Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 5

Uhudhuriaji Wetu wa Mikutano Unafunua Nini Kutuhusu?

Uhudhuriaji Wetu wa Mikutano Unafunua Nini Kutuhusu?

Endeleeni “kukitangaza kifo cha Bwana, mpaka atakapokuja.”​—1 KOR. 11:26.

WIMBO 18 Tunathamini Fidia

MUHTASARI *

1-2. (a) Yehova huona nini mamilioni ya watu wanapokusanyika kwa ajili ya Mlo wa Jioni wa Bwana? (Tazama picha kwenye jalada.) (b) Tutazungumzia nini katika makala hii?

WAZIA mambo ambayo Yehova huona anapotazama mamilioni ya watu ulimwenguni kote wakikusanyika kwa ajili ya Mlo wa Jioni wa Bwana. Haangalii tu idadi kubwa ya watu waliohudhuria, bali pia anamtambua mtu mmoja-mmoja aliyehudhuria. Kwa mfano, anawaona wale ambao kila mwaka hawakosi kamwe kuhudhuria. Miongoni mwao huenda kuna watu ambao wamehudhuria licha ya kwamba wanakabili mateso makali. Wengine hawahudhurii mikutano kwa ukawaida, lakini wanahudhuria Ukumbusho kwa sababu wanaona ni lazima kufanya hivyo. Pia, Yehova anawatambua wale wanaohudhuria Ukumbusho kwa mara ya kwanza, labda wakitaka kujua jinsi tukio hilo linavyokuwa.

2 Kwa hakika, Yehova anafurahi anapoona watu wengi sana wakihudhuria Ukumbusho. (Luka 22:19) Hata hivyo, jambo kuu kwa Yehova si idadi ya watu wanaohudhuria. Anapendezwa zaidi na sababu inayowafanya wahudhurie; Yehova anaangalia nia yao. Katika makala hii, tutazungumzia swali hili muhimu: Mbali na kuhudhuria mwadhimisho wa kila mwaka wa Ukumbusho, kwa nini pia tunahudhuria mikutano ya kila juma ambayo Yehova huwaandalia wale wanaompenda?

(Tazama fungu la 1 na 2) *

UNYENYEKEVU HUTUCHOCHEA KUHUDHURIA

3-4. (a) Kwa nini tunahudhuria mikutano? (b) Uhudhuriaji wetu wa mikutano hufunua nini kutuhusu? (c) Kama inavyotajwa kwenye andiko la 1 Wakorintho 11:23-26, kwa nini hatupaswi kukosa Ukumbusho?

3 Sababu kuu inayotufanya tuhudhurie mikutano ya kutaniko ni kwamba mikutano ni sehemu ya ibada yetu. Pia, tunahudhuria mikutano kwa sababu tunafundishwa na Yehova mikutanoni. Watu wenye kiburi hawapendi kufundishwa jambo lolote. (3 Yoh. 9) Tofauti nao, sisi tuna hamu ya kufundishwa na Yehova na tengenezo lake.—Isa. 30:20; Yoh. 6:45.

4 Tunapohudhuria mikutano, tunaonyesha kwamba sisi ni wanyenyekevu, yaani, tuko tayari na tuna nia ya kufundishwa. Sisi huhudhuria tukio muhimu la Ukumbusho wa kifo cha Yesu, si tu kwa sababu tunahisi kwamba ni lazima tufanye hivyo, bali pia kwa sababu tunataka kutii kwa unyenyekevu amri hii ya Yesu: “Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka.” (Soma 1 Wakorintho 11:23-26.) Mkutano huo huimarisha tumaini letu la wakati ujao na kutukumbusha kwamba Yehova anatupenda sana. Hata hivyo, Yehova anajua kwamba tunahitaji kutiwa moyo na kuimarishwa zaidi ya mara moja kwa mwaka. Hivyo anatuandalia mikutano ya kila juma na kutuhimiza tuhudhurie. Unyenyekevu hutuchochea kutii. Tunatumia saa kadhaa kila juma kutayarisha na kuhudhuria mikutano hiyo.

