Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 50

Yehova Ameandaa Njia ya Kukuweka Huru

Yehova Ameandaa Njia ya Kukuweka Huru

‘Tangaza uhuru kwa wakaaji wote nchini.’—LAW. 25:10.

WIMBO 22 Ufalme Umesimamishwa–Na Uje!

MUHTASARI *

1-2. (a) Mwadhimisho wa Miaka 50 ni nini? (Tazama sanduku “ Mwadhimisho wa Miaka 50 Ni Nini?”) (b) Kulingana na Luka 4:16-18, Yesu alizungumzia nini?

KATIKA nchi fulani, maadhimisho ya pekee hufanywa ili kusherehekea miaka 50 ya utawala wa mfalme au malkia. Sherehe za kuadhimisha mwaka huo hufanywa kwa siku moja, juma moja, au hata muda mrefu zaidi, lakini mwishowe huisha, na shangwe iliyoambatana na sherehe hiyo husahaulika baada ya muda mfupi.

2 Tutachunguza Mwadhimisho wa Miaka 50 ulio bora zaidi, bora kuliko ule uliofanywa mwaka mzima, katika kila mwaka wa 50 katika taifa la Israeli. Mwadhimisho huo wa kale wa Miaka 50 uliwaweka huru watu waliousherehekea. Kwa nini jambo hilo linatupendeza leo? Kwa sababu maadhimisho hayo katika Israeli yanatukumbusha maandalizi bora ya uhuru unaodumu ambao Yehova anatuandalia hata sasa; uhuru ambao Yesu pia alizungumzia.—Soma Luka 4:16-18.

Mwadhimisho wa Miaka 50 ulileta shangwe kwa sababu watumwa walirudishwa kwa familia zao na kumiliki tena ardhi yao (Tazama fungu la 3) *

3. Kama inavyotajwa katika Mambo ya Walawi 25:8-12, Waisraeli walinufaikaje na Mwadhimisho wa Miaka 50?

3 Ili kuelewa kile alichomaanisha Yesu alipozungumzia uhuru, acheni tuchunguze mpango wa Mwadhimisho wa Miaka 50 ambao Mungu aliandaa kwa ajili ya watu wake wa kale. Yehova aliwaambia Waisraeli hivi: “Mtautakasa mwaka wa 50 na kutangaza uhuru kwa wakaaji wote nchini. Utakuwa Mwadhimisho wa Miaka 50, na kila mmoja atarudi kwenye urithi wake na kila mmoja wenu atarudi kwa familia yake.(Soma Mambo ya Walawi 25:8-12.) Katika makala iliyotangulia, tulichunguza jinsi Waisraeli walivyonufaika na Sabato ya kila juma. Hata hivyo, Waisraeli walinufaikaje na Mwadhimisho wa Miaka 50? Tuseme kwamba Mwisraeli fulani alikuwa na deni kubwa na hivyo alilazimika kuuza ardhi yake ili kulipia deni hilo. Katika Mwadhimisho wa Miaka 50, alirudishiwa ardhi hiyo. Hivyo, mwanamume huyo ‘angerudi kwenye urithi wake,’ na urithi wa watoto wake usingepotea. Katika kisa kingine, mwanamume aliyekabili hali ngumu angemuuza mtoto wake mmoja au yeye mwenyewe utumwani ili kulipia deni lake. Katika Mwadhimisho wa Miaka 50, mtumwa alipaswa ‘kurudi kwa familia yake.’ Hivyo, hakuna yeyote ambaye angekuwa mtumwa wa kudumu bila tumaini lolote! Yehova ni mwenye ufikirio sana!

4-5. Kwa nini tunapaswa kupendezwa na Mwadhimisho wa kale wa Miaka 50?

4 Mwadhimisho wa Miaka 50 ulikuwa na faida gani nyingine? Yehova alisema hivi: “Hakuna yeyote kati yenu anayepaswa kuwa maskini, kwa sababu hakika Yehova atawabariki katika nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa mwimiliki kama urithi” (Kum. 15:4) Hilo ni tofauti sana na ulimwengu wa leo ambamo matajiri wanazidi kuwa matajiri na maskini wanazidi kuwa maskini!

