwamba familia yake inanufaika na programu ya kawaida ya Ibada ya Familia. Pia, baba Mkristo atashiriki na familia yake katika huduma ya shambani kwa ukawaida.

KUWAFUNDISHA WATOTO KUMPENDA YEHOVA

9-10. Wazazi wanaweza kufanya nini ili kuwasaidia watoto wao?

9 Wazazi wanaweza kufanya mambo gani ili kuwasaidia watoto wao kujifunza kumpenda Yehova? Wazazi wanaweza kufanya nini ili kuwalinda watoto wao dhidi ya maadili yaliyopotoka ya ulimwengu huu? Fikiria baadhi ya hatua ambazo wazazi wanaweza kuchukua.

10 Sali kwa Yehova ukiomba msaada wake. Ona kielelezo cha Manoa na mke wake waliokuja kuwa wazazi wa Samsoni. Manoa alipotambua kwamba yeye na mke wake wangepata mwana, walimsihi Yehova awape mwongozo wa jinsi ya kumlea mtoto wao.

11. Wazazi wanaweza kuiga jinsi gani mfano wa Manoa kama inavyotajwa katika Waamuzi 13:8?

11 Nihad na Alma wanaoishi Bosnia na Herzegovina walijifunza kutokana na mfano wa Manoa. Wanasema hivi: “Sawa na Manoa, tulimsihi Yehova atupe mwongozo wa jinsi ya kuwa wazazi wazuri. Yehova alijibu sala zetu kupitia njia nyingi kama vile, Maandiko, machapisho yanayotegemea Biblia, mikutano ya kutaniko na makusanyiko.”—Soma Waamuzi 13:8.

12. Yosefu na Maria waliwawekea mfano gani watoto wao?

12 Fundisha kwa kuweka mfano. Ni kweli kwamba mambo unayosema ni ya muhimu, hata hivyo mambo utakayofanya huenda yakawa na matokeo makubwa zaidi kwa mtoto wako. Tuna uhakika kwamba Yosefu na Maria waliwawekea mfano mzuri sana watoto wao kutia ndani Yesu. Yosefu alifanya kazi kwa bidii ili kuitunza familia yake. Kwa kuongezea, Yosefu alitia moyo familia yake kuthamini mambo ya kiroho. (Kum. 4:9, 10) Ijapokuwa kulingana na Sheria Yosefu hakuhitajiwa kuipeleka familia yake Yerusalemu “kila mwaka” ili kusheherekea Pasaka, bado alifanya hivyo. (Luka 2:41, 42) Katika siku zake, baadhi ya akina baba huenda waliona safari hiyo ya familia nzima kuwa usumbufu, inayopoteza muda, na yenye gharama kubwa. Hata hivyo, ni wazi kwamba Yosefu alithamini mambo ya kiroho, naye aliwafundisha watoto wake kufanya hivyo. Pia, Maria aliyajua vizuri Maandiko. Ni wazi kwamba Maria aliwafundisha watoto wake kulipenda Neno la Mungu kupitia maneno na matendo yake.

13. Wenzi wa ndoa fulani walifuata jinsi gani mfano wa Yosefu na Maria?

13 Nihad na Alma, waliotajwa mapema, walifuata mfano wa Yosefu na Maria. Kufanya hivyo kuliwasaidia jinsi gani kumfundisha mwana wao kumpenda na kumtumikia Mungu? Wanasema hivi: “Kupitia maisha yetu, tulijitahidi kumwonyesha mwana wetu jinsi ilivyo vema kuishi kulingana na kanuni za Yehova.” Nihad anaongeza: “Jitahidi kuwa aina ya mtu ambaye unataka mtoto wako awe.”

14. Kwa nini wazazi wanahitaji kujua watoto wao wanashirikiana na nani?

14 Wasaidie watoto wako wachague marafiki wazuri. Wazazi wote wanapaswa kujua watoto wao wanashirikiana na nani na wanafanya nini. Hilo linatia ndani wazazi kujua watoto wao wanawasiliana na nani kupitia mitandao ya kijamii na simu zao. Njia ya watoto ya kufikiri na kutenda inaweza kuathiriwa na wale wanaoshirikiana nao.—1 Kor. 15:33.

15. Wazazi wanaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Jessie?

15 Wazazi wanaweza kufanya nini ikiwa hawajui kutumia kompyuta au vifaa vya mkononi? Jessie, baba anayeishi nchini Ufilipino, anasema hivi: “Hatukujua mengi kuhusu teknolojia. Lakini hilo halikutuzuia kuwasaidia watoto wetu wajue hatari za kutumia vifaa vya kielektroni.” Jessie hakupiga marufuku watoto kutumia vifaa hivyo eti kwa kuwa hakujua kuvitumia. Anaeleza hivi: “Niliwatia moyo watoto wangu kutumia vifaa vya kielektroni ili kujifunza lugha mpya, kujitayarisha kwa ajili ya mikutano, na kusoma Biblia kila siku.” Ikiwa wewe ni mzazi, je, umesoma na kuzungumza na watoto wako kuhusu ushauri mzuri kuhusu kutuma jumbe na picha mtandaoni unaopatikana kwenye sehemu ya “Matineja” kwenye tovuti ya jw.org®? Je, umetazama pamoja nao video Je, Vifaa Vyako Vinakudhibiti? na Tumia Mitandao ya Kijamii kwa Hekima? * Habari hizo zitafaa sana unapowafundisha watoto wako jinsi ya kutumia kwa hekima vifaa vya kielektroni.—Met. 13:20.

