Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 3

Unaweza Kulindaje Moyo Wako?

Unaweza Kulindaje Moyo Wako?

“Ulinde moyo wako kuliko vitu vyote unavyolinda.”​—MET. 4:23.

WIMBO 36 Tuulinde Moyo Wetu

MUHTASARI *

1-3. (a) Kwa nini Yehova alimpenda Sulemani, na alimpatia baraka gani? (b) Tutajibu maswali gani katika makala hii?

SULEMANI, mfalme wa Israeli, alikuwa kijana tu alipoanza kutawala. Mwanzoni mwa utawala wake, Yehova alimtokea katika ndoto na kumwambia hivi: “Niombe unachotaka nikupe.” Sulemani alimwambia hivi: “Mimi ni kijana tu na sina uzoefu. . . . Basi nipe mimi mtumishi wako moyo mtiifu ili niwahukumu watu wako.” (1 Fal. 3:5-10) “Moyo mtiifu!” Hilo lilikuwa ombi lililoonyesha sifa ya kiasi kwelikweli! Haishangazi kwamba Yehova alimpenda Sulemani! (2 Sam. 12:24) Mungu wetu alifurahishwa sana na jibu la mfalme huyo kijana hivi kwamba akampa “moyo wenye hekima na uelewaji.”​—1 Fal. 3:12.

2 Sulemani alipata baraka nyingi alipoendelea kuwa mwaminifu. Alipata pendeleo la kujenga hekalu “kwa ajili ya jina la Yehova Mungu wa Israeli.” (1 Fal. 8:20) Akawa maarufu sana kwa sababu ya hekima aliyopewa na Mungu. Na mambo aliyosema alipoongozwa na roho ya Mungu yameandikwa katika vitabu vitatu vya Biblia. Mojawapo ya vitabu hivyo ni kitabu cha Methali.

3 Moyo unatajwa mara mia moja hivi katika kitabu cha Methali. Kwa mfano, tunasoma hivi katika andiko la Methali 4:23: “Ulinde moyo wako kuliko vitu vyote unavyolinda.” Katika mstari huo, neno “moyo” linamaanisha nini? Tutajibu swali hilo katika makala hii. Pia, tutapata majibu ya maswali haya mawili: Shetani hujaribu kudhuru au kupotosha moyo wetu jinsi gani? Na tunaweza kufanya nini ili kulinda moyo wetu? Ili tuendelee kuwa waaminifu kwa Mungu, tunahitaji kupata majibu ya maswali hayo muhimu.

“MOYO” NI NINI?

4-5. (a) Andiko la Zaburi 51:6, linatusaidiaje kuelewa maana ya neno “moyo”? (b) Mfano kuhusu afya yetu unaweza kutusaidiaje kuelewa umuhimu wa kuzingatia jinsi tulivyo kwa ndani?

4 Katika andiko la Methali 4:23, neno “moyo” linarejelea “utu wa ndani” au ‘utu wa sirini.’ (Soma Zaburi 51:6 na maelezo ya chini.) Kwa maneno mengine, neno “moyo” linarejelea mawazo ya ndani kabisa ya mtu, hisia zake, nia yake, na tamaa yake. Linarejelea jinsi tulivyo hasa kwa ndani, si tu jinsi tunavyoonekana kwa nje.

5 Fikiria jinsi mfano kuhusu afya yetu unavyoweza kutusaidia kuelewa umuhimu wa kuzingatia jinsi tulivyo kwa ndani. Kwanza, ili tuwe na afya nzuri ya kimwili, ni lazima tule chakula chenye lishe na kufanya mazoezi kwa ukawaida. Vivyo hivyo, ili tuwe na afya nzuri ya kiroho ni lazima tujilishe chakula cha kiroho chenye lishe, na kuonyesha kwa ukawaida kwamba tuna imani kwa Yehova. Tunaonyesha kwamba tuna imani kwa Yehova kwa kutumia maishani mambo tunayojifunza na kwa kuwaeleza wengine kuhusu imani yetu. (Rom. 10:8-10; Yak. 2:26) Pili, kwa msingi wa jinsi tunavyoonekana kwa nje, huenda tukafikiri kwamba tuna afya nzuri, ingawa bila kujua huenda tuna ugonjwa fulani. Katika maana hiyohiyo, kwa msingi wa ratiba yetu nzuri ya kiroho, huenda tukafikiri kwamba imani yetu ni yenye nguvu, lakini huenda tamaa zisizofaa zinasitawi ndani yetu. (1 Kor. 10:12; Yak. 1:14, 15) Ni lazima tukumbuke kwamba Shetani angependa kutudhuru kupitia njia yake ya kufikiri. Anaweza kutumia njia gani hususa kutudhuru? Na tunaweza kujilindaje?

