Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unamjua Yehova Kama Noa, Danieli, na Ayubu?

Je, Unamjua Yehova Kama Noa, Danieli, na Ayubu?

“Waovu hawawezi kuelewa haki, lakini wale wanaomtafuta Yehova wanaweza kuelewa mambo yote.”—MET. 28:5.

NYIMBO: 126, 150

1-3. (a) Ni nini kitakachotusaidia kuendelea kuwa waaminifu kwa Mungu katika siku hizi za mwisho? (b) Tutachunguza nini katika makala hii?

KADIRI siku za mwisho zinavyokaribia kwisha, waovu wanaendelea ‘kuchipuka kama magugu.’ (Zab. 92:7) Hivyo, hatushangai kuona kwamba watu wameacha kufuata viwango vya maadili. Katika mazingira hayo, tunawezaje kuwa “watoto wadogo kuhusiana na ubaya” na wakati uleule kuwa “watu wazima katika uelewaji [wetu]”?—1 Kor. 14:20.

2 Jibu linapatikana katika andiko letu la msingi ambalo kwa sehemu linasema: “Wale wanaomtafuta Yehova wanaweza kuelewa mambo yote”—yaani, mambo yote wanayopaswa kuelewa ili kumpendeza. (Met. 28:5) Wazo linalofanana na hilo linapatikana kwenye andiko la Methali 2:7, 9, linalosema kwamba Yehova “huwahifadhia wanyoofu hekima inayotumika.” Kwa njia hiyo wanyoofu wanaweza “[kuelewa] lililo la uadilifu na la haki na lililo sawa, njia yote ya lililo jema.”

3 Noa, Danieli, na Ayubu walijipatia hekima hiyo. (Eze. 14:14) Na hivyo ndivyo ilivyo kwa watu wa Mungu leo. Vipi wewe binafsi? Je, ‘unaelewa mambo yote’ unayopaswa kuelewa ili kumpendeza Yehova? Siri ya kufanya hivyo ni kupata ujuzi sahihi kumhusu yeye. Tukiwa na wazo hilo akilini, acheni tufikirie (1) mambo yaliyomsaidia Noa, Danieli, na Ayubu kumjua Mungu, (2) jinsi ujuzi huo ulivyowanufaisha, na (3) jinsi tunavyoweza kusitawisha imani kama yao.

NOA ALITEMBEA PAMOJA NA MUNGU KATIKA ULIMWENGU MWOVU

4. Ni jambo gani lililomsaidia Noa kumjua Yehova, na ujuzi sahihi kumhusu Mungu ulimsaidiaje?

4 Mambo yaliyomsaidia Noa kumjua Yehova. Tangu mwanzoni mwa historia ya wanadamu, wanaume na wanawake wenye imani walijifunza kumhusu Mungu kupitia njia tatu za msingi: kwa kuchunguza uumbaji, kupitia wanadamu wengine waliomwogopa Mungu, na kwa kujionea baraka zinazotokana na kuishi kupatana na kanuni na viwango vya Mungu vya uadilifu. (Isa. 48:18) Kwa kuchunguza uumbaji, Noa angeweza kuona uthibitisho mwingi kwamba Mungu yupo na kujifunza kuhusu sifa zake nyingi zisizoonekana, kama vile “nguvu zake za milele na Uungu.” (Rom. 1:20) Hivyo, Noa hakuamini tu kwamba kuna Mungu, bali pia alisitawisha imani yenye nguvu kumwelekea.

5. Noa alipataje habari kuhusu kusudi la Mungu kwa wanadamu?

5 Imani “hufuata jambo lililosikiwa.” (Rom. 10:17) Noa alipataje habari kumhusu Yehova? Hapana shaka alijifunza mambo mengi kutoka kwa watu wake wa ukoo. Watu wake wa ukoo walitia ndani Lameki baba yake, ambaye alikuwa mwanamume mwenye imani na ambaye alikuwa hai kabla Adamu hajafa. (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.) Walitia ndani pia Methusela babu yake na Yaredi babu ya babu yake ambaye aliishi wakati uleule na Noa kwa miaka 366. * (Luka 3:36, 37) Inaelekea ni kutoka kwa wanaume hao na labda pia wake zao ambapo Noa alijifunza kuhusu mwanzo wa wanadamu, kuhusu kusudi la Mungu kwamba wanadamu waadilifu waijaze dunia, na kuhusu uasi wa Edeni. Noa mwenyewe alijionea matokeo mabaya ya uasi huo. (Mwa. 1:28; 3:16-19, 24) Kwa vyovyote vile, mambo ambayo alijifunza yalimgusa moyo, nayo yalimchochea kumtumikia Mungu.—Mwa. 6:9.

