Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 2

Unaweza Kuwa “Chanzo cha Faraja Nyingi”

Unaweza Kuwa “Chanzo cha Faraja Nyingi”

‘Hawa ni wafanyakazi wenzangu kwa ajili ya Ufalme wa Mungu, nao wamekuwa chanzo cha faraja nyingi kwangu.’—KOL. 4:11.

WIMBO 90 Tianeni Moyo

MUHTASARI *

1. Watumishi wengi waaminifu wa Yehova hukabili hali gani zenye mkazo?

ULIMWENGUNI pote, watumishi wengi wa Yehova wanakabili hali ngumu zenye mikazo na zinazosababisha maumivu mengi. Je, umejionea hilo katika kutaniko lenu? Baadhi ya Wakristo ni wagonjwa sana au wamefiwa na mpendwa wao. Wengine wanakabili huzuni kwa sababu mtu wa familia yao au rafiki wa karibu ameacha kweli. Na bado wengine wanateseka kwa sababu ya misiba ya asili. Ndugu na dada hao wote wanahitaji faraja. Tunaweza kuwasaidiaje?

2. Kwa nini nyakati nyingine mtume Paulo alihitaji faraja?

2 Mtume Paulo alikabili mambo mengi yaliyohatarisha maisha yake. (2 Kor. 11:23-28) Pia, alilazimika kuvumilia “mwiba katika mwili,” ambao huenda ulikuwa tatizo fulani la afya. (2 Kor. 12:7) Alilazimika pia kukabiliana na hali yenye kuvunja moyo wakati Dema, ambaye pindi fulani alikuwa mfanyakazi mwenzake, alimwacha “kwa sababu aliupenda mfumo wa mambo wa sasa.” (2 Tim. 4:10) Paulo alikuwa Mkristo jasiri aliyetiwa mafuta kwa roho ambaye aliwasaidia wengine bila ubinafsi, lakini nyakati nyingine hata yeye alivunjika moyo.—Rom. 9:1, 2.

3. Paulo alipata faraja na msaada kutoka wapi?

3 Paulo alipata faraja na msaada aliohitaji. Jinsi gani? Bila shaka, Yehova alitumia roho yake takatifu ili kumtia nguvu. (2 Kor. 4:7; Flp. 4:13) Pia, Yehova alimfariji kupitia Wakristo wenzake. Paulo aliwataja baadhi ya wafanyakazi wenzake kuwa “chanzo cha faraja nyingi.” (Kol. 4:11) Miongoni mwa wafanyakazi hao aliowataja kwa majina ni Aristarko, Tikiko, na Marko. Walimtia nguvu Paulo na kumsaidia aendelee kuvumilia. Ni sifa gani zilizowasaidia Wakristo hao watatu wawe wafariji wazuri hivyo? Tunaweza kuigaje mfano wao mzuri tunapojitahidi kuwafariji na kuwatia moyo wengine?

UWE MSHIKAMANIFU KAMA ARISTARKO

Kama Aristarko, tunaweza kuwa marafiki washikamanifu kwa kushikamana na ndugu na dada zetu katika nyakati nzuri na pia “nyakati za taabu” (Tazama fungu la 4 na 5) *

4. Aristarko alithibitikaje kuwa rafiki mshikamanifu wa Paulo?

4 Aristarko, Mkristo Mmakedonia kutoka Thesalonike, alithibitika kuwa rafiki mshikamanifu wa Paulo. Tunasoma kwa mara ya kwanza kuhusu Aristarko, Paulo alipotembelea Efeso wakati wa safari yake ya tatu ya umishonari. Akiwa pamoja na Paulo, Aristarko alikamatwa na kikundi cha wafanya ghasia. (Mdo. 19:29) Hatimaye alipoachiliwa, hakuhangaikia usalama wake, bali aliendelea kushikamana na Paulo. Miezi kadhaa baadaye huko Ugiriki, bado Aristarko alikuwa pamoja na Paulo hata ingawa wapinzani waliendelea kutishia maisha ya Paulo. (Mdo. 20:2-4) Karibu mwaka wa 58 W.K., Paulo alipopelekwa Roma akiwa mfungwa, Aristarko aliandamana pamoja naye katika safari hiyo ndefu na walivunjikiwa na meli wakiwa pamoja. (Mdo. 27:1, 2, 41) Inaonekana kwamba walipofika Roma, Aristarko alifungwa gerezani pamoja na Paulo kwa muda fulani. (Kol. 4:10) Haishangazi kwamba Paulo alitiwa moyo na kufarijiwa na rafiki huyo mshikamanifu!

