Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 3

Umati Mkubwa wa Kondoo Wengine Unamsifu Mungu na Kristo

Umati Mkubwa wa Kondoo Wengine Unamsifu Mungu na Kristo

“Wokovu unatoka kwa Mungu wetu, anayeketi kwenye kiti cha ufalme, na kwa Mwanakondoo.”​—UFU. 7:10.

WIMBO 14 Kumsifu Mfalme Mpya wa Dunia

MUHTASARI *

1. Hotuba iliyotolewa katika kusanyiko la mwaka wa 1935 ilikuwa na matokeo gani kwa kijana fulani?

KIJANA fulani alibatizwa mwaka wa 1926, alipokuwa na umri wa miaka 18. Wazazi wake walikuwa Wanafunzi wa Biblia kama Mashahidi wa Yehova walivyokuwa wakijulikana wakati huo. Walikuwa na wana watatu na mabinti wawili ambao waliwafundisha wamtumikie Yehova Mungu na kumwiga Yesu Kristo. Kama ilivyokuwa kawaida kwa Wanafunzi wote wa Biblia wakati huo, kijana huyo mnyoofu alishiriki mkate na divai kila mwaka kwenye Mlo wa Jioni wa Bwana. Hata hivyo, mtazamo wake kuhusu maisha ulibadilishwa kabisa na hotuba ya kihistoria iliyokuwa na kichwa: “Mkutano Mkubwa.” Hotuba hiyo ilitolewa mwaka wa 1935 na J. F. Rutherford katika kusanyiko huko Washington, D.C., Marekani. Ni jambo gani lililofunuliwa katika kusanyiko hilo?

2. Ni kweli gani yenye kusisimua iliyofunuliwa katika hotuba ya Ndugu Rutherford?

2 Katika hotuba yake, Ndugu Rutherford aliwatambulisha wale ambao wangefanyiza “mkutano mkubwa” (Union Version), au “umati mkubwa,” unaotajwa kwenye Ufunuo 7:9. Kabla ya wakati huo, umati huo ulionwa kuwa kundi la pili la watu wenye tumaini la kwenda mbinguni ambao uaminifu wao ulikuwa mdogo kuliko wa watiwa-mafuta. Ndugu Rutherford alitumia Maandiko kufafanua kwamba wale wanaofanyiza umati mkubwa hawakuchaguliwa ili wakaishi mbinguni, bali wao ni kondoo wengine * wa Kristo watakaookoka “dhiki kuu” na kuishi milele duniani. (Ufu. 7:14) Yesu aliahidi hivi: “Nami nina kondoo wengine, ambao si wa zizi hili; hao pia nitawaleta, nao wataisikiliza sauti yangu, nao watakuwa kundi moja, mchungaji mmoja.” (Yoh. 10:16) Kondoo hao wanarejelea Mashahidi wa Yehova washikamanifu walio na tumaini la kuishi milele katika dunia paradiso. (Mt. 25:31-33, 46) Acheni tuone jinsi uelewaji huo mpya wa kweli ya Biblia ulivyobadili maisha ya watu wengi wa Yehova, kutia ndani yule ndugu wa miaka 18.—Zab. 97:11; Met. 4:18.

UELEWAJI MPYA ULIOBADILI MAISHA YA MAELFU YA WATU

3-4. Kwenye kusanyiko la mwaka 1935, maelfu ya wahudhuriaji walitambua nini kuhusu tumaini lao, na kwa nini?

3 Pindi ya kusisimua ilifika kwenye kusanyiko msemaji alipowaambia hivi wahudhuriaji: “Tafadhali, nyote mlio na tumaini la kuishi milele duniani simameni.” Kulingana na shahidi aliyekuwepo siku hiyo, zaidi ya nusu ya wahudhuriaji 20,000 hivi walisimama. Kisha, Ndugu Rutherford akatangaza hivi: “Tazameni! Mkutano mkubwa!” Tangazo hilo lilifuatiwa na sauti za kushangilia. Wale waliosimama walitambua kwamba hawakuwa wamechaguliwa ili wakaishi mbinguni. Walijua kwamba hawakuwa wametiwa mafuta kwa roho ya Mungu. Siku iliyofuata ya kusanyiko, Mashahidi wapya 840 walibatizwa, wengi wao wakiwa kondoo wengine.

