Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 4

Mlo Usiohusisha Mengi Unatufundisha Nini Kuhusu Mfalme Wetu wa Mbinguni?

Mlo Usiohusisha Mengi Unatufundisha Nini Kuhusu Mfalme Wetu wa Mbinguni?

“Huu unamaanisha mwili wangu. . . . Hii inamaanisha ‘damu yangu ya agano.’”—MT. 26:26-28.

WIMBO 16 Msifuni Yah kwa Mwana Wake Mtiwa Mafuta

MUHTASARI *

1-2. (a) Kwa nini hatushangai kuona kwamba Yesu alitufundisha kuadhimisha kifo chake kwa njia isiyohusisha mengi? (b) Tutachunguza sifa gani za Yesu?

JE, UNAWEZA kueleza ni mambo gani ambayo hutendeka kwenye Ukumbusho wa kila mwaka wa kifo cha Kristo? Hapana shaka kwamba wengi wetu tunaweza kukumbuka mambo ya msingi ambayo hutendeka kwenye Mlo wa Jioni wa Bwana. Kwa nini? Kwa sababu mlo huo unahusisha mambo machache sana. Hata hivyo, hilo ni tukio muhimu sana. Hivyo huenda tukauliza, ‘Kwa nini mlo huo unahusisha mambo machache sana hivyo?’

2 Wakati wa huduma yake duniani, Yesu alijulikana kwa kufundisha kweli muhimu kwa njia nyepesi, iliyo wazi, na rahisi kuelewa. (Mt. 7:28, 29) Kwa njia hiyohiyo, alitufundisha jinsi ya kuadhimisha * kifo chake kwa njia yenye kuheshimika na isiyohusisha mengi. Acheni tuchunguze kwa undani mlo huo wa Ukumbusho na pia baadhi ya mambo ambayo Yesu alisema na kutenda. Tutaelewa vizuri zaidi jinsi Yesu alivyo mnyenyekevu, jasiri, na mwenye upendo, na tutajifunza jinsi tunavyoweza kumwiga vizuri zaidi.

YESU NI MNYENYEKEVU

Mkate na divai inayotumiwa katika Ukumbusho inatukumbusha kwamba Yesu alitoa uhai wake kwa ajili yetu na kwamba sasa yeye ni Mfalme wetu anayetawala mbinguni (Tazama fungu la 3 hadi 5)

3. Kama tunavyosoma kwenye Mathayo 26:26-28, Mlo wa Ukumbusho ambao Yesu alianzisha ulihusisha nini, na vitu viwili alivyotumia vinafananisha nini?

3 Yesu alianzisha Ukumbusho wa kifo chake akiwa pamoja na mitume wake 11 waaminifu. Alitumia chakula kilichokuwa kimebaki baada ya mlo wa Pasaka na kuanzisha mwadhimisho huo usiohusisha mengi. (Soma Mathayo 26:26-28.) Alitumia tu mkate usiotiwa chachu na divai iliyokuwepo. Yesu aliwaambia mitume wake kwamba vitu hivyo viwili vya msingi vilifananisha damu yake na mwili wake mkamilifu, ambao baada ya muda mfupi angeutoa kwa ajili yao. Inaelekea mlo huo muhimu usiohusisha mengi haukuwashangaza mitume. Kwa nini?

4. Ushauri ambao Yesu alimpa Martha unatusaidiaje kuelewa sababu iliyomfanya Yesu atumie vitu vichache kwenye mlo wa Ukumbusho?

4 Fikiria kilichotendeka miezi kadhaa mapema katika mwaka wa tatu wa huduma ya Yesu alipowatembelea Lazaro, Martha, na Maria, rafiki zake. Katika mazingira hayo ya kustarehesha, Yesu alianza kufundisha. Martha alikuwepo, lakini alikuwa na shughuli nyingi za kutayarisha mlo mkubwa kwa ajili ya mgeni wake mwenye kuheshimika. Alipoona hilo, Yesu alimrekebisha Martha kwa fadhili, na kumsaidia aone kwamba haikuwa lazima nyakati zote kutayarisha mlo wenye mambo mengi. (Luka 10:40-42) Baadaye, Yesu mwenyewe alitumia shauri hilo saa chache kabla ya kifo chake cha kidhabihu. Alihakikisha kwamba mlo wa Ukumbusho haukuhusisha mengi. Jambo hilo linatufundisha nini kumhusu Yesu?

