Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Upendo wa Aina Gani Unaoleta Furaha ya Kweli?

Ni Upendo wa Aina Gani Unaoleta Furaha ya Kweli?

“Wenye furaha ni watu ambao Mungu wao ni Yehova!”—ZAB. 144:15.

NYIMBO: 111, 109

1. Kwa nini kipindi tunachoishi ni cha pekee sana?

TUNAISHI katika kipindi cha pekee sana katika historia ya wanadamu. Kama Biblia ilivyotabiri, Yehova anakusanya “umati mkubwa . . . kutoka mataifa yote na makabila na jamii na lugha.” Wale wanaokusanywa wanafanyiza “taifa lenye nguvu,” ambalo lina watu zaidi ya milioni nane wenye furaha ‘wanaomtolea Mungu utumishi mtakatifu mchana na usiku.’ (Ufu. 7:9, 15; Isa. 60:22) Hakujawahi kuwa na kipindi kingine chenye watu wengi sana wanaompenda Mungu na wanadamu wenzao kama kipindi hiki.

2. Ni upendo gani usiofaa ambao watu waliojitenga na Mungu huonyesha? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

2 Hata hivyo, Maandiko yaliyoongozwa na roho yalitabiri kwamba katika siku zetu watu waliojitenga na Mungu wangeonyesha upendo usiofaa—upendo wenye ubinafsi. Mtume Paulo aliandika hivi: “Katika siku za mwisho . . . , watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, . . . wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu.” (2 Tim. 3:1-4) Upendo huo wenye ubinafsi haupatani hata kidogo na upendo wa Kikristo; ni tofauti kabisa na upendo huo. Watu wanaofuatilia malengo yenye ubinafsi hawawezi kupata furaha wanayotarajia. Kwa kweli, upendo wa aina hiyo hutokeza ulimwengu ambao ni ‘mgumu kushughulika nao.’

3. Tutachunguza nini katika makala hii, na kwa nini?

3 Paulo alitambua kwamba Wakristo wangekuwa hatarini kwa sababu ya kuenea kwa upendo huo wenye ubinafsi. Hivyo, alitoa onyo kwamba ‘tujiepushe’ na wale wanaoonyesha upendo huo usiofaa. (2 Tim. 3:5) Hata hivyo, hatuwezi kuepuka kabisa kushirikiana na watu wa aina hiyo. Kwa hiyo, tunaweza kujiepushaje na mitazamo inayotuzunguka ya ulimwengu na kujitahidi kumpendeza Yehova, Mungu mwenye upendo? Acheni tuone tofauti kati ya upendo wa kimungu na upendo unaofafanuliwa kwenye 2 Timotheo 3:2-4. Kufanya hivyo kutatusaidia kuchanganua na kuboresha upendo tunaopaswa kuonyesha, aina ya upendo ambao utatufanya turidhike kikweli na kuwa na furaha.

UNAMPENDA MUNGU AU UNAJIPENDA MWENYEWE?

4. Kwa nini si vibaya kujipenda kwa kiwango kinachofaa?

4 Akiongozwa na roho ya Mungu, mtume Paulo aliandika hivi: “Watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe.” Je, ni vibaya kujipenda? Hapana, ni jambo la kawaida na hata inafaa kujipenda kwa kiwango kinachofaa. Yehova alituumba hivyo. Yesu alisema hivi: “Lazima umpende jirani yako kama unavyojipenda mwenyewe.” (Marko 12:31) Ikiwa hatujipendi, hatuwezi kuwapenda jirani zetu. Pia Maandiko yanasema, “Waume wanapaswa kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Mwanamume anayempenda mke wake anajipenda mwenyewe, kwa maana hakuna mtu anayeuchukia mwili wake, bali huulisha na kuutunza.” (Efe. 5:28, 29) Hivyo, inafaa kujipenda kwa kiwango kinachofaa.

5. Unaweza kuwafafanuaje watu wanaojipenda wenyewe kupita kiasi?

5 Upendo unaotajwa kwenye 2 Timotheo 3:2 ni upendo usiofaa. Ni upendo uliopotoka, upendo wenye ubinafsi. Watu wanaojipenda wenyewe kupita kiasi hujifikiria kuliko ilivyo lazima. (Soma Waroma 12:3.) Jambo kuu maishani mwao ni wao wenyewe. Hawawajali wengine hata kidogo. Mambo yanapoenda kombo, wao huwa na mwelekeo wa kuwalaumu wengine badala ya kuwajibika kwa matendo yao. Kitabu kimoja kinachofafanua Biblia kinawalinganisha watu wanaojipenda wenyewe na ‘nungunungu ambaye hujikunja na kuwa kama mpira, akifurahia manyoya laini yenye joto upande wa ndani huku akielekeza nje miiba yake yenye ncha kali.’ Watu kama hao wenye ubinafsi hawana furaha ya kweli.