4 Baada ya hotuba, yule ndugu kijana aliyetajwa mwanzoni na maelfu wengine, waliacha kushiriki mkate na divai kwenye Mlo wa Jioni wa Bwana. Ndugu mmoja alieleza kwa unyenyekevu hisia ambazo wengi walikuwa nazo aliposema hivi: “Ukumbusho wa mwaka wa 1935 ndio uliokuwa wa mwisho kwangu kushiriki mifano. Nilitambua kwamba Yehova hakuwa ametumia roho yake takatifu kuweka ndani yangu tumaini la kwenda mbinguni; badala yake, nilikuwa na tumaini la kuishi duniani na kushiriki katika kazi la kuifanya iwe paradiso.” (Rom. 8:16, 17; 2 Kor. 1:21, 22) Tangu wakati huo, idadi ya umati mkubwa imekuwa ikiongezeka na wamekuwa wakifanya kazi bega kwa bega pamoja na mabaki * ya Wakristo watiwa-mafuta.

5. Yehova anawaonaje wale ambao wameacha kushiriki mifano ya Ukumbusho?

5 Yehova anawaonaje wale walioacha kushiriki mifano ya Ukumbusho baada ya mwaka wa 1935? Vipi ikiwa leo Shahidi aliyebatizwa, kwa unyoofu anashiriki mkate na divai kwenye Mlo wa Jioni wa Bwana, lakini baadaye anatambua kwamba kwa kweli yeye si mtiwa-mafuta? (1 Kor. 11:28) Baadhi ya watu wameshiriki mifano kwa sababu hawakuelewa tumaini lao. Lakini ikiwa kwa unyoofu watakubali kwamba walikosea, waache kushiriki mifano, na waendelee kumtumikia Yehova kwa uaminifu, bila shaka atawakubali kama sehemu ya kondoo wengine. Hata ingawa hawashiriki mkate na divai, bado wanahudhuria Ukumbusho kwa sababu wanathamini sana kile ambacho Yehova na Yesu wamefanya kwa ajili yao.

TUMAINI LA PEKEE

6. Yesu amewaagiza malaika wafanye nini?

6 Kwa kuwa dhiki kuu inakaribia sana, lingekuwa jambo linalofaa kwetu kuchunguza mambo mengine ambayo kitabu cha Ufunuo sura ya 7 kinasema kuhusu Wakristo watiwa-mafuta na umati mkubwa wa kondoo wengine. Yesu anawaagiza malaika waendelee kuzishika zile pepo nne za uharibifu. Hawapaswi kuziruhusu pepo hizo zivume juu ya dunia hadi Wakristo wote watiwa-mafuta watakapotiwa muhuri, yaani, watakapopata kibali cha mwisho cha Yehova. (Ufu. 7:1-4) Kwa sababu ya uaminifu wao, ndugu za Kristo waliotiwa mafuta wanapata thawabu ya kuwa wafalme na makuhani pamoja naye mbinguni. (Ufu. 20:6) Wale wote wanaofanyiza sehemu ya kimbingu ya familia ya Mungu wanatazamia kwa hamu kuwaona wale watiwa-mafuta 144,000 wakiwa wamepokea thawabu yao ya mbinguni.

Umati mkubwa wakiwa wamevaa kanzu nyeupe na kushika matawi ya mitende mikononi mwao, wamesimama mbele ya kiti cha ufalme chenye utukufu cha Mungu na mbele ya Mwanakondoo (Tazama fungu la 7)

7. Kama andiko la Ufunuo 7:9, 10 linavyoonyesha, Yohana aliwaona nani katika maono, nao walikuwa wakifanya nini? (Tazama picha kwenye jalada.)

7 Baada ya Yohana kuzungumza kuhusu wale wafalme na makuhani 144,000, anaona jambo fulani lenye kusisimua, “umati mkubwa” wa wale waliookoka Har–Magedoni. Tofauti na kikundi cha kwanza, kikundi cha pili ni kikubwa zaidi na hakina idadi kamili. (Soma Ufunuo 7:9, 10.) “Wamevaa kanzu nyeupe,” kuonyesha kwamba wamejitunza wenyewe “bila doa” kutokana na ulimwengu wa Shetani na wameendelea kuwa washikamanifu kwa Mungu na Kristo. (Yak. 1:27) Wanapaza sauti wakisema kwamba wameokolewa kwa sababu ya kile ambacho Yehova na Yesu, Mwanakondoo wa Mungu, wamefanya. Pia, wameshika matawi ya mitende, jambo linaloonyesha kwamba wanamkubali kwa shangwe Yesu akiwa Mfalme aliyewekwa rasmi na Yehova.—Linganisha Yohana 12:12, 13.

