Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tofauti Kati ya Watu Wanaomtumikia Yehova na Wasiomtumikia

Tofauti Kati ya Watu Wanaomtumikia Yehova na Wasiomtumikia

“Nanyi mtaona . . . tofauti kati ya mtu mwadilifu na mtu mwovu, kati ya yule anayemtumikia Mungu na yule asiyemtumikia.”—MAL. 3:18.

NYIMBO: 127, 101

1, 2. Watu wa Mungu wanakabili changamoto gani? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

WAHUDUMU wengi wa afya huwatunza watu walioathiriwa na magonjwa ya kuambukiza. Wao huwatunza wagonjwa kwa sababu wanataka kuwasaidia. Hata hivyo, wanahitaji kujilinda wasiambukizwe magonjwa hayo wanayojaribu kutibu. Vivyo hivyo, wengi wetu leo tunaishi na kufanya kazi na watu walioathiriwa na mitazamo na tabia zinazopingana na sifa zinazompendeza Mungu. Hiyo ni changamoto kubwa sana kwetu.

2 Siku hizi za mwisho zimejaa maadili yaliyopotoka. Barua ya pili ambayo mtume Paulo alimwandikia Timotheo inafafanua tabia za watu waliojitenga na Mungu, tabia ambazo zingezidi kuenea siku baada ya siku. (Soma 2 Timotheo 3:1-5, 13.) Ingawa huenda tukashtuka kuona jinsi tabia hizo zilivyoenea, tunaweza kuathiriwa na tabia hizo na mitazamo ya watu hao. (Met. 13:20) Katika makala hii, tutachunguza tofauti kubwa iliyopo kati ya tabia za watu wa siku za mwisho na sifa za watu wa Mungu. Pia, tutaona jinsi tunavyoweza kujilinda tusiathiriwe na tabia zisizofaa na wakati huohuo tuendelee kuwasaidia wengine kiroho.

3. Orodha ya sifa zinazotajwa kwenye 2 Timotheo 3:2-5 inawahusu nani?

3 Mtume Paulo alisema kwamba “siku za mwisho” zingetokeza “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” Kisha aliorodhesha sifa 19 zisizofaa ambazo watu wangekuwa nazo katika kipindi hicho. Orodha hiyo ni sawa na ile inayopatikana katika Waroma 1:29-31. Hata hivyo, orodha ambayo Paulo aliandika kwenye barua yake kwa Timotheo inatia ndani mambo ambayo hayatajwi mahali pengine popote katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Katika orodha hiyo, Paulo anaanza kwa kusema maneno haya: “Kwa maana watu watakuwa . . . ” Hata hivyo, si watu wote walio na tabia kama hizo. Wakristo wanaonyesha sifa tofauti kabisa.—Soma Malaki 3:18.

TUNA MAONI GANI KUJIHUSU?

4. Ungewafafanuaje watu waliojaa kiburi?

4 Baada ya kutaja kwamba watu wengi wangekuwa wenye kujipenda wenyewe na wenye kupenda pesa, Paulo aliandika pia kwamba watu wangekuwa wenye kujidai, wenye majivuno, na waliojaa kiburi, tabia zinazodhihirisha mtazamo wa kujiona kuwa bora kwa sababu ya uwezo, sura, utajiri, au cheo. Watu wenye tabia kama hizo hutamani sana wasifiwe-sifiwe na kuonwa kuwa wa pekee. Msomi mmoja aliandika hivi kumhusu mtu aliyejaa kiburi: “Moyoni mwake ana madhabahu ndogo ambapo yeye mwenyewe hupiga magoti ili kujiinamia.” Baadhi ya watu wamesema kwamba kiburi kinachukiza sana hivi kwamba hata watu wenye kiburi huchukizwa na watu wenye kiburi.

5. Ni kwa njia gani hata watu waaminifu wameingia katika mtego wa kuwa na kiburi?

5 Bila shaka Yehova anachukizwa sana na kiburi. Anachukia “macho ya kiburi.” (Met. 6:16, 17) Kiburi humzuia mtu asimkaribie Mungu. (Zab. 10:4) Ni sehemu ya utu wa Ibilisi. (1 Tim. 3:6) Inasikitisha kwamba hata baadhi ya watumishi washikamanifu wa Yehova wameathiriwa na kiburi. Mfalme Uzia wa Yuda alikuwa mwaminifu kwa miaka mingi. “Hata hivyo,” Biblia inasema, “mara tu alipokuwa na nguvu, moyo wake ukawa na kiburi ambacho kilisababisha aangamie, naye alikosa kutenda kwa uaminifu kumwelekea Yehova Mungu wake kwa kuwa aliingia katika hekalu la Yehova ili kufukiza uvumba kwenye madhabahu ya uvumba.” Baadaye, Mfalme Hezekia aliingia katika mtego wa kuwa na kiburi, ingawa si kwa muda mrefu.—2 Nya. 26:16; 32:25, 26.

