Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ukumbusho Huwaunganisha Watu wa Mungu

Ukumbusho Huwaunganisha Watu wa Mungu

“Jinsi ilivyo vema na jinsi inavyopendeza . . . kukaa pamoja kwa umoja!”—ZAB. 133:1.

NYIMBO: 18, 14

1, 2. Ni tukio gani la mwaka wa 2018 litakalowaunganisha watu kuliko tukio lingine lolote, na kwa nini? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

JUA linapoanza kutua Machi 31, 2018, watu wa Mungu na wengine wengi wenye kupendezwa watakusanyika kwa ajili ya mwadhimisho wa kila mwaka wa Mlo wa Jioni wa Bwana. Dunia inapoendelea kuzunguka kwenye mhimili wake, mamilioni watakusanyika ili kuadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Kila mwaka, tukio hilo huwaunganisha watu kwa njia yenye kustaajabisha sana kuliko tukio lingine lolote duniani!

2 Tunaweza kuwazia jinsi ambavyo Yehova na Yesu wanafurahi wanapowaona wakazi wa dunia wakihudhuria tukio hilo la pekee, tangu siku hiyo inapoanza hadi inapokamilika. Biblia ilitabiri kwamba “umati mkubwa, ambao hakuna mtu [ambaye angeweza] kuuhesabu, kutoka mataifa yote na makabila na jamii na lugha” ungesema hivi kwa sauti kubwa: “Wokovu unatoka kwa Mungu wetu, anayeketi kwenye kiti cha ufalme, na kwa Mwanakondoo.” (Ufu. 7:9, 10) Inapendeza kuona jinsi ambavyo Yehova na Yesu wanaheshimiwa sana kupitia mwadhimisho wa kila mwaka wa Ukumbusho!

3. Makala hii itajibu maswali gani?

3 Maswali yafuatayo yatajibiwa katika makala hii. (1) Sisi binafsi tunaweza kujitayarishaje kwa ajili ya Ukumbusho na kunufaika kwa kuhudhuria? (2) Ukumbusho huchochea umoja wa watu wa Mungu katika njia zipi? (3) Sisi binafsi tunaweza kuchangiaje umoja huo? (4) Je, kutakuwa na Ukumbusho wa mwisho? Ikiwa ndivyo, utakuwa lini?

JINSI YA KUJITAYARISHA NA KUNUFAIKA KWA KUHUDHURIA

4. Kwa nini ni muhimu sana tuwepo kwenye Ukumbusho?

4 Tafakari umuhimu wa kuhudhuria Ukumbusho. Kumbuka kwamba mikutano ya kutaniko ni sehemu ya ibada yetu. Bila shaka, Yehova na Yesu huwaona wale wote wanaojitahidi kuhudhuria mkutano huu muhimu zaidi katika mwaka. Na kwa kweli, tungependa waone kwamba sababu pekee ya kufanya tusihudhurie Ukumbusho ni kwamba afya au hali zinatuzuia kabisa kuhudhuria. Tunapoonyesha kwa matendo kwamba mikutano ya ibada ni muhimu kwetu, tunampa Yehova sababu zaidi za kuhifadhi jina letu katika “kitabu cha kumbukumbu,” yaani, “kitabu cha uzima”—kinachoandikwa majina ya wale wote walio na tumaini la kupata uzima wa milele.—Mal. 3:16; Ufu. 20:15.

5. Katika siku zinazotangulia Ukumbusho, tunawezaje ‘kujijaribu kama tuko katika imani’?

5 Katika siku zinazotangulia siku ya Ukumbusho, tunaweza kutenga wakati kusali na kuchunguza kwa makini uhusiano wetu na Yehova. (Soma 2 Wakorintho 13:5.) Tunaweza kufanya hivyo jinsi gani? Kwa ‘kujijaribu kama tuko katika imani.’ Ili tufanye hivyo, inafaa tujiulize hivi: ‘Je, ninaamini kabisa kwamba mimi ni sehemu ya tengenezo pekee ambalo Yehova amelikubali ili litimize mapenzi yake? Je, ninafanya yote niwezayo ili kuhubiri na kufundisha habari njema ya Ufalme? Je, matendo yangu yanaonyesha kwamba ninaamini kabisa kuwa hizi ni siku za mwisho na kwamba mwisho wa utawala wa Shetani umekaribia? Je, uhakika nilionao sasa kumwelekea Yehova na Yesu unalingana na ule niliokuwa nao nilipojiweka wakfu kwa Yehova Mungu?’ (Mt. 24:14; 2 Tim. 3:1; Ebr. 3:14) Kutafakari majibu ya maswali kama hayo kutatusaidia kuendelea kuthibitisha jinsi sisi wenyewe tulivyo.

