Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Shangwe​—Sifa Inayotoka kwa Mungu

Shangwe​—Sifa Inayotoka kwa Mungu

KWA kawaida watu hutamani kuwa na maisha yenye shangwe. Lakini katika siku hizi za mwisho, kila mtu anapambana na hali ambazo ni “ngumu kushughulika nazo.” (2 Tim. 3:1) Ukosefu wa haki, afya mbaya, ukosefu wa ajira, huzuni, au mambo mengine yanayosababisha mahangaiko na majonzi yanaweza kuwafanya baadhi ya watu wapoteze shangwe yao hatua kwa hatua. Hata watumishi wa Mungu wanaweza kuvunjika moyo na kupoteza shangwe yao. Ikiwa umepatwa na hali hiyo, unaweza kufanya nini ili kurudisha shangwe uliyokuwa nayo mwanzoni?

Ili tupate jibu la swali hilo, tunahitaji kwanza kuelewa maana ya shangwe ya kweli na jinsi ambavyo wengine wamedumisha shangwe yao licha ya matatizo. Kisha tutajifunza mambo tunayoweza kufanya ili kudumisha na hata kuongeza shangwe tuliyo nayo.

SHANGWE NI NINI?

Hatupaswi kufikiri kwamba kuwa wenye shangwe kunamaanisha tu kusisimuka au kuwa wachangamfu. Kwa mfano, baada ya kunywa pombe nyingi mlevi anaweza kuanza kucheka sana. Hata hivyo, anapotokwa na ulevi, kicheko chake huisha naye hurudia maisha yaliyojaa huzuni na matatizo. Uchangamfu wake wa muda mfupi haukuwa shangwe ya kweli.—Met. 14:13.

Tofauti na hilo shangwe ni sifa inayotoka moyoni. Imefafanuliwa kuwa “hisia ambayo mtu hupata kwa sababu ya kupata kitu fulani kizuri au kutarajia jambo fulani zuri.” Shangwe ni hali ya kuwa na furaha, hali ambayo huendelea kuwepo iwe mambo yanayotuzunguka ni mazuri au mabaya. (1 The. 1:6) Kwa kweli, mtu anaweza kusumbuliwa na jambo fulani lakini bado akawa na shangwe moyoni. Kwa mfano, mitume walipigwa mijeledi kwa sababu ya kuzungumza kumhusu Kristo. Lakini licha ya hayo “[walitoka] mbele ya Sanhedrini, wakishangilia kwa sababu walikuwa wamestahili kuvunjiwa heshima kwa ajili ya jina lake.” (Mdo. 5:41) Ni wazi kwamba hawakuwa wakishangilia kwa sababu ya kupigwa mijeledi. Lakini kwa kuwa walikuwa watumishi wa Mungu, walipata shangwe ya kweli kwa kudumisha utimilifu wao kwake.

Hatuzaliwi tukiwa na shangwe kama hiyo, wala haijitokezi tu. Kwa nini? Kwa sababu shangwe ya kweli ni sehemu ya tunda la roho takatifu ya Mungu. Kwa msaada wa roho ya Mungu, tunaweza kusitawisha kikamili “utu mpya,” ambao unatia ndani sifa ya shangwe. (Efe. 4:24; Gal. 5:22) Na tunapositawisha sifa ya shangwe, inakuwa rahisi zaidi kwetu kukabiliana na mikazo ya maisha.

VIELELEZO AMBAVYO TUNGEPENDA KUIGA

Yehova alikusudia mambo mazuri yawepo duniani, bali si mambo mabaya tunayojionea leo hii. Hata hivyo, matendo maovu ya wengine hayamnyang’anyi Yehova shangwe yake. Neno la Mungu linasema hivi: “Katika makao yake kuna nguvu na shangwe.” (1 Nya. 16:27) Isitoshe, mambo mazuri yanayotimizwa na watumishi wake huufanya “moyo [wa Yehova] ushangilie.”—Met. 27:11.