16. Wazazi wengi wamefanya nini, na matokeo yamekuwa nini?

16 Wazazi wengi hujitahidi kutafuta fursa ili watoto wao washirikiane na watu wenye mfano mzuri katika kumtumikia Mungu. Kwa mfano, N’Déni na Bomine, wenzi wa ndoa wanaoishi nchini Côte d’Ivoire, mara nyingi walialika mwangalizi wa mzunguko kufikia nyumbani kwao. N’Déni anasema hivi: “Kufanya hivyo kulimsaidia sana mwana wetu. Alianza upainia na sasa anatumikia akiwa mwangalizi wa mzunguko wa badala.” Je, unaweza kuandaa fursa kama hizo kwa ajili ya watoto wako?

17-18. Wazazi wanapaswa kuanza lini kufundisha watoto wao?

17 Anza kuwazoeza watoto mapema iwezekanavyo. Ili kupata matokeo mazuri, wazazi wanapaswa kuanza mapema kuwazoeza watoto wao. (Met. 22:6) Mfikirie Timotheo ambaye baadaye alianza kusafiri na mtume Paulo. Eunike, mama ya Timotheo, na Loisi nyanya yake, walimzoeza Timotheo “tangu utoto mchanga.”—2 Tim. 1:5; 3:15.

18 Wenzi wengine kutoka nchini Côte d’Ivoire, Jean-Claude na Peace waliweza kulea watoto wao wote sita na kuwasaidia wampende na kumtumikia Yehova. Ni nini kilichowasaidia wafanikiwe? Walifuata mfano wa Eunike na Loisi. Wanasema hivi: “Tulikazia Neno la Mungu kwa watoto wetu tangu walipokuwa wachanga, muda mfupi tu walipozaliwa.”—Kum. 6:6, 7.

19. Kukazia Neno la Mungu akilini mwa watoto wako kunamaanisha nini?

19 Ni nini maana ya ‘kukazia’ Neno la Yehova akilini mwa watoto wako? ‘Kukazia’ kunamaanisha “kufundisha na kukazia jambo kwa kurudia-rudia.” Ili kufanya hivyo, wazazi wanapaswa kuwa na kawaida ya kutumia wakati pamoja na watoto wao. Huenda nyakati nyingine wazazi wakavunjika moyo kwa sababu ya kurudia-rudia maagizo kwa watoto wao. Hata hivyo, wazazi wanaweza kuona jambo hilo kuwa njia ya kuwasaidia watoto wao kuelewa na kulitumia Neno la Mungu.

Wazazi wanapaswa kujua jinsi ya kumzoeza kila mtoto (Tazama fungu la 20) *

20. Eleza jinsi Zaburi 127:4 inavyoweza kutumiwa katika kulea watoto.

20 Uwe na utambuzi. Zaburi 127 inafananisha watoto na mishale. (Soma Zaburi 127:4.) Watoto hutofautiana kama tu ambavyo mishale hutengenezwa kutokana na vitu mbalimbali na hutofautiana urefu. Hivyo, wazazi wanapaswa kujua jinsi ya kumzoeza kila mtoto. Wenzi wa ndoa nchini Israel waliofanikiwa kulea watoto wao wawili wamtumikie Yehova, walisema hivi kuhusu kile kilichowasaidia: “Tulijifunza Biblia kibinafsi na kila mtoto.” Ni kweli kwamba kila kichwa cha familia ataamua ikiwa atafanya hivyo au la.

YEHOVA ATAKUSAIDIA

21. Yehova anawapatia wazazi msaada gani?

21 Huenda pindi fulani wazazi wakahisi kulemewa na changamoto wanazokabili, lakini watoto ni zawadi kutoka kwa Yehova. Sikuzote yuko tayari kuwasaidia na anasikiliza sala za wazazi. Na anajibu sala hizo kupitia Biblia, machapisho yetu, na mifano na ushauri kutoka kwa wazazi wenye uzoefu walio kutanikoni.

22. Ni mambo gani bora ambayo wazazi wanaweza kuwapa watoto wao?

22 Baadhi ya watu husema kwamba kulea mtoto ni mradi unaochukua miaka 20, hata hivyo wazazi hawakomi kuwa wazazi baada ya kipindi hicho. Kati ya mambo bora ambayo wazazi wanaweza kuwapa watoto wao ni upendo, wakati wao, na mazoezi yanayotegemea Biblia. Kila mtoto ataitikia mazoezi hayo kwa njia tofauti na mwingine. Hata hivyo, wengi waliolelewa na wazazi wanaompenda Yehova wanahisi kama Joanna Mae, dada kutoka bara la Asia aliyesema hivi: “Ninapokumbuka mazoezi niliyopewa na wazazi wangu, ninathamini sana kwamba walinitia nidhamu na kunifundisha kumpenda Yehova. Hawakunipa uhai tu bali pia walinisaidia kutambua kusudi la maisha.” (Met. 23:24, 25) Wakristo wengi wanahisi vivyo hivyo.

WIMBO 59 Msifuni Yah Pamoja Nami

^ fu. 5 Je, wenzi wa ndoa wanapaswa kuwa na watoto? Ikiwa wataamua kufanya hivyo, je, wazae watoto wangapi? Wanaweza kuwafundisha watoto wao kumpenda na kumtumikia Yehova jinsi gani? Makala hii ina mifano ya akina ndugu na dada wa siku zetu na inaonyesha kanuni za Biblia zitakazotusaidia kujibu maswali hayo.

^ fu. 15 Tazama pia kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1, sura ya 36, na Buku la 2, sura ya 11.

^ fu. 60 MAELEZO YA PICHA: Wenzi wa ndoa Wakristo wakizungumza ikiwa watapata watoto na wakichunguza shangwe na majukumu yatakayohusika.

^ fu. 64 MAELEZO YA PICHA: Wenzi wakijifunza na watoto wao kila mmoja kwa muda wake kwa sababu ya tofauti ya umri na uwezo wa kila mtoto.