5. Kulingana na Methali 17:17, tunawezaje kuwa marafiki washikamanifu?

5 Kama Aristarko, tunaweza kuwa marafiki washikamanifu kwa kushikamana na ndugu na dada zetu katika nyakati nzuri na pia “nyakati za taabu.” (Soma Methali 17:17.) Hata baada ya hali ngumu kupita, huenda bado ndugu au dada yetu akahitaji kuendelea kufarijiwa. Frances, * dada ambaye wazazi wake wote wawili walikufa kwa ugonjwa wa saratani ndani ya miezi mitatu, anasema hivi: “Ninahisi kwamba matatizo mazito hutuathiri kwa muda mrefu. Ninawathamini sana marafiki washikamanifu wanaokumbuka kwamba bado nina maumivu, ingawa muda fulani umepita tangu wazazi wangu walipokufa.”

6. Sifa ya ushikamanifu itatuchochea tufanye nini?

6 Marafiki washikamanifu hujidhabihu ili kuwasaidia ndugu na dada zao. Kwa mfano, ndugu anayeitwa Peter aliambiwa na daktari kwamba ana ugonjwa mbaya sana ambao ungemsababishia kifo. Kathryn, mke wake, anasema: “Wenzi fulani katika kutaniko letu waliandamana nasi kwenda kwa daktari ambako tulijulishwa kuhusu ugonjwa wa Peter. Papo hapo, waliamua kwamba hawangetuacha tupambane peke yetu na hali hiyo ngumu, na sikuzote wamekuwa karibu nasi kila tulipohitaji msaada wao.” Inafariji sana kuwa na marafiki wa kweli, wanaoweza kutusaidia kuvumilia matatizo yetu!

UWE MWENYE KUTEGEMEKA KAMA TIKIKO

Kama Tikiko, tunaweza kuwa marafiki wanaotegemeka wengine wanapokabili matatizo (Tazama fungu la 7 hadi 9) *

7-8. Kulingana na Wakolosai 4:7-9, Tikiko alithibitikaje kuwa mwenye kutegemeka?

7 Tikiko, Mkristo kutoka wilaya ya Asia ya Roma, alikuwa rafiki mwenye kutegemeka sana wa Paulo. (Mdo. 20:4) Karibu mwaka wa 55 W.K., Paulo alifanya mipango ya kukusanya michango ili kuwasaidia Wakristo huko Yudea, na huenda alimkabidhi Tikiko mgawo huo muhimu. (2 Kor. 8:18-20) Baadaye, Paulo alipofungwa gerezani kwa mara ya kwanza huko Roma, Tikiko alitumikia akiwa mjumbe wake binafsi. Aliwasilisha jumbe na barua zenye kutia moyo za Paulo kwa makutaniko huko Asia.​—Kol. 4:7-9.

8 Tikiko aliendelea kuwa rafiki mwenye kutegemeka wa Paulo. (Tito 3:12) Wakati huo, si Wakristo wote waliokuwa wenye kutegemeka kama Tikiko. Karibu mwaka wa 65 W.K., Paulo alipokuwa amefungwa kwa mara ya pili gerezani, aliandika kwamba Wakristo wengi katika mkoa wa Asia waliepuka kushirikiana naye, huenda kwa sababu waliwaogopa wapinzani. (2 Tim. 1:15) Tofauti nao, Tikiko alikuwa mwenye kutegemeka, hivi kwamba Paulo akampa mgawo mwingine. (2 Tim. 4:12) Kwa hakika, Paulo alithamini sana kuwa na Tikiko aliyekuwa rafiki mzuri.

9. Tunaweza kumwiga Tikiko jinsi gani?

9 Tunaweza kumwiga Tikiko kwa kuwa marafiki wanaotegemeka. Kwa mfano, hatutoi tu ahadi ya kuwasaidia ndugu na dada zetu wenye uhitaji, bali pia tunawatendea mambo hususa yatakayowasaidia. (Mt. 5:37; Luka 16:10) Ndugu zetu wenye uhitaji wanapojua kwamba wanaweza kututegemea, wanafarijika sana. Dada mmoja anaeleza sababu: “Unahisi ukiwa mtulivu kwa sababu unajua kwamba ndugu aliyeahidi kukusaidia atafika kwa wakati ili kutimiza ahadi yake.”

10. Kulingana na Methali 18:24, wale wanaokabili hali ngumu au waliovunjika moyo wanaweza kupata wapi faraja?

10 Mara nyingi wale wanaokabili hali ngumu au waliovunjika moyo, hufarijika wanapozungumza na rafiki mwenye kutegemeka. (Soma Methali 18:24.) Bijay, ndugu aliyevunjika moyo baada ya mwanaye kutengwa na ushirika, alisema hivi: “Nilitamani sana kumfunulia hisia zangu mtu mwenye kutegemeka.” Carlos, ambaye alipoteza pendeleo alilopenda sana kwa sababu ya kosa alilofanya, anasema hivi: “Nilihitaji ‘mahali salama’ ambapo ningeweza kueleza hisia zangu waziwazi bila kuhisi kwamba ninahukumiwa.” Carlos alitambua kwamba mahali hapo salama ni kwa wazee wa kutaniko, ambao walimsaidia kukabiliana na tatizo lake. Pia, alifarijika kujua kwamba wazee walikuwa wenye busara na hawangefunua mambo aliyosema.