5. Mlo wa jioni unatufundisha nini kumhusu Yesu, na hilo linapatanaje na andiko la Wafilipi 2:5-8?

5 Yesu alikuwa mnyenyekevu katika kila jambo alilosema na kutenda. Hivyo, haishangazi kwamba alionyesha unyenyekevu mkubwa usiku wa mwisho wa maisha yake hapa duniani. (Mt. 11:29) Alijua kwamba alikuwa karibu kutoa dhabihu kubwa kupita zote zilizowahi kutolewa na kwamba Yehova angemfufua na kumpa cheo chenye utukufu mbinguni. Licha ya hilo, Yesu hakujielekezea fikira isivyo lazima kwa kuanzisha mwadhimisho wa kifo chake uliohusisha mambo mengi. Badala yake, aliwaambia wanafunzi wake kwamba walipaswa kumkumbuka mara moja kwa mwaka kupitia mlo huo. (Yoh. 13:15; 1 Kor. 11:23-25) Mlo huo usiohusisha mengi na uliofaa pindi hiyo, unaonyesha kwamba Yesu hakujikweza. Tunafurahi kwamba unyenyekevu ni mojawapo ya sifa za Mfalme wetu wa mbinguni.​—Soma Wafilipi 2:5-8.

6. Tunaweza kuigaje unyenyekevu wa Yesu tunapokabili majaribu?

6 Tunaweza kuigaje unyenyekevu wa Yesu? Kwa kutanguliza masilahi ya wengine. (Flp. 2:3, 4) Fikiria kuhusu usiku wa mwisho wa maisha ya Yesu duniani. Yesu alijua kwamba baada ya muda mfupi angekufa kifo chenye maumivu makali; hata hivyo, aliwahangaikia sana mitume wake waaminifu ambao wangemwombolezea baada ya kifo chake. Hivyo, alitumia usiku huo wa mwisho kuwafundisha, kuwatia moyo, na kuwafariji. (Yoh. 14:25-31) Kwa unyenyekevu Yesu aliwahangaikia wengine zaidi kuliko alivyojihangaikia. Alituwekea mfano bora sana!

YESU NI JASIRI

7. Yesu alionyeshaje ujasiri mkubwa muda mfupi baada ya kuanzisha Mlo wa Jioni wa Bwana?

7 Muda mfupi baada ya Yesu kuanzisha Mlo wa Jioni wa Bwana, alionyesha ujasiri mkubwa. Jinsi gani? Yesu alikubali mapenzi ya Baba yake yatendeke, ingawa alijua kwamba angeuawa kwa sababu ya kosa lenye aibu la kukufuru. (Mt. 26:65, 66; Luka 22:41, 42.) Yesu alidumisha utimilifu kikamilifu ili kuliheshimu jina la Yehova, kutetea enzi Yake kuu, na kuwafungulia wanadamu wanaotubu njia ya kupata uhai usio na mwisho. Wakati huohuo, Yesu aliwatayarisha wafuasi wake kwa ajili ya mambo ambayo wangekabili punde si punde.

8. (a) Yesu aliwaambia nini mitume wake waaminifu? (b) Katika miaka iliyofuata baada ya kifo chake, wanafunzi wa Yesu waliigaje mfano wake wa ujasiri?

8 Pia, Yesu alionyesha ujasiri kwa kukazia uangalifu mahitaji ya mitume wake waaminifu badala ya kukazia fikira wasiwasi ambao huenda alikuwa nao. Mlo alioanzisha baada ya kumfukuza Yuda, ungewakumbusha wale wote ambao wangetiwa mafuta kuhusu manufaa ya damu yake iliyomwagwa na manufaa ya kuwa washiriki pamoja naye katika agano jipya. (1 Kor. 10:16, 17) Ili kuwasaidia wastahili kupokea mwito wao mbinguni, Yesu aliwaambia wafuasi wake mambo ambayo yeye na Baba yake walitarajia kutoka kwao. (Yoh. 15:12-15) Pia, Yesu aliwaambia mitume wake kuhusu majaribu ambayo wangekabili. Kisha aliwatia moyo waige mfano wake kwa kuwahimiza hivi: “Jipeni moyo!” (Yoh. 16:1-4a, 33) Miaka mingi baadaye, wanafunzi wa Yesu walikuwa wakiendelea kuiga mfano wake wa kujidhabihu na wa ujasiri. Walitegemezana walipokabili majaribu mbalimbali ingawa kufanya hivyo kungefanya wateseke.​—Ebr. 10:33, 34.

9. Tunaweza kumwigaje Yesu kwa kuonyesha ujasiri?

9 Vivyo hivyo leo, tunamwiga Yesu kwa kuonyesha ujasiri. Kwa mfano, tunahitaji ujasiri ili kuwasaidia ndugu zetu wanaoteswa kwa sababu ya imani yao. Nyakati nyingine, huenda ndugu zetu wakafungwa gerezani isivyo haki. Hilo linapotokea, tunapaswa kufanya yote tuwezayo kuwasaidia, kutia ndani kuwatetea. (Flp. 1:14; Ebr. 13:19) Njia nyingine ya kuonyesha ujasiri ni kwa kuendelea kuhubiri “kwa ujasiri.” (Mdo. 14:3) Kama Yesu, tumeazimia kuhubiri ujumbe wa Ufalme, ingawa huenda watu wakatupinga au kututesa. Hata hivyo, nyakati nyingine huenda tukakosa ujasiri. Tunaweza kufanya nini?