8. Andiko la Ufunuo 7:11, 12 linatuambia nini kuhusu familia ya kimbingu ya Yehova?

8 Soma Ufunuo 7:11, 12. Ni nini kilichotokea wakati wale walio mbinguni walipouona umati mkubwa? Yohana anaona familia yote ya kimbingu ya Yehova ikijawa na shangwe na kumsifu Mungu wanapouona umati mkubwa. Familia ya Yehova ya mbinguni itafurahi kuona utimizo wa maono hayo, wakati umati mkubwa utakapookoka dhiki kuu.

9. Kulingana na andiko la Ufunuo 7:13-15, wale wa umati mkubwa wanafanya nini sasa?

9 Soma Ufunuo 7:13-15. Yohana anaeleza kwamba umati mkubwa ‘umefua kanzu zao na kuzifanya nyeupe katika damu ya Mwanakondoo.’ Hilo linamaanisha kwamba wana dhamiri safi na wana msimamo wa uadilifu mbele za Yehova. (Isa. 1:18) Wao ni Wakristo waliojiweka wakfu na kubatizwa, ambao wana imani yenye nguvu katika dhabihu ya Yesu Kristo, na wana uhusiano wa kibinafsi pamoja na Yehova. (Yoh. 3:36; 1 Pet. 3:21) Hivyo, wanastahili kusimama mbele ya kiti cha ufalme cha Mungu na kumtolea “utumishi mtakatifu mchana na usiku” katika ua wa duniani wa hekalu lake la kiroho. Hata sasa, wanatimiza kwa bidii sehemu kubwa ya kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi, wakitanguliza masilahi ya Ufalme wa Mungu mbele ya masilahi yao ya kibinafsi.—Mt. 6:33; 24:14; 28:19, 20.

Washiriki wenye shangwe wa umati mkubwa wa kondoo wengine waliookoka dhiki kuu (Tazama fungu la 10)

10. Umati mkubwa umehakikishiwa nini, nao wataona ahadi gani ikitimizwa?

10 Umati mkubwa utakaookoka dhiki kuu una hakika kwamba Mungu ataendelea kuwatunza, kwa sababu “yule anayeketi kwenye kiti cha ufalme atatandaza hema lake juu yao.” Hatimaye, ahadi ambayo kondoo wengine wamesubiri kwa hamu kuona ikitimia, itatimizwa kikamili: “[Mungu] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena.”—Ufu. 21:3, 4.

11-12. (a) Kama andiko la Ufunuo 7:16, 17 linavyoonyesha, umati mkubwa utapata baraka gani wakati ujao? (b) Kondoo wengine wanaweza kufanya nini kwenye Ukumbusho, na kwa nini?

11 Soma Ufunuo 7:16, 17. Sasa, baadhi ya watu wa Yehova wanateseka kutokana na njaa kwa sababu hawana pesa za kutosha kununua chakula au kwa sababu ya machafuko na vita. Wengine wamefungwa kwa sababu ya imani yao. Hata hivyo, wale wa umati mkubwa wanashangilia kujua kwamba watakapookoka uharibifu wa mfumo huu mwovu wa mambo, sikuzote watakuwa na chakula kingi cha kimwili na cha kiroho. Mfumo mwovu wa Shetani utakapoharibiwa, umati mkubwa hautapatwa na ‘joto lenye kuunguza’ la hasira ya Yehova atakalomimina juu ya mataifa. Baada ya dhiki kuu kuisha, Yesu atawaongoza waokokaji wa dhiki kuu kwenye ‘maji ya uzima wa milele.’ Hebu wazia jinsi umati mkubwa ulivyo na tumaini la pekee. Kati ya mabilioni ya watu waliowahi kuishi, huenda wasife kamwe!—Yoh. 11:26.

