Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 4

Endelea Kusitawisha Upendo Mwororo

Endelea Kusitawisha Upendo Mwororo

“Katika upendo wa kindugu iweni na upendo mwororo kwa mtu na mwenzake.”​—ROM. 12:10.

WIMBO 109 Pendaneni Sana Kutoka Moyoni

MUHTASARI *

1. Ni nini kinachoonyesha kwamba leo familia nyingi hazina upendo wa asili?

BIBLIA ilitabiri kwamba katika siku za mwisho, watu hawangekuwa na “upendo wa asili.” (2 Tim. 3:1, 3) Leo, tunajionea unabii huo ukitimizwa. Kwa mfano, katika mamilioni ya familia, wenzi wa ndoa wametalikiana na kubaki wakiwa wamekasirikiana, na watoto wakihisi hawapendwi. Hata familia zinazoishi kwenye nyumba moja huenda zisiwe na uhusiano wa karibu. Mshauri fulani wa familia anasema hivi: “Baba, mama, na watoto hawana mawasiliano mazuri na wanatumia muda mwingi kwenye kompyuta, tablet, simu za mkononi au michezo ya video. Ingawa watu hao wa familia wanaishi katika nyumba moja, hawajuani vizuri.”

2-3. (a) Kulingana na Waroma 12:10, tunapaswa kuwaonyesha nani upendo mwororo? (b) Tutachunguza nini katika makala hii?

2 Tusingependa kufinyangwa na ulimwengu huu usio na upendo. (Rom. 12:2) Badala yake, tunahitaji kusitawisha upendo mwororo, si kuelekea watu wetu wa familia tu, bali pia wale ambao ni ndugu zetu katika imani. (Soma Waroma 12:10.) Upendo mwororo ni nini? Ni maneno ambayo kihususa yanafafanua urafiki wa karibu ulio miongoni mwa watu wa familia. Tunapaswa kusitawisha aina hiyo ya upendo kuelekea familia yetu ya kiroho, yaani, ndugu na dada zetu Wakristo. Tunapowaonyesha wengine upendo mwororo, tunasaidia kudumisha umoja ambao ni sehemu muhimu ya ibada ya kweli.—Mika 2:12.

3 Ili kutusaidia kusitawisha na kuonyesha upendo mwororo, acheni tuone yale tunayoweza kujifunza kutokana na mifano ya Biblia.

YEHOVA “NI MWENYE UPENDO MWORORO SANA”

4. Andiko la Yakobo 5:11 linatueleza nini kuhusu kina cha upendo wa Yehova?

4 Biblia inafunua sifa maridadi za Yehova. Kwa mfano, inasema kwamba “Mungu ni upendo.” (1 Yoh. 4:8) Ufafanuzi huo pekee unatosha kutuvuta kwake. Lakini Biblia inasema pia kwamba Yehova “ni mwenye upendo mwororo sana.” (Soma Yakobo 5:11.) Hiyo ni njia nzuri sana ya kufafanua kina cha hisia ambazo Yehova anazo kutuelekea!

5. Yehova anaonyeshaje sifa ya rehema, nasi tunaweza kumwigaje?

5 Ona kwamba andiko la Yakobo 5:11 linahusianisha upendo mwororo wa Yehova na sifa nyingine inayotufanya tumkaribie, yaani, rehema yake. (Kut. 34:6) Njia moja ambayo Yehova anatuonyesha rehema ni kwa kutusamehe makosa tunayofanya. (Zab. 51:1) Katika Biblia, sifa ya rehema inahusisha mengi zaidi ya kusamehe. Rehema ni hisia yenye nguvu inayotoka ndani kabisa ya moyo wa mtu anapomwona mtu mwingine akitaabika, naye anachochewa kujitahidi kumsaidia mtu huyo. Yehova anaifafanua tamaa yake yenye kina ya kutusaidia kuwa ni yenye nguvu zaidi kuliko hisia ambazo mama anazo kwa mtoto wake. (Isa. 49:15) Tunapotaabika, rehema ya Yehova inamchochea atusaidie. (Zab. 37:39; 1 Kor. 10:13) Tunaweza kuwaonyesha rehema ndugu na dada zetu kwa kuwasamehe na kutoweka kinyongo wanapotukosea. (Efe. 4:32) Lakini njia nyingine muhimu tunayoweza kuonyesha rehema ni kwa kuwategemeza ndugu na dada zetu wanapopitia hali ngumu maishani. Upendo unapotuchochea kuwaonyesha rehema wengine, tutakuwa tukimwiga Yehova ambaye ni mfano bora zaidi wa kuonyesha upendo mwororo.—Efe. 5:1.

