Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 1

Uwe na Uhakika Kwamba “Neno la Mungu Ni Kweli”

Uwe na Uhakika Kwamba “Neno la Mungu Ni Kweli”

ANDIKO LA MWAKA WA 2023: “Kiini hasa cha neno lako ni kweli.”​—ZAB. 119:160.

WIMBO 96 Kitabu cha Mungu Ni Hazina

MUHTASARI a

1. Kwa nini watu wengi leo wanaitilia shaka Biblia?

 LEO, watu wengi wana shaka. Hawajui wamtumaini nani. Hawana uhakika ikiwa wale wanaowaheshimu, yaani, wanasiasa, wanasayansi, na wafanyabiashara kwa kweli wanajali masilahi yao. Kwa kuongezea, hawawaheshimu viongozi wa kidini wanaodai kuwa Wakristo. Haishangazi kwamba wanatilia shaka Biblia, kitabu ambacho viongozi hao wa kidini wanadai kukifuata.

2. Kulingana na Zaburi 119:160, tunaweza kuwa na uhakika kuhusu jambo gani?

2 Tukiwa watumishi wa Yehova tuna uhakika kwamba yeye ni “Mungu wa ukweli” na anajali masilahi yetu. (Zab. 31:5; Isa. 48:17) Tunajua kwamba tunaweza kuamini mambo tunayosoma katika Biblia​—kwamba “kiini hasa cha neno [la Mungu] ni kweli.” b (Soma Zaburi 119:160.) Tunakubaliana na kile ambacho msomi fulani wa Biblia aliandika: “Hakuna uwongo wowote katika mambo ambayo Mungu amesema na maneno yake kamwe hayawezi kukosa kutimia. Watu wa Mungu wanaweza kuamini kile anachosema kwa sababu wanamwamini Mungu ambaye amesema maneno hayo.”

3. Tutachunguza nini katika makala hii?

3 Tunawezaje kuwasaidia wengine wawe na uhakika kama wetu kuhusu Neno la Mungu? Acheni tuchunguze sababu tatu zinazofanya tuiamini Biblia. Tutachunguza usahihi wa maandishi yake, utimizo wa unabii wa Biblia, na nguvu za Biblia za kubadili maisha.

UJUMBE WA BIBLIA UMEHIFADHIWA KWA USAHIHI

4. Kwa nini baadhi ya watu wanatilia shaka usahihi wa Biblia?

4 Yehova Mungu aliwatumia wanaume waaminifu 40 hivi kuandika vitabu vya Biblia. Hata hivyo, hakuna hati za awali ambazo zinapatikana leo. c Leo, tuna nakala zilizonakiliwa za hati hizo. Hilo linawafanya baadhi ya watu watilie shaka ikiwa yale tunayosoma katika Biblia leo yanapatana kwa usahihi na ujumbe ulioandikwa mwanzoni. Je, uliwahi kujiuliza ni kwa nini tuna uhakika kwamba Biblia ni sahihi?

Wanakili wenye ustadi wa Maandiko ya Kiebrania walifanya jitihada za pekee ili kuhakikisha kwamba nakala zao za Neno la Mungu zilikuwa sahihi (Tazama fungu la 5)

5. Ni mambo gani yaliyohusika katika kunakili Maandiko ya Kiebrania? (Tazama picha kwenye jalada.)

5 Ili kuhifadhi ujumbe wake ulioongozwa kwa roho, Yehova aliagiza kwamba ujumbe huo unakiliwe. Aliwaagiza wafalme Waisraeli wajiandikie nakala za Sheria na akawaweka rasmi Walawi kuwafundisha watu Sheria hiyo. (Kum. 17:18; 31:24-26; Neh. 8:7) Baada ya Wayahudi kupelekwa uhamishoni huko Babiloni, kikundi cha waandishi wenye ustadi kilianza kutokeza nakala nyingi za Maandiko ya Kiebrania. (Ezra 7:6, maelezo ya chini) Wanaume hao walikuwa makini. Mwishowe, waandishi walianza kuhesabu si maneno tu, bali pia herufi ili kuhakikisha kwamba walinakili kila kitu kwa usahihi. Ingawa hivyo, kwa sababu ya kutokamilika kwa wanadamu, maandishi ya Biblia yalikuwa na baadhi ya makosa madogo. Hata hivyo, nakala nyingi za maandishi hayo zilitokezwa, hivyo, baadaye makosa hayo yangeweza kutambuliwa. Jinsi gani?

