Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 1

“Usihangaike, kwa Maana Mimi Ni Mungu Wako”

“Usihangaike, kwa Maana Mimi Ni Mungu Wako”

“Usiogope, kwa maana mimi niko pamoja nawe. Usihangaike, kwa maana mimi ni Mungu wako. Nitakutia nguvu, naam, nitakusaidia.”​—ISA. 41:10.

WIMBO 7 Yehova, Nguvu Yetu

MUHTASARI *

1-2. (a) Ujumbe unaopatikana katika andiko la Isaya 41:10 ulimwimarishaje dada Yoshiko? (b) Yehova alihakikisha ujumbe huo umehifadhiwa kwa faida ya nani?

DADA Mkristo mwaminifu anayeitwa Yoshiko alipokea habari mbaya. Daktari wake alimwambia kwamba alikuwa na miezi michache tu ya kuishi. Alitendaje? Yoshiko alikumbuka mstari fulani wa Biblia alioupenda sana, Isaya 41:10. (Soma.) Kisha kwa utulivu akamwambia daktari wake kwamba hakuwa na woga, kwa sababu Yehova alikuwa akiushika kwa nguvu mkono wake. * Ujumbe wenye kufariji ulio katika mstari huo ulimsaidia dada yetu mpendwa kumtumaini Yehova kikamili. Mstari huohuo unaweza kutusaidia kuendelea kuwa watulivu tunapokabili majaribu makali. Ili kuelewa jinsi unavyoweza kutusaidia, acheni kwanza tuchunguze kwa nini Mungu alimpa Isaya ujumbe huo.

2 Mwanzoni, Yehova alimwongoza Isaya aandike maneno hayo ili awafariji Wayahudi ambao baadaye wangepelekwa uhamishoni huko Babiloni. Hata hivyo, Yehova alihakikisha kwamba ujumbe huo umehifadhiwa, si tu kwa ajili ya faida ya Wayahudi ambao wangepelekwa uhamishoni, bali pia kwa faida ya watumishi wake wote tangu wakati huo na kuendelea. (Isa. 40:8; Rom. 15:4) Leo tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” na kuliko wakati mwingine wowote, tunahitaji maneno yenye kutia moyo yanayopatikana katika kitabu cha Isaya.—2 Tim. 3:1.

3. (a) Ni ahadi zipi zilizo katika andiko la Isaya 41:10, ambalo ndilo andiko la mwaka wa 2019? (b) Kwa nini tunahitaji uhakikisho tunaopata katika ahadi hizo?

3 Katika makala hii, tutakazia ahadi tatu za Yehova zinazoimarisha imani zilizo katika andiko la Isaya 41:10: (1) Yehova atakuwa pamoja nasi, (2) yeye ni Mungu wetu, na (3) atatusaidia. Tunahitaji uhakikisho * kama huo kwa sababu kama Yoshiko, tunakabili hali ngumu maishani. Wakati huohuo, tunalazimika kukabiliana na mikazo kwa sababu ya hali mbaya za ulimwengu. Baadhi yetu hata wanavumilia mateso kutoka kwa serikali zenye nguvu. Acheni sasa tuchunguze ahadi hizo tatu, moja baada ya nyingine.

“MIMI NIKO PAMOJA NAWE”

4. (a) Tutaanza kwa kuchunguza ahadi gani? (Tazama pia maelezo ya chini.) (b) Yehova anatumia maneno gani kuonyesha jinsi anavyohisi kutuelekea? (c) Maneno hayo ya Mungu yanakufanya uhisije?

4 Kwanza, Yehova anatufariji kwa maneno haya: “Usiogope, kwa maana mimi niko pamoja nawe.” * Yehova anaonyesha kwamba yuko pamoja nasi kwa kutuelekezea fikira zake zote na kutuonyesha upendo wake mwororo. Ona jinsi anavyotuonyesha hisia zake nyororo na za ndani sana. “Ulikuwa mwenye thamani machoni pangu,” asema Yehova. “Uliheshimiwa, nami nimekupenda.” (Isa. 43:4) Hakuna kitu chochote ulimwenguni kinachoweza kumfanya Yehova aache kuwapenda wale wanaomtumikia; ushikamanifu wake kwetu hauwezi kuyumbishwa. (Isa. 54:10) Upendo wake kwetu na urafiki wetu pamoja naye hutufanya tuwe na ujasiri mwingi. Atatulinda, kama alivyomlinda Abramu (Abrahamu) rafiki yake. Yehova alimwambia hivi: “Usiogope, Abramu. Mimi ni ngao yako.”—Mwa. 15:1.