Tunaweza kumwiga Yehova kwa kuepuka kuhangaika kupita kiasi ikiwa mambo hayaendi kama tulivyotarajia. Badala ya kupoteza shangwe yetu, tunaweza kukazia fikira mambo mazuri tuliyo nayo kwa sasa huku tukingojea kwa subira mambo mazuri ya wakati ujao. *

Pia, kuna vielelezo vingi katika Biblia vya watu waliodumisha shangwe yao licha ya matatizo. Mmoja wao ni Abrahamu ambaye alivumilia hali zilizohatarisha maisha yake na hali ngumu zilizosababishwa na wengine. (Mwa. 12:10-20; 14:8-16; 16:4, 5; 20:1-18; 21:8, 9) Licha ya hali hizo zenye mikazo mingi, Abrahamu alidumisha shangwe moyoni mwake. Alifanyaje hivyo? Tumaini la kuishi katika ulimwengu mpya chini ya utawala wa Kimasihi lilikuwa halisi akilini mwake. (Mwa. 22:15-18; Ebr. 11:10) Yesu alisema hivi: “Baba yenu Abrahamu alishangilia sana tazamio la kuona siku yangu.” (Yoh. 8:56) Tunaweza kumwiga Abrahamu kwa kutafakari kuhusu shangwe tutakayopata wakati ujao.—Rom. 8:21.

Kama Abrahamu, mtume Paulo na mwandamani wake Sila walikazia fikira ahadi za Mungu. Walikuwa na imani yenye nguvu, na waliendelea kudumisha shangwe yao licha ya kukumbana na matatizo. Kwa mfano, baada ya kupigwa vibaya sana na kufungwa gerezani, “katikati ya usiku, Paulo na Sila walikuwa wakisali na kumsifu Mungu kwa wimbo.” (Mdo. 16:23-25) Ingawa waliimarishwa na tumaini walilokuwa nalo, Paulo na Sila walikuwa na shangwe kwa sababu walikuwa wakiteseka kwa ajili ya jina la Kristo. Tunaweza kumwiga Paulo na Sila kwa kuendelea kukumbuka mambo mazuri tunayopata kwa sababu ya kumtumikia Mungu kwa uaminifu.—Flp. 1:12-14.

Leo, undugu wetu unatia ndani mifano mingi mizuri ya watu ambao wamedumisha shangwe yao licha ya kukabili majaribu. Kwa mfano, katika mwezi wa Novemba 2013, Kimbunga Haiyan kilipiga kwenye eneo lililo katikati ya nchi ya Filipino, na kuharibu zaidi ya nyumba 1000 za familia za Mashahidi. George, ambaye nyumba yake iliharibiwa kabisa katika jiji la Tacloban, anasema hivi: “Licha ya mambo yote yaliyotukia, akina ndugu wana furaha. Ni vigumu kwangu kueleza shangwe tunayohisi.” Kila mara tunapokabili matatizo makubwa, tutaendelea kuwa na shangwe ikiwa tutatafakari na kuthamini mambo ambayo Yehova ametufanyia. Yehova ameandaa mambo gani mengine yanayotupatia sababu za kuwa na shangwe?

SABABU ZA KUWA NA SHANGWE

Hakuna sababu kubwa zaidi ya kuwa na shangwe kuliko kuwa na uhusiano mzuri na Mungu. Hebu fikiria hili: Tunamjua Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote. Yeye ni Baba yetu, Mungu wetu, na Rafiki yetu!—Zab. 71:17, 18.

Pia, tunathamini zawadi ya uhai na uwezo tulio nao wa kuifurahia. (Mhu. 3:12, 13) Tukiwa viumbe wenye akili ambao Yehova ametuvuta kwake, tunaelewa kusudi la Mungu kutuelekea. (Kol. 1:9, 10) Hivyo, tunajua kusudi halisi la maisha yetu na tunajua kwa nini tupo hai. Kwa upande mwingine, watu wengi hawajui vizuri kusudi la kuwa hai. Akikazia tofauti hiyo, Paulo aliandika hivi: “‘Jicho halijaona na sikio halijasikia, wala hayajawaziwa katika moyo wa mwanadamu mambo ambayo Mungu amewatayarishia wale wanaompenda.’ Kwa maana Mungu ameyafunua kwetu kupitia roho yake.” (1 Kor. 2:9, 10) Je, hatushangilii kwa sababu tunaelewa mapenzi ya Yehova na kusudi lake?

Fikiria jambo lingine ambalo Yehova amewafanyia watu wake. Je, hatufurahi kwamba dhambi zetu zinaweza kusamehewa? (1 Yoh. 2:12) Kwa sababu ya rehema za Mungu, tuna tumaini hakika kwamba ulimwengu mpya utakuja hivi karibuni. (Rom. 12:12) Hata sasa, Yehova amewezesha kuwe na kikundi chenye kuburudisha cha waabudu wenzetu. (Zab. 133:1) Pia, Neno la Mungu linatuhakikishia kwamba Yehova huwalinda watu wake dhidi ya Shetani na roho wake waovu. (Zab. 91:11) Tukitafakari kuhusu baraka hizo zote tunazopata kutoka kwa Mungu, shangwe yetu itakuwa yenye kina na itazidi kuongezeka.—Flp. 4:4.