JINSI SHETANI ANAVYOJARIBU KUDHURU MOYO WETU

6. Lengo la Shetani ni nini, naye hujaribu kulitimiza jinsi gani?

6 Shetani anataka tuwe kama yeye—mwasi anayepuuza viwango vya Yehova na anayechochewa na roho ya ubinafsi. Shetani hawezi kutulazimisha tufikiri na kutenda kama anavyotenda. Hivyo, yeye hujaribu kutimiza lengo lake kwa kutumia njia nyinginezo. Kwa mfano, ametuzingira na watu ambao tayari amewapotosha. (1 Yoh. 5:19) Anatarajia kwamba tutachagua kushirikiana nao, hata ingawa tunajua kwamba marafiki wabaya “huharibu” au “hupotosha” jinsi tunavyofikiri na kutenda. (1 Kor. 15:33; maelezo ya chini) Mbinu hiyo ilifanikiwa kumpotosha Mfalme Sulemani. Alioa wanawake wengi wa kipagani, na hatimaye “wakawa na uvutano mkubwa kwake” na “hatua kwa hatua wake zake wakaugeuza moyo wake” mbali na Yehova.​—1 Fal. 11:3; maelezo ya chini.

Unaweza kulinda moyo wako jinsi gani ili usiathiriwe na njia ya Shetani ya kufikiri? (Tazama fungu la 7) *

7. Shetani hutumia njia gani nyingine kueneza njia yake ya kufikiri, na kwa nini tunapaswa kujihadhari nayo?

7 Shetani hutumia sinema na vipindi vya televisheni kueneza njia yake ya kufikiri. Anaelewa kwamba mbali na kutuburudisha, masimulizi ya hadithi hutufundisha jinsi ya kufikiri, kuhisi, na kutenda. Yesu alitumia vizuri mbinu hiyo ya kufundisha. Kwa mfano alisimulia hadithi ya Msamaria mwema na ya mwana aliyeondoka nyumbani na kutumia vibaya urithi wake. (Mt. 13:34; Luka 10:29-37; 15:11-32) Hata hivyo, wale walioathiriwa na njia ya Shetani ya kufikiri wanaweza kutumia mbinu ya kusimulia hadithi ili kutupotosha. Tunahitaji kuwa na usawaziko. Sinema na vipindi vya televisheni vinaweza kutuburudisha na kutuelimisha bila kuathiri njia yetu ya kufikiri. Lakini ni lazima tujihadhari. Tunapochagua burudani, ni vema kujiuliza hivi, ‘Je, sinema hii au kipindi hiki cha televisheni kinanifundisha kwamba ni sawa kuruhusu niongozwe na tamaa zangu za mwili?’ (Gal. 5:19-21; Efe. 2:1-3) Unapaswa kufanya nini ukigundua kwamba kipindi fulani kinaendeleza njia ya Shetani ya kufikiri? Kiepuke kabisa kama unavyoepuka ugonjwa fulani hatari unaoambukiza!