6. Makosa katika nakala za Biblia yanawezaje kutambuliwa?

6 Leo, wasomi wana njia yenye kutegemeka ya kutambua makosa yaliyofanywa na wale walionakili maandishi ya Biblia. Kwa mfano, tuseme kwamba wanaume 100 wanaambiwa wanakili kwa mkono maneno yaliyo kwenye ukurasa fulani. Mmoja wa wanaume hao anafanya kosa dogo anaponakili. Njia moja tunayoweza kutambua kosa lake ni kwa kulinganisha nakala yake na zile nakala nyingine. Vivyo hivyo, kwa kulinganisha baadhi ya hati za Biblia, wasomi wanaweza kutambua makosa au mambo fulani ambayo mwandishi aliondoa.

7. Wale walionakili Biblia walikuwa makini kadiri gani?

7 Wale walionakili hati za Biblia walijitahidi sana kufanya hivyo kwa usahihi. Fikiria mfano unaothibitisha jambo hilo. Hati ya kale zaidi inayopatikana na iliyokamilika ya Maandiko ya Kiebrania iliandikwa mwaka wa 1008 au 1009 W.K. Inaitwa Kodeksi ya Leningrad. Hata hivyo, hivi karibuni hati nyingi za Biblia na vipande vya Biblia vilivyoandikwa miaka 1,000 hivi kabla ya Kodeksi ya Leningrad vimepatikana. Huenda mtu akafikiri kwamba baada ya kunakili tena na tena hati hizo kwa kipindi cha miaka 1,000, maandishi ya Kodeksi ya Leningrad yangekuwa tofauti sana na maandishi yaliyopatikana katika hati hizo za zamani zaidi. Lakini hilo si kweli. Wasomi walipolinganisha hati za mapema zaidi na zile zilizopatikana baadaye, walitambua kwamba ingawa kulikuwa na tofauti ndogo katika maneno, kwa ujumla maana ya ujumbe uliopatikana katika Biblia haukubadilika.

8. Kuna tofauti gani kati ya nakala za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo na nakala za maandishi mengine ya kale?

8 Wakristo wa mapema waliiga mfano wa wale walionakili Maandiko ya Kiebrania. Walinakili kwa makini vitabu 27 vya Maandiko ya Kigiriki, ambavyo walivitumia katika mikutano na katika kazi yao ya kuhubiri. Baada ya kulinganisha hati zilizopo za Maandiko ya Kigiriki na maandishi mengine ya kipindi hichohicho cha wakati, msomi mmoja alifikia mkataa huu: “Kwa ujumla [nakala za Maandiko ya Kigiriki] zinapatikana kwa wingi zaidi, . . . na mara nyingi zimekamilika zaidi.” Kitabu Anatomy of the New Testament kinasema: “Unaweza kuwa na uhakika kwamba kile unachosoma katika tafsiri nzuri ya kisasa [ya Maandiko ya Kigiriki] kina ujumbe uleule ambao uliandikwa na waandikaji wa zamani.”

9. Kulingana na Isaya 40:8, ni jambo gani lililo hakika kuhusu ujumbe wa Biblia?

9 Kwa karne nyingi, jitihada za waandishi wengi za kunakili kwa umakini zimechangia kuwepo kwa Biblia iliyo sahihi ambayo tunasoma na kujifunza leo. d Bila shaka, Yehova ndiye aliyehakikisha kwamba ujumbe wake kwa wanadamu ungehifadhiwa kwa usahihi. (Soma Isaya 40:8.) Hata hivyo, huenda wengine wakasema kwamba kuhifadhiwa kwa Biblia hakuthibitishi kwamba imeongozwa na roho ya Mungu. Acheni sasa tuchunguze uthibitisho unaoonyesha kwamba Biblia imeongozwa na roho ya Mungu.