6. Ni mambo gani ambayo huenda yangemfanya Daudi awe na kiburi, lakini kwa nini hakuwa na kiburi?

6 Baadhi ya watu huingiwa na kiburi kwa sababu wana sura nzuri, umashuhuri, kipawa cha muziki, nguvu nyingi za kimwili, au cheo kikubwa. Daudi alikuwa na mambo hayo yote lakini aliendelea kuwa mnyenyekevu maisha yake yote. Baada ya kumuua Goliathi na kupewa binti ya Mfalme Sauli awe mke wake, Daudi alisema hivi: “Mimi ni nani na watu wangu wa ukoo ni nani, au familia ya baba yangu katika Israeli, hata mfalme awe baba mkwe wangu?” (1 Sam. 18:18) Ni nini kilichomsaidia Daudi aendelee kuwa mnyenyekevu? Daudi alikuwa na sifa, uwezo, na mapendeleo kwa sababu Mungu ‘aliinama chini,’ au alijinyenyekeza na kumkazia uangalifu. (Zab. 113:5-8) Daudi alijua kwamba hakuna jambo lolote alilokuwa nalo ambalo halikutoka kwa Yehova.—Linganisha 1 Wakorintho 4:7.

7. Ni nini kitakachotusaidia kuwa wanyenyekevu?

7 Kama Daudi, watu wa Yehova leo hujitahidi kuwa wanyenyekevu. Tunastaajabishwa kujua kwamba Yehova, ambaye ndiye Mkuu Zaidi ulimwenguni, huonyesha sifa yenye kuvutia ya unyenyekevu. (Zab. 18:35) Tungependa kufuata shauri hili lililoongozwa na roho: “Jivikeni upendo mwororo wenye huruma, fadhili, unyenyekevu, upole, na subira.” (Kol. 3:12) Pia tunajua kwamba upendo “haujigambi, haujivuni.” (1 Kor. 13:4) Tunapokuwa wanyenyekevu tunaweza kuwavuta watu kwa Yehova. Kama tu ambavyo waume wanaweza kuvutwa bila neno kupitia mwenendo wa wake zao, vivyo hivyo wengine wanaweza kuvutwa kwa Mungu kupitia unyenyekevu wa watu wake.—1 Pet. 3:1.

JINSI TUNAVYOWATENDEA WENGINE

8. (a) Baadhi ya watu leo wana maoni gani kuhusu kuwatii wazazi? (b) Maandiko yanawatia moyo watoto wafanye nini?

8 Paulo alieleza jinsi ambavyo watu wa siku za mwisho wangewatendea wengine. Aliandika kwamba katika siku za mwisho watoto hawangewatii wazazi wao. Ingawa nyakati nyingine tabia hiyo inakubalika na kuungwa mkono kwenye vitabu, sinema, na vipindi vya televisheni, kutotii hufanya umoja uliopo katika familia, ambayo ndiyo msingi wa jamii, udhoofike. Kwa muda mrefu watu wametambua ukweli huo. Katika milki ya kale ya Ugiriki, mwanamume aliyempiga mzazi wake, alipoteza haki zake zote za kiraia; chini ya sheria za Roma, kitendo cha mtu kumpiga baba yake kilionwa kuwa sawa na kuua. Maandiko ya Kiebrania na Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo huwatia moyo watoto wawaheshimu wazazi wao.—Kut. 20:12; Efe. 6:1-3.

9. Ni nini kitakachowasaidia watoto wawatii wazazi wao?

9 Watoto wanaweza kujilinda wasiathiriwe na roho ya kutotii kwa kutafakari mambo ambayo wazazi wao wamewatendea. Watachochewa kuthamini mambo hayo ikiwa wataelewa kwamba utii ni takwa la Mungu ambaye ndiye Baba yetu sote. Watoto wanaposema mambo mazuri kuwahusu wazazi wao, wanaweza kuwachochea vijana wengine waanze kuwa na maoni mazuri kuwahusu wazazi wao pia. Bila shaka, ikiwa wazazi hawana upendo wa asili kuelekea watoto wao, huenda ikawa vigumu kwa watoto kuwatii kutoka moyoni. Kwa upande mwingine, mtoto anapohisi kwamba wazazi wake wanampenda kikweli, atachochewa kuwatii hata anaposhawishiwa kutotii. Austin anakiri hivi: “Ingawa nyakati nyingine nilishawishika kufanya mambo niliyokatazwa na wazazi wangu, walinipa miongozo ambayo haikunibana, walinieleza sababu ya sheria walizotoa, na kuzungumza nami kwa uhuru. Mambo hayo yalinisaidia niwe mtiifu. Niliona kwamba wananijali na hilo lilinichochea nitamani kuwafurahisha.”