8. Wazazi wanaweza kuwasaidiaje watoto wao kulinda moyo wao?

8 Wazazi, mna jukumu la pekee la kuwalinda watoto wenu dhidi ya jitihada za Shetani za kudhuru mioyo yao. Bila shaka mnafanya yote mwezayo ili kuwalinda watoto wenu wasipatwe na magonjwa halisi. Mnadumisha nyumba ikiwa safi, na kutupa kitu chochote kinachoweza kuwafanya ninyi au watoto wenu wawe wagonjwa. Kwa njia hiyohiyo mnahitaji kuwaepusha watoto wenu na sinema, vipindi vya televisheni, michezo ya kompyuta, na tovuti zinazoweza kufanya waathiriwe na njia ya Shetani ya kufikiri. Yehova amewapa jukumu la kutunza afya ya kiroho ya watoto wenu. (Met. 1:8; Efe. 6:1, 4) Hivyo, msiogope kuweka sheria zinazotegemea viwango vya Biblia. Wajulisheni watoto wenu mambo wanayoweza kutazama na mambo ambayo hawapaswi kutazama, na mwasaidie kuelewa sababu za uamuzi mliofikia. (Mt. 5:37) Watoto wenu wanapoendelea kukua, wazoezeni kutambua jinsi ya kutofautisha yaliyo sawa na yasiyo sawa kulingana na viwango vya Yehova. (Ebr. 5:14) Kumbukeni kwamba watoto wenu watajifunza mengi kwa kuwasikiliza lakini watajifunza mengi hata zaidi kupitia mambo mnayofanya.​—Kum. 6:6, 7; Rom. 2:21.

9. Shetani anaendeleza wazo gani, na kwa nini wazo hilo ni hatari?

9 Pia, Shetani hujaribu kudhuru moyo wetu kwa kutufanya tutegemee hekima ya wanadamu badala ya njia ya Yehova ya kufikiri. (Kol. 2:8) Fikiria wazo moja linaloendelezwa na Shetani kwamba lengo kuu maishani linapaswa kuwa kupata utajiri. Huenda watu wanaofikiri kwa njia hiyo wakapata utajiri au wakashindwa kuupata. Vyovyote vile, wako hatarini. Kwa nini? Kwa sababu huenda wakaelekeza fikira zao zote katika shughuli za kuchuma pesa hivi kwamba wako tayari kuhatarisha afya yao, uhusiano wa kifamilia, na hata urafiki wao pamoja na Mungu ili tu watimize lengo lao. (1 Tim. 6:10) Tunafurahi kwamba Baba yetu wa mbinguni mwenye hekima anatusaidia tuwe na maoni yenye usawaziko kuhusu pesa.​—Mhu. 7:12; Luka 12:15.

TUNAWEZA KULINDAJE MOYO WETU?

Kama walinzi na walinda malango wa kale, kaa macho na uchukue hatua ili mambo yenye kupotosha yasiingie moyoni mwako (Tazama fungu la 10 na 11) *

10-11. (a) Tunapaswa kufanya nini ili kujilinda? (b) Walinzi wa nyakati za kale walifanya kazi gani, na dhamiri yetu inaweza kutendaje kama mlinzi?

10 Ili tufanikiwe kulinda moyo wetu, ni lazima tutambue hatari na kuchukua hatua upesi ili kujilinda. Neno linalotafsiriwa ‘linda’ katika Methali 4:23 hutukumbusha kazi inayofanywa na mlinzi. Katika siku za Mfalme Sulemani, walinzi walisimama wakiwa macho juu ya kuta za jiji na kutoa onyo ikiwa wangeona hatari fulani. Kuwa na picha hiyo akilini hutusaidia kuelewa kile tunachopaswa kufanya ili tusimruhusu Shetani apotoshe njia yetu ya kufikiri.

11 Katika nyakati za kale walinzi walifanya kazi kwa ukaribu na walinda malango. (2 Sam. 18:24-26) Kwa kufanya kazi pamoja, walisaidiana kulinda jiji kwa kuhakikisha kwamba malango yamefungwa ikiwa adui angekaribia. (Neh. 7:1-3) Dhamiri * yetu iliyozoezwa na Biblia inaweza kutenda kama mlinzi na kutuonya Shetani anapojaribu kushambulia moyo wetu, au kwa maneno mengine anapojaribu kupotosha mawazo, hisia, nia, na tamaa zetu. Kila mara dhamiri yetu inapotuonya, tunapaswa kuisikiliza na kwa njia ya mfano kufunga malango ya moyo wetu.