5 Tukiwa Wakristo hatuko chini ya Sheria ya Musa. Hilo linamaanisha kwamba hatufuati mpango wa kale wa Mwadhimisho wa Miaka 50 wa kuwaweka huru watumwa, kusamehe madeni, na kurudisha ardhi ya urithi. (Rom. 7:4; 10:4; Efe. 2:15) Licha ya hilo, tuna kila sababu ya kupendezwa na Mwadhimisho huo. Kwa nini? Kwa sababu tunaweza kufurahia uhuru unaotukumbusha mpango huo ambao Yehova aliwawekea Waisraeli.

YESU ALITANGAZA UHURU

6. Wanadamu wanahitaji kuwekwa huru kutokana na nini?

6 Tunahitaji kuwekwa huru kwa sababu sisi sote ni watumwa wa dhambi—utumwa ulio mbaya sana. Kwa sababu sisi ni wenye dhambi, tunazeeka, tunaugua, na kufa. Tunajionea uthibitisho wa jambo hilo tunapojiangalia katika kioo au tunapoenda kumwona daktari. Pia, tunavunjika moyo tunapotenda dhambi. Mtume Paulo alikiri kwamba alichukuliwa “mateka kwa sheria ya dhambi iliyo ndani ya mwili [wake].” Aliongezea hivi: “Maskini mimi! Ni nani atakayeniokoa kutoka katika mwili unaopatwa na kifo hiki?”—Rom. 7:23, 24.

7. Isaya alitabiri nini kuhusu uhuru?

7 Tunafurahi kwamba Mungu amefanya mpango ili tuokolewe au tuwekwe huru kutokana na dhambi. Yesu ndiye anayeweza kutuokoa. Zaidi ya miaka 700 kabla ya Yesu kuja duniani, nabii Isaya alitabiri kuhusu uhuru mkubwa. Uhuru huo ungetimiza mengi zaidi kuliko yale yaliyotimizwa na Mwadhimisho wa Miaka 50 katika Israeli. Aliandika hivi: “Roho ya Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova iko juu yangu, kwa sababu Yehova alinitia mafuta niwatangazie wapole habari njema. Alinituma kuyafunga majeraha ya waliovunjika moyo, kuwatangazia mateka uhuru.” (Isa. 61:1) Unabii huo unamhusu nani?

8. Unabii wa Isaya kuhusu kuwekwa huru ulimhusu nani?

8 Unabii huo muhimu kuhusu kuwekwa huru ulianza kutimizwa Yesu alipoanza huduma yake. Alipoenda kwenye sinagogi katika mji wa nyumbani wa Nazareti, Yesu alisoma maneno hayo ya Isaya mbele ya Wayahudi waliokusanyika hapo. Yesu alijirejelea aliposema hivi: “Roho ya Yehova iko juu yangu, kwa sababu alinitia mafuta ili niwatangazie maskini habari njema. Alinituma niwatangazie mateka uhuru na vipofu kuona tena, kuwaweka huru waliopondeka, kuhubiri mwaka wa Yehova unaokubalika.” (Luka 4:16-19) Yesu alitimizaje unabii huo?

WATU WA KWANZA KUWEKWA HURU

Yesu anatangaza uhuru katika sinagogi la Nazareti (Tazama fungu la 8-9)

9. Watu wengi katika siku za Yesu walitazamia uhuru wa aina gani?

9 Uhuru aliotabiri Isaya na ambao Yesu alisoma ulianza kutolewa katika karne ya kwanza. Yesu alithibitisha hilo alipotangaza hivi: “Leo andiko hili ambalo mmetoka kusikia limetimia.” (Luka 4:21) Huenda wengi waliomsikiliza Yesu akisoma walitazamia mabadiliko fulani ya kisiasa ambayo yangewaweka huru kutokana na utawala wa Roma. Huenda watu hao walihisi kama wanaume fulani wawili waliosema hivi: “Tulitazamia kwamba yeye ndiye angekomboa Israeli.” (Luka 24:13, 21) Lakini tunajua kwamba Yesu hakuwachochea wafuasi wake waasi utawala wa Roma wenye kukandamiza. Badala yake, aliwaagiza wamlipe “Kaisari vitu vya Kaisari.” (Mt. 22:21) Hivyo basi, Yesu alileta uhuru wa aina gani wakati huo?