JINSI YA KUONGEZA SHANGWE YAKO

Je, inawezekana kwa Mkristo ambaye tayari ana shangwe kuongeza shangwe yake? Yesu alisema hivi: “Nimewaambia mambo haya, ili shangwe yangu iwe ndani yenu na shangwe yenu ijae.” (Yoh. 15:11) Je, hilo halionyeshi kwamba shangwe yetu inaweza kuongezeka? Unaweza kulinganisha jitihada za kuongeza shangwe yako na jinsi tunavyochochea moto. Ni lazima uongeze kuni kwenye moto ili moto uongezeke. Vivyo hivyo, ni lazima ujilishe kiroho ili shangwe yako iongezeke. Kumbuka: Shangwe huchochewa na roho takatifu. Hivyo, utakuwa na shangwe nyingi zaidi ikiwa utamwomba Yehova roho yake takatifu kwa ukawaida na ikiwa utasali na kutafakari kuhusu Neno lake lililoongozwa na roho.—Zab. 1:1, 2; Luka 11:13.

Vilevile, utaongeza shangwe yako kwa kujihusisha kikamili katika kazi zinazomfurahisha Yehova. (Zab. 35:27; 112:1) Kwa nini? Kwa sababu tuliumbwa ili ‘tumwogope Mungu wa kweli na tushike amri zake, kwa maana huo ndio wajibu wote wa mwanadamu.’ (Mhu. 12:13) Kwa maneno mengine, tuliumbwa ili tufanye mapenzi ya Mungu. Hivyo, kiasili tunafurahia zaidi maisha tunapomtumikia Yehova. *

FAIDA ZA KUWA NA SHANGWE

Kadiri tunavyositawisha shangwe inayotoka kwa Mungu, ndivyo tutakavyopata faida nyingine zinazozidi hisia tulizo nazo za shangwe. Kwa mfano, tutamfurahisha zaidi Baba yetu wa mbinguni tukiendelea kumtumikia kwa shangwe hata iwe tunakabili matatizo ya aina gani. (Kum. 16:15; 1 The. 5:16-18) Pia, shangwe ya kweli itatusaidia kupinga mwelekeo wa kufuatia maisha ya kupenda vitu vya kimwili na badala yake tutatafuta fursa za kujidhabihu zaidi kwa ajili ya Ufalme wa Mungu. (Mt. 13:44) Tunapojionea manufaa tunayopata kwa kujidhabihu kwa njia hiyo, shangwe yetu itaongezeka, tutafurahia hali njema zaidi maishani, na tutachangia furaha ya wengine.—Mdo. 20:35; Flp. 1:3-5.

“Ikiwa una furaha na umeridhika na maisha yako sasa, inaelekea kwamba utakuwa na afya nzuri wakati ujao.” Hivyo ndivyo mtafiti mmoja kutoka Chuo Kikuu cha Nebraska nchini Marekani alivyoandika baada ya kuchunguza utafiti mbalimbali uliofanywa kuhusu afya. Maneno yake yanaungwa mkono na Biblia, ambayo inasema hivi: “Moyo wenye shangwe ni dawa nzuri.” (Met. 17:22) Naam, kadiri shangwe yako inavyozidi kuongezeka, inaelekea ndivyo afya yako itakavyozidi kuwa nzuri zaidi.

Hivyo, licha ya kwamba tunaishi katika nyakati zenye mikazo mingi, tunaweza kusitawisha shangwe ya kweli na inayodumu kwa kupokea roho takatifu ambayo tunapata tunaposali, tunapojifunza, na tunapotafakari Neno la Yehova. Pia, tunaongeza shangwe yetu tunapotafakari kuhusu baraka tulizo nazo sasa, tunapoiga imani ya wengine, na tunapojitahidi kufanya mapenzi ya Mungu. Tukifanya hayo yote, tunaweza kujionea ukweli wa Zaburi 64:10, inayosema hivi: “Mwadilifu atashangilia kwa sababu ya Yehova na kumkimbilia.”

^ fu. 10 Sifa ya subira itazungumziwa katika makala itakayofuata katika mfululizo huu kuhusu “tunda la roho.”

^ fu. 20 Soma kuhusu njia nyingine za kuongeza shangwe yako katika sanduku, “ Njia Nyingine za Kuongeza Shangwe.”