12-13. Huenda tukashawishiwa kufanya nini, lakini tunapaswa kutendaje?

12 Fikiria mfano wa jinsi tunavyoweza kujilinda ili tusiathiriwe na njia ya Shetani ya kufikiri. Yehova ametufundisha kwamba “uasherati na kila namna ya ukosefu wa usafi [haupaswi kutajwa] kamwe miongoni [mwetu].” (Efe. 5:3) Lakini tutafanya nini ikiwa wafanyakazi au wanafunzi wenzetu wanaanza kuzungumzia mambo mapotovu kingono? Tunajua kwamba tunapaswa “kukataa matendo yasiyompendeza Mungu na tamaa za ulimwengu.” (Tito 2:12) Huenda mlinzi, yaani, dhamiri yetu ikatuonya. (Rom. 2:15) Lakini je, tutaisikiliza? Huenda tukashawishiwa kuwasikiliza wafanyakazi au wanafunzi wenzetu na kutazama picha wanazoonyeshana. Lakini huo ndio wakati wa kufunga malango ya jiji kwa kubadili mazungumzo au kuondoka.

13 Tunahitaji ujasiri ili tusishinikizwe na wengine kufikiri au kutenda mambo mabaya. Tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova anaona jitihada tunazofanya, naye atatupatia nguvu na hekima tunayohitaji ili kupinga mawazo ya Shetani. (2 Nya. 16:9; Isa. 40:29; Yak. 1:5) Hata hivyo, tunaweza kufanya nini kingine ili tuendelee kulinda moyo wetu?

KAA MACHO

14-15. (a) Tunapaswa kufungua moyo wetu ili kuruhusu nini, na tunaweza kufanya hivyo jinsi gani? (b) Andiko la Methali 4:20-22 linatusaidiaje kunufaika zaidi na usomaji wetu wa Biblia? (Tazama pia sanduku “Jinsi ya Kutafakari.”)

14 Ili kulinda moyo wetu, hatupaswi tu kukataa mambo yanayoweza kutupotosha, bali pia tunapaswa kukubali mambo yatakayotunufaisha. Fikiria tena kuhusu mfano wa jiji lililozingirwa na kuta. Mlinda malango alifunga malango ya jiji ili maadui wasilishambulie, lakini nyakati nyingine alifungua malango ili kuruhusu chakula na bidhaa nyingine ziingizwe jijini. Ikiwa malango ya jiji hayangefunguliwa, wakaaji wa jiji wangekosa chakula. Vivyo hivyo, tunahitaji kufungua moyo wetu kwa ukawaida ili kuruhusu njia ya Mungu ya kufikiri ituongoze.

15 Biblia ina mawazo ya Yehova, hivyo kila mara tunapoisoma, tunaruhusu mawazo yake yaongoze fikira, hisia, na matendo yetu. Tunaweza kufanya nini ili tunufaike zaidi na usomaji wetu wa Biblia? Sala ni muhimu. Dada mmoja Mkristo anasema hivi: “Kabla ya kusoma Biblia, mimi husali kwa Yehova na kumwomba anisaidie ‘nione wazi mambo yanayostaajabisha’ yanayopatikana katika Neno lake.” (Zab. 119:18) Pia, tunahitaji kutafakari kuhusu mambo tunayosoma. Tunaposali, kusoma, na kutafakari kuyahusu, Neno la Mungu hufika “ndani kabisa moyoni” mwetu, nasi huanza kupenda njia ya Yehova ya kufikiri.​—Soma Methali 4:20-22; Zab. 119:97.