Kwa msaada wa Yehova tunaweza kupita katikati ya majaribu yanayoonekana kama mafuriko au mwali wa moto (Tazama fungu la 5 na 6) *

5-6. (a) Tunajuaje kwamba Yehova anatamani kutusaidia tunapokabili hali ngumu maishani mwetu? (b) Mfano wa Yoshiko unatufundisha nini?

5 Tunajua kwamba Yehova anatamani kutusaidia tunapokabili majaribu kwa sababu anawaahidi hivi watu wake: “Unapopita katika maji, nitakuwa pamoja nawe, na unapopita katika mito, haitafurika na kukufunika. Unapotembea katika moto, hutateketea, wala mwali wa moto hautakuunguza.” (Isa. 43:2) Maneno hayo yanamaanisha nini?

6 Yehova hajatuahidi kwamba ataondoa changamoto zinazofanya maisha yawe magumu, lakini hataruhusu “mito” ya matatizo ituzamishe au “mwali wa moto” wa majaribu utuletee madhara yoyote ya kudumu. Anatuhakikishia kwamba atakuwa pamoja nasi, akitusaidia ‘kupita’ katikati ya changamoto hizo. Yehova atafanya nini? Atatusaidia kutuliza wasiwasi ili tuweze kudumisha utimilifu wetu kwake, hata tukikabili kifo. (Isa. 41:13) Dada Yoshiko, aliyetajwa mwanzoni, alijionea ukweli wa jambo hilo. Binti yake anasema hivi: “Tulishangazwa na utulivu ambao Mama alikuwa nao. Kwa kweli tuliona kwamba Yehova alikuwa amempa amani ya moyoni. Hadi siku aliyokufa, Mama alizungumza na wauguzi na wagonjwa wengine kumhusu Yehova na ahadi zake.” Tunajifunza nini kutokana na mfano wa Yoshiko? Tunapotumaini ahadi ya Mungu inayosema kwamba “nitakuwa pamoja nawe,” sisi pia tutakuwa jasiri na imara tunapoendelea kuvumilia majaribu.

“MIMI NI MUNGU WAKO”

7-8. (a) Ni uhakikisho upi wa pili tutakaozungumzia, nao unamaanisha nini? (b) Kwa nini Yehova aliwaambia Wayahudi waliokuwa uhamishoni: ‘Msihangaike’? (c) Ni maneno gani yanayopatikana katika Isaya 46:3, 4 ambayo kwa hakika yalituliza mioyo ya watu wa Mungu?

7 Sasa ona uhakikisho huu wa pili ulioandikwa na Isaya: “Usihangaike, kwa maana mimi ni Mungu wako.” Mstari huo unamaanisha nini? Katika lugha ya awali neno ‘kuhangaika’ katika mstari huo linatoa wazo la “mtu anayetazama nyuma mara kwa mara akihofia kwamba anaweza kupatwa na hatari fulani” au “mtu anayetazama huku na huku anapojikuta hatarini.”