6, 7. Tumaini liliimarishaje imani ya Noa?

6 Tumaini huimarisha imani. Wazia jinsi Noa alivyohisi alipojifunza kwamba jina lake, ambalo huenda linamaanisha “Pumziko; Faraja,” liliashiria tumaini! (Mwa. 5:29, maelezo ya chini) Kwa mwongozo wa roho ya Mungu, Lameki alisema hivi: “Huyu [Noa] atatufariji katika . . . kazi inayoumiza ya mikono yetu kwa sababu ya ardhi iliyolaaniwa na Yehova.” Noa alimtumaini Mungu. Kama Abeli na Enoko walioishi kabla yake, Noa aliamini kwamba kungekuwa na “uzao” ambao ungemponda nyoka kichwani.—Mwa. 3:15.

7 Ingawa huenda Noa hakuelewa mambo yote kuhusu unabii ulio katika andiko la Mwanzo 3:15, hapana shaka alitambua kwamba unabii huo ulihusisha ukombozi. Zaidi ya hilo, ahadi hiyo iliyotolewa Edeni ilipatana na ujumbe uliotangazwa na Enoko, ambaye pia alitabiri kuhusu hukumu ya Mungu dhidi ya waovu. (Yuda 14, 15) Kwa hakika, imani na tumaini ambalo Noa alikuwa nalo liliimarishwa na ujumbe wa Enoko, ambao utapata utimizo wake wa mwisho katika Har–Magedoni!

8. Ujuzi sahihi kumhusu Mungu ulimlinda Noa katika njia zipi?

8 Jinsi ujuzi sahihi kumhusu Mungu ulivyomnufaisha Noa. Ujuzi sahihi kumhusu Mungu ulimsaidia Noa kuwa na imani na hekima inayotoka kwa Mungu, mambo ambayo yalimlinda, hasa kutokana na madhara ya kiroho. Kwa mfano, kwa kuwa Noa “alitembea pamoja na Mungu wa kweli,” hakutembea na watu wasiomwogopa Mungu, yaani, hakushirikiana nao. Hakupumbazwa na malaika waovu waliojivika miili ya kibinadamu, ambao hapana shaka uwezo wao usio wa kawaida uliwavutia wanadamu wasio na imani na ufahamu—hata labda kufikia hatua ya kuwaabudu. (Mwa. 6:1-4, 9) Pia, Noa alijua kwamba wanadamu walikuwa wameambiwa wazaane na kuijaza dunia. (Mwa. 1:27, 28) Hivyo, lazima iwe alijua kwamba lilikuwa kosa na jambo lisilo la asili kwa malaika waliojivika miili ya kibinadamu kufanya ngono na wanawake. Jambo hilo lilidhihirishwa wazi mahusiano hayo yalipotokeza watoto wasio wa kawaida. Baada ya muda, Mungu alimwambia Noa kwamba angeleta Gharika duniani. Kwa kuwa Noa aliamini kwamba Mungu angeleta Gharika, alichochewa kujenga safina na hivyo kuiokoa familia yake.—Ebr. 11:7.

9, 10. Tunaweza kuigaje imani ya Noa?

9 Jinsi tunavyoweza kusitawisha imani kama ya Noa. Siri ya kufanya hivyo ni kujifunza Neno la Mungu kwa bidii, kutumia mambo tunayojifunza, na kuruhusu ujuzi huo utufinyange na kutuongoza. (1 Pet. 1:13-15) Kisha imani na hekima inayotoka kwa Mungu itatulinda kutokana na mbinu za Shetani zenye ujanja na kutokana na roho mbaya ya ulimwengu. (2 Kor. 2:11) Roho hiyo huwachochea watu wapende ukatili na ukosefu wa maadili. Pia, huwachochea watu wakazie fikira tamaa za mwili. (1 Yoh. 2:15, 16) Roho hiyo inaweza pia kuwafanya watu walio dhaifu kiroho kupuuza uthibitisho wa kwamba siku ile kuu ya Mungu imekaribia. Ona kwamba Yesu alipolinganisha siku zetu na siku za Noa, hakukazia ukatili au ukosefu wa maadili, bali alikazia hatari ya kupuuza mambo ya kiroho.—Soma Mathayo 24:36-39.