10. Yesu aliwaweka watu huru kutokana na nini?

10 Mwana wa Mungu alikuja kuwasaidia watu kupata uhuru wa aina mbili. Kwanza, Yesu aliwaweka huru kutokana na mafundisho yenye kukandamiza ya viongozi wa kidini. Wayahudi wengi wakati huo walikuwa watumwa wa mapokeo ya wanadamu na mafundisho ya uwongo. (Mt. 5:31-37; 15:1-11) Viongozi hao waliodai kwamba wanawasaidia wengine kumtumikia Mungu, ingawa wao wenyewe hawakuwa wakimtumikia Mungu kwa njia sahihi; ni kana kwamba walikuwa vipofu. Kwa kuwa walimkataa Masihi na nuru ya kiroho aliyotoa, walibaki katika giza na dhambi. (Yoh. 9:1, 14-16, 35-41) Kupitia mafundisho yake sahihi na mfano wake mzuri, Yesu aliwaonyesha wapole uhuru wa kiroho.—Marko 1:22; 2:23–3:5.

11. Taja njia ya pili ambayo Yesu alitumia kuwapa wanadamu uhuru.

11 Pili, Yesu aliwaweka huru wanadamu kutokana na utumwa wa dhambi waliyorithi. Kwa msingi wa dhabihu ya Yesu, Mungu angeweza kuwasamehe wote wanaoonyesha imani na kukubali fidia aliyoandaa. (Ebr. 10:12-18) Yesu alisema hivi: “Mwana akiwaweka ninyi huru, kwa kweli mtakuwa huru.” (Yoh. 8:36) Kwa hakika uhuru huo ulikuwa bora kuliko uhuru uliotolewa kwa Waisraeli wakati wa Mwadhimisho wa Miaka 50! Kwa mfano, mwanamume aliyewekwa huru wakati wa Mwadhimisho huo angeweza kuwa mtumwa tena, na hatimaye angekufa.

12. Ni nani watakaokuwa wa kwanza kunufaika na uhuru uliotangazwa na Yesu?

12 Katika siku ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K., Yehova aliwatia mafuta kwa roho takatifu mitume na wanaume na wanawake wengine waaminifu. Aliwafanya kuwa wana ili wakati ujao wafufuliwe kwenda mbinguni na kutawala pamoja na Yesu. (Rom. 8:2, 15-17) Hao ndio wa kwanza kunufaika na uhuru ambao Yesu alitangaza katika sinagogi la Nazareti. Wanaume na wanawake hao hawakuwa tena watumwa wa mafundisho ya uwongo ya viongozi wa dini ya Kiyahudi na mapokeo yao yasiyopatana na Maandiko. Pia, Mungu aliwahesabu kuwa wamewekwa huru kutokana na matokeo mabaya ya dhambi. Maadhimisho ya Miaka 50 ya mfano yaliyoanza na kutiwa mafuta kwa wafuasi wa Kristo mwaka wa 33 W.K. yatakoma mwishoni mwa Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Yesu. Ni mambo gani yatakayokuwa yametimizwa kufikia wakati huo?

MAMILIONI YA WATU WATAWEKWA HURU

13-14. Mbali na Wakristo watiwa-mafuta, ni nani wengine wanaopata uhuru aliotangaza Yesu?

13 Katika siku zetu, mamilioni ya watu wanyoofu kutoka katika mataifa yote ni sehemu ya “kondoo wengine.” (Yoh. 10:16) Hawajachaguliwa na Mungu kutawala pamoja na Yesu mbinguni. Badala yake wanatumaini linalotajwa katika Biblia la kuishi milele duniani. Je, una tumaini hilo?