8 Kwa nini Yehova aliwaambia Wayahudi ambao wangepelekwa uhamishoni Babiloni ‘wasihangaike’? Kwa sababu alijua kwamba wakaaji wa nchi hiyo wangeingiwa na woga. Ni nini ambacho kingesababisha woga huo? Mwishoni mwa kipindi cha miaka 70 tangu Wayahudi wapelekwe uhamishoni, jiji la Babiloni lingeshambuliwa na majeshi yenye nguvu ya Umedi na Uajemi. Yehova angetumia jeshi hilo kuwaweka huru watu wake kutoka utekwani Babiloni. (Isa. 41:2-4) Wababiloni na watu wa mataifa mengine walioishi nyakati hizo walipojua kwamba adui alikuwa akikaribia, walijaribu kujipa ujasiri kwa kuambiana: “Uwe imara.” Pia, walijitengenezea miungu mingi zaidi ya sanamu, wakitumaini kwamba ingewalinda. (Isa. 41:5-7) Kwa upande mwingine, Yehova alituliza mioyo ya Wayahudi waliokuwa uhamishoni kwa kusema hivi: “Wewe [tofauti na majirani wako] ni mtumishi wangu, Ee Israeli . . . Usihangaike, kwa maana mimi ni Mungu wako.” (Isa. 41:8-10) Ona kwamba Yehova alisema: “Mimi ni Mungu wako.” Kwa maneno hayo, Yehova aliwahakikishia waabudu wake washikamanifu kwamba hakuwa amewasahau—bado alikuwa Mungu wao, na bado walikuwa watu wake. Aliwaambia hivi: “Nitakubeba . . . na kukuokoa.” Hapana shaka kwamba maneno hayo yenye kufariji na yenye kutia moyo yaliwaimarisha Wayahudi waliokuwa uhamishoni.​—Soma Isaya 46:3, 4.

9-10. Kwa nini hatuna haja ya kuwa na wasiwasi? Toa mfano.

9 Leo, kuliko wakati mwingine wowote, watu wanaotuzunguka wamejawa na mahangaiko kwa sababu hali za ulimwengu zinazidi kuwa mbaya. Bila shaka, sisi pia tunaathiriwa na matatizo hayohayo. Lakini hakuna haja ya kuogopa. Yehova anatuambia, “Mimi ni Mungu wako.” Kwa nini maneno hayo yanatupatia sababu yenye nguvu ya kuendelea kuwa watulivu?

10 Fikiria mfano huu: Abiria wawili, Jim na Ben, wako ndani ya ndege inayokumbwa na msukosuko kwa sababu ya upepo mkali. Ndege inapoendelea kutikiswa huku na huku, sauti inasikika kwenye kikuza sauti ikisema: “Hakikisheni mmefunga mikanda. Tutakabili msukosuko kwa kipindi fulani.” Jim anashikwa na wasiwasi mwingi. Lakini rubani anaendelea kusema: “Msihangaike. Mimi ni rubani wenu, kila kitu kitakuwa sawa.” Sasa, Jim anatikisa kichwa na kusema, “Tuna uhakika gani na anachosema?” Hata hivyo, anatambua kwamba Ben hana wasiwasi hata kidogo. Jim anamuuliza, “Kwa nini huonekani ukiwa na wasiwasi?” Ben anatabasamu na kusema, “Kwa sababu ninamjua rubani huyu vizuri sana. Ni baba yangu!” Kisha Ben anamwambia hivi: “Acha nikueleze kuhusu baba yangu. Nina hakika kwamba ukimjua na ukijua ujuzi alio nao, wewe pia hutakuwa na wasiwasi.”

11. Mfano wa abiria wawili unatufundisha mambo gani?

11 Tunajifunza mambo gani kutokana na mfano huo? Kama Ben, sisi pia hatuna wasiwasi kwa sababu tunamjua vizuri sana Yehova, Baba yetu wa mbinguni. Tunajua kwamba atatuongoza salama salimini ili tufanikiwe kupita katikati ya matatizo yaliyo kama dhoruba tunayokabili katika siku hizi za mwisho za mfumo huu. (Isa. 35:4) Tunamtumaini Yehova, hivyo tunaendelea kuwa watulivu huku ulimwengu ukiwa umelemewa na woga. (Isa. 30:15) Pia, tunatenda kama Ben tunapowaambia majirani wetu sababu za kumtumaini Mungu. Hivyo, wao pia wanaweza kuwa na uhakika kwamba hata iwe wanakabili changamoto gani, Yehova atawategemeza.

“NITAKUTIA NGUVU [NA] NITAKUSAIDIA”

12. (a) Ni uhakikisho upi wa tatu tutakaozungumzia? (b) Maneno “mkono” wa Yehova yanatukumbusha ukweli gani?