UNABII WA BIBLIA UNATEGEMEKA

Left: C. Sappa/DeAgostini/Getty Images; right: Image © Homo Cosmicos/Shutterstock

Unabii wa Biblia umetimizwa na unaendelea kutimizwa (Tazama fungu la 10 na 11) f

10. Toa mfano wa utimizo wa unabii unaothibitisha ukweli wa 2 Petro 1:21. (Tazama picha.)

10 Biblia ina unabii mwingi ambao ulitimizwa, na baadhi ya unabii huo ulitimizwa mamia ya miaka baada ya kuandikwa. Historia inaonyesha kwamba unabii huo ulitimizwa. Jambo hilo halitushangazi kwa sababu tunajua kwamba Yehova ndiye Mtungaji wa unabii wa Biblia. (Soma 2 Petro 1:21.) Fikiria unabii kuhusu kuanguka kwa jiji la kale la Babiloni. Katika karne ya nane K.W.K., nabii Isaya aliongozwa na roho kutabiri kwamba jiji lenye nguvu la Babiloni lingeshindwa. Hata alitaja jina la yule ambaye angelishinda jiji hilo, yaani, Koreshi, na akatabiri kihususa jinsi ambavyo jiji hilo lingeshindwa. (Isa. 44:27–45:2) Pia, Isaya alitabiri kwamba mwishowe jiji la Babiloni lingeharibiwa na lingeachwa ukiwa kabisa. (Isa. 13:19, 20) Na ndivyo ilivyokuwa. Babiloni lilishindwa na Wamedi na Waajemi mwaka wa 539 K.W.K., na mahali ambapo jiji hilo kuu lilikuwa sasa kuna rundo la magofu. Tazama Video Biblia Ilitabiri Kuanguka kwa Jiji la Babiloni katika toleo la kielektroni la kitabu Furahia Maisha Milele! somo la 3, jambo kuu la 5.

11. Eleza jinsi Danieli 2:41-43 inavyotimizwa leo.

11 Kutimizwa kwa unabii unaopatikana katika Biblia si jambo la wakati uliopita tu; leo pia tunaona utimizo wa unabii mbalimbali. Kwa mfano, fikiria utimizo wenye kustaajabisha wa unabii wa Danieli kuhusu Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani. (Soma Danieli 2:41-43.) Unabii huo ulitabiri kwa usahihi kwamba serikali hiyo kuu ya ulimwengu ingekuwa na “nguvu kwa sehemu” kama chuma na “dhaifu kwa sehemu” kama udongo wa mfinyanzi. Hilo limethibitika kuwa kweli. Serikali za Uingereza na Marekani zimeonyesha nguvu kama za chuma kwa kutimiza sehemu kubwa katika kushinda vile Vita viwili vya Ulimwengu na wanaendelea kuwa na nguvu nyingi za kijeshi. Hata hivyo, nguvu zao zimekuwa zikidhoofishwa na raia wao, ambao mara kwa mara wanaandamana ili kutetea haki zao kupitia vyama vya wafanyakazi, kampeni za kutetea haki za raia, na harakati za kupigania uhuru. Hivi karibuni, mtaalamu fulani wa siasa za ulimwengu alisema hivi: “Leo hakuna nchi nyingine ya kidemokrasia yenye maendeleo makubwa ya viwanda ulimwenguni ambayo imegawanyika au kuvurugika kisiasa kuliko nchi ya Marekani.” Katika miaka ya karibuni, Uingereza, sehemu ya pili ya serikali hiyo kuu, imegawanyika kihususa kwa sababu ya maoni yaliyotofautiana kuhusu uhusiano wake pamoja na nchi nyingine za Umoja wa Ulaya. Migawanyiko hiyo imefanya iwe vigumu sana kwa Serikali Kuu ya Uingereza na Marekani kutenda kwa uthabiti.