6. (a) Njia pekee ya kupata uzima ni ipi? (b) Kila mwaka, mzee mmoja hujitayarishaje kwa ajili ya Ukumbusho, nawe unawezaje kufanya jambo kama hilo?

6 Soma na kutafakari habari za Kimaandiko zinazozungumzia umuhimu wa Ukumbusho. (Soma Yohana 3:16; 17:3.) Njia pekee ya kupata uzima wa milele ni kwa ‘kumjua’ Yehova na ‘kumwamini’ Yesu, Mwana Wake mzaliwa pekee. Ili ujitayarishe kwa ajili ya Ukumbusho, kwa nini usichague miradi ya kujifunza itakayokusaidia kumkaribia zaidi Yehova na Yesu? Fikiria kile ambacho mzee fulani wa kutaniko, ambaye ametumikia kwa muda mrefu, amekuwa akifanya. Kwa miaka mingi, amekuwa akitunza makala za Mnara wa Mlinzi zinazozungumzia hasa Ukumbusho na upendo ambao Yehova na Yesu wametuonyesha. Katika majuma yanayotangulia Ukumbusho, yeye husoma tena makala hizo na kutafakari umuhimu wa mwadhimisho huo. Pindi fulani, yeye huongeza makala moja au mbili kwenye makala alizohifadhi. Mzee huyo ametambua kwamba anajifunza mambo mapya kila mwaka kwa kusoma tena makala hizo na kusoma na kutafakari usomaji wa Biblia wa Ukumbusho. Jambo muhimu hata zaidi, anahisi kwamba upendo wake kwa Yehova na Yesu huongezeka mwaka baada ya mwaka. Mradi kama huo wa kujifunza unaweza kukusaidia kumpenda na kumthamini zaidi Yehova na Yesu, na hivyo kunufaika kikamili zaidi na Ukumbusho.

JINSI UKUMBUSHO UNAVYOCHOCHEA UMOJA WETU

7. (a) Yesu alisali kuhusu nini katika usiku ambao Mlo wa Jioni wa Bwana ulianzishwa? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova amejibu sala ya Yesu?

7 Katika usiku ambao Mlo wa Jioni wa Bwana ulianzishwa, Yesu alisali kwamba wafuasi wake wote waunganishwe na kufurahia umoja ambao yeye na Baba yake wanafurahia. (Soma Yohana 17:20, 21.) Kwa hakika, Yehova amejibu sala hiyo ya Mwana wake mpendwa, na sasa mamilioni wanaamini kwamba Yehova alimtuma Mwana wake. Kati ya mikutano yote ya watu wa Mungu, Ukumbusho ndio mkutano unaotoa uthibitisho usioweza kupingwa wa umoja ambao Mashahidi wa Yehova wanao. Watu wa mataifa na jamii mbalimbali hukutanika pamoja ulimwenguni pote. Katika maeneo mengine, ni jambo lenye kudharaulika au lisilo la kawaida kwa watu wa jamii tofauti kukusanyika pamoja kwenye mkutano wa kidini. Lakini umoja kama huo ni wenye kupendeza machoni pa Yehova na Yesu!

8. Yehova alimpa Ezekieli ujumbe gani unaohusu umoja?

8 Tukiwa watu wa Yehova hatushangazwi na umoja tunaofurahia. Isitoshe, Yehova alitabiri kuhusu umoja huo. Fikiria ujumbe ambao alimpa nabii Ezekieli kuhusu kuunganishwa kwa vijiti viwili, kijiti kimoja “kwa ajili ya Yuda” na kijiti kingine “kwa ajili ya Yosefu.” (Soma Ezekieli 37:15-17.) Makala ya “Maswali Kutoka Kwa Wasomaji” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Julai 2016 ilieleza hivi: “Yehova alimpa Ezekieli ujumbe wa tumaini akiahidi kuliunganisha taifa la Israeli baada ya kurudi kwenye Nchi ya Ahadi. Pia, ujumbe huo ulitabiri kuunganishwa kwa watu wa Mungu kulikoanza katika kipindi cha siku za mwisho.”

9. Utimizo wa unabii wa Ezekieli unaonekana jinsi gani kila mwaka katika Ukumbusho?

9 Kuanzia mwaka wa 1919 na kuendelea, hatua kwa hatua Yehova alianza kuwapanga upya na kuwaunganisha tena watiwa mafuta ambao wanafananishwa na kijiti “kwa ajili ya Yuda.” Kisha, kadiri wale walio na tumaini la kuishi duniani, ambao wanafananishwa na kijiti “kwa ajili ya Yosefu,” walivyozidi kujiunga na watiwa mafuta, vikundi vyote viwili vikawa “kundi moja.” (Yoh. 10:16; Zek. 8:23) Yehova aliahidi kuunganisha vijiti hivyo na kuvifanya kuwa kijiti kimoja mkononi mwake. (Eze. 37:19) Sasa vikundi vyote viwili vinatumikia kwa umoja chini ya Mfalme mmoja—Yesu Kristo aliyetukuzwa, ambaye anatajwa kwa njia ya kinabii kuwa ‘Daudi, mtumishi’ wa Mungu. (Eze. 37:24, 25) Umoja wenye thamani unaoelezwa katika kitabu cha Ezekieli huonekana wazi kila mwaka watiwa mafuta na “kondoo wengine” wanapokusanyika ili kuadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Yesu! Hata hivyo, sisi mmoja-mmoja tunaweza kufanya nini ili kuchangia umoja huo?