12 Fikiria uhakikisho huu wa tatu ulioandikwa na Isaya: “Nitakutia nguvu, naam, nitakusaidia.” Tayari Isaya alikuwa ameeleza jinsi ambavyo Yehova angewatia nguvu, au kuwaimarisha watu wake, aliposema: “Yehova atakuja kwa nguvu, na mkono wake utatawala kwa ajili yake.” (Isa. 40:10) Kwa kawaida, Biblia hutumia neno “mkono” kwa njia ya mfano kumaanisha nguvu. Hivyo, maneno ‘mkono wa Yehova utatawala’ yanatukumbusha kwamba Yehova ni Mfalme mwenye nguvu. Alitumia nguvu zake zisizoweza kushindwa kuwategemeza na kuwalinda watumishi wake wakati uliopita, na anaendelea kuwaimarisha na kuwalinda wale wanaoendelea kumtumaini leo.—Kum. 1:30, 31; Isa. 43:10, maelezo ya chini.

Hakuna silaha itakayofanikiwa dhidi ya mkono wa Yehova wenye nguvu unaoandaa ulinzi (Tazama fungu la 12 hadi 16) *

13. (a) Ni wakati gani hasa ambapo Yehova hutimiza ahadi yake kwamba atatutia nguvu? (b) Ni ahadi gani ambayo hututia nguvu na kutupatia uhakika mwingi?

13 Yehova anaahidi hivi: “Nitakutia nguvu,” naye hutimiza ahadi hiyo hasa maadui wanapotutesa. Leo, katika sehemu fulani za ulimwengu, maadui wetu wanajitahidi juu chini kusimamisha kazi yetu ya kuhubiri au hata kupiga marufuku tengenezo letu. Licha ya hayo, hatuhangaiki kupita kiasi kuhusu mashambulizi hayo. Yehova ametupatia uhakikisho unaotutia nguvu na kutupatia uhakika mwingi. Anatuahidi hivi: “Hakuna silaha yoyote itakayotokezwa dhidi yako itakayofanikiwa.” (Isa. 54:17) Maneno hayo yanatukumbusha kuhusu mambo matatu muhimu na ya hakika.

14. Kwa nini mashambulizi kutoka kwa maadui wa Mungu hayatushangazi?

14 Kwanza, tukiwa wafuasi wa Kristo, tunatarajia kwamba tutachukiwa. (Mt. 10:22) Yesu alitabiri kwamba wanafunzi wake wangeteswa sana katika siku za mwisho. (Mt. 24:9; Yoh. 15:20) Pili, unabii wa Isaya unatuonya kwamba maadui wetu hawatatuchukia tu, bali pia watatumia silaha mbalimbali dhidi yetu. Silaha hizo zinatia ndani uwongo wenye hila, uwongo wa waziwazi, na mateso ya kikatili. (Mt. 5:11) Yehova hatawazuia maadui wetu kutumia silaha hizo kutushambulia. (Efe. 6:12; Ufu. 12:17) Lakini hatuna sababu ya kuogopa. Kwa nini?

15-16. (a) Ni jambo gani la tatu tunalohitaji kukumbuka, na andiko la Isaya 25:4, 5 linaungaje mkono jambo hilo? (b) Andiko la Isaya 41:11, 12 linafafanuaje hali itakayowapata wale wanaopigana vita dhidi yetu?

15 Fikiria jambo la tatu tunalohitaji kukumbuka. Yehova alisema kwamba “hakuna silaha” itakayotumiwa dhidi yetu “itakayofanikiwa.” Kama tu ambavyo ukuta hutulinda kutokana na dhoruba ya mvua inayosababisha maangamizi, ndivyo Yehova anavyotulinda dhidi ya “mlipuko wa waonevu.” (Soma Isaya 25:4, 5.) Maadui wetu hawatafanikiwa kamwe kutusababishia madhara yoyote ya kudumu.—Isa. 65:17.

16 Pia, Yehova hutusaidia kuimarisha zaidi tumaini letu kwake kwa kufafanua waziwazi mambo yatakayowapata wale “wanaowaka hasira dhidi” yetu. (Soma Isaya 41:11, 12.) Hata maadui wetu watushambulie vikali jinsi gani au mapambano dhidi yetu yaongezeke kadiri gani, mwisho wa mambo hayo yote ni mmoja: Maadui wote wa watu wa Mungu “watafanywa kuwa si kitu na wataangamia.”

