Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Umpe Yule Aliye na Kila Kitu?

Kwa Nini Umpe Yule Aliye na Kila Kitu?

“Ee Mungu wetu, tunakushukuru na kulisifu jina lako linalovutia.”—1 NYA. 29:13.

NYIMBO: 80, 50

1, 2. Yehova hutumiaje mali zake kwa ukarimu?

YEHOVA ni Mungu mkarimu. Vitu vyote tulivyo navyo vimetoka kwake. Yehova anamiliki dhahabu yote pamoja na fedha na maliasili zote zilizopo duniani, naye huzitumia kuendeleza uhai. (Zab. 104:13-15; Hag. 2:8) Biblia ina masimulizi mengi ya jinsi Yehova alivyotumia kimuujiza rasilimali zake ili kuwaandalia watu wake mahitaji yao.

2 Kwa miaka 40, Yehova aliwaandalia Waisraeli mana na maji walipokuwa nyikani. (Kut. 16:35) Hivyo, “hawakukosa chochote.” (Neh. 9:20, 21) Kupitia nabii Elisha, Yehova alifanya muujiza kwa kuzidisha kiasi kidogo cha mafuta ambacho mjane fulani mwaminifu alikuwa nacho. Zawadi hiyo aliyopokea kutoka wa Mungu ilimsaidia mjane huyo kulipa madeni yake na kubaki na pesa za kutosha kwa ajili yake na watoto wake. (2 Fal. 4:1-7) Kwa msaada wa Yehova, Yesu aliwaandalia watu chakula kimuujiza na pia pesa kulipokuwa na uhitaji.—Mt. 15:35-38; 17:27.

3. Tutazungumzia nini katika makala hii?

3 Yehova ana mali nyingi anazoweza kutumia ili kutegemeza viumbe wake walio duniani. Licha ya hilo, bado anawaalika watumishi wake watumie vitu vyao vya kimwili kutegemeza kazi ya tengenezo lake. (Kut. 36:3-7; soma Methali 3:9.) Kwa nini Yehova anatarajia tumpe vitu vyetu vyenye thamani? Watumishi waaminifu wa zamani walitegemezaje kifedha utendaji wa watu waliomwakilisha Yehova? Leo, tengenezo hutumiaje michango inayotolewa? Tutapata majibu ya maswali hayo katika makala hii.

KWA NINI TUNAMPA YEHOVA VITU VYETU?

4. Tunamthibitishia Yehova nini tunapotegemeza kazi yake?

4 Tunampa Yehova vitu vyetu kwa sababu tunampenda na kumthamini. Tunaguswa moyo sana tunapotafakari mambo yote ambayo Yehova ametutendea. Alipokuwa akieleza kuhusu mambo ambayo yangehitajika katika mradi wa ujenzi wa hekalu, Mfalme Daudi alikiri kwamba vitu vyote tunavyopokea hutoka kwa Yehova na chochote tunachompa kimetoka kwa vitu ambavyo tayari Yehova ametupatia.—Soma 1 Mambo ya Nyakati 29:11-14.

5. Maandiko yanaonyeshaje kwamba kutoa bila ubinafsi ni sehemu muhimu ya ibada ya kweli?

5 Kutoa ni sehemu ya ibada yetu kwa Yehova. Kupitia maono, mtume Yohana aliwasikia watumishi wa Yehova walio mbinguni wakisema hivi: “Unastahili, Ee Yehova Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilitokea navyo vikaumbwa.” (Ufu. 4:11) Je, hukubali kwamba Yehova anastahili utukufu wote na heshima tunayompa kwa kutoa vitu bora zaidi tulivyo navyo? Kupitia Musa, Yehova aliwaamuru Waisraeli wafike mbele zake wakati wa sherehe tatu zilizofanywa kila mwaka. Kutoa kulikuwa sehemu ya ibada katika sherehe hizo, hivyo Waisraeli hawakupaswa “kwenda mbele za Yehova mikono mitupu.” (Kum. 16:16) Vivyo hivyo leo, kutoa bila ubinafsi kwa sababu tunathamini na kuunga mkono kazi inayotimizwa na sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova ni sehemu muhimu ya ibada yetu.

6. Kwa nini kutoa hutunufaisha? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

6 Kutoa hutunufaisha. Tunanufaika tunapotoa kwa ukarimu badala ya kuwa wapokeaji tu. (Soma Methali 29:21.) Fikiria mtoto anayewapa wazazi wake zawadi aliyonunua kwa pesa kidogo ambazo wamempa. Unafikiri wazazi wake wataionaje zawadi hiyo? Huenda mwana au binti anayefanya upainia na anayeishi na wazazi akaona kwamba inafaa kuwapa wazazi wake kiasi fulani cha pesa ili kugharimia baadhi ya gharama za nyumbani. Ingawa huenda wazazi wasitarajie mtoto wao afanye hivyo, wanaweza kukubali zawadi hizo kwa sababu wanajua ni njia ambayo mtoto anaonyesha kwamba anathamini mambo yote anayotendewa na wazazi wake. Vivyo hivyo, Yehova anajua kwamba tunapompa vitu vyetu vyenye thamani sisi wenyewe hunufaika.