10 Jiulize hivi: ‘Je, maisha yangu yanaonyesha kwamba kweli mimi ninamjua Yehova? Je, imani yangu inanichochea, si tu kuishi kulingana na viwango vya Mungu vya uadilifu, bali pia kuvitangaza kwa wengine?’ Majibu yako kwa maswali hayo yatakusaidia kujua ikiwa wewe pia ‘unatembea pamoja na Mungu wa kweli.’

DANIELI ALIONYESHA HEKIMA INAYOTOKA KWA MUNGU KATIKA JIJI LA KIPAGANI

11. (a) Tunajifunza nini kuhusu malezi ya Danieli kutokana na jinsi alivyojitoa kwa Mungu akiwa kijana? (b) Ungependa kuiga sifa zipi za Danieli?

11 Mambo yaliyomsaidia Danieli kumjua Yehova. Ni wazi kwamba Danieli alizoezwa vizuri na wazazi wake ambao walimfundisha kumpenda Yehova na Neno lake. Isitoshe, Danieli aliendelea kumpenda Yehova na Neno lake maisha yake yote. Hata alipokuwa mzee, bado aliendelea kujifunza Maandiko kwa makini. (Dan. 9:1, 2) Sala ya unyenyekevu na ya kutoka moyoni ya nabii huyo inayopatikana katika Danieli 9:3-19, inaonyesha kwa njia yenye kuvutia kwamba Danieli alikuwa na ujuzi wenye kina kumhusu Mungu na jinsi Mungu alivyoshughulika na Waisraeli. Kwa nini usitumie muda fulani kusoma na kutafakari sala hiyo, ukikazia fikira yale ambayo sala hiyo inakufundisha kumhusu Danieli?

12-14. (a) Danieli alionyesha hekima inayotoka kwa Mungu katika njia zipi? (b) Danieli alibarikiwa jinsi gani kwa kushikamana na Mungu kwa ujasiri?

12 Jinsi ujuzi sahihi kumhusu Mungu ulivyomnufaisha Danieli. Maisha katika jiji la kipagani la Babiloni yalikuwa na changamoto nyingi hasa kwa Wayahudi waaminifu. Kwa mfano, Yehova aliwaambia hivi Wayahudi: “Tafuteni amani kwa ajili ya jiji ambamo nimewapeleka uhamishoni.” (Yer. 29:7) Wakati huohuo, Mungu alitaka wamwabudu yeye peke yake. (Kut. 34:14) Ni nini kilichomsaidia Danieli atimize mambo hayo mawili kwa njia yenye usawaziko? Alikuwa na hekima kutoka kwa Mungu ambayo ilimsaidia kuelewa kanuni iliyohusu kuheshimu mamlaka za ulimwengu kwa kiwango kinachostahili. Karne nyingi baadaye, Yesu alifundisha kuhusu kanuni hiyohiyo.—Luka 20:25.

13 Fikiria kile ambacho Danieli alifanya wakati agizo rasmi kutoka kwa mfalme lilipowakataza watu kusali kwa mungu au mwanadamu yeyote isipokuwa mfalme kwa siku 30. (Soma Danieli 6:7-10.) Danieli angeweza kutoa udhuru kwa kusema: ‘Siku thelathini si nyingi!’ Lakini hakuruhusu agizo la mfalme limfanye apuuze wajibu wake wa Kimaandiko. Bila shaka, angeweza kusali kisirisiri ili asionekane na watu. Alijua kwamba desturi yake ya kusali kila siku ilijulikana sana na watu. Danieli aliamua kutoruhusu jambo lolote liwafanye watu wafikiri kwamba ameacha kumtumikia Yehova, ingawa kufanya hivyo kungehatarisha maisha yake.

