Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Yeye Humpa Nguvu Mtu Aliyechoka”

“Yeye Humpa Nguvu Mtu Aliyechoka”

Andiko la mwaka wa 2018: “Wale wanaomtumaini Yehova watapata nguvu tena.”—ISA. 40:31.

NYIMBO: 3, 47

1. Tunakabili mikazo gani, lakini kwa nini Yehova ana sababu ya kupendezwa na watumishi wake waaminifu? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

KAMA mjuavyo, maisha katika mfumo huu wa mambo yamejaa matatizo. Na wengi miongoni mwenu mnakabiliana na matatizo makubwa ya afya. Wengine wanawatunza watu wao wa ukoo waliozeeka, ingawa umri wao pia umesonga. Na wengine wanapambana kuandalia familia zao, si vitu vya starehe, bali mahitaji ya lazima. Na tunajua kwamba wengi wanakabiliana na matatizo kadhaa kwa wakati uleule, si tatizo moja tu! Wakati mwingi na pia nguvu nyingi za kihisia hutumika kuyashughulikia, bila kutaja pesa nyingi zinazotumika. Licha ya hayo, uhakika mlio nao katika ahadi za Mungu ni thabiti, na imani yenu kuhusu wakati ujao ulio bora haiyumbiyumbi. Bila shaka, hilo linampendeza sana Yehova!

2. Andiko la Isaya 40:29 linatutia moyo jinsi gani, lakini tunapaswa kujihadhari tusifanye kosa gani zito?

2 Lakini je, nyakati nyingine wewe huhisi kana kwamba huna nguvu za kuendelea kuvumilia mikazo ya maisha? Ikiwa ndivyo, si wewe tu unayekabili hali hiyo. Biblia inaeleza kwamba mara nyingi watumishi waaminifu wa kale walihisi kwamba hawawezi kuendelea kuvumilia. (1 Fal. 19:4; Ayu. 7:7) Hata hivyo, badala ya kukata tamaa, walimtegemea Yehova. Hawakutamauka kwa sababu Mungu wetu “humpa nguvu mtu aliyechoka.” (Isa. 40:29) Inasikitisha kwamba leo baadhi ya watu wa Mungu wameona kwamba njia bora zaidi ya kukabiliana na mikazo maishani ni ‘kupumzika’ kwa kuacha utendaji wao wa kiroho, kana kwamba utendaji wetu wa Kikristo ni mzigo wenye kulemea na si baraka. Hivyo, wanaacha kusoma Neno la Mungu, kuhudhuria mikutano ya kutaniko, na kushiriki katika huduma ya shambani—jambo ambalo Shetani anatamani sana wafanye.

3. (a) Tunaweza kupingaje jitihada za Shetani za kutudhoofisha? (b) Tutachunguza nini katika makala hii?

3 Ibilisi anajua vizuri kwamba tunaposhiriki kikamili katika utendaji wa Kikristo tunaimarika, naye hataki tuwe imara. Hivyo, unapohisi umechoka sana kimwili na kihisia, usijitenge na Yehova. Endelea kumkaribia zaidi, kwa maana ‘atakufanya uwe imara, atakutia nguvu.’ (1 Pet. 5:10; Yak. 4:8) Katika makala hii, tutachunguza mambo mawili yanayoweza kutufanya tupunguze bidii katika utumishi wetu kwa Mungu na tutazungumzia jinsi ambavyo kutumia kanuni za Biblia kunaweza kutusaidia kukabiliana na hali hizo. Lakini kwanza, acheni tuzungumzie uwezo wa Yehova wa kutuimarisha, kama unavyofafanuliwa kwenye andiko la Isaya 40:26-31.