ZOEA LA KUTOA KATIKA NYAKATI ZA BIBLIA

7, 8. Watu wa Yehova wa nyakati za Biblia waliweka kielelezo gani katika kutoa michango kuhusiana na (a) miradi hususa? (b) kutegemeza kazi ya Yehova kwa ujumla?

7 Maandiko yana masimulizi mengi ya watu waliotoa michango kutoka katika mali zao. Katika visa fulani, watu wa Yehova walitoa michango kwa ajili ya miradi hususa. Kwa mfano, Musa aliwaomba watu watoe michango kwa ajili ya ujenzi wa hema la ibada, kama Mfalme Daudi alivyofanya kwa ajili ya ujenzi wa hekalu. (Kut. 35:5; 1 Nya. 29:5-9) Wakati wa Mfalme Yehoashi, makuhani walirekebisha nyumba ya Yehova kwa kutumia pesa zilizokusanywa. (2 Fal. 12:4, 5) Akina ndugu katika kutaniko la mapema la Kikristo walipojulishwa kuhusu uhitaji uliozuka kwa sababu ya njaa kali, “[waliamua] kila mmoja kulingana na uwezo wake, watume msaada kwa akina ndugu walioishi Yudea.”—Mdo. 11:27-30.

8 Katika visa vingine, watu wa Yehova waliwategemeza kifedha wale waliosimamia kazi. Chini ya Sheria ya Musa, Walawi hawakupokea urithi kama makabila mengine. Badala yake, Waisraeli waliwapa sehemu ya kumi ambayo iliwasaidia Walawi wakazie fikira utumishi wao katika hema la ibada. (Hes. 18:21) Baadaye Yesu na wanafunzi wake pia walinufaika na ukarimu walioonyeshwa na wanawake “waliokuwa wakiwahudumia kwa mali zao.”—Luka 8:1-3.

9. Katika nyakati za Biblia watu walipata wapi michango waliyotoa?

9 Bila shaka, watu walipata michango waliyotoa kutoka vyanzo mbalimbali. Waisraeli walipotoa michango kwa ajili ya ujenzi wa hema la ibada nyikani, inaelekea michango waliyotoa ilitia ndani vitu walivyobeba kutoka Misri. (Kut. 3:21, 22; 35:22-24) Katika karne ya kwanza, baadhi ya Wakristo waliuza mali zao kama vile mashamba au nyumba na kuwaletea mitume pesa hizo. Nao mitume wakawapa michango hiyo wale waliokuwa na uhitaji. (Mdo. 4:34, 35) Wengine walikuwa na kawaida ya kutoa michango ya kutegemeza kazi kwa kutenga kiasi fulani cha pesa. (1 Kor. 16:2) Hivyo, watu wa matabaka yote, iwe walikuwa matajiri sana au maskini hohehahe, walishiriki kutoa michango.—Luka 21:1-4.

ZOEA LA KUTOA KATIKA SIKU ZETU

10, 11. (a) Tunaweza kuwaigaje watumishi wa Yehova wa nyakati za Biblia walioonyesha ukarimu? (b) Unahisije kuhusu pendeleo ulilonalo la kutegemeza kazi ya Ufalme?

10 Leo, sisi pia tunaweza kuombwa tutoe michango kwa ajili ya kusudi fulani hususa. Kwa mfano, je, kutaniko lenu lina mpango wa kujenga Jumba jipya la Ufalme? Au je, Jumba la Ufalme mnalotumia linafanyiwa ukarabati kwa sasa? Huenda tukajulishwa kwamba fedha zinahitajika kwa ajili ya ukarabati wa ofisi ya tawi, kutegemeza kusanyiko, au kuwasaidia ndugu zetu waliokumbwa na misiba ya asili. Pia, tunatoa michango ili kuwategemeza wale wanaofanya kazi katika makao makuu ya ulimwenguni pote na kwenye ofisi za tawi duniani kote. Michango yetu hutumiwa kuwategemeza wamishonari, mapainia wa pekee, na waangalizi wa mzunguko. Hapana shaka kwamba kutaniko lenu pia limeweka azimio la kutegemeza kifedha mradi wa ulimwenguni pote wa kujenga Majumba ya Kusanyiko na Majumba ya Ufalme. Jambo hilo huwanufaisha ndugu zetu duniani kote.