6. Kumpenda Mungu humfanya mtu awe na sifa zipi?

6 Mtume Paulo anataja kujipenda wenyewe kuwa jambo la kwanza katika orodha ya sifa zisizofaa ambazo zingeenea sana katika siku za mwisho. Wasomi wa Biblia wanadokeza kwamba sifa hiyo inatajwa ikiwa ya kwanza kwa sababu sifa zinazofuata hutokana nayo. Kinyume cha hilo, watu wanaompenda Mungu huonyesha sifa tofauti kabisa. Biblia huhusianisha upendo wa kimungu na shangwe, amani, subira, fadhili, wema, imani, upole, na kujizuia. (Gal. 5:22, 23) Mtunga zaburi aliandika hivi: “Wenye furaha ni watu ambao Mungu wao ni Yehova!” (Zab. 144:15) Yehova ni Mungu mwenye furaha, na watu wake huonyesha sifa hiyo. Zaidi ya hilo, tofauti na watu wanaojipenda wenyewe na wanaopenda tu kupokea, watumishi wa Yehova wanafurahia kujitoa kwa manufaa ya wengine.—Mdo. 20:35.

Tunaweza kuepukaje kuwa wenye kujipenda wenyewe? (Tazama fungu la 7)

7. Ni maswali gani yatakayotusaidia kuchanganua upendo wetu kwa Mungu?

7 Tunaweza kutambuaje ikiwa upendo wetu kwa Mungu umeanza kupungua na kwamba tumeanza kujipenda wenyewe zaidi? Fikiria himizo hili lililo katika Wafilipi 2:3, 4: “Msifanye jambo lolote kwa ugomvi au kwa kujisifu, bali kwa unyenyekevu mwaone wengine kuwa bora kuliko ninyi, huku mkiangalia, si faida zenu wenyewe, bali pia faida za wengine.” Tunaweza kujiuliza hivi: ‘Je, ninatumia shauri hilo maishani? Je, ninataka kutoka moyoni kufanya mapenzi ya Mungu? Je, mimi hujitahidi kuwasaidia watu kutanikoni na katika huduma ya shambani?’ Si rahisi nyakati zote kujitoa kwa ajili ya wengine. Jitihada nyingi inahitajika na pia kujidhabihu. Lakini je, kuna jambo lingine lolote linaloweza kutupatia furaha zaidi kuliko kujua kwamba tuna kibali cha Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote?

8. Kumpenda Mungu kumewachochea wengine wafanye nini?

8 Kumpenda Mungu kumewachochea wengine waache kazi nzuri zenye mshahara mnono ili wamtumikie Yehova kikamili zaidi. Ericka, dada anayeishi Marekani ni daktari. Lakini badala ya kufuatilia cheo chenye umashuhuri katika taaluma ya kitiba, aliamua kuwa painia wa kawaida na ametumikia pamoja na mume wake katika nchi kadhaa. Anapokumbuka kipindi hicho, anasema hivi: “Mambo mengi ambayo tulijionea katika eneo la lugha ya kigeni, na marafiki wengi ambao tulipata, yameboresha maisha yetu kwelikweli. Bado mimi ni daktari, lakini ninapotumia muda mwingi zaidi na nguvu zangu kuwasaidia watu wapone kiroho na kuwasaidia ndugu na dada zangu kutanikoni, ninaridhika sana na kupata shangwe nyingi.”

JE, UNAJIWEKEA HAZINA MBINGUNI AU DUNIANI?

9. Kwa nini kupenda pesa hakuwezi kuleta furaha?

9 Paulo aliandika kwamba watu wangekuwa “wenye kupenda pesa.” Miaka kadhaa iliyopita, painia fulani nchini Ireland alizungumza na mwanamume mmoja kuhusu Mungu. Mwanamume huyo alichomoa noti ya pesa, akaiinua, na kumwambia hivi kwa kiburi: “Huyu ndiye mungu wangu!” Ingawa watu wengi hawawezi kusema hivyo waziwazi, ulimwengu huu umejaa watu wanaopenda pesa na vitu vinavyoweza kununuliwa na pesa hizo. Lakini Biblia inatuonya hivi: “Anayependa fedha hatatosheka na fedha, wala anayependa mali hatatosheka na mapato.” (Mhu. 5:10) Watu kama hao hawawezi kamwe kuridhika na pesa, nao hujisababishia “maumivu mengi” kwa kujitahidi kujikusanyia pesa hizo.—1 Tim. 6:9, 10.