JINSI TUNAVYOWEZA KUMTUMAINI YEHOVA ZAIDI

Tunaweza kumtumaini Yehova zaidi kwa kusoma kwa ukawaida kumhusu katika Biblia (Tazama fungu la 17 na 18) *

17-18. (a) Kusoma Biblia kunaweza kutusaidiaje kumtumaini Mungu zaidi? Toa mfano. (b) Kutafakari kuhusu andiko la mwaka wa 2019 kutatusaidiaje?

17 Tutamtumaini Yehova zaidi tunapomjua vizuri zaidi. Na njia pekee ya kumjua Mungu vizuri zaidi ni kwa kusoma Biblia kwa makini na kisha kutafakari kuhusu mambo tunayosoma. Biblia ina habari zenye kutegemeka za jinsi ambavyo Yehova aliwalinda watu wake wakati uliopita. Habari hizo hutusaidia kuwa na uhakika kwamba Yehova atatutunza hata sasa.

18 Fikiria ulinganisho wenye kuvutia sana ambao Isaya anatumia kuonyesha jinsi Yehova anavyotulinda. Anamfananisha Yehova na mchungaji na watumishi wa Mungu na wanakondoo. Isaya anasema hivi kumhusu Yehova: “Atawakusanya pamoja wanakondoo kwa mkono wake, naye atawabeba kwenye kifua chake.” (Isa. 40:11) Tunapohisi Yehova ametukumbatia kwa mikono yake yenye nguvu, tunajihisi tukiwa salama na watulivu. Ili kutusaidia tuendelee kuwa watulivu licha ya matatizo tunayokabili, mtumwa mwaminifu na mwenye busara amechagua Isaya 41:10 kuwa andiko la mwaka wa 2019, “Usihangaike, kwa maana mimi ni Mungu wako.” Tafakari kuhusu maneno hayo yenye kufariji. Yatakuimarisha unapokabili hali ngumu zitakazokupata wakati ujao.

WIMBO 38 Atakupa Nguvu

^ fu. 5 Andiko lililochaguliwa la mwaka wa 2019 linatupatia sababu tatu za kuendelea kuwa watulivu hata mambo mabaya yanapotokea ulimwenguni au katika maisha yetu. Makala hii itazungumzia sababu hizo na itatusaidia tupunguze wasiwasi wetu na tumtumaini Yehova zaidi. Tafakari andiko la mwaka huu. Likariri ikiwezekana. Litakuimarisha ili ufaulu kukabiliana na hali ngumu zitakazokupata wakati ujao.

^ fu. 3 UFAFANUZI WA MANENO: Uhakikisho ni taarifa ya kweli au ahadi ya kwamba kwa hakika jambo fulani litatendeka. Uhakikisho mbalimbali ambao Yehova hutupatia hutusaidia kupunguza wasiwasi unaoletwa na matatizo ambayo huenda yakatokea maishani mwetu.

^ fu. 4 MAELEZO YA CHINI: Neno “Usiogope” linatajwa mara tatu kwenye Isaya 41:10, 13, na 14.. Mistari hiyo inarudia kutaja neno “Mimi” (likimrejelea Yehova). Kwa nini Yehova alimwongoza Isaya aandike neno “Mimi” mara nyingi hivyo? Ili kukazia ukweli fulani muhimu kwamba tunaweza kuondoa woga wetu ikiwa tu tutamtumaini Yehova.

^ fu. 52 MAELEZO YA PICHA: Washiriki wa familia wanakabili hali ngumu kazini, matatizo ya kiafya, upinzani katika huduma, na shuleni.

^ fu. 54 MAELEZO YA PICHA: Mashahidi wanavamiwa na polisi wakifanya mkutano kwenye nyumba ya mtu binafsi, lakini ndugu na dada ni watulivu.

^ fu. 56 MAELEZO YA PICHA: Kufanya Ibada ya Familia kwa ukawaida hutuimarisha tuendelee kuvumilia.