14 Yehova alimbariki Danieli kwa sababu alifanya uamuzi kwa ujasiri na kushikamana kwa dhati na uamuzi huo, hivyo akamwokoa asife kifo cha kikatili. Kwa kweli, jambo hilo lilifanya jina la Yehova litangazwe kotekote hata kufikia sehemu za mbali sana za Milki ya Umedi na Uajemi!—Dan. 6:25-27.

15. Tunaweza kusitawishaje imani kama ya Danieli?

15 Jinsi tunavyoweza kusitawisha imani kama ya Danieli. Siri ya kuwa na imani yenye nguvu si kusoma tu Neno la Mungu, bali ni ‘kulielewa.’ (Mt. 13:23) Tungependa kujua maoni ya Yehova kuhusu mambo, na hilo linatia ndani kuelewa kanuni za Biblia. Hivyo, tunahitaji kutafakari mambo tunayosoma. Ni muhimu pia kusali kwa ukawaida kutoka moyoni, hasa tunapokabili majaribu au hali nyingine ngumu. Tunaposali kwa imani ili tupate hekima na nguvu, Yehova atatupatia mambo hayo kwa ukarimu.—Yak. 1:5.

AYUBU ALITUMIA KANUNI ZA MUNGU—NYAKATI MBAYA NA NZURI

16, 17. Ni mambo gani yaliyomsaidia Ayubu kupata ujuzi sahihi kumhusu Mungu?

16 Mambo yaliyomsaidia Ayubu kumjua Yehova. Ayubu hakuwa Mwisraeli. Hata hivyo, alikuwa mtu wa ukoo wa mbali wa Abrahamu, Isaka, na Yakobo, na Yehova alikuwa amewafunulia mambo fulani kujihusu na kuhusu kusudi lake kwa wanadamu. Hivyo kwa njia fulani, Ayubu alijifunza kuhusu kweli hizo zenye thamani. (Ayu. 23:12) Alisema hivi: “Masikio yangu yamesikia habari zako.” (Ayu. 42:5) Isitoshe, Yehova mwenyewe alisema kwamba Ayubu alisema kweli kumhusu.—Ayu. 42:7, 8.

Imani yetu huimarishwa tunapotazama uumbaji na kuona sifa za Mungu zisizoonekana (Tazama fungu la 17)

17 Pia, kupitia uumbaji, Ayubu aliona sifa nyingi za Mungu zisizoonekana. (Ayu. 12:7-9, 13) Baadaye, Elihu na Yehova walitumia mambo fulani kuhusu uumbaji kumkumbusha Ayubu jinsi mwanadamu alivyo duni kwa kulinganishwa na ukuu wa Mungu. (Ayu. 37:14; 38:1-4) Neno la Yehova liligusa moyo wa Ayubu kwa sababu alimwambia Mungu hivi kwa unyenyekevu: “Sasa ninajua kwamba unaweza kufanya mambo yote na kwamba hakuna jambo lolote unalokusudia lisilowezekana kwako. . . . Ninatubu katika mavumbi na majivu.”—Ayu. 42:2, 6.

18, 19. Ayubu alionyesha katika njia zipi kwamba anamjua Mungu vizuri?

18 Jinsi ujuzi sahihi kumhusu Mungu ulivyomnufaisha Ayubu. Ayubu alikuwa na ufahamu wenye kina kuhusu kanuni za Mungu. Alimjua Yehova vizuri, naye alitenda kupatana na ujuzi huo. Fikiria hili: Ayubu alijua kwamba hawezi kudai anampenda Mungu na wakati uleule kuwatendea bila fadhili wanadamu wenzake. (Ayu. 6:14) Hakujikweza juu ya wengine bali aliwahangaikia wote kwa upendo kama ndugu zake, matajiri kwa maskini. Alisema hivi: “Je, Yule aliyeniumba tumboni mwa mama yangu hakuwaumba wao pia?” (Ayu. 31:13-22) Ni wazi kwamba Ayubu hakuruhusu fahari na utajiri aliokuwa nao mwanzoni uathiri maoni yake kujielekea au kuwaelekea wengine. Alikuwa tofauti sana na watu wengi wenye mamlaka na utajiri wa ulimwengu huu!

