Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kenneth E. Cook, Jr., na Jamie, mke wake

Mshiriki Mpya wa Baraza Linaloongoza

Mshiriki Mpya wa Baraza Linaloongoza

JUMATANO asubuhi, Januari 24, 2018, washiriki wa familia ya Betheli ya Marekani na Kanada walifurahia kusikia tangazo hili la pekee: Ndugu Kenneth Cook, Jr., sasa ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova.

Ndugu Cook alizaliwa na kulelewa huko Pennsylvania, Marekani. Alijifunza kweli kutoka kwa mwanafunzi mwenzake muda mfupi kabla ya kuhitimu shule ya sekondari na alibatizwa Juni 7, 1980. Alianza utumishi wa wakati wote akiwa painia wa kawaida Septemba 1, 1982. Baada ya kufanya upainia kwa miaka miwili, alialikwa Betheli, ambapo alianza utumishi huo Oktoba 12, 1984, huko Wallkill, New York.

Kwa miaka 25 iliyofuata Ndugu Cook alishughulikia migawo mbalimbali kwenye kiwanda cha uchapishaji na pia kwenye Ofisi ya makao ya Betheli. Alifunga ndoa na Dada Jamie, mwaka wa 1996, kisha Jamie akajiunga naye katika utumishi wa Betheli huko Wallkill. Katika mwezi wa Desemba 2009, Ndugu na Dada Cook waliombwa wakatumikie katika Kituo cha Elimu cha Watchtower huko Patterson, New York, ambapo Ndugu Cook alipewa mgawo katika Idara ya Kushughulikia Maswali ya Wasomaji. Mwezi wa Aprili 2016, baada ya kurudi Wallkill kwa muda mfupi, Ndugu na Dada Cook walipewa mgawo wa kutumikia huko Brooklyn, New York. Miezi mitano baadaye, walihamia kwenye makao makuu mapya ya ulimwenguni pote huko Warwick, New York. Januari 2017, Ndugu Cook aliwekwa rasmi kuwa msaidizi wa Halmashauri ya Uandikaji ya Baraza Linaloongoza.