10. Aguri aliandika nini kuhusu utajiri na umaskini?

10 Bila shaka, sisi sote tunahitaji pesa. Kwa kadiri fulani, pesa ni ulinzi. (Mhu. 7:12) Lakini je, inawezekana mtu akawa na furaha ya kweli ikiwa ana pesa za kushughulikia mahitaji yake ya msingi tu? Ndiyo, inawezekana! (Soma Mhubiri 5:12.) Aguri mwana wa Yake aliandika hivi: “Usinipe umaskini wala utajiri. Acha nile tu fungu langu la chakula.” Ni rahisi kuelewa kwa nini Aguri hakutaka kuwa maskini hohehahe. Alieleza kwamba hakutaka ashawishike kuiba kwa sababu wizi ungemvunjia Mungu heshima. Lakini kwa nini alisali kwamba asipate utajiri? Aliandika hivi: “Ili nisishibe na kukukana na kusema, ‘Yehova ni nani?’” (Met. 30:8, 9) Huenda unawajua watu wanaotumainia utajiri wao badala ya kumtumaini Mungu.

11. Yesu alitoa shauri gani kuhusu pesa?

11 Watu wanaopenda pesa hawawezi kumpendeza Mungu. Yesu alisema hivi: “Hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili; kwa maana atamchukia mmoja na kumpenda mwingine, au atashikamana na mmoja na kumdharau mwingine. Hamwezi kutumikia Mungu na Utajiri.” Alikuwa ametangulia kusema hivi: “Acheni kujiwekea hazina duniani, ambako nondo na kutu hula na ambako wezi huvunja na kuiba. Badala yake, jiwekeeni hazina mbinguni, ambako hazitaliwa na nondo wala kutu, na ambako wezi hawatavunja na kuiba.”—Mt. 6:19, 20, 24.

12. Kuishi maisha rahisi kunaweza kutusaidiaje kumtumikia Mungu? Toa mfano.

12 Watu wengi wametambua kwamba kuishi maisha rahisi huwafanya wawe na furaha zaidi na kuwapa muda mwingi zaidi wa kumtumikia Yehova. Jack, ndugu anayeishi Marekani, aliuza nyumba yake kubwa na biashara yake kwa sababu alijua kufanya hivyo kungemwezesha kufanya upainia pamoja na mke wake. Anakumbuka hivi: “Haikuwa rahisi kuuza nyumba yetu maridadi na ardhi tuliyomiliki. Hata hivyo, kwa miaka mingi ningerudi nyumbani nikiwa nimechoshwa na matatizo kazini. Mke wangu, ambaye alikuwa painia wa kawaida, alikuwa na furaha sikuzote. Alikuwa akisema hivi, ‘Mimi ninamtumikia mwajiri bora zaidi!’ Kwa kuwa sasa mimi pia ni painia, sote tunamfanyia kazi mwajiri yuleyule, Yehova.”

Tunaweza kuepukaje kuwa wenye kupenda pesa? (Tazama fungu la 13)

13. Tunaweza kufanya nini ili kuchanganua maoni yetu kuhusu pesa?

13 Ili kuchanganua maoni yetu kuhusu pesa, tunaweza kuchunguza kwa unyoofu maoni yetu kuhusu maswali haya: ‘Je, ninaamini kabisa yale ambayo Biblia inasema kuhusu pesa na, je, ninaishi kupatana na maoni hayo? Je, jambo kuu maishani mwangu ni kutafuta pesa? Je, ninathamini zaidi vitu vya kimwili kuliko uhusiano wangu pamoja na Yehova au na watu wengine? Je, kweli ninaamini kwamba Yehova ataniandalia mahitaji yangu?’ Tunaweza kuwa na uhakika kwamba hatawatamausha kamwe wale wanaomtumaini.—Mt. 6:33.

JE, UNAMTAFUTA YEHOVA AU UNATAFUTA RAHA?

14. Tunapaswa kuwa na maoni gani yaliyosawazika kuhusu raha?

14 Kama ilivyotabiriwa, watu wengi leo ni “wenye kupenda raha.” Kama tu ambavyo si kosa kujipenda kwa kiwango kinachofaa au kuwa na maoni yanayofaa kuhusu pesa, vilevile si vibaya kuwa na maoni yaliyosawazika kuhusu raha. Yehova hataki tujinyime kupita kiasi au tujiepushe na utendaji wenye kujenga na unaofurahisha. Biblia huwatia moyo hivi watu waaminifu: “Nenda, ule chakula chako kwa shangwe, na unywe divai yako kwa moyo mchangamfu.”—Mhu. 9:7.