19 Ayubu alipinga namna zote za ibada ya sanamu—hata jambo hilo halikuingia moyoni mwake. Alijua kwamba ibada ya uwongo, kutia ndani kutumikia utajiri kungekuwa sawa na kumkana “Mungu wa kweli aliye juu.” (Soma Ayubu 31:24-28.) Aliiona ndoa kuwa kifungo kitakatifu kati ya mwanamume na mwanamke. Hata alifanya agano pamoja na macho yake kwamba asimtazame bikira kwa njia isiyofaa. (Ayu. 31:1) Kumbuka kwamba wakati huo Mungu alikuwa akiruhusu ndoa za wake wengi. Hivyo, ikiwa Ayubu angetaka, angeweza kuoa mke wa pili. * Hata hivyo, inaonekana kwamba alitumia kigezo ambacho Mungu aliweka kuhusu ndoa katika Edeni, naye akakifuata kama sheria. (Mwa. 2:18, 24) Miaka 1,600 hivi baadaye, Yesu Kristo aliwafundisha wasikilizaji wake washikamane na kanuni hizohizo za uadilifu kuhusu ndoa na usafi wa kiadili.—Mt. 5:28; 19:4, 5.

20. Ujuzi sahihi kumhusu Yehova na viwango vyake utatusaidiaje kuchagua marafiki na burudani zinazofaa?

20 Jinsi tunavyoweza kusitawisha imani kama ya Ayubu. Kwa mara nyingine tena, siri ni kuwa na ujuzi sahihi kumhusu Yehova na kuruhusu ujuzi huo uongoze nyanja zote za maisha yetu. Kwa mfano, mtunga zaburi Daudi alisema kwamba Yehova “humchukia mtu yeyote anayependa ukatili,” na Daudi alituonya tusishirikiane “na watu wadanganyifu.” (Soma Zaburi 11:5; 26:4.) Maandiko hayo yanakusaidia kuelewa nini kuhusu jinsi Mungu anavyoona mambo? Kuelewa maoni ya Mungu kunapaswa kutuchochea tuwe na maoni gani kuhusu mambo tunayopaswa kutanguliza maishani, matumizi ya Intaneti, marafiki, na burudani? Majibu yako yatakusaidia kutambua unamjua Yehova kwa kadiri gani. Ili tuendelee kubaki bila doa katika ulimwengu wa sasa ulio mgumu kushughulika nao na uliojaa uovu, ni lazima tuzoeze “nguvu [zetu] za utambuzi” ili tutofautishe, si tu jambo lililo sawa na lisilo sawa, bali pia jambo la hekima na lisilo la hekima.—Ebr. 5:14; Efe. 5:15.

21. Ni nini kitakachotusaidia “kuelewa mambo yote” tunayopaswa kuelewa ili kumpendeza Baba yetu wa mbinguni?

21 Kwa kuwa Noa, Danieli, na Ayubu walimtafuta Yehova kwa moyo wao wote, Yehova aliruhusu wampate. Aliwasaidia “kuelewa mambo yote” waliyopaswa kuelewa ili kumpendeza. Hivyo, wakawa mifano ya uadilifu, nao walifanikiwa kwelikweli maishani. (Zab. 1:1-3) Kwa hiyo, jiulize hivi, ‘Je, ninamjua Yehova vizuri kama Noa, Danieli, na Ayubu?’ Ukweli ni kwamba kwa sababu ya kuongezeka kwa nuru ya kiroho, unaweza kumjua vizuri hata zaidi! (Met. 4:18) Basi, chimba kwa kina ndani ya Neno la Mungu. Litafakari. Na usali upate roho takatifu. Ukifanya hivyo utamkaribia zaidi Baba yako wa mbinguni. Nawe utatenda kwa ufahamu na hekima katika ulimwengu wa sasa usiomwogopa Mungu.—Met. 2:4-7.

^ fu. 5 Pia Enoko babu ya Noa “aliendelea kutembea na Mungu wa kweli.” Hata hivyo, “Mungu alimchukua” miaka 69 hivi kabla ya Noa kuzaliwa.—Mwa. 5:23, 24.

^ fu. 19 Noa pia angeweza kufanya hivyo. Alikuwa na mke mmoja tu, licha ya kwamba watu walianza kuoa wake wengi muda mfupi tu baada ya uasi katika Edeni.—Mwa. 4:19.