5. Kwa nini watu wanyenyekevu hukubali mwaliko wa Yehova?

5 Kila mwaka, watu wengi wanyenyekevu hukubali mwaliko wa kufundishwa na Yehova. (Isa. 50:4) Wao hufurahia kuhudhuria Ukumbusho na kisha huanza kuhudhuria mikutano mingine. (Zek. 8:20-23) Sote kwa pamoja, tunafurahia kufundishwa na kuongozwa na Yehova, “msaidizi [wetu] na mwokozi [wetu].” (Zab. 40:17) Kwa kweli, je, kuna jambo lolote lenye kufurahisha zaidi au hata muhimu zaidi kuliko kukubali mwaliko wa kufundishwa na Yehova na Yesu, Mwana wake anayempenda sana?​—Mt. 17:5; 18:20; 28:20.

6. Unyenyekevu ulimsaidiaje mwanamume fulani kuhudhuria Ukumbusho?

6 Kila mwaka, sisi hujitahidi kuwaalika watu wengi iwezekanavyo kwenye Ukumbusho wa kifo cha Yesu. Watu wengi wanyenyekevu wamenufaika kwa kukubali mwaliko huo. Fikiria mfano mmoja. Miaka kadhaa iliyopita, mwanamume fulani alipokea mwaliko wa Ukumbusho, lakini akamwambia ndugu aliyemwalika kwamba hataweza kuhudhuria. Hata hivyo, jioni siku ya Ukumbusho, ndugu huyo alishangaa kumwona mwanamume huyo akiingia ndani ya Jumba la Ufalme. Mwanamume huyo alifurahi sana kuona jinsi alivyokaribishwa kwa uchangamfu hivi kwamba akaanza kuhudhuria mikutano kila juma. Kwa kweli, kwa mwaka mzima alikosa mkutano mara tatu tu. Ni nini kilichomsaidia kuchukua hatua hiyo? Alikuwa mnyenyekevu vya kutosha kubadili uamuzi wake. Baadaye, ndugu aliyekuwa amemwalika alisema hivi, “Mwanamume huyo ni mnyenyekevu sana.” Hapana shaka kwamba Yehova alimvuta Kwake, na sasa yeye ni ndugu aliyebatizwa.​—2 Sam. 22:28; Yoh. 6:44.

7. Mambo tunayojifunza mikutanoni na katika Biblia hutusaidiaje kuwa wanyenyekevu?

7 Mambo tunayojifunza mikutanoni na katika Biblia yanaweza kutusaidia kuwa wanyenyekevu. Majuma machache kabla ya Ukumbusho, kwa kawaida mikutano yetu hukazia mfano wa Yesu na unyenyekevu alioonyesha kwa kutoa uhai wake kuwa fidia. Na siku chache kabla ya Ukumbusho, tunahimizwa tusome masimulizi ya Biblia kuhusu matukio yaliyotukia wakati wa kifo na ufufuo wa Yesu. Mambo tunayojifunza katika mikutano hiyo na habari tunazosoma katika masimulizi hayo ya Biblia hutufanya tuthamini zaidi dhabihu ambayo Yesu alitoa kwa ajili yetu. Tunachochewa kuiga unyenyekevu wake na kufanya mapenzi ya Yehova, hata inapokuwa vigumu kwetu kufanya hivyo.—Luka 22:41, 42.

UJASIRI HUTUSAIDIA KUHUDHURIA

8. Yesu alionyeshaje ujasiri?

8 Pia, tunajitahidi kumwiga Yesu kwa kuonyesha ujasiri. Fikiria kuhusu ujasiri ambao Yesu alionyesha siku chache kabla ya kifo chake. Alijua vizuri kwamba baada ya muda mfupi maadui wake wangemwaibisha, wangempiga, na kumuua. (Mt. 20:17-19) Lakini bado alikuwa tayari kufa. Wakati ulipofika, aliwaambia hivi mitume wake waaminifu waliokuwa pamoja naye katika bustani ya Gethsemane: “Simameni twende. Tazama! Msaliti wangu amekaribia.” (Mt. 26:36, 46) Na umati uliokuwa umebeba silaha ulipokuja kumkamata, Yesu aliukaribia, akajitambulisha, na kuwaamuru wanajeshi wawaache mitume wake waende. (Yoh. 18:3-8) Huo ulikuwa ujasiri mkubwa kwelikweli! Leo, Wakristo watiwa-mafuta na kondoo wengine hujitahidi kumwiga Yesu kwa kuonyesha ujasiri. Jinsi gani?

Unapoonyesha ujasiri kwa kuhudhuria mikutano ya Kikristo unawaimarisha wengine (Tazama fungu la 9) *

9. (a) Kwa nini huenda tukahitaji ujasiri ili kuhudhuria mikutano kwa ukawaida? (b) Mfano wetu unaweza kuwa na matokeo gani kwa ndugu zetu waliofungwa gerezani kwa sababu ya imani yao?

