Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 1

“Basi, Nendeni Mkafanye Wanafunzi”

“Basi, Nendeni Mkafanye Wanafunzi”

ANDIKO LA MWAKA WA 2020: “Basi, nendeni mkafanye wanafunzi . . . , mkiwabatiza.”​—MT. 28:19.

WIMBO 79 Wafundishe Kusimama Imara

MUHTASARI *

1-2. Malaika anawaambia nini wanawake waliofika kwenye kaburi la Yesu, naye Yesu anawapatia maagizo gani?

NI ASUBUHI na mapema, Nisani 16, 33 W.K. Kikundi chenye huzuni cha wanawake wanaomwogopa Mungu kinaelekea kwenye kaburi ambalo mwili wa Bwana Yesu Kristo ulizikwa zaidi ya saa 36 zilizopita. Wanapofika kaburini wakiwa na kusudi la kuupaka mwili wa Yesu manukato na mafuta yenye marashi, wanashangaa kukuta kaburi likiwa tupu! Malaika anawaambia wanafunzi hao kwamba Yesu amefufuliwa kutoka kwa wafu, na kuongezea hivi: “Anawatangulia kwenda Galilaya. Mtamwona huko.”—Mt. 28:1-7; Luka 23:56; 24:10.

2 Baada ya wanawake hao kuondoka kaburini, Yesu mwenyewe anawafikia na kuwapa maagizo yafuatayo: “Nendeni, mkawajulishe ndugu zangu ili waende Galilaya, na huko wataniona.” (Mt. 28:10) Hapana shaka kwamba Yesu alikuwa na maagizo fulani muhimu sana ambayo alitaka kuwapa wanafunzi wake, kwa sababu jambo la kwanza alilofanya baada ya kufufuliwa lilikuwa kupanga mkutano huo!

NI NANI WANAOPEWA AMRI?

Baada ya kufufuliwa, Yesu anakutana na mitume wake na wengine huko Galilaya na kuwaagiza ‘waende wakafanye wanafunzi’ (Tazama fungu la 3 na 4)

3-4. Kwa nini tunaweza kusema kwamba amri iliyo kwenye Mathayo 28:19, 20 haikutolewa tu kwa mitume? (Tazama picha kwenye jalada.)

3 Soma Mathayo 28:16-20. Katika mkutano huo ambao Yesu alipanga, alieleza kuhusu kazi muhimu sana ambayo wanafunzi wake wangetimiza katika karne ya kwanza—kazi ambayo sisi pia tunatimiza leo. Yesu alisema hivi: “Basi, nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . na kuwafundisha kushika mambo yote niliyowaamuru.”

4 Yesu anataka wafuasi wake wote wahubiri. Hakuwapa amri hiyo wale mitume wake 11 waaminifu peke yao. Kwa nini tuna uhakika huo? Je, ni mitume peke yao waliokuwepo wakati amri ya kufanya wanafunzi ilipotolewa kwenye mlima huko Galilaya? Kumbuka kwamba malaika aliwaambia hivi wanawake hao: “Mtamwona huko [Galilaya].” Hivyo, hapana shaka kwamba wanawake hao waaminifu walikuwepo katika mkutano huo. Na si hivyo tu. Mtume Paulo anafunua kwamba Yesu “aliwatokea ndugu zaidi ya 500 kwa wakati mmoja.” (1 Kor. 15:6) Wapi?

5. Andiko la 1 Wakorintho 15:6 linatufundisha nini?

5 Tuna sababu nzuri za kufikia mkataa kwamba Paulo alikuwa akirejelea mkutano huo wa Galilaya unaotajwa kwenye Mathayo sura ya 28. Sababu zipi hizo? Kwanza, wanafunzi wengi wa Yesu walikuwa Wagalilaya. Hivyo, mahali palipofaa zaidi kwa ajili ya mkutano huo mkubwa wa watu palikuwa kwenye mlima huko Galilaya, badala ya Yerusalemu kwenye nyumba ya mtu binafsi. Pili, Yesu aliyekuwa amefufuliwa, tayari alikuwa amekutana na mitume wake 11 huko Yerusalemu kwenye nyumba ya mtu binafsi. Ikiwa Yesu alitaka kuwapa mitume wake pekee amri ya kuhubiri na kufanya wanafunzi, angefanya hivyo Yerusalemu badala ya kuwaagiza mitume hao pamoja na wanawake na watu wengine wakutane naye Galilaya.—Luka 24:33, 36.