WALE WANAOMTUMAINI YEHOVA WATAPATA NGUVU TENA

4. Tunaweza kujifunza nini kutokana na andiko la Isaya 40:26?

4 Soma Isaya 40:26. Hakuna mtu ambaye amefaulu kuhesabu nyota zote angani. Wanasayansi wanaamini kwamba kundi la nyota la Kilimia pekee lina nyota bilioni 400 hivi. Hata hivyo, Yehova huipa kila nyota jina. Tunajifunza nini? Ikiwa Yehova anapendezwa kibinafsi na uumbaji wake usio na uhai, wazia jinsi anavyohisi kukuelekea wewe ambaye unamtumikia si kwa sababu unaongozwa na silika, bali kwa sababu unampenda! (Zab. 19:1, 3, 14) Baba yetu mpendwa anajua kila kitu kukuhusu. ‘Hata amehesabu nywele zote za kichwa chako.’ (Mt. 10:30) Na mtunga zaburi anatuhakikishia hivi: “Yehova anajua mambo wanayokabili watu wasio na lawama.” (Zab. 37:18) Naam, anajua majaribu yote unayokabili, naye anaweza kukupa nguvu ya kuvumilia kila moja ya majaribu hayo.

5. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anaweza kutupatia nguvu?

5 Soma Isaya 40:28. Yehova ndiye Chanzo cha nguvu zote zenye msukumo. Kwa mfano, fikiria kuhusu kiasi cha nishati ambacho Yehova amewezesha jua letu kutokeza. Mwandishi wa mambo ya kisayansi David Bodanis anaeleza hivi: “Kiasi cha nishati kinachotokezwa na jua letu kila sekunde kinalingana na nishati inayopatikana kwenye [mabilioni ya mabomu ya atomu].” Mtafiti mwingine alieleza kwamba “katika kila sekunde jua hutokeza . . . kiasi cha nishati kinachoweza kutosheleza mahitaji ya wanadamu kwa miaka 200,000”! Je, kuna yeyote anayeweza kutilia shaka kwamba Yule anayelipatia jua nishati atatupatia nguvu tunazohitaji ili kukabiliana na tatizo lolote?

6. Nira ya Yesu ni laini katika maana gani, na kujua hilo hufanya tuhisije?

6 Soma Isaya 40:29. Kumtumikia Yehova hutuletea shangwe nyingi. Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Chukueni nira yangu.” Kisha akasema hivi: “Nanyi mtapata burudisho kwa ajili yenu. Kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.” (Mt. 11:28-30) Maneno hayo ni ya kweli kabisa! Huenda nyakati nyingine tukahisi tumechoka sana kabla ya kuondoka nyumbani ili kuhudhuria mkutano au kushiriki katika huduma ya shambani. Lakini tunahisije tunaporudi nyumbani? Tunahisi tukiwa tumeburudika na tukiwa tayari kukabiliana na changamoto za maisha. Kwa hakika, nira ya Yesu ni laini!

7. Simulia jambo lililoonwa linaloonyesha ukweli wa Mathayo 11:28-30.

7 Dada mmoja tutakayemwita Kayla ana ugonjwa wa kuchoka daima, kushuka moyo, na kipandauso. Kwa sababu ya hali yake, nyakati nyingine inakuwa vigumu kwake kuhudhuria mikutano ya kutaniko. Hata hivyo, baada ya kujitahidi kuhudhuria mkutano fulani aliandika hivi: “Hotuba iliyotolewa ilizungumza kuhusu kuvunjika moyo. Hotuba hiyo ilitolewa kwa njia yenye huruma na ufikirio hivi kwamba nilitokwa na machozi. Hilo lilinikumbusha kwamba mikutanoni ndipo mahali ninapopaswa kuwa.” Anafurahi sana kwamba alijitahidi kuhudhuria mikutano!

8, 9. Mtume Paulo alimaanisha nini alipoandika: “Ninapokuwa dhaifu, ndipo ninapokuwa na nguvu”?