12 Kondoo wengine wana tumaini zuri sana nao wanamshukuru Yehova na Yesu kwa tumaini hilo! Ingawa Yehova hajawachagua wakaishi mbinguni, haimaanishi kwamba thamani yao ni ndogo machoni pa Yehova. Washiriki wa vikundi vyote viwili wanaweza kumsifu Mungu na Kristo. Njia moja ambayo wanafanya hivyo ni kwa kuhudhuria Mlo wa Jioni wa Bwana.

MSIFU MUNGU NA KRISTO KWA MOYO WAKO WOTE KWENYE UKUMBUSHO

Mkate na divai inayopitishwa wakati wa Ukumbusho hutukumbusha kwamba Yesu alikufa badala yetu ili tupate uzima (Tazama fungu la 13 hadi 15)

13-14. Kwa nini kila mtu anapaswa kuhudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo?

13 Katika miaka ya hivi karibuni, kwa wastani mtu mmoja kati ya kila watu 1,000 wanaohudhuria Ukumbusho hushiriki mkate na divai. Makutaniko mengi hayana watu wanaoshiriki mifano miongoni mwa wahudhuriaji. Watu wengi wanaohudhuria Ukumbusho wana tumaini la kuishi duniani. Basi, kwa nini wanahudhuria Mlo wa Jioni wa Bwana? Sababu inayowafanya wahudhurie ni sawa na ile inayowafanya watu wahudhurie harusi ya rafiki yao. Wanahudhuria kwa sababu wanataka kuonyesha kwamba wanawapenda na kuwaunga mkono wale waliofunga ndoa. Hivyo, kondoo wengine wanahudhuria Ukumbusho kwa sababu wanataka kuonyesha kwamba wanampenda na kumuunga mkono Kristo na watiwa-mafuta. Pia, kondoo wengine wanahudhuria ili kuonyesha uthamini wao kwa dhabihu ya Yesu inayowawezesha kuishi milele duniani.

14 Sababu nyingine muhimu inayowafanya kondoo wengine wahudhurie Ukumbusho ni ili kutii amri ya Yesu. Yesu alipoanzisha mlo huo wa pekee pamoja na mitume wake waaminifu, aliwaambia hivi: “Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka.” (1 Kor. 11:23-26) Hivyo, wanaendelea kuhudhuria Mlo wa Jioni wa Bwana maadamu kuna watiwa-mafuta walio hai hapa duniani. Isitoshe, kondoo wengine wanamwalika kila mtu ahudhurie Ukumbusho pamoja nao.

15. Kila mmoja wetu anaweza kufanya nini ili kumsifu Mungu na Kristo kwenye Ukumbusho?

15 Kwenye Ukumbusho, tunapata fursa ya kumsifu Mungu na Kristo kwa nyimbo na sala. Hotuba itakayotolewa mwaka huu ina kichwa: “Onyesha Kwamba Unathamini Mambo Ambayo Mungu na Kristo Wamekufanyia!” Itaongeza uthamini wetu kwa Yehova na Kristo. Mifano itakapopitishwa, sote tutakaohudhuria tutakumbushwa kile kinachofananishwa na mifano hiyo, yaani, mwili na damu ya Yesu. Tutakumbuka kwamba Yehova aliruhusu Mwana wake afe badala yetu ili tuweze kupata uzima. (Mt. 20:28) Kila mtu anayempenda Baba yetu wa mbinguni na Mwana wake atataka kuhudhuria Ukumbusho.

MSHUKURU YEHOVA KWA TUMAINI ALILOKUPA

16. Watiwa-mafuta na kondoo wengine wanafanana kwa njia gani?

16 Tofauti kati ya Wakristo watiwa-mafuta na kondoo wengine haitegemei thamani yao machoni pa Mungu. Vikundi vyote viwili vina thamani ileile machoni pa Mungu. Isitoshe, alilipa gharama ileile, uhai wa Mwana wake mpendwa, kwa ajili ya vikundi vyote viwili, yaani, watiwa-mafuta na kondoo wengine. Tofauti iliyopo kati ya vikundi hivyo viwili ni kwamba washiriki wake wana matumaini tofauti. Ni lazima washiriki wa vikundi vyote viwili waendelee kubaki washikamanifu kwa Mungu na Kristo. (Zab. 31:23) Na kumbuka kwamba roho ya Mungu inaweza kutenda kwa nguvu ileile kwetu sote. Hilo linamaanisha kwamba Yehova humpa roho yake takatifu kila mtu kulingana na uhitaji wake.