6. Andiko la Mathayo 28:20 linaonyeshaje kwamba amri ya kufanya wanafunzi inatuhusu sisi leo, na watu wanaitii amri hiyo kwa kiwango gani?

6 Fikiria sababu ya tatu muhimu. Amri ya Yesu ya kufanya wanafunzi haikuwahusu tu Wakristo wa karne ya kwanza. Tunajuaje? Yesu alimalizia maagizo yake kwa wafuasi wake kwa kusema: “Mimi nipo pamoja nanyi sikuzote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 28:20) Kama Yesu alivyosema, leo kazi hiyo ya kufanya wanafunzi imepamba moto. Fikiria jambo hilo! Kila mwaka, watu wapatao 300,000 hubatizwa na kuwa Mashahidi wa Yehova na wanafunzi wa Yesu Kristo!

7. Tutazungumzia nini, na kwa nini?

7 Watu wengi wanaojifunza Biblia hufanya maendeleo na kubatizwa. Hata hivyo, baadhi ya watu tunaojifunza Biblia kwa ukawaida pamoja nao husita kuwa wanafunzi wa Kristo. Wanafurahia kujifunza, lakini hawafanyi maendeleo na kufikia hatua ya ubatizo. Ikiwa unamfundisha Biblia mtu fulani, tuna uhakika kwamba unatamani kumsaidia atumie mambo anayojifunza na awe mwanafunzi wa Kristo. Makala hii itazungumzia jinsi tunavyoweza kuufikia moyo wa mwanafunzi na jinsi ya kumsaidia kukua kiroho. Kwa nini tunahitaji kuzungumzia habari hii? Kwa sababu wakati utafika ambapo tutahitaji kuamua ikiwa tutaendelea kujifunza naye au la.

JITAHIDI KUFIKIA MOYO

8. Kwa nini inaweza kuwa changamoto kufikia moyo wa mwanafunzi?

8 Yehova anataka watu wamtumikie kwa sababu wanampenda. Hivyo, lengo letu ni kuwasaidia wanafunzi wetu waelewe kwamba Yehova anawajali sana kibinafsi na anawapenda sana. Tunataka kuwasaidia wamwone Yehova kama “baba wa mayatima na mlinzi wa wajane.” (Zab. 68:5) Kadiri wanafunzi wako wanavyotambua jinsi Mungu anavyowapenda sana, inaelekea ndivyo watakavyoguswa moyo, na upendo wao kwa Mungu utazidi kuongezeka. Ni jambo gumu kwa baadhi ya wanafunzi kumwona Yehova akiwa Baba yao anayewapenda kwa sababu baba yao mzazi hakuwaonyesha upendo na wororo. (2 Tim. 3:1, 3) Hivyo, unapomfundisha mwanafunzi Biblia, kazia sifa za Yehova zenye kuvutia. Wasaidie wanafunzi wako waelewe kwamba Mungu wetu anayetupenda anataka wapate uzima wa milele, na yuko tayari kuwasaidia ili wafikie lengo hilo. Ni nini kingine tunachoweza kufanya?

9-10. Tunapaswa kutumia vitabu gani tunapojifunza Biblia pamoja na wanafunzi wetu, na kwa nini tuvitumie vitabu hivyo?

9 Tumia kitabu “Biblia Inatufundisha Nini?” na “Jinsi ya Kudumu Katika Upendo wa Mungu.” Machapisho hayo yameandaliwa kihususa ili kutusaidia kufikia mioyo ya wanafunzi wetu. Kwa mfano, sura ya 1 ya kitabu Biblia Inatufundisha inajibu maswali kama vile: Je, Mungu anatujali?, Mungu anahisije watu wanapoteseka?, na Je, unaweza kuwa rafiki ya Yehova? Vipi kuhusu kitabu Dumu Katika Upendo wa Mungu? Kitabu hicho kitamsaidia mwanafunzi wako aelewe jinsi ambavyo kutumia kanuni za Biblia kunaweza kuboresha maisha yake na kumsaidia kumkaribia Yehova. Hata ikiwa tayari umejifunza vitabu hivyo pamoja na wengine, jitayarishe vizuri kwa ajili ya kila kipindi cha funzo, na uzingatie akilini mahitaji hususa ya mwanafunzi wako.