16. Ndugu na dada wengi wamenufaikaje kwa kutazama JW Broadcasting?

16 Pia, tunaweza kuruhusu njia ya Mungu ya kufikiri ituongoze kwa kutazama video mbalimbali zinazopatikana kwenye JW Broadcasting®. Wenzi fulani wa ndoa walisema hivi: “Kwa kweli programu za kila mwezi ni jibu la sala zetu! Zimetuimarisha na kututia moyo tulipojihisi tukiwa wapweke au wenye huzuni. Na tunapenda sana kusikiliza nyimbo zinazotolewa kila mwezi kwenye JW Broadcasting. Sisi huzisikiliza tunapopika, tunapofanya usafi, au tukinywa chai.” Programu hizo hutusaidia kulinda moyo wetu. Pia, zinatufundisha kufikiri kama Yehova na kutusaidia tusishinikizwe kuiga njia ya Shetani ya kufikiri.

17-18. (a) Kama andiko la 1 Wafalme 8:61 linavyoonyesha, tunapata manufaa gani tunapotumia maishani mambo ambayo Yehova anatufundisha? (b) Mfano wa Mfalme Hezekia unatufundisha nini? (c) Kupatana na sala ya Daudi inayopatikana katika Zaburi 139:23, 24, tunaweza kumwomba Yehova atupatie nini?

17 Kila mara tunapojionea manufaa tunayopata kwa kufanya yaliyo sawa imani yetu huzidi kuwa na nguvu. (Yak. 1:2, 3) Tunajihisi vizuri kwa sababu tumemfanya Yehova ajionee fahari kutuita watoto wake, na hivyo tunatamani kumpendeza hata zaidi. (Met. 27:11) Kila tunapokabili jaribu fulani, tunapata fursa ya kuonyesha kwamba hatumtumikii Baba yetu mwenye upendo kwa moyo nusunusu. (Zab. 119:113) Badala yake, tunathibitisha kwamba tunampenda Yehova kwa moyo kamili, moyo ulioazimia kikamili kutii amri zake na kufanya mapenzi yake.​—Soma 1 Wafalme 8:61.

18 Je, tutakosea? Ndiyo; sisi si wakamilifu. Ukijikwaa, kumbuka mfano wa Mfalme Hezekia. Alikosea. Lakini alitubu na akaendelea kumtumikia Yehova “kwa moyo kamili.” (Isa. 38:3-6; 2 Nya. 29:1, 2; 32:25, 26) Hivyo basi, acheni tupinge jitihada za Shetani za kutuathiri kupitia njia yake ya kufikiri. Acheni tusali kwamba tusitawishe “moyo mtiifu.” (1 Fal. 3:9; soma Zaburi 139:23, 24.) Tutaendelea kuwa waaminifu kwa Yehova ikiwa tutalinda moyo wetu kuliko vitu vyote tunavyolinda.

WIMBO 54 “Hii Ndiyo Njia”

^ fu. 5 Je, tutaendelea kuwa waaminifu kwa Yehova, au tutamruhusu Shetani atushawishi tumwache Mungu wetu? Jibu la swali hilo halitegemei tunakabili majaribu makali kadiri gani, bali jinsi tunavyolinda moyo wetu. Neno “moyo” linamaanisha nini? Shetani hujaribu kupotosha moyo wetu jinsi gani? Na tunaweza kuulindaje? Makala hii itajibu maswali hayo muhimu.

^ fu. 11 UFAFANUZI WA MANENO: Yehova alitupatia uwezo wa kuchunguza mawazo, hisia, na matendo yetu na uwezo huo hutusaidia kujihukumu ikiwa tumefanya lililo sahihi au lisilo sahihi. Biblia inauita uwezo huo dhamiri. (Rom. 2:15; 9:1) Dhamiri iliyozoezwa na Biblia ni ile inayoongozwa na viwango vya Yehova vinavyopatikana katika Biblia ili kuamua ikiwa mawazo, matendo, au maneno yetu ni mazuri au mabaya.

^ fu. 56 MAELEZO YA PICHA: Ndugu anatazama televisheni kisha picha chafu inatokea. Ni lazima aamue hatua atakayochukua.

^ fu. 58 MAELEZO YA PICHA: Mlinzi katika nyakati za kale anaona hatari nje ya jiji. Anawatahadharisha walinda malango walio chini, nao wanachukua hatua haraka kwa kufunga malango na kuyatia makomeo kwa upande wa ndani.