15. Ni raha ya aina gani inayotajwa kwenye 2 Timotheo 3:4?

15 Andiko la 2 Timotheo 3:4 linazungumza kuhusu kufuatilia raha bila kumfikiria Mungu. Ona kwamba mstari huo hausemi kwamba watu wangependa raha zaidi ya kumpenda Mungu kana kwamba wangempenda Mungu kwa kiasi fulani. Mstari huo unasema wangependa raha ‘badala ya kumpenda Mungu.’ Msomi mmoja aliandika hivi: “Kwa hakika [mstari] huu haumaanishi kwamba wanampenda Mungu kwa kadiri fulani. Unamaanisha kwamba hawampendi Mungu hata kidogo.” Hilo ni onyo zito sana kwa wale wanaositawisha upendo usiofaa kuelekea raha! Maneno “wanaopenda raha” yanawafafanua vizuri wale ambao “wanakengeushwa na . . . raha za maisha.”—Luka 8:14.

16, 17. Yesu aliweka mfano gani kuhusu kufuatilia raha?

16 Yesu alionyesha mtazamo uliosawazika kabisa kuhusu raha. Alihudhuria ‘karamu ya ndoa’ na “karamu kubwa.” (Yoh. 2:1-10; Luka 5:29) Alipokuwa kwenye karamu ya ndoa, alibadilisha kimuujiza maji kuwa divai, na hivyo kuongeza divai iliyokuwa imepungua. Katika pindi nyingine, alipinga maoni ya watu waliojiona kuwa waadilifu ambao walimchambua kwa sababu ya kula na kunywa.—Luka 7:33-36.

17 Hata hivyo, Yesu hakujiingiza katika maisha ya kufuatilia raha. Alimtanguliza Yehova na akajitoa bila kuchoka kwa ajili ya wengine. Ili watu wengi wapate kuishi, alivumilia kwa hiari kifo chenye maumivu makali kwenye mti wa mateso. Akizungumza na wale ambao wangefuata hatua zake, Yesu alisema hivi: “Wenye furaha ni ninyi, watu wanapowashutumu na kuwatesa na kuwasingizia kila aina ya uovu kwa sababu yangu. Furahini na kushangilia sana, kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni, kwa maana hivyo ndivyo walivyowatesa manabii waliokuwapo kabla yenu.”—Mt. 5:11, 12.

Tunaweza kuepukaje kuwa wenye kupenda raha? (Tazama fungu la 18)

18. Ni maswali gani yanayoweza kutusaidia kujua tunapenda raha kwa kadiri gani?

18 Ni nini kinachoweza kutusaidia kujua tunafuatilia raha kwa kadiri gani? Inafaa tujiulize hivi: ‘Je, burudani huchukua nafasi ya kwanza badala ya mikutano na utumishi wa shambani? Je, niko tayari kujinyima mambo fulani kwa sababu ninataka kumtumikia Mungu? Ninapochagua mambo ya kujifurahisha, je, mimi hufikiria maoni ya Yehova kuhusu mambo hayo?’ Ikiwa tunampenda Mungu kikweli, tutakuwa waangalifu ili tujiepushe na mambo yasiyompendeza na hata mambo tunayokisia kwamba hayatampendeza.—Soma Mathayo 22:37, 38.

JINSI YA KUPATA FURAHA

19. Ni nani ambao hawawezi kamwe kuwa na furaha ya kweli?

19 Hatimaye, baada ya miaka 6,000 hivi ya kuteseka kwa wanadamu, ulimwengu wa Shetani umekaribia mwisho wake. Dunia imejaa watu wanaojipenda sana, wanaopenda pesa, na kupenda raha. Hao ni watu wanaofanya juu chini wapate vitu wanavyotamani, watu wanaotanguliza tamaa zao wenyewe maishani. Watu kama hao hawawezi kamwe kuwa na furaha ya kweli. Kinyume cha hilo, mtunga zaburi aliandika hivi: “Mwenye furaha ni yule ambaye Mungu wa Yakobo ni msaidizi wake, ambaye anamtumaini Yehova Mungu wake.”—Zab. 146:5.

20. Kumpenda Mungu kumekuleteaje furaha?

20 Upendo kumwelekea Mungu unaendelea kusitawi miongoni mwa watu wa Yehova, na idadi yao inazidi kuongezeka mwaka baada ya mwaka. Jambo hilo linathibitisha kwamba Ufalme wa Mungu unatawala na hivi karibuni utaleta baraka tele hapa duniani. Shangwe ya kweli na inayodumu hutokana na kufanya mapenzi ya Mungu na kujua kwamba tunafanya mambo yanayompendeza Yule Aliye Mkuu Zaidi. Na wale wanaompenda Yehova watakuwa na shangwe milele! Katika makala inayofuata, tutachunguza baadhi ya sifa zinatokana na upendo wenye ubinafsi na jinsi sifa hizo zinavyotofautiana na sifa zinazoonyeshwa na watumishi wa Yehova.