10. Tunapaswa kufanya nini majuma machache kabla ya Ukumbusho, na kwa nini?

10 Tunaweza kuongeza ujasiri wetu kwa kutafakari kuhusu tumaini tulilo nalo kwa sababu ya dhabihu ya fidia ya Kristo. (Yoh. 3:16; Efe. 1:7) Majuma machache kabla ya Ukumbusho, tuna fursa ya pekee ya kuthamini fidia hata zaidi. Katika kipindi hicho, fuatana na usomaji wa Biblia wa Ukumbusho na usali na kutafakari kuhusu matukio ya kabla na baada ya kifo cha Yesu. Kisha tutakapokusanyika kwa ajili ya Mlo wa Jioni wa Bwana, tutaelewa vizuri zaidi umuhimu wa mifano ya Ukumbusho na dhabihu isiyoweza kulinganishwa na chochote inayofananishwa na mifano hiyo. Tunapoelewa vizuri mambo ambayo Yesu na Yehova wametufanyia na kuelewa jinsi yanavyotunufaisha sisi na wapendwa wetu, tumaini letu huwa na nguvu zaidi, na tutachochewa kuvumilia kwa ujasiri mpaka mwisho.​—Ebr. 12:3.

11-12. Tumejifunza nini kufikia sasa?

11 Kufikia hapa, tumejifunza kwamba Mlo wa Jioni wa Bwana hautukumbushi tu kuhusu fidia yenye thamani ya Yesu, bali pia kuhusu unyenyekevu na ujasiri wake wa pekee. Tunafurahi kwamba Yesu anaendelea kuonyesha sifa hizo akiwa Kuhani wetu Mkuu mbinguni, ambaye hutuombea! (Ebr. 7:24, 25) Ili kuonyesha kwamba tunathamini fidia kutoka moyoni, ni lazima tuadhimishe kwa ushikamanifu kifo cha Yesu, kama tu alivyoamuru. (Luka 22:19, 20) Tunafanya hivyo katika siku inayolingana na Nisani 14, ambayo ndiyo tarehe muhimu zaidi katika mwaka.

12 Mlo wa Jioni wa Bwana usiohusisha mengi unaweza kutufundisha sifa nyingine iliyomchochea Yesu afe kwa ajili yetu. Alipokuwa mwanadamu duniani, alijulikana kwa sifa hiyo. Sifa gani?

YESU NI MWENYE UPENDO

13. Andiko la Yohana 15:9 na 1 Yohana 4:8-10 linafafanuaje upendo ambao Yehova na Yesu wameonyesha, na ni nani wanaonufaika na upendo huo?

13 Katika kila jambo alilotenda, Yesu alionyesha kikamilifu upendo mwingi ambao Yehova anao kutuelekea. (Soma Yohana 15:9; 1 Yohana 4:8-10.) Zaidi ya yote, Yesu alichochewa kutoka moyoni kutoa uhai wake kwa ajili yetu. Iwe sisi ni watiwa-mafuta au “kondoo wengine,” tunanufaika na upendo ambao Yehova na Mwana wake wametuonyesha kupitia dhabihu hiyo. (Yoh. 10:16; 1 Yoh. 2:2) Fikiria pia kuhusu mifano inayotumiwa katika Ukumbusho; hiyo pia inafunua kwamba Yesu anawapenda na kuwafikiria sana wanafunzi wake. Jinsi gani?

Akichochewa na upendo, Yesu alianzisha mwadhimisho wa Ukumbusho usiohusisha mengi ambao ungeweza kufanywa kwa karne nyingi chini ya hali mbalimbali (Tazama fungu la 14 hadi 16) *

14. Yesu aliwaonyesha wanafunzi wake upendo jinsi gani?

14 Yesu aliwaonyesha upendo wafuasi wake watiwa-mafuta kwa kuanzisha mwadhimisho usiohusisha mengi, badala ya desturi ambayo ingekuwa ngumu kufuata. Kadiri wakati ulivyopita, wanafunzi hao watiwa-mafuta wangehitaji kuadhimisha Ukumbusho kila mwaka, wakifanya hivyo chini ya hali mbalimbali, hata wakiwa gerezani. (Ufu. 2:10) Je, walifaulu kumtii Yesu? Ndiyo!

15-16. Baadhi ya ndugu na dada wamefanikiwaje kuadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana chini ya hali ngumu?