8 Soma Isaya 40:30. Licha ya uwezo mbalimbali tulio nao, kuna mambo ambayo hatuwezi kutimiza kwa nguvu zetu wenyewe. Sote tunapaswa kutambua jambo hilo. Ingawa mtume Paulo alikuwa na uwezo wa kutimiza mambo mengi, kuna mambo fulani yaliyomzuia kutimiza yote aliyotaka kufanya. Alipomweleza Mungu mahangaiko yake, Mungu alimwambia hivi: “Nguvu zangu zinakamilika katika udhaifu.” Paulo alielewa kile ambacho Mungu alimaanisha. Alisema hivi: “Ninapokuwa dhaifu, ndipo ninapokuwa na nguvu.” (2 Kor. 12:7-10) Alimaanisha nini?

9 Paulo alitambua kwamba uwezo wake ulikuwa na mipaka na alihitaji msaada kutoka chanzo cha juu zaidi. Roho takatifu ya Mungu ingempa Paulo nguvu alizohitaji. Na si hilo tu, roho takatifu ya Mungu ingemwezesha Paulo kutimiza mambo ambayo hangeweza kamwe kutimiza kwa nguvu zake mwenyewe. Na ndivyo ilivyo kwetu pia. Ikiwa nguvu tulizonazo zinatoka kwa Yehova, tutakuwa wenye nguvu kwelikweli!

10. Yehova alimsaidiaje Daudi kukabiliana na changamoto maishani mwake?

10 Katika maisha yake mtunga zaburi Daudi alijionea mara nyingi nguvu za roho takatifu ya Mungu. Aliimba hivi: “Kwa msaada wako ninaweza kukabiliana na kundi la wavamizi; kwa nguvu za Mungu ninaweza kuupanda ukuta.” (Zab. 18:29) Kuna kuta fulani, yaani, matatizo ambayo hatuwezi ‘kupanda’ kwa nguvu zetu wenyewe; tunahitaji msaada kutoka kwa Yehova.

11. Fafanua jinsi roho takatifu inavyotusaidia kukabiliana na matatizo yetu.

11 Soma Isaya 40:31. Tai hatumii nguvu zake pekee anaporuka na kupaa kwa mwendo mrefu. Mikondo ya hewa yenye joto humwinua tai, hivyo hatumii nguvu nyingi. Kwa hiyo, unapokabili hali fulani ngumu, mkumbuke tai. Msihi Yehova ‘akuinue’ kwa msaada wa “msaidizi, roho takatifu.” (Yoh. 14:26) Jambo linalofurahisha ni kwamba tunaweza kupata roho takatifu wakati wowote tunapoihitaji—saa 24 kwa siku. Nyakati fulani huenda tukahisi kwamba tunahitaji sana msaada kutoka kwa Mungu hali ya kutoelewana inapotokea kati yetu na mshiriki fulani wa kutaniko. Lakini kwa nini hali kama hizo hutokea?

12, 13. (a) Kwa nini hali za kutoelewana hutokea miongoni mwa Wakristo? (b) Simulizi la Yosefu linatufundisha nini kumhusu Yehova?

12 Hali ya kutoelewana kati ya ndugu na dada hutokea kwa sababu sisi si wakamilifu. Kwa sababu hiyo, kuna nyakati ambazo maneno au matendo ya waabudu wenzetu huenda yakatuudhi, au huenda sisi tukawaudhi kwa maneno au matendo yetu. Hilo linaweza kuwa jaribu kali. Kama ilivyo na majaribu mengine, Yehova hutupatia fursa ya kuonyesha utimilifu wetu kwa kujifunza kufanya kazi kwa umoja pamoja na wanaume na wanawake waliojiweka wakfu kwake na anaowapenda licha ya kwamba wao si wakamilifu.