14 Hata sasa unapokea baadhi ya baraka zinazofurahiwa na wale watakaokuwa watawala kwenye Ufalme wa Mungu wa mbinguni. Unaweza kuomba msamaha wa dhambi zako kupitia imani yako katika damu ya Yesu. Hilo linakuwezesha kuwa na msimamo mzuri na dhamiri njema mbele za Mungu. (Efe. 1:7; Ufu. 7:14, 15) Pia, wazia baraka nyingi tunazofurahia kwa sababu ya kuwa huru kutokana na mafundisho ya uwongo. Yesu alisema: “Nanyi mtaijua kweli, nayo kweli itawaweka ninyi huru.” (Yoh. 8:32) Ni shangwe iliyoje kuwa na uhuru huo.

15. Tunaweza kutazamia uhuru na baraka gani wakati ujao?

15 Unaweza kutarajia uhuru mkubwa zaidi. Hivi karibuni, Yesu atachukua hatua mara moja ili kuangamiza dini ya uwongo na serikali za wanadamu zisizotenda haki. Mungu ataulinda “umati mkubwa” wa watumishi wake, na kuwaruhusu wafurahie baraka katika dunia paradiso. (Ufu. 7:9, 14) Watu wengi sana watafufuliwa na kupata fursa ya kuwekwa huru kutokana na madhara ya dhambi ya Adamu.—Mdo. 24:15.

16. Ni uhuru gani mkubwa zaidi watakaopata wanadamu wakati ujao?

16 Wakati wa Utawala wa Miaka Elfu Moja, Yesu pamoja na watawala wenzake watawasaidia wanadamu kuwa wakamilifu kimwili na kiroho. Pindi hiyo ya kurudishwa upya na kuwekwa huru itakuwa kama Mwadhimisho wa Miaka 50 wa Waisraeli. Matokeo ni kwamba watu wote wanaomtumikia Yehova duniani kwa ushikamanifu watakuwa wakamilifu, bila dhambi.

Katika ulimwengu mpya, tutafurahia kufanya kazi bora na zenye kuridhisha (Tazama fungu la 17)

17. Andiko la Isaya 65:21-23 linatabiri nini kuhusu watu wa Mungu? (Tazama picha kwenye jalada.)

17 Ufafanuzi wa jinsi maisha yatakavyokuwa duniani wakati ujao unapatikana katika unabii wa Isaya 65:21-23. (Soma.) Tutakuwa na mengi ya kufanya wakati huo. Biblia inaonyesha kwamba wakati huo, watu wa Mungu watakuwa wakifanya kazi zenye kuridhisha. Mwishoni mwa kipindi hicho, tuna hakika kwamba “uumbaji wenyewe pia utawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.”—Rom. 8:21.

18. Kwa nini tuna hakika kwamba tutakuwa na wakati ujao ulio mzuri?

18 Kama tu Yehova alivyowasaidia Waisraeli kuwa na usawaziko ilipohusu kazi na kupumzika, ndivyo atakavyofanya kwa watu wake wakati wa Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Kristo. Bila shaka, kutakuwa na pindi za utendaji wa kiroho. Ibada kwa Mungu ni jambo la muhimu leo ili kuwa na furaha, na tutakuwa na muda wa kutosha wa kufanya hivyo katika ulimwengu mpya. Naam, tuna sababu nzuri ya kushangilia kwa ajili ya kazi yetu njema na utendaji wa kiroho tunaotazamia wakati wanadamu waaminifu watakapofurahia maisha katika Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Kristo.

WIMBO 142 Kushikilia Tumaini Letu

^ fu. 5 Yehova aliandaa mpango wa pekee wa kutangaza uhuru katika Israeli la kale. Ulikuwa Mwadhimisho wa Miaka 50 au Yubile. Wakristo hawako chini ya Sheria ya Musa; hata hivyo, mwadhimisho huo una maana kwetu. Katika makala hii, tutachunguza jinsi ambavyo mwadhimisho huo unatukumbusha maandalizi ambayo Yehova amefanya kwa ajili yetu na jinsi tunavyoweza kunufaika na mpango huo.

^ fu. 61 MAELEZO YA PICHA: Katika Mwadhimisho wa Miaka 50, wanaume waliokuwa watumwa waliwekwa huru na kurudi kwa familia zao na kumiliki tena ardhi yao.