Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

Mambo Yote Yanawezekana kwa Yehova

Mambo Yote Yanawezekana kwa Yehova

“KIFO hakitakuwapo tena, na hata wafu watafufuliwa.” Mke wangu, Mairambubu, alisikia maneno hayo alipokuwa akisafiri ndani ya basi. Alikuwa na hamu ya kujua na kujifunza mengi zaidi. Basi liliposimama na abiria kushuka, alimfuata upesi mwanamke aliyekuwa amesema maneno hayo. Jina la mwanamke huyo lilikuwa Apun Mambetsadykova, na alikuwa Shahidi wa Yehova. Siku hizo, ilikuwa hatari kuzungumza na Mashahidi wa Yehova, lakini mambo tuliyojifunza kutoka kwa Apun yalibadili maisha yetu.

KUFANYA KAZI ASUBUHI MPAKA JIONI

Nilizaliwa mwaka wa 1937 kwenye shamba la ushirika karibu na jiji la Tokmok, nchini Kyrgyzstan. Mimi na familia yetu ni wa jamii ya Wakyrgyz, na tunazungumza Kikyrgyz. Wazazi wangu walikuwa vibarua wa shambani, na walifanya kazi kwenye shamba hilo la ushirika kuanzia asubuhi mpaka jioni. Vibarua walipewa chakula kwa ukawaida, lakini walilipwa mshahara wao kwa pesa taslimu mara moja tu kwa mwaka. Mama alipambana sana ili kunitunza mimi na mdogo wangu wa kike. Baada ya kwenda shule kwa miaka mitano tu, mimi pia nilianza kufanya kazi kila siku kwenye shamba la ushirika.

Milima ya Teskey Ala-Too

Katika eneo nililoishi kulikuwa na umaskini mwingi, na mtu alichoka sana kufanya kazi ili ajiruzuku. Nikiwa kijana, sikufikiria kwa uzito kuhusu kusudi la uhai au kuhusu wakati wangu ujao. Sikuwazia kamwe kwamba kweli zenye kuvutia kumhusu Yehova Mungu na kusudi lake zingebadili maisha yangu. Jinsi ujumbe huo ulivyofika na kuenea hapa nchini Kyrgyzstan ni hadithi yenye kusisimua. Yote hayo yalianzia katika eneo la nyumbani kwetu lililoko kaskazini mwa Kyrgyzstan.

WATU WALIOHAMISHWA ZAMANI WALETA KWELI KYRGYZSTAN

Kweli kumhusu Yehova Mungu iliingia nchini Kyrgyzstan miaka ya 1950. Ili watu wajifunze kweli, walihitaji kushinda sera fulani iliyokuwa imekita mizizi. Kwa nini? Nchi ambayo sasa inajulikana kuwa Kyrgyzstan ilikuwa sehemu ya Muungano wa Jamhuri za Kisoshalisti za Sovieti (USSR). Kotekote katika Muungano huo, Mashahidi wa Yehova hawakujihusisha na mambo ya kisiasa. (Yoh. 18:36) Kwa sababu hiyo, walinyanyaswa kwa kuwa walionwa kuwa maadui wa serikali ya Kikomunisti. Lakini hakuna sera yoyote inayoweza kuzuia Neno la Mungu lipenye katika mioyo ya watu wanyoofu. Kwa hakika, mojawapo ya mambo yenye thamani sana ambayo nimejifunza katika kipindi chote cha maisha yangu ni kwamba “mambo yote yanawezekana” kwa Yehova.—Marko 10:27.

Emil Yantzen

Mnyanyaso ambao Mashahidi wa Yehova walikabili ulifanya idadi yao iongezeke nchini Kyrgyzstan. Jinsi gani? Eneo la Siberia ambapo maadui wa serikali ya Kikomunisti walipelekwa uhamishoni, lilikuwa pia sehemu ya Muungano wa USSR. Watu hao waliohamishwa walipoachiliwa huru, wengi wao walikuja Kyrgyzstan, na baadhi yao walikuwa Mashahidi. Emil Yantzen alikuwa mmoja wao, na alikuwa amezaliwa nchini Kyrgyzstan mwaka wa 1919. Emil alikuwa amepelekwa katika kambi ya mateso na akiwa huko alikutana na Mashahidi wa Yehova. Alikubali kweli na akarudi nyumbani mwaka wa 1956. Emil aliishi karibu na mji wa Sokuluk, ulio katika eneo la nyumbani kwetu. Kutaniko la kwanza nchini Kyrgyzstan lilianzishwa katika mji wa Sokuluk mwaka wa 1958.