9 Ili tuhudhurie mikutano kwa ukawaida, huenda tukahitaji kuonyesha ujasiri tunapokabili hali ngumu. Baadhi ya ndugu na dada zetu huhudhuria mikutano licha ya kwamba wamelemewa na huzuni, wamevunjika moyo, au wana matatizo ya afya. Wengine huhudhuria mikutano kwa ujasiri licha ya kwamba wanapingwa vikali na watu wa familia au mamlaka za serikali. Fikiria kidogo jinsi mfano wetu unavyowagusa ndugu zetu waliofungwa gerezani kwa sababu ya imani yao. (Ebr. 13:3) Wanaposikia kwamba tunaendelea kumtumikia Yehova licha ya majaribu tunayopitia, wanatiwa nguvu kuendelea kudumisha imani, ujasiri, na utimilifu wao. Mtume Paulo alihisi vivyo hivyo. Alipokuwa gerezani huko Roma, alishangilia kila mara aliposikia kwamba ndugu zake walikuwa wakimtumikia Mungu kwa uaminifu. (Flp. 1:3-5, 12-14) Muda mfupi kabla au baada tu ya kuachiliwa huru, Paulo aliwaandikia barua Waebrania. Katika barua hiyo aliwahimiza Wakristo hao waaminifu waache ‘upendo wao wa kindugu uendelee’ na wasiache kamwe kukusanyika pamoja.—Ebr. 10:24, 25; 13:1.

10-11. (a) Tunapaswa kumwalika nani kwenye Ukumbusho? (b) Andiko la Waefeso 1:7 linatupatia sababu gani ya kufanya hivyo?

10 Tunaonyesha ujasiri tunapowaalika watu wetu wa ukoo, wafanyakazi wenzetu, na jirani zetu kwenye Ukumbusho. Kwa nini tunawaalika? Kwa sababu tunathamini sana mambo ambayo Yehova na Yesu wametufanyia hivi kwamba hatuwezi kujizuia kuwaalika wengine waje kwenye Ukumbusho. Tungependa wao pia wajifunze jinsi wanavyoweza kunufaika na ‘fadhili zisizostahiliwa’ za Yehova alizoonyesha kupitia fidia.—Soma Waefeso 1:7; Ufu. 22:17.

11 Tunapoonyesha ujasiri kwa kukusanyika pamoja, tunaonyesha pia sifa nyingine yenye kuvutia ambayo Mungu na Mwana wake wameonyesha kwa njia za pekee.

UPENDO HUTUCHOCHEA KUHUDHURIA

12. (a) Mikutano yetu hufanya upendo wetu kwa Yehova na Yesu uongezeke jinsi gani? (b) Andiko la 2 Wakorintho 5:14, 15, linatutia moyo tumwige Yesu kwa kufanya nini?

12 Kumpenda Yehova na Yesu hutuchochea kuhudhuria mikutano. Kisha mambo tunayojifunza mikutanoni hufanya upendo wetu kwa Yehova na Yesu, Mwana wake uongezeke. Kwenye mikutano, sisi hukumbushwa kwa ukawaida mambo ambayo wametufanyia. (Rom. 5:8) Ukumbusho hasa hutukumbusha jinsi upendo wao ulivyo mkubwa, hata kuwaelekea wale ambao hawatambui thamani ya fidia. Kwa shukrani nyingi, tunachochewa kujitahidi kumwiga Yesu katika maisha yetu ya kila siku. (Soma 2 Wakorintho 5:14, 15.) Zaidi ya hilo, mioyo yetu inatusukuma kumsifu Yehova kwa kuandaa fidia. Njia moja ya kumsifu ni kwa kutoa maelezo kutoka moyoni tunapokuwa mikutanoni.