JINSI KILA MMOJA WETU ANAVYOWEZA KUCHANGIA UMOJA

10. Tunaweza kufanya nini ili kuchangia umoja miongoni mwa watu wa Mungu?

10 Njia ya kwanza ya kuchangia umoja wa watu wa Mungu ni kusitawisha sifa ya unyenyekevu. Alipokuwa duniani, Yesu aliwahimiza wanafunzi wake wawe wanyenyekevu. (Mt. 23:12) Tukiwa wanyenyekevu moyoni, hatutakuwa na roho ya ulimwengu ya kujikweza. Badala yake, unyenyekevu wetu utatusaidia kujitiisha kwa wale wanaoongoza, na roho hiyo ya utii ni muhimu ili kuwe na umoja kutanikoni. Zaidi ya yote, unyenyekevu wetu utamfurahisha Mungu, ambaye “huwapinga wenye majivuno, lakini huwapa wanyenyekevu fadhili zisizostahiliwa.”—1 Pet. 5:5.

11. Kutafakari maana ya mifano ya Ukumbusho kutatusaidiaje kuchangia umoja?

11 Njia ya pili ya kuchangia umoja ni kutafakari maana ya mifano inayotumiwa katika Ukumbusho. Kabla ya usiku huo wa pekee, na hasa jioni hiyo ya Ukumbusho, fikiria kwa uzito maana ya mkate usiotiwa chachu na divai nyekundu. (1 Kor. 11:23-25) Mkate unafananisha mwili wa Yesu usio na dhambi uliotolewa kuwa dhabihu, na divai inafananisha damu yake iliyomwagwa. Lakini tunahitaji kufanya mengi zaidi ya kuelewa tu maana ya mifano hiyo. Kumbuka kwamba dhabihu ya fidia ya Kristo inahusisha upendo mkuu zaidi ulioonyeshwa katika njia mbili—upendo ambao Yehova alionyesha kwa kumtoa Mwana wake kwa niaba yetu, na upendo ambao Yesu alionyesha kwa kutoa uhai wake kwa hiari kwa ajili yetu. Kutafakari upendo ambao Yehova na Yesu walituonyesha kunapaswa kutuchochea kuwapenda pia. Nao upendo ambao sisi pamoja na waabudu wenzetu tunao kumwelekea Yehova hutuunganisha na kuimarisha kifungo chetu cha umoja.

Tunapowasamehe wengine tunachangia umoja (Tazama fungu la 12 na 13)

12. Katika mfano wa mfalme na watumwa wake, Yesu alionyeshaje wazi kwamba Yehova anatarajia tuwe tukiwasamehe wengine?

12 Njia ya tatu ya kuchangia umoja ni kuwasamehe wengine kwa hiari. Tunapowasamehe wanaotukosea, tunaonyesha kwamba tunathamini msamaha wa dhambi zetu wenyewe ambao unawezekana tu kwa sababu ya dhabihu ya fidia ya Kristo. Fikiria mfano wa Yesu unaopatikana katika Mathayo 18:23-34. Jiulize hivi: ‘Je, ninachochewa kutumia yale ambayo Yesu alifundisha? Je, mimi huwaonyesha subira waabudu wenzangu na kuelewa hali zao? Je, niko tayari kuwasamehe wale wanaonikosea?’ Ni kweli kwamba makosa hutofautiana, na kuna makosa ambayo ni vigumu sana kwa wanadamu wasio wakamilifu kusamehe. Hata hivyo, mfano huo unatufundisha kile ambacho Yehova anatarajia tufanye. (Soma Mathayo 18:35.) Yesu anaonyesha wazi kwamba Yehova hatatusamehe ikiwa hatutawasamehe ndugu zetu iwapo kuna msingi mzuri wa kufanya hivyo. Hilo ni jambo zito sana! Tunalinda na kudumisha umoja wetu wenye thamani tunapowasamehe wengine kama Yesu alivyotufundisha kufanya.