Yehova hakumwacha Yosefu na hatakuacha wewe pia (Tazama fungu la 13)

13 Yehova hazuii watumishi wake wasipatwe na majaribu, kama simulizi la Yosefu linavyoonyesha. Akiwa kijana, ndugu zake wa kambo walimuuza utumwani Misri kwa sababu walimwonea wivu. (Mwa. 37:28) Yehova aliona kilichokuwa kikitendeka na bila shaka alihuzunika kuona jinsi Yosefu, rafiki yake mwadilifu, alivyokuwa akitendewa. Lakini hakuingilia kati. Baadaye, Yosefu aliposhtakiwa kwa uwongo kwamba amejaribu kumbaka mke wa Potifa na kufungwa gerezani, bado Yehova hakuingilia kati. Lakini je, Mungu alikuwa amemwacha Yosefu? La, hasha! Badala yake: “Yehova alifanikisha jambo lolote alilofanya [Yosefu].”—Mwa. 39:21-23.

14. Tunaweza kupata manufaa gani ya kiroho na ya kimwili kwa ‘kuacha’ hasira?

14 Ona mfano mwingine. Ni watu wachache sana ambao wametendewa vibaya kama Daudi alivyotendewa. Hata hivyo, rafiki huyo wa Mungu hakuruhusu kinyongo kimtawale. Badala yake, aliandika hivi: “Acha hasira na uache ghadhabu; usikasirike na kuanza kutenda uovu.” (Zab. 37:8) Sababu muhimu sana ya ‘kuacha’ hasira ni kwamba tunataka kumwiga Yehova, ambaye “hajatutendea kulingana na dhambi zetu.” (Zab. 103:10) Lakini kuna manufaa mengine tunayopata kwa ‘kuacha’ hasira. Hasira inaweza kusababisha matatizo ya afya kama vile shinikizo la damu na matatizo ya kupumua. Inaweza kuathiri ini na kongosho, na kusababisha matatizo kwenye mfumo wa kumeng’enya chakula. Mara nyingi, tunapokuwa na hasira hatuwezi kufikiri vizuri. Na nyakati nyingine, mlipuko wa hasira hufuatwa na kipindi kirefu cha kushuka moyo. Kwa upande mwingine, Biblia inasema kwamba “moyo mtulivu huupa mwili uzima.” (Met. 14:30) Hivyo basi, tunaweza kushughulikiaje hisia zetu zilizoumizwa na kumpata tena ndugu yetu? Tunaweza kufaulu kufanya hivyo kwa kutumia ushauri wenye hekima wa Biblia.

TUNAPOVUNJWA MOYO NA NDUGU ZETU

15, 16. Tunapaswa kufanya nini ndugu yetu anapotukosea?

15 Soma Waefeso 4:26. Hatushangai tunapotendewa vibaya na watu wa ulimwengu. Lakini mwabudu mwenzetu au mshiriki wa familia anaposema au kutenda jambo linalotuumiza, huenda tukavunjika moyo sana. Vipi ikiwa hatuwezi kusahau jambo hilo? Je, tutaendelea kuweka kinyongo kwa miaka mingi, au tutafuata ushauri wenye hekima wa Biblia na kusuluhisha mambo haraka? Tusiposhughulikia hali hiyo haraka, itakuwa vigumu hata zaidi kufanya amani na ndugu yetu.

16 Tuseme ndugu yako amekukosea na umeshindwa kuachilia jambo hilo. Unaweza kuchukua hatua zipi zinazofaa ili kufanya amani? Kwanza, sali kwa Yehova kwa bidii. Mwombe akusaidie uwe na mazungumzo yenye kujenga pamoja na ndugu yako. Kumbuka kwamba yeye ni rafiki ya Yehova. (Zab. 25:14) Mungu anampenda. Yehova huwatendea rafiki zake kwa fadhili, na anatazamia tuwatendee vivyo hivyo pia. (Met. 15:23; Mt. 7:12; Kol. 4:6) Kisha, tafakari mambo ambayo ungependa kusema. Usikate kauli kwamba ndugu yako alikusudia kukuumiza; usifanye haraka kumhukumu. Uwe tayari kukubali kwamba huenda ulichangia hali hiyo ya kutoelewana. Unaweza kuanzisha mazungumzo kwa kusema hivi: “Huenda sipaswi kuumizwa na jambo hili, lakini ulipozungumza nami jana, nilihisi . . . ” Ikiwa mazungumzo hayo hayataenda kama ulivyotarajia, tafuta fursa nyingine ya kufanya amani. Wakati huohuo, endelea kusali kwa ajili ya ndugu yako; mwombe Yehova ambariki. Mwombe Mungu akusaidie kukazia fikira sifa nzuri za ndugu yako. Haidhuru utapata matokeo gani, unaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atafurahi kuona ukijitahidi kumpata ndugu yako, ambaye ni rafiki ya Mungu.