11 Kila mmoja wetu anaweza kutegemeza kazi ambayo Yehova anatimiza katika siku hizi za mwisho. Michango mingi hutolewa bila kujua ni nani aliyeitoa. Sisi huweka michango hiyo katika masanduku ya michango au tunaitoa kupitia Tovuti ya jw.org bila kumjulisha yeyote kiasi tunachotoa. Huenda tukahisi kwamba mchango wetu ni mdogo sana. Hata hivyo, idadi kubwa ya michango inayotolewa leo haitoki tu kwa watu wachache wanaotoa michango mikubwa, badala yake hutoka kwa watu wengi wanaotoa michango midogo-midogo. Hata ndugu zetu walio na hali ngumu za kiuchumi wana tamaa kama ya Wamakedonia ambao walikuwa katika “umaskini mkubwa” lakini bado waliomba sana wapate pendeleo la kutoa, nao walifanya hivyo kwa ukarimu.—2 Kor. 8:1-4.

12. Tengenezo linafanya jitihada gani kuhakikisha kwamba michango inatumiwa vizuri?

12 Kupitia sala, Baraza Linaloongoza hujitahidi kuhakikisha kwamba pesa za tengenezo zinatumika kwa uaminifu na busara. (Mt. 24:45) Pesa zinazopatikana hupangwa na kutumiwa kulingana na bajeti iliyopangwa. (Luka 14:28) Katika nyakati za Biblia, wale waliotunza michango iliyowekwa wakfu walifuata utaratibu uliowekwa ili kuhakikisha kwamba michango inatumiwa kama ilivyokusudiwa. Kwa mfano, Ezra alisafiri kurudi Yerusalemu akiwa na michango aliyokuwa amepewa na mfalme Mwajemi. Michango hiyo ilitia ndani dhahabu, fedha, na vitu vingine vyenye thamani ambavyo kulingana na makadirio ya sasa ni zaidi ya dola milioni 100 za Marekani. Ezra aliiona michango hiyo kuwa matoleo ya hiari kwa Yehova na akapanga utaratibu hususa uliowezesha vitu hivyo vyenye thamani visafirishwe salama katika eneo lenye hatari. (Ezra 8:24-34) Mtume Paulo alikusanya michango na kuitoa kama msaada kwa ajili ya akina ndugu huko Yudea. Alichukua hatua za kuhakikisha kwamba wale waliopeleka michango hiyo walishughulikia “mambo yote kwa unyoofu, si machoni pa Yehova tu bali pia machoni pa wanadamu.” (Soma 2 Wakorintho 8:18-21.) Kama Paulo na Ezra, leo tengenezo letu huweka mikakati thabiti kuhusu jinsi ya kushughulikia na kutumia michango.

13. Tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu mabadiliko ya karibuni yaliyofanywa na tengenezo ili kurahisisha kazi?

13 Huenda familia fulani ikafanya mabadiliko ili kusawazisha kiasi cha pesa walizo nazo na matumizi yao, au wanaweza kufanya mabadiliko ili warahisishe maisha na kupunguza gharama na hivyo kutimiza mengi zaidi katika kazi ya Yehova. Hivyo ndivyo tengenezo la Yehova linavyofanya pia. Katika miaka ya hivi karibuni, kumekuwa na miradi mingi mipya yenye kusisimua. Nyakati nyingine, hilo lilisababisha pesa nyingi zaidi zitumike kuliko pesa zilizopatikana. Hivyo, tengenezo hutafuta njia za kupunguza gharama na kurahisisha kazi ili litimize mambo mengi kadiri iwezekanavyo kwa kutumia michango yenu mnayotoa kwa ukarimu.

MCHANGO WAKO HUTIMIZA NINI?

Michango unayotoa husaidia kazi yetu ya ulimwenguni pote (Tazama fungu la 14 hadi 16)

14-16. (a) Ni baadhi ya mambo gani yanayotimizwa kupitia michango unayotoa? (b) Maandalizi hayo yamekunufaisha katika njia zipi?

14 Watumishi wengi wa Yehova ambao wamemtumikia kwa muda mrefu wamesikika wakisema kwamba hakujawahi kamwe kuwa na kipindi chenye maandalizi mengi ya kiroho kama hiki. Fikiria mambo yafuatayo. Katika miaka ya hivi karibuni tumejionea kuanzishwa kwa Tovuti ya jw.org na JW Broadcasting. Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inaendelea kuchapishwa katika lugha nyingi zaidi. Katika mwaka wa 2014/2015, baadhi ya viwanja vikubwa zaidi katika majiji 14 kotekote duniani vilitumiwa kufanyia makusanyiko ya kimataifa ya siku tatu yenye kichwa “Endeleeni Kuutafuta Kwanza Ufalme wa Mungu!” Wale waliohudhuria makusanyiko hayo walifurahia sana.