10 Hata hivyo, tuseme kwamba mwanafunzi anapendezwa na habari fulani iliyo kwenye chapisho ambalo halipatikani kwenye Sanduku Letu la Vifaa vya Kufundishia. Unaweza kumtia moyo ajisomee mwenyewe chapisho hilo ili mwendelee kujifunza Biblia kwa kutumia mojawapo ya vitabu tulivyozungumzia vya kujifunzia Biblia.

Anza kila kipindi cha funzo kwa sala (Tazama fungu la 11)

11. Tunapaswa kuanza lini kufungua na kufunga kila kipindi cha funzo kwa sala, na tunaweza kumsaidiaje mwanafunzi aelewe umuhimu wa kufanya hivyo?

11 Anza kila kipindi cha funzo kwa sala. Kwa ujumla, ni jambo linalofaa sana kuanza kutoa sala bila kukawia baada ya kuanzisha funzo. Na kwa kawaida unaweza kufanya hivyo katika majuma machache ya kwanza baada ya kuanza kujifunza rasmi pamoja na mwanafunzi wako. Tunapaswa kumsaidia mwanafunzi atambue kwamba anaweza tu kulielewa Neno la Mungu kwa msaada wa roho ya Mungu. Baadhi ya walimu wa Biblia hufafanua sababu inayotufanya tusali wakati wa funzo kwa kuzungumzia andiko la Yakobo 1:5, linalosema: “Ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima, na aendelee kumwomba Mungu.” Kisha wao humuuliza mwanafunzi, “Tunaweza kuombaje hekima kutoka kwa Mungu?” Ni wazi mwanafunzi atasema kwamba tunapaswa kusali kwa Mungu.

12. Unaweza kutumiaje andiko la Zaburi 139:2-4 kumsaidia mwanafunzi kuboresha sala zake?

12 Mfundishe mwanafunzi wako jinsi ya kusali. Mhakikishie kwamba Yehova anataka kusikia sala zake za kutoka moyoni. Mweleze kwamba anaposali kibinafsi kwa Yehova anaweza kumfunulia yaliyo moyoni na kumweleza hisia ambazo huenda angesita kumwambia mtu mwingine yeyote. Isitoshe, tayari Yehova anajua mawazo yetu ya ndani kabisa. (Soma Zaburi 139:2-4.) Pia, tunaweza kumtia moyo mwanafunzi amwombe Yehova amsaidie kubadili mawazo yasiyofaa na kushinda mazoea mabaya. Kwa mfano, mfikirie mtu ambaye amekuwa akijifunza Biblia kwa muda fulani lakini anapenda sikukuu ambayo chanzo chake ni cha kipagani. Anajua kwamba ni kosa kuisherehekea, lakini bado anafurahia mambo fulani yanayohusiana na sikukuu hiyo. Mtie moyo amweleze Yehova kihususa jinsi anavyohisi na amsihi amsaidie apende tu mambo ambayo Mungu anapenda.—Zab. 97:10.

Mwalike mwanafunzi wako wa Biblia ahudhurie mikutano (Tazama fungu la 13)

13. (a) Kwa nini tunapaswa kuwaalika wanafunzi wetu wahudhurie mikutano bila kukawia? (b) Tunaweza kufanya nini ili mwanafunzi ajihisi akiwa huru anapokuwa kwenye Jumba la Ufalme?

13 Mwalike mwanafunzi wako ahudhurie mikutano bila kukawia. Mambo ambayo mwanafunzi wako ataona na kusikia katika mikutano ya Kikristo yanaweza kugusa moyo wake na kumsaidia afanye maendeleo. Mwonyeshe video Ni Nini Hutendeka Katika Jumba la Ufalme? na umkaribishe kwa uchangamfu mwandamane pamoja naye kwenda mikutanoni. Ikiwezekana, jitolee kumsaidia gharama za usafiri. Inafaa kuandamana pamoja na wahubiri mbalimbali unapoenda kujifunza pamoja na mwanafunzi wako. Kwa njia hiyo, mwanafunzi atafahamiana na wengine kutanikoni, na atajihisi akiwa huru anapohudhuria mikutano yetu.