YONATHANI NA DAUDI—‘WALISHIKAMANA NA KUWA MARAFIKI WA KARIBU SANA’

6. Yonathani na Daudi walionyeshana upendo mwororo jinsi gani?

6 Biblia ina masimulizi ya watu wasio wakamilifu ambao walionyesha upendo mwororo. Fikiria mfano wa Yonathani na Daudi. Biblia inasema hivi: “Yonathani na Daudi wakashikamana na kuwa marafiki wa karibu sana, na Yonathani akaanza kumpenda kama alivyojipenda mwenyewe.” (1 Sam. 18:1) Daudi alikuwa ametiwa mafuta ili amrithi Mfalme Sauli. Baada ya hapo, Sauli alianza kumwonea wivu Daudi, na alijaribu kumuua. Lakini Yonathani, mwana wa Sauli, hakujiunga na baba yake alipokuwa akijaribu kumuua Daudi. Yonathani na Daudi waliweka ahadi kwamba wataendelea kuwa marafiki sikuzote na kutegemezana.—1 Sam. 20:42.

Tofauti ya umri haikuwazuia Yonathani na Daudi kuwa marafiki wa karibu (Tazama fungu la 6 hadi 9)

7. Ni sababu gani moja ambayo huenda ingewazuia Yonathani na Daudi kuwa marafiki?

7 Upendo mwororo uliokuwa kati ya Yonathani na Daudi ni wenye kustaajabisha hata zaidi tunapofikiria baadhi ya mambo ambayo yangeweza kuwazuia kuwa marafiki. Kwa mfano, Yonathani alimzidi umri Daudi kwa miaka 30 hivi. Yonathani angeweza kufikiri kwamba hawezi kuwa na urafiki wa karibu na mtu mwenye umri mdogo sana na asiye na uzoefu maishani. Hata hivyo, Yonathani hakumwona au kumtendea Daudi kama mtu aliye duni machoni pake.

8. Unafikiri ni kwa nini Yonathani alikuwa rafiki mzuri sana kwa Daudi?

8 Yonathani angeweza kumwonea wivu Daudi. Akiwa mwana wa Mfalme Sauli angeweza kusisitiza kwamba yeye ndiye aliyekuwa mrithi halali wa kiti cha ufalme. (1 Sam. 20:31) Lakini Yonathani alikuwa mnyenyekevu na mshikamanifu kwa Yehova. Hivyo, aliunga mkono kabisa uamuzi wa Yehova wa kumchagua Daudi kuwa mfalme ambaye angefuata. Pia, alikuwa mshikamanifu kwa Daudi, hata wakati ambapo kufanya hivyo kulimkasirisha sana Sauli.—1 Sam. 20:32-34.

9. Je, Yonathani alishindana na Daudi au kumwonea wivu? Eleza.

9 Yonathani alikuwa na upendo mwororo kumwelekea Daudi, hivyo hakushindana naye au kumwonea wivu. Yonathani alikuwa mpiga mishale mwenye ustadi na mpiganaji hodari mwenye ujasiri. Yeye pamoja na Sauli, baba yake, walijulikana kwa sifa ya kuwa “wepesi kuliko tai” na “wenye nguvu kuliko simba.” (2 Sam. 1:22, 23) Hivyo, Yonathani angeweza kujigamba kuhusu matendo yake ya uhodari. Hata hivyo, Yonathani hakushindana na Daudi au kumwekea kinyongo. Badala yake, Yonathani alimpenda Daudi kwa sababu ya ujasiri wake na jinsi alivyomtegemea Yehova. Isitoshe, ni baada ya Daudi kumuua Goliathi ndipo Yonathani alipoanza kumpenda Daudi kama anavyojipenda mwenyewe. Tunaweza kuwaonyeshaje ndugu na dada zetu upendo mwororo kama huo?

TUNAWEZA KUONYESHAJE UPENDO MWORORO LEO?