15 Wengi wameshukuru sana kwa manufaa ya pekee wanayopata katika tengenezo la Yehova. Kwa mfano, wenzi fulani wa ndoa kutoka nchi moja huko Asia waliandika hivi kuhusu JW Broadcasting: “Tunatumikia katika jiji fulani dogo. Hivyo, nyakati nyingine sisi huhisi ni kana kwamba tumetengwa na wengine, nasi husahau jinsi kazi ya Yehova inavyotimizwa kwa njia kubwa. Lakini mara tu tunapotazama programu mbalimbali za JW Broadcasting, tunakumbuka kwamba sisi ni sehemu ya undugu wa ulimwenguni pote. Ndugu na dada zetu katika eneo hili wanafurahia sana programu za JW Broadcasting. Mara kwa mara tunawasikia wakisema kwamba wanahisi wakiwa karibu zaidi na washiriki wa Baraza Linaloongoza baada ya kutazama programu za kila mwezi. Sasa kuliko wakati mwingine wowote, wanajivunia sana kuwa sehemu ya tengenezo la Mungu.”

16 Ulimwenguni pote, karibu Majumba ya Ufalme 2,500 yanajengwa au kufanyiwa ukarabati mkubwa kwa sasa. Walipoanza kutumia Jumba lao jipya la Ufalme, washiriki wa kutaniko moja huko Honduras waliandika hivi: “Tunafurahi sana kuwa sehemu ya familia ya Yehova ya ulimwenguni pote na undugu wetu, ambao ulisaidia kutimiza ndoto yetu ya kuwa na Jumba la Ufalme katika eneo letu.” Wengi pia wameeleza hisia zao za shukrani baada ya kupokea Biblia au machapisho yaliyotafsiriwa katika lugha yao, kupokea msaada walipokumbwa na msiba wa asili, au kuona jinsi watu wanavyoitikia wanapohubiriwa katika mahubiri ya hadharani au kupitia mpango wa kuhubiri katika majiji makubwa.

17. Kuna uthibitisho gani unaoonyesha kwamba Yehova anategemeza tengenezo lake?

17 Watu wanaotutazama hawaelewi tunawezaje kutimiza mambo hayo yote kupitia michango ya hiari tu. Baada ya kutembelea majengo yetu ya uchapishaji, msimamizi fulani wa kampuni moja kubwa alishangaa kwamba kazi yote hufanywa na wajitoleaji na hutegemezwa na michango ya hiari bila harakati za kuchangisha pesa. Alisema kwamba katika hali za kawaida hilo haliwezekani. Tunakubaliana naye! Tunajua hilo linawezekana tu kwa sababu Yehova anategemeza kazi hiyo.—Ayu. 42:2.

BARAKA TUNAZOPATA KWA KUMPA YEHOVA

18. (a) Tunapata baraka zipi tunapotoa ili kutegemeza kazi ya Ufalme? (b) Tunaweza kuwazoezaje watoto wetu na wapya kushiriki katika kutoa?

18 Yehova ametupa pendeleo la kutegemeza kazi kubwa inayoendelea leo. Anatuhakikishia kwamba tutapata baraka tunapotegemeza kazi ya Ufalme. (Mal. 3:10) Yehova anatuahidi kwamba mtu mkarimu atapata ufanisi. (Soma Methali 11:24, 25.) Pia, kutoa hufanya tuwe na furaha, kwa kuwa “kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Mdo. 20:35) Kupitia maneno na mfano wetu, tuna pendeleo la kuwazoeza watoto wetu na wapya kuthamini pendeleo walilonalo la kushiriki katika kutoa na jinsi ambavyo kufanya hivyo kutawaletea baraka nyingi.

19. Makala hii imekutia moyo kufanya nini?

19 Vitu vyote tulivyo navyo vimetoka kwa Yehova. Kumpa Yehova vitu tulivyo navyo kunaonyesha kwamba tunampenda na tunathamini mambo yote ambayo amefanya kwa ajili yetu. (1 Nya. 29:17) Walipokuwa wakichanga kwa ajili ya ujenzi wa hekalu, “watu walishangilia kwa sababu walitoa matoleo hayo ya hiari, kwa maana walimtolea Yehova matoleo hayo ya hiari kwa moyo kamili.” (1 Nya. 29:9) Basi, acheni sisi pia tuendelee kupata shangwe na furaha kwa kumpa Yehova vitu ambavyo tumepokea kutoka katika mkono wake.