15 Tangu wakati huo mpaka sasa, Wakristo wa kweli wamejitahidi kuhakikisha kwamba wanaadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Yesu. Wamefuata kadiri wawezavyo utaratibu wa kuadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana, nyakati nyingine chini ya hali ngumu. Fikiria mifano ifuatayo. Alipokuwa katika kifungo cha upweke katika gereza moja nchini China, Ndugu Harold King alihitaji kuwa mbunifu. Aliandaa kisiri mifano ya Ukumbusho, akitumia vitu alivyokuwa navyo. Pia, alihesabu siku kwa makini ili ajue tarehe ya Ukumbusho. Tarehe ya Ukumbusho ilipofika, aliimba, akasali, na kutoa hotuba ya Kimaandiko akiwa peke yake gerezani.

16 Fikiria mfano mwingine. Kikundi fulani cha akina dada waliokuwa wamefungwa katika kambi ya mateso wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu walihatarisha maisha yao ili kuadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana. Hata hivyo, kwa kuwa mlo huo hauhusishi mengi, walifanikiwa kuadhimisha Ukumbusho kisiri. Wanaeleza hivi: “Tulisimama kuzunguka meza ndogo iliyofunikwa kwa kitambaa cheupe na iliyokuwa na mifano. Tulitumia mshumaa kwa sababu mwangaza wa umeme ungefanya tugunduliwe. . . . Tuliweka upya nadhiri zetu za dhati kwa Baba yetu kwamba tutatumia nguvu zetu zote kulitetea jina Lake takatifu.” Walionyesha imani ya pekee sana! Na Yesu alionyesha upendo mkubwa sana kwa kufanya iwe rahisi kwetu kuadhimisha Ukumbusho hata chini ya hali ngumu!

17. Tunaweza kujiuliza maswali gani?

17 Kadiri Ukumbusho unavyokaribia, ni vizuri kujiuliza maswali yafuatayo: ‘Ninaweza kumwigaje Yesu vizuri zaidi inapohusu kuwaonyesha wengine upendo? Je, ninajali zaidi mahitaji ya waabudu wenzangu kuliko mahitaji yangu mwenyewe? Je, ninatazamia ndugu na dada zangu watimize mengi zaidi kuliko wanavyoweza, au ninatambua mambo yanayopita uwezo wao?’ Acheni sikuzote tumwige Yesu kwa kuwaonyesha wengine “hisia-mwenzi.”​—1 Pet. 3:8.

ZINGATIA AKILINI MAMBO HAYO

18-19. (a) Tuna hakika kuhusu jambo gani? (b) Umeazimia kufanya nini?

18 Takwa la kuadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Kristo halitaendelea kuwapo kwa muda mrefu. Yesu “atakapokuja” wakati wa dhiki kuu, atawakusanya kwenda mbinguni watu wake “waliochaguliwa” watakaokuwa wamebaki duniani, na Ukumbusho hautaadhimishwa tena.​—1 Kor. 11:26; Mt. 24:31.

19 Hata baada ya kuacha kuadhimisha Ukumbusho, tuna hakika kwamba watu wa Yehova wataendelea kukumbuka sana mlo huo usiohusisha mengi unaoonyesha unyenyekevu, ujasiri, na upendo mkubwa zaidi uliowahi kuonyeshwa na mwanadamu. Hapana shaka kwamba wale walioadhimisha Ukumbusho watawasimulia wale wote watakaokuwa hai wakati huo kuhusu mlo huo wa pekee. Lakini ili tunufaike na mlo huo leo, ni lazima tuazimie kuiga unyenyekevu, ujasiri, na upendo wa Yesu. Tukiiga sifa hizo, tuna uhakika kwamba tutapokea thawabu yetu kutoka kwa Yehova.​—2 Pet. 1:10, 11.

WIMBO 13 Kristo, Kielelezo Chetu

^ fu. 5 Hivi karibuni, tutaadhimisha kifo cha Yesu Kristo kwenye Mlo wa Jioni wa Bwana. Mlo huo usiohusisha mengi unatufundisha mengi kuhusu unyenyekevu, ujasiri, na upendo wa Yesu. Katika makala hii, tutazungumzia jinsi tunavyoweza kuiga sifa nzuri alizoonyesha.

^ fu. 2 UFAFANUZI WA MANENO: Kuadhimisha kunamaanisha kufanya jambo fulani la pekee ili kukumbuka au kuheshimu tukio au mtu fulani muhimu.

^ fu. 56 MAELEZO YA PICHA Maigizo ya watumishi waaminifu wakiadhimisha Ukumbusho katika kutaniko la karne ya kwanza; katika karne ya 19; katika kambi ya mateso ya Wanazi; na katika siku zetu kwenye Jumba la Ufalme lisilo na kuta katika nchi moja yenye joto ya Amerika Kusini.