MSAIDIE MWANAFUNZI WAKO KUKUA KIROHO

14. Ni nini kinachoweza kumchochea mwanafunzi wa Biblia awasaidie wengine?

14 Lengo letu ni kuwasaidia wanafunzi wetu wa Biblia wakue kiroho. (Efe. 4:13) Mtu anapokubali kujifunza Biblia pamoja nasi, huenda jambo kuu linalomvutia ni jinsi ambavyo funzo hilo litamnufaisha yeye binafsi. Hata hivyo, kadiri upendo wake kwa Yehova unavyoongezeka, inaelekea ndivyo atakavyoanza kufikiria jinsi anavyoweza kuwasaidia wengine, kutia ndani wale ambao tayari ni sehemu ya kutaniko. (Mt. 22:37-39) Wakati unaofaa utakapofika, usisite kumweleza kuhusu pendeleo la kutegemeza kifedha kazi ya Ufalme.

Mfundishe mwanafunzi anachopaswa kufanya matatizo yanapotokea (Tazama fungu la 15)

15. Tunaweza kumsaidiaje mwanafunzi wa Biblia atende kwa njia inayofaa matatizo yanapotokea?

15 Mfundishe mwanafunzi wa Biblia jinsi ya kutenda matatizo yanapotokea. Kwa mfano, tuseme kwamba mwanafunzi wako ambaye ni mhubiri ambaye hajabatizwa anakwambia kwamba amekwazwa na ndugu au dada fulani kutanikoni. Badala ya kutetea upande wowote, kwa nini usimtajie kanuni za Kimaandiko anazoweza kutumia kushughulikia hali hiyo? Anaweza kuamua kumsamehe ndugu au dada huyo au, ikiwa anashindwa kufanya hivyo, aende kwa mtu aliyemkosea na azungumze naye kwa fadhili na upendo akiwa na lengo la ‘kumpata ndugu yake.’ (Linganisha Mathayo 18:15.) Msaidie mwanafunzi wako kutayarisha mambo atakayosema. Mwonyeshe jinsi ya kutumia JW Library®, Mwongozo wa Utafiti wa Mashahidi wa Yehova, na tovuti ya jw.org® ili ajifunze njia mbalimbali zitakazomsaidia kushughulikia hali hiyo. Kadiri anavyopata mazoezi ya kutosha kabla ya kubatizwa, ndivyo itakavyokuwa rahisi zaidi kwake kuwa na uhusiano mzuri pamoja na wengine kutanikoni baada ya kubatizwa.

16. Kwa nini inafaa kuwaalika wahubiri wengine unapojifunza na mwanafunzi wako wa Biblia?

16 Waalike wengine kutanikoni—kutia ndani mwangalizi wa mzunguko anayezuru—unapojifunza na mwanafunzi wako. Kwa nini? Mbali na sababu zilizotajwa awali, huenda wahubiri wengine wakamsaidia mwanafunzi wako kwa njia ambazo wewe huwezi. Kwa mfano, tuseme kwamba mwanafunzi wako amejitahidi mara kadhaa kuacha kuvuta sigara lakini ameshindwa. Mwalike kwenye funzo hilo Shahidi ambaye alifanikiwa kushinda zoea hilo huenda baada ya kujitahidi mara kadhaa. Shahidi huyo anaweza kutoa ushauri unaofaa ambao mwanafunzi wako anahitaji kupata. Ikiwa huhisi huru kuongoza funzo hilo unapokuwa na ndugu mwenye uzoefu, mwombe ndugu huyo aongoze funzo hilo siku hiyo. Sikuzote, usisite kutumia uzoefu wa wengine. Kumbuka kwamba lengo letu ni kumsaidia mwanafunzi akue kiroho.

JE, NISITISHE FUNZO?

17-18. Unapaswa kuzingatia mambo gani unapofikiria kusitisha funzo la Biblia?

17 Ikiwa mwanafunzi wako wa Biblia hafanyi maendeleo, wakati utafika ambapo utahitaji kujiuliza, ‘Je, nisitishe funzo?’ Unapochanganua hali ya mwanafunzi wako, unapaswa kufikiria uwezo wake. Wengine huchukua muda mrefu kufanya maendeleo ya kiroho. Jiulize: ‘Je, mwanafunzi wangu anafanya maendeleo kwa kiwango kinacholingana na hali yake?’ ‘Je, ameanza “kushika,” au kutumia mambo anayojifunza?’ (Mt. 28:20) Huenda ikachukua muda mrefu kwa mwanafunzi kufikia hatua ya ubatizo, lakini hatua kwa hatua anapaswa kuwa akifanya mabadiliko maishani mwake.