Victor Vinter

Mwaka mmoja hivi baadaye, Victor Vinter alihamia Sokuluk. Ndugu huyo mwaminifu alikabili hali ngumu tena na tena. Katika pindi mbili tofauti, alitumikia vifungo vya miaka mitatu gerezani kwa kutojihusisha na mambo ya kisiasa; halafu akatumikia kifungo cha miaka mingine kumi gerezani na kisha akapelekwa uhamishoni kwa miaka mitano. Lakini licha ya hayo, mnyanyaso haukuzuia ibada ya kweli iendelee kuenea.

KWELI YAFIKA KARIBU NA NYUMBANI

Eduard Varter

Kufikia mwaka wa 1963 kulikuwa na Mashahidi 160 hivi nchini Kyrgyzstan na wengi wao walikuwa na asili ya Ujerumani, Ukrainia, na Urusi. Mmoja wao alikuwa Eduard Varter, ndugu ambaye alikuwa amerudi kutoka uhamishoni na ambaye alikuwa amebatizwa huko Ujerumani mwaka wa 1924. Katika miaka ya 1940, Wanazi walimpeleka Eduard kwenye kambi ya mateso, na miaka michache baadaye, Wakomunisti wa Muungano wa USSR wakampeleka uhamishoni. Mwaka wa 1961 ndugu huyo mwaminifu alihamia katika mji wa Kant, ulio karibu sana na mji wa nyumbani.

Elizabeth Fot; Aksamai Sultanalieva

Pia, Elizabeth Fot, mtumishi mwingine mwaminifu wa Yehova aliishi katika mji wa Kant. Alifanya kazi ya kushona nguo. Kwa kuwa alikuwa fundi stadi, wataalamu kama vile madaktari na walimu walikuja kwake ili awashonee nguo. Mmoja wa wateja wake alikuwa mwanamke aliyeitwa Aksamai Sultanalieva, ambaye alikuwa ameolewa na mtu fulani mwenye cheo katika ofisi ya mwendesha-mashtaka wa umma. Siku moja, Aksamai alikuja kwa Elizabeth kuchukua nguo fulani, na aliuliza maswali mengi kuhusu kusudi la uhai na hali ya wafu. Elizabeth alijibu maswali yake moja kwa moja kwa kutumia Biblia. Punde si punde, Aksamai akawa mhubiri mwenye bidii wa habari njema.

Nikolai Chimpoesh

Karibu na kipindi hicho, Nikolai Chimpoesh, kutoka Moldova, aliwekwa kuwa mwangalizi wa mzunguko na alitumikia kwa miaka 30 hivi. Nikolai hakuyazungukia tu makutaniko, bali pia alisimamia kazi ya kunakili na kusambazwa kwa machapisho yetu. Hata hivyo, wenye mamlaka waligundua kazi yake. Hivyo, Eduard Varter alimpa Nikolai ushauri huu wenye kutia moyo: “Wenye mamlaka watakapokuhoji, waambie wazi kwamba sisi hupokea machapisho yetu kutoka makao makuu yaliyoko Brooklyn. Mtazame ofisa wa KGB moja kwa moja usoni. Huna sababu ya kuogopa.”—Mt. 10:19.

Apun Mambetsadykova

Muda mfupi baada ya mazungumzo hayo, Nikolai aliombwa kufika katika makao makuu ya KGB yaliyokuwa katika mji wa Kant. Anasimulia kilichotukia: “Ofisa huyo aliniuliza mahali tunakotoa machapisho yetu. Nikamwambia tunayatoa Brooklyn. Hakujua aseme nini. Aliniruhusu tu niondoke na hakuwahi kuniita tena.” Mashahidi kama hao jasiri waliendelea kueneza habari njema kwa tahadhari katika eneo la nyumbani kaskazini mwa Kyrgyzstan. Kweli zenye thamani kumhusu Yehova mwishowe zilipofikia familia yetu miaka ya 1980, mke wangu Mairambubu, ndiye aliyekuwa wa kwanza kuzisikia.

MKE WANGU ATAMBUA KWELI MARA MOJA

Mairambubu anatoka katika eneo la Naryn nchini Kyrgyzstan. Siku moja katika mwezi wa Agosti 1974, alimtembelea mdogo wangu wa kike na ndipo tulipokutana kwa mara ya kwanza. Papo hapo nikampenda Mairambubu. Na siku hiyohiyo tukafunga ndoa.

Januari 1981 Mairambubu alipokuwa ndani ya basi akielekea sokoni, alisikia mazungumzo yaliyotajwa mwanzoni mwa simulizi hili. Mke wangu alitaka kusikia habari zaidi, hivyo akamuuliza mwanamke huyo jina lake na kumwomba anwani yake. Mwanamke huyo alimwambia kwamba anaitwa Apun, ingawa alifanya hivyo kwa tahadhari kwa sababu hata katika miaka ya 1980, shughuli za Mashahidi wa Yehova zilikuwa zimepigwa marufuku. Badala ya kumpa anwani yake, Apun alichukua anwani ya mke wangu. Mke wangu alifika nyumbani akiwa amesisimuka sana.