11. Tunaweza kuwa rafiki anayetegemeka au kutumainika jinsi gani?

11 Ili tuwe marafiki wanaotegemeka au kutumainika tunahitaji kusitawisha sifa ya subira. Zhanna alipoachwa na mume wake, alipata faraja kwa kuwafunulia rafiki zake wa karibu hisia zake. Anasema hivi: “Walinisikiliza kwa subira ingawa huenda nilisema mambo yaleyale tena na tena.” Wewe pia unaweza kuwa rafiki mzuri kwa kuwa msikilizaji mzuri.

UWE TAYARI KUWATUMIKIA WENGINE KAMA MARKO

Matendo yenye fadhili ya Marko yalimsaidia Paulo aendelee kuvumilia, nasi tunaweza kuwasaidia ndugu zetu nyakati za taabu (Tazama fungu la 12 hadi 14) *

12. Marko alikuwa nani, na alionyeshaje roho ya kujitolea?

12 Marko alikuwa Mkristo Myahudi kutoka Yerusalemu. Barnaba, binamu yake, alikuwa mmishonari aliyejulikana sana. (Kol. 4:10) Inaonekana kwamba familia ya Marko ilikuwa na hali nzuri ya kiuchumi, lakini Marko hakutanguliza vitu vya kimwili maishani mwake. Katika maisha yake yote, Marko alikuwa na roho ya kujitolea. Alifurahia kuwatumikia wengine. Kwa mfano, katika pindi kadhaa Marko alitumikia pamoja na mtume Paulo na mtume Petro walipokuwa wakitimiza majukumu yao, na huenda alishughulikia mahitaji yao ya kimwili. (Mdo. 13:2-5; 1 Pet. 5:13) Paulo alimfafanua Marko kuwa ‘mfanyakazi mwenzake kwa ajili ya Ufalme wa Mungu’ na alikuwa ‘msaada wa kumtia nguvu.’—Kol. 4:10, 11, maelezo ya chini.

13. Andiko la 2 Timotheo 4:11 linaonyeshaje kwamba Paulo alithamini utumishi wa Marko?

13 Marko alikuwa kati ya marafiki wa karibu wa Paulo. Kwa mfano, Paulo alipokuwa gerezani kwa mara ya mwisho huko Roma, mwaka wa 65 W.K. hivi, aliandika barua yake ya pili kwa Timotheo. Katika barua hiyo, Paulo alimwambia Timotheo aende Roma pamoja na Marko. (2 Tim. 4:11) Bila shaka, Paulo alithamini jinsi Marko alivyotumikia kwa uaminifu wakati uliopita, hivi kwamba akaomba Marko awepo katika kipindi hicho muhimu. Marko alimsaidia Paulo kwa njia hususa, labda kwa kumletea chakula au vifaa vya kuandikia. Hapana shaka kwamba msaada na kitia-moyo ambacho Paulo alipata kilimsaidia avumilie siku za mwisho za maisha yake kabla ya kuuawa.

14-15. Andiko la Mathayo 7:12 linatufundisha nini kuhusu kuwasaidia wengine kwa njia hususa?

14 Soma Mathayo 7:12. Tunapokabili hali ngumu, sisi huwathamini sana ndugu wanaotusaidia kwa njia hususa! Ryan, ambaye baba yake alikufa ghafla katika aksidenti mbaya, anasema hivi: “Kuna mambo mengi ya kawaida ambayo unashindwa kutimiza unapokabili hali ngumu. Lakini msaada hususa, hata ikiwa unaonekana kuwa mdogo sana, unasaidia sana.”

15 Tukiwa makini na wenye utambuzi, inaelekea kwamba tutapata njia hususa za kuwasaidia wengine. Kwa mfano, dada mmoja aliamua kwamba atakuwa akijitolea kuwapeleka kwa daktari Peter na Kathryn, wenzi wa ndoa waliotajwa awali. Peter na Kathryn hawangeweza tena kuendesha gari, hivyo dada huyo alitayarisha ratiba ya wajitoleaji kutanikoni ili wawe wakiwasafirisha kwa zamu. Je, mpango huo uliwasaidia? Kathryn anasema, “Tulihisi kana kwamba tumetua mzigo mzito.” Sikuzote kumbuka kwamba matendo yako madogo-madogo ya fadhili yanaweza kuwafariji sana wengine.