13. Tunapofanya amani na wengine tunachangiaje umoja?

13 Tunapowasamehe wengine tunaonyesha kwamba tunapenda kufanya amani. Kumbuka shauri la mtume Paulo linalosema kwamba tunapaswa “[kujitahidi] sana kudumisha roho ya umoja katika kifungo cha muungano cha amani.” (Efe. 4:3) Katika majira haya ya Ukumbusho na hasa jioni hiyo ya Ukumbusho, fikiria kwa uzito jinsi unavyowatendea wengine. Jiulize hivi: ‘Je, watu huona waziwazi kwamba mimi ni mtu asiyewawekea wengine kinyongo? Je, ninajulikana kuwa mtu anayefanya juu chini kuchangia amani na umoja?’ Hayo ni maswali muhimu sana tunayopaswa kutafakari katika kipindi hiki cha mwaka.

14. Tunaweza kuonyeshaje kwamba ‘tunavumiliana kwa upendo’?

14 Njia ya nne ya kuchangia umoja ni kumwiga Yehova, Mungu wa upendo. Tunamwiga kwa kuwapenda wengine. (1 Yoh. 4:8) Hatungependa kamwe kusema hivi kuwahusu waabudu wenzetu, “Ni lazima niwapende kwa sababu ni ndugu zangu lakini si lazima nipendezwe nao”! Fikira za namna hiyo ni kinyume na shauri la Paulo linalosema kwamba tunapaswa ‘kuvumiliana kwa upendo.’ (Efe. 4:2) Ona kwamba hakusema tunapaswa tu ‘kuvumiliana.’ Aliongeza kwamba tunapaswa kuvumiliana “kwa upendo.” Hivyo, kuna tofauti. Katika makutaniko yetu kuna watu wa namna mbalimbali ambao Yehova amewavuta kwake. (Yoh. 6:44) Kwa kuwa Yehova amewavuta kwake, lazima kuwe na jambo linalomfanya awapende. Basi ni nani miongoni mwetu anayeweza kusema kwamba mwabudu mwenzetu hastahili kuonyeshwa upendo? Hatupaswi kamwe kukataa kuwaonyesha ndugu zetu upendo ambao Yehova ametuamuru tuwaonyeshe!—1 Yoh. 4:20, 21.

UKUMBUSHO WA MWISHO UTAKUWA LINI?

15. Tunajuaje kwamba kutakuwa na Ukumbusho wa mwisho?

15 Siku moja Ukumbusho utaadhimishwa kwa mara ya mwisho. Tunajuaje? Katika barua yake ya kwanza kwa Wakorintho iliyoongozwa na roho, Paulo aliwaandikia Wakristo watiwa mafuta kwamba kwa kukumbuka kifo cha Yesu kila mwaka “[wanaendelea] kukitangaza kifo cha Bwana, mpaka atakapokuja.” (1 Kor. 11:26) Neno “atakapokuja” linarejelea tukio lilelile la ‘kuja’ kwa Yesu ambalo alitaja katika unabii wake kuhusu wakati wa mwisho. Akizungumza kuhusu dhiki kuu ambayo imekaribia sana, Yesu alisema hivi: “Ishara ya Mwana wa binadamu [itaonekana] mbinguni, na makabila yote ya dunia yatajipigapiga kwa huzuni, nayo yatamwona Mwana wa binadamu akija juu ya mawingu ya mbinguni akiwa na nguvu na utukufu mwingi. Kisha [Yesu] atawatuma malaika zake pamoja na sauti kubwa ya tarumbeta, nao watawakusanya watu wake waliochaguliwa kutoka kwenye zile pepo nne za dunia, kuanzia mwisho mmoja wa mbingu mpaka mwisho mwingine.” (Mt. 24:29-31) Tukio hilo la ‘kukusanywa kwa waliochaguliwa’ linarejelea wakati ambapo Wakristo wote watiwa mafuta watakaokuwa wangali duniani watapokea thawabu yao ya kwenda mbinguni. Jambo hilo litatukia muda mfupi baada ya dhiki kuu kuanza lakini kabla ya vita ya Har–Magedoni. Kisha wale 144,000 watashirikiana na Yesu kuwashinda wafalme wa dunia. (Ufu. 17:12-14) Ukumbusho wa mwisho utakaoadhimishwa kabla ya tukio hilo la kukusanywa kwa watiwa mafuta kwenda mbinguni utakuwa ndio wa mwisho kuadhimishwa kwa sababu Yesu atakuwa ‘amekuja.’

16. Kwa nini umeazimia kuhudhuria Ukumbusho mwaka huu?

16 Basi, acheni tuazimie kunufaika kibinafsi kwa kuhudhuria Ukumbusho Machi 31, 2018. Na tumwombe Yehova atusaidie kuendelea kuchangia umoja wa watu wake! (Soma Zaburi 133:1.) Kumbuka, siku moja tutaadhimisha Ukumbusho wa mwisho. Kwa sasa, na tufanye yote tuwezayo ili kuhudhuria Ukumbusho na kuthamini umoja wenye kupendeza tunaofurahia wakati wa Ukumbusho.