12. Unabii wa Biblia unatupatia usadikisho gani?

12 Unabii mwingi ambao tayari umetimizwa unaimarisha uhakika wetu kuhusu kutegemeka kwa ahadi za Mungu za wakati ujao. Tunahisi kama mtunga zaburi aliyesali hivi kwa Yehova: “Ninautamani sana wokovu wako, kwa maana neno lako ni tumaini langu.” (Zab. 119:81) Kwa fadhili, kupitia kurasa za Biblia, Yehova ametuahidi “wakati ujao na tumaini.” (Yer. 29:11) Tumaini letu la wakati ujao halitegemei jitihada za wanadamu, bali linategemea ahadi za Yehova. Acheni tuendelee kuimarisha tumaini letu katika Neno la Mungu kwa kuwa wanafunzi wenye bidii wa unabii wa Biblia.

USHAURI UNAOTEGEMEA BIBLIA UNAWASAIDIA MAMILIONI YA WATU

13. Kulingana na Zaburi 119:66 138, ni jambo gani lingine linalothibitisha kwamba Biblia inategemeka?

13 Ili kupata uthibitisho mwingine unaoonyesha kwamba tunaweza kuitumaini Biblia, fikiria matokeo mazuri ambayo watu hupata wanapofuata ushauri wake. (Soma Zaburi 119:66, 138.) Kwa mfano, wenzi wa ndoa ambao walikuwa karibu kutalikiana sasa ndoa zao zina furaha na umoja. Watoto wao wanafurahia kulelewa kwa upendo kwenye nyumba ya Kikristo ambapo wanahisi salama na kwamba wanapendwa.​—Efe. 5:22-29.

14. Simulia mfano unaoonyesha jinsi kutumia kweli za Biblia kunavyobadili maisha ya mtu yawe mazuri zaidi.

14 Kwa kutumia ushauri wenye hekima wa Biblia, hata wahalifu hatari wamefanya mabadiliko makubwa maishani. Fikiria jinsi ushauri wa Biblia ulivyomsaidia mfungwa anayeitwa Jack. e Alikuwa mhalifu mwenye ukatili aliyejulikana kuwa mfungwa hatari zaidi kati ya wafungwa waliohukumiwa kifo. Lakini siku moja Jack alihudhuria funzo la Biblia. Aliguswa moyo sana na fadhili alizoonyeshwa na akina ndugu waliokuwa wakiongoza funzo hilo, naye akaanza kujifunza Biblia pia. Alipoanza kutumia kweli za Biblia maishani, mwenendo na hata utu wake ulianza kubadilika na kuwa mzuri zaidi. Baada ya muda, Jack alistahili kuwa mhubiri na akabatizwa. Aliwahubiria kwa bidii wafungwa wenzake kuhusu Ufalme wa Mungu na akawasaidia angalau wafungwa wanne wajifunze kweli. Siku yake ya kuuawa ilipofika, Jack alikuwa mtu tofauti kabisa. Mmoja wa mawakili wake alisema hivi: “Jack wa sasa si yule niliyemjua miaka 20 iliyopita. Mafundisho ya Mashahidi wa Yehova yalibadili maisha yake.” Ingawa Jack aliuawa, mfano wake unaonyesha wazi tunaweza kulitumaini Neno la Mungu na kwamba lina nguvu za kubadili maisha ya mtu yawe mazuri zaidi.—Isa. 11:6-9.

Ushauri wa Biblia umebadili maisha ya watu wengi kutoka katika malezi mbalimbali yawe mzuri zaidi (Tazama fungu la 15) g

15. Kutumia kweli za Biblia maishani kunafanya watu wa Yehova wawe tofauti jinsi gani? (Tazama picha.)

15 Kwa sababu wanatumia kweli ya Biblia maishani, watu wa Yehova wana umoja. (Yoh. 13:35; 1 Kor. 1:10) Amani na umoja wetu unaonekana wazi hasa kwa sababu leo ulimwenguni kuna migawanyiko ya kisiasa, kikabila, na kijamii. Kuona umoja kati ya watu wa Yehova kulimchochea kwa njia kubwa mwanamume kijana anayeitwa Jean. Alilelewa katika nchi moja ya Kiafrika. Vita vya wenyewe kwa wenyewe vilipotokea alijiunga na jeshi, lakini baadaye alikimbilia nchi jirani. Akiwa huko alikutana na Mashahidi wa Yehova. Jean anasema hivi: “Nilijifunza kwamba wafuasi wa dini ya kweli hawajihusishi katika mambo ya kisiasa na hawana migawanyiko. Badala yake, wanapendana.” Anaendelea kusema hivi: “Nilikuwa nimetoa maisha yangu ili kupigania nchi yangu. Lakini nilipojifunza kweli ya Biblia, nilichochewa kuweka wakfu maisha yangu kwa Yehova.” Jean alibadilika kabisa. Badala ya kupigana dhidi ya watu walio na malezi tofauti na yake, sasa anamhubiria kila mtu anayekutana naye kweli ya Biblia inayowaunganisha watu. Kwa kuwa ushauri wa Biblia una matokeo mazuri kwa watu wanaotoka katika malezi mbalimbali, hilo linathibitisha kwa njia kubwa kwamba tunaweza kutumaini Neno la Mungu.