10. Maneno “pendaneni sana kutoka moyoni” yanamaanisha nini?

10 Biblia inatuambia hivi: “Pendaneni sana kutoka moyoni.” (1 Pet. 1:22) Yehova anatuwekea kielelezo bora. Upendo wake ni mwingi sana kutuelekea hivi kwamba ikiwa sisi ni washikamanifu kwake, hakuna chochote kinachoweza kuvunja kifungo hicho cha upendo. (Rom. 8:38, 39) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa kuwa “sana” linaleta wazo la kujinyoosha, au hata kujikakamua. Nyakati nyingine huenda tukahitaji “kujinyoosha” na “kujikakamua” ili tuweze kuwaonyesha upendo mwororo waamini wenzetu. Wengine wanapotukosea, tunahitaji kuendelea ‘kuvumiliana kwa upendo, tukijitahidi sana kudumisha roho ya umoja katika kifungo cha muungano cha amani.’ (Efe. 4:1-3) Tunapojitahidi kudumisha ‘kifungo hicho cha amani,’ hatutakazia mapungufu ya ndugu zetu. Tutajitahidi kadiri tuwezavyo kuwaona ndugu zetu kama Yehova anavyowaona.—1 Sam. 16:7; Zab. 130:3.

Euodia na Sintike walihimizwa wawe na akili moja—jambo ambalo sikuzote huenda isiwe rahisi kufanya tunapokuwa na waamini wenzetu (Tazama fungu la 11)

11. Kwa nini nyakati nyingine huenda ikawa vigumu kusitawisha upendo mwororo?

11 Si rahisi sikuzote kuwaonyesha upendo mwororo ndugu na dada zetu, hasa ikiwa tunajua udhaifu wao mbalimbali. Inaonekana kwamba baadhi ya Wakristo wa karne ya kwanza walikabili changamoto hiyo. Kwa mfano, inaelekea Euodia na Sintike hawakuwa na tatizo kufanya kazi “pamoja na [Paulo] kwa ajili ya habari njema.” Lakini kwa sababu fulani, haikuwa rahisi kwa wao wenyewe kuelewana. Hivyo, Paulo aliwahimiza “wawe na akili moja katika Bwana.”—Flp. 4:2, 3.

Wazee wa kutaniko wenye umri mkubwa na mdogo wanaweza kusitawisha urafiki wa karibu sana pamoja (Tazama fungu la 12)

12. Tunaweza kusitawishaje upendo mwororo kuwaelekea ndugu na dada zetu?

12 Tunaweza kusitawishaje upendo mwororo kuelekea ndugu na dada zetu leo? Tunapowajua vizuri zaidi waamini wenzetu, huenda ikawa rahisi zaidi kuwaelewa na kusitawisha upendo mwororo kuwaelekea. Umri na malezi yetu havipaswi kuwa kikwazo. Kumbuka kwamba Yonathani alimzidi umri Daudi kwa miaka 30 hivi; lakini alisitawisha urafiki wa karibu pamoja naye. Je, unaweza kuanzisha urafiki pamoja na ndugu au dada ambaye ana umri mkubwa au mdogo kuliko wewe? Kwa kufanya hivyo, utaonyesha kwamba ‘unaupenda ushirika mzima wa akina ndugu.’—1 Pet. 2:17.

Tazama fungu la 12 *

13. Kwa nini huenda tusiwe na uhusiano uleule wa karibu pamoja na kila mtu kutanikoni?

13 Je, kuwa na upendo mwororo kuwaelekea waamini wenzetu kunamaanisha kwamba tutakuwa na uhusiano uleule wa karibu pamoja na kila mtu kutanikoni? Hapana, kihalisi hilo halingewezekana. Ni jambo la kawaida kuwa na uhusiano wa karibu zaidi na baadhi ya watu kuliko wengine kwa sababu ya kuwa na mapendezi yanayofanana. Yesu aliwaita mitume wake wote “rafiki,” lakini alikuwa na upendo wa kipekee kumwelekea Yohana. (Yoh. 13:23; 15:15; 20:2) Hata hivyo, Yesu hakumwonyesha upendeleo Yohana. Kwa mfano, Yohana na Yakobo, ndugu yake, walipoomba wapewe nafasi za pekee katika Ufalme wa Mungu, Yesu aliwaambia hivi: “Kuketi upande wangu wa kuume au wa kushoto sina haki ya kutoa.” (Marko 10:35-40) Kama Yesu, hatupaswi kuwaonyesha upendeleo rafiki zetu wa karibu. (Yak. 2:3, 4) Kuonyesha upendeleo kunaweza kusababisha migawanyiko—jambo ambalo halina nafasi katika kutaniko la Kikristo.—Yuda 17-19.