18 Hata hivyo, vipi ikiwa umejifunza Biblia kwa muda fulani na mtu ambaye haonyeshi kwamba anathamini funzo lake? Fikiria hali hii: Mwanafunzi wako amemaliza kujifunza kitabu Biblia Inatufundisha na labda hata ameanza kitabu Dumu Katika Upendo wa Mungu, lakini hajawahi kuhudhuria mkutano wowote wa kutaniko—hata Ukumbusho! Na mara kwa mara anaahirisha funzo kwa sababu zisizo na msingi. Katika hali kama hiyo, ingefaa uzungumze naye waziwazi. *

19. Unaweza kumwambia nini mtu ambaye haonyeshi kwamba anathamini funzo lake la Biblia, na maelezo yake yanaweza kukusaidiaje?

19 Unaweza kumuuliza hivi mwanafunzi wako wa Biblia, ‘Unafikiri ni kipingamizi gani kikubwa zaidi utakacholazimika kushinda ili uwe Shahidi wa Yehova?’ Huenda mwanafunzi akajibu, ‘Ninapenda kujifunza Biblia, lakini siwezi kamwe kuwa Shahidi wa Yehova!’ Ikiwa huo ndio mtazamo wake baada ya kujifunza kwa muda fulani, je, kweli kuna sababu yoyote ya kuendelea kujifunza naye? Kwa upande mwingine, huenda mwanafunzi wako kwa mara ya kwanza akakufunulia jambo linalomzuia kufanya maendeleo. Kwa mfano, huenda anahisi kwamba hawezi kamwe kuhubiri nyumba kwa nyumba. Hivyo, kwa kuwa sasa unajua jinsi anavyohisi, unaweza kumsaidia kwa njia nzuri.

Usipoteze muda kujifunza na mtu ambaye hafanyi maendeleo (Tazama fungu la 20)

20. Kuelewa andiko la Matendo 13:48 kunaweza kutusaidiaje kuamua ikiwa tunahitaji kusitisha funzo la Biblia au la?

20 Inasikitisha kwamba baadhi ya wanafunzi wa Biblia ni kama Waisraeli wa siku za Ezekieli. Yehova alimwambia hivi Ezekieli kuwahusu: “Tazama! Kwao, wewe ni kama wimbo wa mapenzi, unaoimbwa kwa sauti tamu na kuchezwa kwa ustadi kwa kinanda. Watasikia maneno yako, lakini hakuna yeyote atakayeyatenda.” (Eze. 33:32) Inaweza kuwa vigumu kwetu kumwambia mtu fulani kwamba tutaacha kujifunza naye. Hata hivyo, “wakati uliobaki umepungua.” (1 Kor. 7:29) Badala ya kutumia muda mwingi kujifunza na mtu ambaye hafanyi maendeleo, tunahitaji kutafuta mtu anayeonyesha wazi kwamba ana “mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele.”—Soma Matendo 13:48.

Huenda kuna watu wengine katika eneo lenu wanaosali ili wapate msaada (Tazama fungu la 20)

21. Andiko letu la mwaka wa 2020 ni gani, na kwa nini linafaa?

21 Andiko letu la mwaka wa 2020 litatusaidia tukazie uangalifu jinsi tunavyoweza kuboresha kazi yetu ya kufanya wanafunzi. Andiko hilo linataja baadhi ya maneno ambayo Yesu alisema wakati wa mkutano muhimu aliofanya kwenye mlima fulani huko Galilaya. Alisema hivi: “Basi, nendeni mkafanye wanafunzi . . , mkiwabatiza.”Mt. 28:19.

Acheni tuazimie kukazia uangalifu jinsi tunavyoweza kuboresha kazi yetu ya kufanya wanafunzi na kuwasaidia wanafunzi wetu wabatizwe (Tazama fungu la 21)

WIMBO 70 Tafuteni Wanaostahili

^ fu. 5 Andiko la mwaka wa 2020 linatutia moyo ‘tufanye wanafunzi.’ Amri hiyo inawahusu watumishi wote wa Yehova. Tunaweza kuchocheaje mioyo ya wanafunzi wetu wa Biblia ili wawe wanafunzi wa Kristo? Makala hii itaonyesha jinsi tunavyoweza kuwasaidia wanafunzi wetu wa Biblia kumkaribia Yehova. Pia, tutazungumzia jinsi ya kuamua ikiwa tutaendelea kujifunza naye au la.

^ fu. 18 Tazama video Kusitisha Mafunzo ya Biblia Yasiyo na Matokeo kwenye JW Broadcasting®.