ENDELEA KULITUMAINI NENO LA MUNGU LA KWELI

16. Kwa nini ni muhimu tuimarishe uhakika wetu katika Neno la Mungu?

16 Kadiri ulimwengu unavyokuwa mbaya zaidi, uhakika wetu katika kweli utajaribiwa. Huenda watu wakajaribu kupanda mbegu za shaka katika akili zetu​—shaka kuhusu ikiwa Biblia ni ya kweli au ikiwa Yehova amemweka rasmi mtumwa mwaminifu na mwenye busara kuwaongoza waabudu wake leo. Lakini ikiwa tunasadiki kwamba sikuzote Neno la Yehova ni la kweli, tutaweza kupinga mashambulizi hayo ya imani yetu. Tutaazimia “kuyatii masharti [ya Yehova] nyakati zote, mpaka mwisho.” (Zab. 119:112) ‘Hatutaaibika’ kuwaambia wengine kuhusu kweli na kuwatia moyo waishi kulingana nayo. (Zab. 119:46) Na tutaweza kuvumilia hali ngumu zaidi maishani, kutia ndani mateso, “kwa subira na shangwe.”—Kol. 1:11; Zab. 119:143, 157.

17. Andiko letu la mwaka litatukumbusha nini?

17 Tunathamini sana kwamba Yehova ametufunulia kweli! Kweli inatuimarisha, inatupatia kusudi hakika maishani, na mwongozo ulio wazi katika ulimwengu unaozidi kuchanganyikiwa na wenye vurugu. Inatupatia tumaini kuhusu wakati ujao bora chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu. Acheni andiko la mwaka wa 2023 litusaidie kusimama imara katika usadikisho wetu kwamba Neno lote la Mungu, yaani, kiini hasa cha Neno hilo, ni kweli!​—Zab. 119:160.

WIMBO 94 Kulithamini Neno la Mungu

a Andiko la mwaka lenye kuimarisha imani limechaguliwa kwa ajili ya mwaka wa 2023: “Kiini hasa cha neno lako ni kweli.” (Zab. 119:160) Bila shaka, unakubaliana na maneno hayo. Lakini watu wengi hawaamini kwamba Biblia inasema ukweli na kwamba inaweza kutupatia mwongozo unaotegemeka. Katika makala hii, tutachunguza mambo matatu yanayoweza kutusaidia kuwasadikisha wale wenye mioyo minyoofu kwamba wanaweza kuitumaini Biblia na ushauri wake.

b UFAFANUZI WA MANENO: Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “kiini” katika mstari huu, linamaanisha ujumla wa kile kinachotumiwa kutengeneza kitu fulani.

c Neno “hati” linarejelea maandishi ya kale yaliyoandikwa kwa mkono.

d Ili kupata habari zaidi kuhusu kuhifadhiwa kwa Biblia, tembelea tovuti ya jw.org kisha kwenye sanduku la tafuta andika “Historia na Biblia.”

e Baadhi ya majina yamebadilishwa.

f MAELEZO YA PICHA: Kupitia amri ya Mungu, jiji lenye utukufu la kale la Babiloni mwishowe lilikuja kuwa magofu.

g MAELEZO YA PICHA: Igizo​—Badala ya kupigana na watu, mwanamume kijana anajifunza kutoka kwenye Biblia jinsi ya kuishi kwa amani na kuwasaidia wengine wafanye vivyo hivyo.