10, 11. (a) Ni sifa gani mbaya ambazo zingeonyesha kwamba watu hawana upendo? (b) Wakristo wa kweli wanawapenda wanadamu wenzao kwa kadiri gani?

10 Paulo aliorodhesha sifa nyingine zinazoonyesha kwamba watu hawangewapenda wengine. Haishangazi anataja kwamba watu wangekuwa wasio na shukrani baada ya kusema kwamba watoto wangekuwa “wasiotii wazazi,” kwani, mtazamo wa kukosa shukrani huonyeshwa na watu ambao hawathamini fadhili ambazo wengine wanawaonyesha. Pia, watu wangekosa ushikamanifu. Nao hawangetaka makubaliano yoyote; wangeonyesha kwamba hawana nia ya kupatana na wengine. Wangekuwa wakufuru na wasaliti, wakiwatukana wanadamu wenzao na hata Mungu mwenyewe. Pia, kungekuwa na wachongezi, yaani, watu ambao wangesema mambo yaliyokusudiwa kuwaharibia wengine sifa. *

11 Tofauti na watu wengi leo wasio na upendo, wale wanaomwabudu Yehova wanawapenda wanadamu wenzao kutoka moyoni. Jambo hilo limethibitika kuwa kweli sikuzote. Yesu alisema kwamba kumpenda jirani—kuwaonyesha upendo wa ga’pe—ndiyo amri ya pili iliyo muhimu zaidi katika Sheria ya Musa, amri ya kwanza ikiwa kumpenda Mungu. (Mt. 22:38, 39) Pia, Yesu alisema kwamba alama ambayo ingewatambulisha Wakristo ni upendo. (Soma Yohana 13:34, 35.) Watu wa Mungu wangewaonyesha hata maadui zao upendo huo wa Kikristo.—Mt. 5:43, 44.

12. Yesu alionyeshaje kwamba anawapenda wengine?

12 Yesu aliwapenda sana wanadamu. Alisafiri kutoka jiji hadi jiji akiwatangazia watu habari njema kuhusu Ufalme wa Mungu. Aliwaponya vipofu, viwete, na viziwi. Pia, aliwafufua wafu. (Luka 7:22) Isitoshe, Yesu alitoa uhai wake kwa ajili ya wanadamu, ingawa wengi wao walimchukia. Yesu aliiga kikamili upendo ambao Baba yake anao. Mashahidi wa Yehova duniani kote humwiga Mungu kwa kuwaonyesha wengine upendo kama huo.

13. Upendo tunaowaonyesha wengine unaweza kuwasaidiaje wamkaribie Yehova?

13 Tunapowapenda wengine tunawachochea watu wamkaribie Baba yetu wa mbinguni. Kwa mfano, mwanamume mmoja kutoka Thailand, aliguswa moyo sana kuona upendo ambao akina ndugu walikuwa nao katika kusanyiko fulani la eneo. Aliporudi nyumbani aliomba afundishwe Biblia mara mbili kwa juma. Aliwahubiria watu wake wote wa ukoo, na miezi sita tu baada ya kusanyiko alitoa mgawo wake wa kwanza wa usomaji wa Biblia kwenye Jumba la Ufalme. Ili kuchunguza tunawapenda wengine kwa kadiri gani, tunaweza kujiuliza hivi: ‘Je, ninajitahidi kuwasaidia wengine katika familia yangu, kutanikoni, na katika huduma? Je, ninajitahidi kuwaona wengine kama Yehova anavyowaona?’

MBWAMWITU NA WANAKONDOO

14, 15. Watu wengi leo huonyesha tabia gani za kinyama, lakini baadhi yao wamefanya mabadiliko gani?

14 Sifa nyingine mbaya zinazoonyeshwa na watu wa siku za mwisho zinawapa Wakristo sababu nyingine ya kujiepusha na watu kama hao. Watu wanaomkataa Mungu wangekuwa wasiopenda wema, au kama tafsiri nyingine zinavyosema, “wanaochukia wema” au “adui wa kila kitu kilicho chema.” Wangekuwa watu wasiojizuia, wakali. Baadhi yao wangekuwa wenye vichwa vigumu, wenye kufanya mambo bila kufikiri, au bila kujali jinsi matendo yao yatakavyowaathiri wengine.