16. Ni somo gani muhimu tunalojifunza kutoka kwa Marko kuhusu kuwafariji wengine?

16 Kwa hakika, Marko, mwanafunzi wa karne ya kwanza alikuwa Mkristo mwenye shughuli nyingi. Alikuwa na migawo mizito ya kitheokrasi, kutia ndani kuandika Injili inayoitwa kwa jina lake. Ingawa hivyo, Marko alitenga wakati wa kumfariji Paulo, na Paulo alijihisi huru kuomba msaada kutoka kwa Marko. Angela, dada ambaye mtu wa familia yake aliuawa kikatili, alithamini sana wengine walipojitolea kumfariji. Anasema hivi: “Marafiki walio tayari kukusaidia, ni wenye kufikika na hawasiti kukusaidia.” Tunaweza kujiuliza hivi: ‘Je, ninajulikana kuwa mtu aliye tayari kuwafariji waabudu wenzangu kwa njia hususa?’

AZIMIA KUWAFARIJI WENGINE

17. Kutafakari andiko la 2 Wakorintho 1:3, 4 kunaweza kutuchocheaje kuwafariji wengine?

17 Hatuhitaji kwenda mbali ili kutafuta ndugu na dada wanaohitaji faraja. Tunaweza hata kushiriki pamoja nao mambo yenye kutia moyo ambayo wengine walituambia walipotufariji. Nino, dada ambaye alimpoteza nyanya (bibi) yake katika kifo anasema hivi: “Yehova anaweza kututumia kuwafariji wengine ikiwa tutamruhusu.” (Soma 2 Wakorintho 1:3, 4.) Frances, dada aliyenukuliwa awali, anasema: “Maneno ya 2 Wakorintho 1:4 ni ya kweli kabisa. Tunaweza kuwafariji wengine kwa njia ileile tuliyofarijiwa.”

18. (a) Kwa nini baadhi ya watu huwa na wasiwasi inapohusu kuwafariji wengine? (b) Tunaweza kufanya nini ili tufanikiwe kuwafariji wengine? Toa mfano.

18 Tunahitaji kuchukua hatua ya kwanza kuwasaidia wengine hata ikiwa tuna wasiwasi. Kwa mfano, huenda tukawa na wasiwasi kwamba hatujui jambo la kusema au la kumtendea mtu anayekabili hali yenye mkazo. Paul, ambaye ni mzee wa kutaniko, anakumbuka jitihada ambazo baadhi ya ndugu walifanya baada ya baba yake kufa. Anasema hivi: “Nilitambua kwamba haikuwa rahisi kwao kuzungumza nami. Hawakujua waseme nini. Lakini bado nilithamini nia yao ya kunifariji na kunitegemeza.” Ndugu anayeitwa Tajon alisema hivi baada ya tetemeko kubwa la ardhi: “Kusema kweli sikumbuki kila ujumbe ambao watu walinitumia baada ya tetemeko hilo, lakini ninachokumbuka ni kwamba walionyesha kuwa wananijali sana kwa kunijulia hali.” Tunaweza kuwa wafariji wenye matokeo ikiwa tunawajali wengine.

19. Kwa nini umeazimia kuwa “chanzo cha faraja nyingi”?

19 Kadiri tunavyozidi kukaribia mwisho wa mfumo huu wa mambo, hali za ulimwengu zitazidi kuzorota na maisha yatazidi kuwa magumu. (2 Tim. 3:13) Tutaendelea kuhitaji faraja kwa sababu ya matatizo tunayojisababishia kwani tumerithi dhambi na sisi si wakamilifu. Jambo moja lililomsaidia mtume Paulo afanikiwe kuendelea kuwa mwaminifu hadi mwisho wa maisha yake ni faraja aliyopata kutoka kwa Wakristo wenzake. Acheni tuendelee kuwa washikamanifu kama Aristarko, wenye kutegemeka kama Tikiko, na walio tayari kuwatumikia wengine kama Marko. Tukifanya hivyo, tutawasaidia ndugu na dada zetu waendelee kuwa imara katika imani.—1 The. 3:2, 3.

^ fu. 5 Mtume Paulo alikabili matatizo mengi maishani mwake. Alipokuwa akikabili hali ngumu, baadhi ya wafanyakazi wenzake walimfariji sana. Tutazungumzia sifa tatu hususa ambazo ziliwasaidia wafanyakazi wenzake wawe wafariji wazuri. Pia, tutazungumzia jinsi tunavyoweza kuiga mfano wao mzuri na kutoa msaada unaohitajika.

^ fu. 5 Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

WIMBO 111 Sababu za Kuwa na Shangwe

^ fu. 56 MAELEZO YA PICHA: Aristarko na Paulo walivunjikiwa na meli wakiwa pamoja.

^ fu. 58 MAELEZO YA PICHA: Tikiko alikabidhiwa mgawo wa kuyapelekea makutaniko barua za Paulo.

^ fu. 60 MAELEZO YA PICHA: Marko alimpa Paulo msaada hususa.