17. Mabaki ya Wakristo watiwa-mafuta wanatazamia nini kwa hamu?

17 Wakristo watiwa-mafuta hawazaliwi wakiwa na tumaini la kimbingu. Tumaini hilo huwekwa mioyoni mwao na Mungu. Wanatafakari kuhusu tumaini lao, wanasali kulihusu, na wanatamani kupokea thawabu yao mbinguni. Hawawezi hata kuwazia jinsi mwili wao wa kiroho utakavyokuwa. (Flp. 3:20, 21; 1 Yoh. 3:2) Hata hivyo, wanatazamia kwa hamu kukutana na Yehova, Yesu, malaika, na watiwa-mafuta wengine. Na wanatamani sana kuwa pamoja nao katika Ufalme wa mbinguni.

18. Kondoo wengine wanatazamia nini kwa hamu?

18 Kondoo wengine wanathamini tumaini ambalo kiasili wanadamu wanalo, tumaini la kuishi milele duniani. (Mhu. 3:11) Wanatarajia kwa hamu wakati ambapo wataweza kusaidia kuigeuza dunia yote iwe paradiso. Wanatazamia kwa hamu siku watakayoweza kujenga nyumba zao, kupanda bustani zao, na kulea watoto wenye afya kamilifu. (Isa. 65:21-23) Wanatazamia kwa hamu kuchunguza mambo mbalimbali kuhusu dunia—milima yake, misitu, na bahari—na kujifunza kuhusu vitu vyote ambavyo Yehova ameumba. Zaidi ya hayo, watasisimka kujua kwamba uhusiano wao na Yehova utaendelea kuimarika na kuwa wa karibu hata zaidi.

19. Ukumbusho unampatia kila mmoja wetu fursa gani, na Ukumbusho utaadhimishwa lini mwaka huu?

19 Yehova amempatia kila mmoja wa watumishi wake waliojiweka wakfu tumaini zuri sana la wakati ujao. (Yer. 29:11) Ukumbusho wa kifo cha Kristo unampatia kila mmoja wetu fursa ya pekee ya kumsifu Mungu na Kristo kwa yale ambayo wamefanya kwa ajili yetu ili tuweze kufurahia uzima usio na mwisho. Bila shaka, Ukumbusho ni mkutano muhimu zaidi ambao hufanywa na Wakristo wa kweli kila mwaka. Mwaka huu, utafanywa siku ya Jumamosi, Machi 27, 2021, baada ya jua kushuka. Watu wengi wataweza kuhudhuria tukio hili kwa uhuru. Wengine watahudhuria licha ya upinzani. Baadhi ya watu watakabiliana na changamoto ya kuadhimisha tukio hili wakiwa gerezani. Huku Yehova, Yesu, na sehemu ya kimbingu ya familia ya Mungu wakitazama, acheni kila kutaniko, kikundi, na mtu mmoja-mmoja afurahie mwadhimisho wa Ukumbusho!

WIMBO 150 Mtafute Mungu Upate Ukombozi

^ fu. 5 Machi 27, 2021, ni siku ya pekee kwa Mashahidi wa Yehova. Jioni ya siku hiyo tutaadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Watu wengi watakaohudhuria watakuwa sehemu ya kikundi ambacho Yesu alikiita “kondoo wengine.” Ni kweli gani yenye kusisimua ambayo ilifunuliwa kuhusu kikundi hicho mwaka wa 1935? Kondoo wengine wana tarajio gani lenye kusisimua litakalotimia baada ya dhiki kuu? Na wakiwa watazamaji kwenye Ukumbusho, kondoo wengine wanaweza kumsifu Mungu na Kristo jinsi gani?

^ fu. 2 UFAFANUZI WA MANENO: Kondoo wengine wanatia ndani wale ambao wamekusanywa katika kipindi cha siku za mwisho. Wanamfuata Kristo na wana tumaini la kuishi milele duniani. Wale wanaofanyiza umati mkubwa ni kondoo wengine ambao watakuwa hai Kristo atakapowahukumu wanadamu wakati wa dhiki kuu, nao wataokoka dhiki kuu.

^ fu. 4 UFAFANUZI WA MANENO: Neno “mabaki” linarejelea Wakristo watiwa-mafuta ambao bado wako duniani na wanashiriki mkate na divai kwenye Mlo wa Jioni wa Bwana.