TUNAPOSUMBULIWA NA MAKOSA YALIYOPITA

17. Yehova anatumia nini kutusaidia kurudia hali nzuri ya kiroho, na kwa nini tunapaswa kutumia uandalizi huo?

17 Watu fulani huhisi kwamba hawastahili kumtumikia Yehova kwa sababu wamefanya dhambi nzito. Hisia za hatia zinaweza kutulemea sana. Mfalme Daudi, ambaye alisumbuliwa na hisia za hatia, alieleza hivi: “Niliponyamaza, mifupa yangu ilidhoofika kwa sababu ya kulia kwa maumivu makali mchana kutwa. Kwa maana usiku na mchana mkono wako ulinilemea.” Jambo la kufurahisha ni kwamba Daudi alishughulikia tatizo hilo kama mtu aliyekomaa kiroho. Aliandika hivi: “Mwishowe nikaungama dhambi yangu kwako; . . . nawe ukanisamehe kosa la dhambi zangu.” (Zab. 32:3-5) Ikiwa umefanya dhambi nzito, Yehova yuko tayari kukusaidia urudie hali nzuri ya kiroho. Lakini lazima ukubali msaada anaoandaa kupitia kutaniko. (Met. 24:16; Yak. 5:13-15) Usikawie—uhai wako wa milele uko hatarini! Vipi ikiwa dhamiri yako bado inakusumbua muda mrefu baada ya kosa lako kusamehewa?

18. Mfano wa Paulo unaweza kuwasaidiaje wale wanaohisi hawafai?

18 Inaonekana kwamba kuna nyakati ambazo mtume Paulo alitaabishwa na makosa yake ya wakati uliopita. Alikiri hivi: “Mimi ni mdogo zaidi kati ya mitume, nami sistahili kuitwa mtume, kwa sababu nililitesa kutaniko la Mungu.” Hata hivyo, Paulo aliongeza hivi: “Lakini kwa fadhili zisizostahiliwa za Mungu mimi niko kama nilivyo.” (1 Kor. 15:9, 10) Yehova alimkubali Paulo jinsi alivyo, na alitarajia Paulo atambue hilo. Ikiwa umetubu kutoka moyoni na kuungama kikweli dhambi ulizofanya zamani, uwe na hakika kwamba Yehova atakuonyesha rehema. Hivyo, mwamini Yehova anaposema kwamba atakusamehe, na ukubali msamaha wake!—Isa. 55:6, 7.

19. Andiko la mwaka wa 2018 ni gani, na kwa nini linafaa?

19 Kadiri mfumo huu wa mambo unavyokaribia mwisho wake, tunatarajia kwamba mikazo ya maisha itaongezeka. Hata hivyo, uwe na hakika kwamba Yule ambaye “humpa nguvu mtu aliyechoka na kuwapa uwezo kamili wale wasio na nguvu,” anaweza kukupatia chochote unachohitaji ili uendelee kuvumilia. (Isa. 40:29; Zab. 55:22; 68:19) Katika mwaka wa 2018, kila mara tunapohudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme tutakumbushwa ujumbe huo muhimu. Ujumbe huo unapatikana katika maneno ya andiko letu la mwaka: “Wale wanaomtumaini Yehova watapata nguvu tena.”Isa. 40:31.