15 Watu wengi ambao hapo awali walikuwa na tabia za kinyama wamebadilika. Mabadiliko hayo yalitabiriwa kwa njia nzuri sana katika unabii fulani wa Biblia. (Soma Isaya 11:6, 7.) Katika unabii huo, tunasoma kuhusu wanyama wa mwituni kama vile mbwamwitu na simba ambao wangeishi kwa amani na wanyama wa kufugwa, kama vile wanakondoo na ndama. Ona kwamba hali hiyo ya utulivu itaenea kotekote “kwa maana kwa hakika dunia itajaa ujuzi kumhusu Yehova.” (Isa. 11:9) Kwa kuwa wanyama hawawezi kujifunza kumhusu Yehova, utimizo wa kiroho wa unabii huo unawahusu wanadamu.

Kutumia kanuni za Biblia hubadili maisha! (Tazama fungu la 16)

16. Biblia imewasaidiaje watu wabadili utu wao?

16 Kuna watu wengi leo ambao hapo awali walikuwa wakali kama mbwamwitu lakini sasa wanaishi kwa amani pamoja na wengine. Unaweza kusoma baadhi ya masimulizi kuhusu maisha yao katika mfululizo wenye kichwa “Biblia Inabadili Maisha,” unaopatikana kwenye Tovuti ya jw.org. Wale ambao tayari wamemjua na kumtumikia Yehova hawafanani na wale wanaoonekana kama watu wanaomwogopa Mungu lakini wakizikana nguvu zake, ambao hujifanya kuwa wanamwabudu Mungu lakini matendo yao yanakana jambo hilo. Badala yake watu ambao zamani walikuwa wakali “[wamevaa] utu mpya ulioumbwa kupatana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na ushikamanifu.” (Efe. 4:23, 24) Watu wanapojifunza kumhusu Mungu wanaona umuhimu wa kuishi kulingana na viwango vyake. Kisha wanachochewa kufanya mabadiliko kuhusiana na imani yao, mitazamo yao, na mwenendo wao. Si rahisi kufanya mabadiliko hayo lakini roho ya Mungu itawasaidia wale wanaotamani kutoka moyoni kufanya mapenzi ya Mungu wafaulu kufanya mabadiliko hayo.

“NAWE JIEPUSHE NAO”

17. Tunaweza kuepukaje kuathiriwa na watu wenye sifa zisizompendeza Mungu?

17 Tofauti kati ya watu wanaomtumikia Mungu na wasiomtumikia inazidi kuonekana wazi. Sisi tunaomtumikia Mungu lazima tuwe waangalifu ili tusiathiriwe na mitazamo mibaya ya watu wengine. Kwa hekima, tunatii shauri lilioongozwa na roho la kujiepusha na watu wanaotajwa katika 2 Timotheo 3:2-5. Bila shaka, hatuwezi kuwaepuka kabisa watu wenye sifa hizo zisizompendeza Mungu. Huenda tukalazimika kufanya kazi pamoja nao, kwenda shuleni pamoja nao, au kuishi pamoja nao. Lakini tunaweza kuepuka kuathiriwa na njia yao ya kufikiri au kuiga sifa zao mbaya. Tutafanikiwa kufanya hivyo ikiwa tutaimarisha hali yetu ya kiroho kwa kujifunza Biblia na kushirikiana kwa ukaribu na wale ambao wameazimia kumtumikia Yehova.

18. Maneno na matendo yetu yanaweza kuwanufaishaje wengine kiroho?

18 Tunapaswa pia kujitahidi kuwasaidia wengine kiroho. Tafuta fursa za kuwahubiria wengine huku ukimwomba Yehova akusaidie useme jambo linalofaa kwa wakati unaofaa. Tunapaswa kuwaambia wengine kwamba sisi ni Mashahidi wa Yehova. Tukifanya hivyo, mwenendo wetu mzuri utamletea Mungu utukufu na si sisi wenyewe. Tumezoezwa “kukataa matendo yasiyompendeza Mungu na tamaa za ulimwengu na kuishi kwa utimamu wa akili, uadilifu, na ujitoaji-kimungu katika mfumo huu wa mambo.” (Tito 2:11-14) Tukijiendesha kwa njia inayompendeza Mungu, wengine wataona jambo hilo, na baadhi yao huenda wakasema: “Tunataka kwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia kwamba Mungu yupo pamoja nanyi.”—Zek. 8:23.

^ fu. 10 Neno “mchongezi” au “mshtaki” katika Kigiriki ni di·aʹbo·los, nalo linatumiwa katika Biblia kumrejelea Shetani, yule mchongezi mwovu wa Mungu.