Mairambubu alisema hivi: “Nimesikia mambo mazuri sana. Mwanamke fulani aliniambia kwamba hivi karibuni watu hawatakufa tena. Hata wanyama wa mwituni hawatakuwa wakali.” Maneno ya mke wangu yalisikika kama hadithi. Nikamwambia, “Acha tumsubiri atutembelee ili atufafanulie zaidi mambo hayo.”

Miezi mitatu baadaye, Apun alitutembelea. Aliendelea kututembelea, nasi tulipata fursa ya kukutana na baadhi ya Mashahidi wa kwanza kutoka jamii ya Wakyrgyz. Dada hao walitufundisha kweli zenye kusisimua kumhusu Yehova na kusudi lake kwa wanadamu. Walitusomea kitabu Kutoka Paradiso Iliyopotea Mpaka Paradiso Iliyopatikana. * Na kwa kuwa kulikuwa na nakala moja tu ya kitabu hicho katika jiji la Tokmok, tulinakili kwa mkono kitabu hicho.

Mojawapo ya mambo tuliyojifunza ni unabii unaopatikana katika kitabu cha Mwanzo 3:15. Yesu atatimiza unabii huo akiwa Mfalme wa Kimasihi aliyewekwa na Mungu. Huo ni ujumbe muhimu ambao kila mtu anapaswa kusikia! Hilo linatupatia sababu zaidi za kutangaza ujumbe huo. (Mt. 24:14) Muda si muda, kweli za Biblia zilianza kubadili maisha yetu.

MIKUTANO NA UBATIZO WAKATI WA MARUFUKU

Ndugu fulani kutoka Tokmok alitualika kwenye harusi. Baada ya muda mfupi, mimi na mke wangu tulitambua kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa tofauti sana. Hakukuwa na kileo chochote katika harusi hiyo, na sherehe iliendeshwa kwa utaratibu. Harusi hiyo ilitofautiana sana na harusi tulizokuwa tumehudhuria, ambapo wageni walikunywa pombe na kulewa, hawakuwa na nidhamu, na walitumia lugha chafu.

Pia, tulihudhuria baadhi ya mikutano katika kutaniko la Tokmok. Mikutano hiyo ilifanywa msituni hali ya hewa iliporuhusu. Ndugu na dada walijua kwamba polisi waliwapeleleza, hivyo ndugu mmoja aliwekwa ili kulinda doria. Katika majira ya baridi kali mikutano ilifanyiwa ndani ya nyumba. Mara kadhaa polisi walifika katika nyumba tuliyofanyia mikutano na walitaka kujua tulichokuwa tukifanya. Mimi na mke wangu Mairambubu tulipobatizwa mwezi wa Julai 1982 katika Mto Chüy, tulihitaji kuwa waangalifu. (Mt. 10:16) Akina ndugu waliwasili katika vikundi vidogo msituni na kukusanyika pamoja. Tuliimba wimbo wa Ufalme na kusikiliza hotuba ya ubatizo.

TUNAPATA FURSA YA KUPANUA HUDUMA YETU

Mwaka wa 1987 ndugu mmoja aliniomba nimtembelee mtu fulani aliyependezwa katika mji wa Balykchy. Ili kufika katika mji huo tulihitaji kusafiri kwa saa nne kwa gari moshi. Baada ya kuhubiri mara kadhaa katika mji wa Balykchy, tuligundua kwamba kulikuwa na watu wengi wanaopendezwa. Hiyo ilikuwa fursa mwafaka ya kupanua utumishi wetu.

Mimi pamoja na Mairambubu tulisafiri mara kwa mara kwenda Balykchy. Tulikaa huko kwa miisho juma kadhaa, tukihubiri na kufanya mikutano. Watu wengi zaidi walianza kuomba machapisho yetu. Tulitumia mishok, gunia la kubebea viazi kusafirisha machapisho yetu kwenda Tokmok. Magunia mawili ya machapisho kila mwezi hayakutosha kukidhi uhitaji uliokuwepo. Hata tulipokuwa tukisafiri kwenda na kurudi kutoka Balykchy, tulipata fursa za kuwahubiria wasafiri wenzetu.

Katika mwaka wa 1995 kutaniko lilianzishwa katika mji wa Balykchy—miaka minane tangu tulipotembelea mji huo kwa mara ya kwanza. Safari za kutoka Tokmok kwenda Balykchy ziligharimu pesa nyingi sana. Tulifaulu jinsi gani ilhali kipato chetu kilikuwa kidogo? Ndugu mmoja alijitolea kwa ukawaida kutuongezea pesa ili kulipia gharama hizo. Yehova aliona tamaa tuliyokuwa nayo ya kupanua utumishi wetu, naye akatufungulia “malango ya mbinguni ya mafuriko.” (Mal. 3:10) Kwa hakika mambo yote yanawezekana kwa Yehova!