13. Tunaweza kuonyeshaje kina cha upendo wetu kwa Yehova na Mwana wake? Eleza.

13 Tunaweza kuonyesha ni kwa kadiri gani tunampenda Yehova na Mwana wake kwa kuwa tayari kudhabihu lolote kwa ajili yao. Mara nyingi, ni lazima tujidhabihu kwa njia mbalimbali ili tuhudhurie mikutano. Makutaniko mengi hufanya mkutano jioni katikati ya juma baada ya saa za kazi wakati ambapo wengi wetu huwa tumechoka. Na mkutano mwingine hufanywa mwishoni mwa juma wakati ambapo watu wengi hupumzika. Je, Yehova anaona kwamba tunahudhuria mikutano yetu ingawa tumechoka? Bila shaka anaona! Kwa kweli, kadiri tunavyojitahidi kufanya kila tunaloweza ili kuhudhuria mikutano, ndivyo Yehova anavyothamini hata zaidi upendo tunaomwonyesha.​—Marko 12:41-44.

14. Yesu alituwekea kielelezo gani cha kuwapenda wengine bila ubinafsi?

14 Yesu alituwekea kielelezo cha kuwapenda wengine bila ubinafsi. Alikuwa tayari kufa kwa ajili ya wanafunzi wake, na kutanguliza mapendezi yao kila siku. Kwa mfano, alikutana pamoja na wafuasi wake hata alipokuwa amechoka au kulemewa na mkazo wa kihisia. (Luka 22:39-46) Na badala ya kukazia jinsi ambavyo angenufaika kutoka kwa wengine, Yesu alihangaikia jinsi ambavyo angeweza kuwanufaisha wengine. (Mt. 20:28) Tukimpenda Yehova na ndugu zetu kama Yesu, tutafanya yote tunayoweza kuhudhuria Mlo wa Jioni wa Bwana na pia mikutano mingine ya kutaniko.

15. Tungependa kuwasaidia nani hasa?

15 Sisi ni sehemu ya undugu pekee wa Wakristo wa kweli, na tunafurahia kutumia wakati wetu mwingi kadiri iwezekanavyo kuwakaribisha wapya wajiunge nasi. Hata hivyo, tungependa hasa kuwasaidia wale ambao ni “ndugu zetu katika imani” lakini kwa sasa wameacha kuhubiri au kuhudhuria mikutano. (Gal. 6:10) Tunaonyesha kwamba tunawapenda sana kwa kuwatia moyo wahudhurie mikutano, na hasa Ukumbusho. Kama Yehova na Yesu, sisi hufurahi sana wakati mtu aliyeacha kutenda anapomrudia Yehova, Baba yetu na Mchungaji wetu mwenye upendo.​—Mt. 18:14.

16. (a) Tunaweza kutiana moyo jinsi gani, na mikutano yetu itatusaidiaje? (b) Kwa nini hiki ndicho kipindi kizuri zaidi cha mwaka cha kukumbuka maneno ya Yesu yaliyo katika Yohana 3:16?

16 Katika majuma yajayo, wakaribishe watu wengi kadiri iwezekanavyo ili wahudhurie Ukumbusho Ijumaa jioni, Aprili 19, 2019. (Tazama sanduku “Je, Utawaalika?”) Acheni tutiane moyo kwa kuhudhuria kwa ukawaida mikutano yote ambayo Yehova ametuandalia. Kadiri mwisho wa mfumo huu wa mambo unavyokaribia, tunahitaji mikutano ili itusaidie kuendelea kuwa wanyenyekevu, jasiri, na wenye upendo. (1 The. 5:8-11) Acheni tuonyeshe kwa moyo wetu wote jinsi tunavyohisi kumhusu Yehova na Mwana wake kwa upendo mkubwa waliotuonyesha!​—Soma Yohana 3:16.

WIMBO 126 Uwe Macho, Simama Imara, Uwe na Nguvu

^ fu. 5 Ukumbusho wa kifo cha Kristo utakaofanywa Ijumaa jioni, Aprili 19, 2019, ndio utakaokuwa mkutano muhimu zaidi katika mwaka. Ni nini kinachotuchochea tuhudhurie mkutano huo? Bila shaka, tunataka kumfurahisha Yehova. Katika makala hii, tutachunguza jinsi uhudhuriaji wetu wa mikutano kila juma na pia Ukumbusho unavyofunua jinsi tulivyo.

^ fu. 50 Picha Kwenye Jalada

Mamilioni ya watu ulimwenguni pote wanakaribishwa kwenye Mlo wa Jioni wa Bwana

^ fu. 52 MAELEZO YA PICHA: Ndugu aliyefungwa gerezani kwa sababu ya imani yake anatiwa moyo na barua kutoka nyumbani. Anafurahi kujua kwamba watu wa familia yake hawajamsahau na ni waaminifu kwa Yehova licha ya misukosuko ya kisiasa katika eneo lao.