14. Kulingana na Wafilipi 2:3, ni nini kitakachotusaidia kuepuka roho ya mashindano?

14 Tunapoonyeshana upendo mwororo, tunalilinda kutanikoni dhidi ya roho ya mashindano. Kumbuka kwamba Yonathani hakujaribu kushindana na Daudi, hakumwona Daudi kama mshindani na kupambana naye kwa ajili ya kiti cha ufalme. Sisi sote tunaweza kuiga mfano wa Yonathani. Usishindane na ndugu na dada zako au kuwaonea wivu kwa sababu ya uwezo wao mbalimbali, ‘bali kwa unyenyekevu wa akili waone wengine kuwa ni bora kuliko wewe.’ (Soma Wafilipi 2:3.) Kumbuka kwamba kila mmoja kutanikoni ana jambo fulani analoweza kuchangia. Tukiendelea kuwa wanyenyekevu, tutaona sifa nzuri za ndugu na dada zetu na kufaidika kutokana na mfano wao wa uaminifu.—1 Kor. 12:21-25.

15. Umejifunza nini kutokana na kisa cha Tanya na familia yake?

15 Tunapokabiliana na majaribu ambayo hatukutarajia, Yehova hutufariji kupitia upendo mwororo na msaada tunaopata kutoka kwa ndugu na dada zetu. Fikiria kilichotokea baada ya familia moja kuhudhuria programu ya Jumamosi kwenye mojawapo ya Makusanyiko ya Kimataifa ya 2019 ya “Upendo Haushindwi Kamwe!” nchini Marekani. Tanya, mama mwenye watoto watatu, anasimulia hivi: “Tulikuwa tukisafiri kutoka kusanyikoni kuelekea hotelini, gari moja lilipopoteza mwelekeo na kuhamia upande wetu na kutugonga. Hakuna aliyeumia, lakini tukiwa tumepigwa na butwaa, tulitoka ndani ya gari na kusimama barabarani. Kisha tukamwona mtu aliyesimama kando ya barabara akitupungia twende kwenye gari lake ili tuwe salama. Alikuwa mmoja wa ndugu zetu ambaye pia alikuwa ametoka kusanyikoni. Na si yeye tu aliyesimamisha gari. Wajumbe watano kutoka Sweden walisimama pia. Akina dada walinikumbatia mimi na binti yangu kwa upendo, jambo ambalo tulihitaji sana! Niliwahakikishia kwamba tungekuwa sawa, lakini hawakukubali kutuacha. Waliendelea kubaki pamoja nasi hata baada ya watoa huduma ya kwanza kufika, na walihakikisha kwamba tuna kila kitu tulichohitaji. Katika kipindi hicho chote kigumu, tulihisi upendo wa Yehova. Tukio hilo liliimarisha upendo wetu kwa ndugu na dada zetu, na kutusaidia tumpende na kumthamini Yehova hata zaidi.” Je, unaweza kukumbuka wakati ulipokuwa na uhitaji, na mwamini mwenzako akakuonyesha upendo mwororo?

16. Tuna sababu gani za kuonyeshana upendo mwororo?

16 Fikiria matokeo tunayopata tunapoonyeshana upendo mwororo. Tunawafariji ndugu na dada zetu wakati wanapokuwa na uhitaji. Tunaimarisha umoja miongoni mwa watu wa Mungu. Tunathibitisha kwamba sisi ni wanafunzi wa Yesu, na jambo hilo linawavutia watu wenye mioyo minyoofu wajiunge na ibada ya kweli. Zaidi ya yote, tunamtukuza Yehova, “Baba wa rehema nyororo na Mungu wa faraja yote.” (2 Kor. 1:3) Acheni sisi sote tuendelee kusitawisha na kuonyeshana upendo mwororo!

WIMBO 130 Uwe Mwenye Kusamehe

^ fu. 5 Yesu alisema kwamba wanafunzi wake wangetambuliwa kwa upendo ambao ungekuwa miongoni mwao. Sisi sote tunajitahidi kuishi kulingana na takwa hilo. Tunaweza kuimarisha upendo wetu kwa ndugu na dada zetu kwa kusitawisha upendo mwororo—aina ya upendo unaoonyeshwa kati ya watu wa karibu wa familia. Makala hii itatusaidia kusitawisha na kudumisha upendo mwororo kuwaelekea wale ambao ni ndugu zetu katika imani.

^ fu. 55 MAELEZO YA PICHA: Mzee kijana anayefaidika kutokana na uzoefu wa mzee mwenye umri mkubwa zaidi, anakaribishwa kwa uchangamfu nyumbani kwa mzee huyo mwenye umri mkubwa. Wao na wake zao wanaonyeshana upendo na ukarimu.