BIDII KATIKA KUTUNZA FAMILIA NA KATIKA HUDUMA

Katika mwaka wa 1992, niliwekwa kuwa mzee wa kutaniko—mzee wa kwanza wa jamii ya Wakyrgyz nchini Kyrgyzstan. Katika kutaniko letu la nyumbani jijini Tokmok, fursa mpya za kuongeza utumishi zilijitokeza. Tulijifunza Biblia na vijana wengi Wakyrgyz ambao walikuja kusoma kwenye taasisi za elimu. Mmoja wa wanafunzi hao ambaye tulijifunza naye Biblia sasa anatumikia katika Halmashauri ya Tawi, na wengine wawili ni mapainia wa pekee. Pia, tulijitahidi kuwasaidia wengine mikutanoni. Katika miaka ya mapema ya 1990, Kirusi ndicho kilichotumiwa mikutanoni na katika machapisho yetu. Lakini idadi kubwa zaidi ya akina ndugu na dada kutanikoni walizungumza Kikyrgyz, lugha yao ya mama. Hivyo niliwatafsiria, jambo lililowasaidia kuelewa kweli za Biblia vizuri zaidi.

Mimi na mke wangu pamoja na watoto wetu wanane mwaka wa 1989

Mimi na Mairambubu tulikuwa na shughuli nyingi ya kuwalea watoto wetu waliokuwa wakiongezeka. Tulihubiri pamoja na watoto wetu na tulienda nao mikutanoni. Binti yetu Gulsayra—aliyekuwa na umri wa miaka 12 tu wakati huo—alifurahia kuzungumza na wapita njia na kuwaambia kuhusu Biblia. Na watoto wetu walifurahia kukariri Maandiko. Hivyo watoto wetu, na baadaye wajukuu wetu, walikuwa na mengi ya kufanya kutanikoni. Kati ya watoto wetu 9 na wajukuu 11 ambao bado wako hai, 16 wanamtumikia Yehova au wanahudhuria mikutano pamoja na wazazi wao.

MABADILIKO MAKUBWA

Ndugu na dada zetu wapendwa walioanza kazi ya Yehova katika eneo letu katika miaka ya 1950, wanaweza kushangazwa na mabadiliko tuliyojionea. Kwanza, tangu miaka ya 1990, tumefurahia uhuru zaidi wa kuhubiri habari njema na kukusanyika katika vikundi vikubwa.

Mimi na mke wangu tukiwa katika huduma

Katika mwaka wa 1991 mimi na mke wangu tulihudhuria kusanyiko la kwanza kabisa katika jiji la Alma-Ata, ambalo sasa linaitwa Almaty, nchini Kazakhstan. Katika mwaka wa 1993, akina ndugu nchini Kyrgyzstan walifanya kusanyiko katika uwanja wa Spartak jijini Bishkek, kwa mara ya kwanza. Wahubiri walisafisha uwanja huo kwa juma zima kabla ya kusanyiko hilo. Msimamizi wa uwanja huo alifurahi sana hivi kwamba alituruhusu tutumie uwanja huo bila malipo.

Katika mwaka wa 1994, tulipiga hatua nyingine kubwa machapisho yetu yalipoanza kuchapishwa katika Kikyrgyz. Sasa machapisho yetu yanatafsiriwa kwa ukawaida katika Kikyrgyz kwenye ofisi ya tawi iliyopo jijini Bishkek. Tunafurahi kwamba katika mwaka wa 1998, kazi ya Mashahidi ilitambuliwa rasmi kisheria nchini Kyrgyzstan. Tengenezo limezidi kukua, na sasa kuna wahubiri zaidi ya 5,000. Leo, kuna makutaniko 83 na vikundi 25 katika Kichina, Kiingereza, Kikyrgyz, Kirusi, Kituruki, Kiuighuri, Kiuzbeki, na Lugha ya Ishara ya Kirusi. Ndugu na dada hao wapendwa kutoka malezi mbalimbali wanamtumikia Yehova kwa umoja. Mabadiliko hayo yote makubwa yamewezeshwa na Yehova.

Pia, Yehova alibadili maisha yangu. Nililelewa katika familia ya wakulima maskini na nilienda shule kwa miaka mitano tu. Lakini Yehova alinitumia kama mzee wa kutaniko na pia kuwafundisha watu wenye elimu kubwa zaidi yangu kweli zenye thamani za Biblia. Kwa hakika, Yehova hufanya hata mambo yasiyo ya kawaida yatendeke. Mambo niliyojionea hunichochea niendelee kwa ushikamanifu kutoa ushahidi kumhusu Yehova, ambaye kwake “mambo yote yanawezekana.”—Mt. 19:26.

^ fu. 21 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova lakini sasa hakichapishwi tena.