Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 4

Yehova Hubariki Jitihada Zetu za Kuadhimisha Ukumbusho

Yehova Hubariki Jitihada Zetu za Kuadhimisha Ukumbusho

“Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka.”​—LUKA 22:19.

WIMBO 19 Mlo wa Jioni wa Bwana

MUHTASARI a

1-2. Kwa nini tunahudhuria Ukumbusho kila mwaka?

 MIAKA 2,000 hivi iliyopita, Yesu alitoa uhai wake kwa ajili yetu, na hivyo akatufungulia njia ya kupata uzima wa milele. Usiku kabla ya kifo chake, Yesu aliwaamuru wafuasi wake wakumbuke tendo hilo la upendo kwa kufanya sherehe ndogo iliyohusisha mkate na divai.​—1 Kor. 11:23-26.

2 Tunatii amri ya Yesu kwa sababu tunampenda sana. (Yoh. 14:15) Kila mwaka wakati wa majira ya Ukumbusho, tunaonyesha kwamba tunathamini mambo aliyotufanyia kwa kutenga muda ili kusali na kutafakari kuhusu maana ya kifo chake. Pia, tunafurahi kufanya mengi zaidi katika huduma ili kuwatia moyo watu wengi iwezekanavyo wajiunge nasi kwenye tukio hilo la pekee. Na bila shaka, tumeazimia kutoruhusu kitu chochote kituzuie kuhudhuria Ukumbusho.

3. Tutachunguza nini katika makala hii?

3 Katika makala hii, tutachunguza njia tatu ambazo watu wa Yehova wamejitahidi sana kuadhimisha kifo cha Yesu: (1) kwa kuadhimisha Ukumbusho kwa njia ambayo Yesu aliwafundisha, (2) kwa kuwaalika wengine kwenye Ukumbusho, na (3) kwa kuadhimisha Ukumbusho licha ya hali zozote ngumu.

KUADHIMISHA UKUMBUSHO KWA NJIA AMBAYO YESU ALIFUNDISHA

4. Ni maswali gani ambayo hujibiwa kila mwaka kwenye Ukumbusho, na kwa nini hatupaswi kuona kweli hizo kuwa mambo ya kawaida? (Luka 22:19, 20)

4 Kila mwaka kwenye Ukumbusho, sisi husikiliza hotuba inayotegemea Biblia ambayo hujibu waziwazi maswali kadhaa. Tunajifunza kwa nini wanadamu wanahitaji fidia, na jinsi kifo cha mtu mmoja kinavyoweza kulipia dhambi za watu wengi. Tunakumbushwa kile kinachowakilishwa na mkate na divai na wale wanaopaswa kula mkate na kunywa divai. (Soma Luka 22:19, 20.) Na pia tunatafakari baraka ambazo wale walio na tumaini la kuishi duniani watapata. (Isa. 35:5, 6; 65:17, 21-23) Hatupaswi kuona kweli hizo kuwa mambo ya kawaida. Mabilioni ya watu hawajui mambo hayo na hawaelewi jinsi dhabihu ya Yesu ilivyo na thamani sana. Pia, hawaadhimishi Ukumbusho wa kifo chake kulingana na njia aliyofundisha. Kwa nini?

5. Baada ya mitume wengi kufa, watu walianzaje kuadhimisha kifo cha Yesu?

5 Muda mfupi baada ya mitume wa Yesu kufa, Wakristo wa uwongo waliingia katika kutaniko. (Mt. 13:24-27, 37-39) Walisema “mambo yaliyopotoka ili kuwavuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.” (Mdo. 20:29, 30) Mojawapo ya “mambo yaliyopotoka” ambayo mwishowe Wakristo wa uwongo walianza kufundisha ni kwamba Yesu hakutoa mwili wake “mara moja kwa wakati wote ili kubeba dhambi za wengi,” kama Biblia inavyosema, badala yake dhabihu yake inapaswa kutolewa tena na tena. (Ebr. 9:27, 28) Leo, watu wengi huamini fundisho hilo la uwongo. Wao hukusanyika kwa ukawaida makanisani—wakati mwingine kila siku—ili kuadhimisha kile ambacho wanakiita “Dhabihu ya Misa.” b Dini nyingine huadhimisha kifo cha Yesu mara chache, lakini wengi wa wafuasi wao hawaelewi waziwazi maana ya dhabihu ya Yesu. Huenda wengine wakajiuliza, ‘Je, kweli kifo cha Yesu kinamaanisha kwamba ninaweza kusamehewa dhambi zangu? ’ Kwa nini wanajiuliza swali hilo? Katika visa fulani, wameathiriwa na wale wanaotilia shaka kwamba dhabihu ya Yesu inafanya iwezekane kusamehewa dhambi. Wafuasi wa kweli wa Yesu wameshughulikiaje hali hiyo?

6. Kufikia mwaka wa 1872, kikundi cha wanafunzi wa Biblia kilikuwa kimefikia mkataa gani?

6 Mwishoni mwa karne ya 19, kikundi cha wanafunzi wa Biblia kilichoongozwa na Charles Taze Russell kilianza kujifunza Maandiko kwa makini. Walitaka kujua ukweli kuhusu thamani ya dhabihu ya Yesu na jinsi kifo chake kinavyopaswa kukumbukwa. Kufikia mwaka wa 1872, walikuwa wamefikia mkataa unaotegemea Biblia kwamba kwa kweli Yesu aliandaa fidia kwa ajili ya wanadamu wote. Baada ya kujifunza mambo hayo hawakukaa kimya. Badala yake, walieneza ujumbe huo kupitia vitabu na magazeti. Muda mfupi baada ya hapo, kwa kuwaiga Wakristo wa karne ya kwanza, walianza kukutana mara moja tu kwa mwaka ili kuadhimisha Ukumbusho.

7. Tunanufaikaje kutokana na utafiti uliofanywa mwanzoni na wanafunzi wa Biblia?

7 Leo, tunanufaika kutokana na utafiti ambao wanaume hao Wakristo wanyoofu walifanya miaka mingi iliyopita. Jinsi gani? Yehova ametusaidia kuelewa ukweli kuhusu dhabihu ya Yesu na kile ambacho inatimiza. (1 Yoh. 2:1, 2) Pia, tumejifunza kwamba Biblia inaeleza kuhusu aina mbili ya matumaini kwa ajili ya wanadamu wanaomfurahisha Mungu, yaani, uhai usioweza kufa mbinguni kwa baadhi yao, na uzima wa milele duniani kwa mamilioni ya wengine. Tunamkaribia Yehova zaidi tunapochunguza jinsi anavyotupenda na jinsi tunavyonufaika sana kibinafsi kutokana na dhabihu ya Yesu. (1 Pet. 3:18; 1 Yoh. 4:9) Basi kama ndugu zetu waaminifu walioishi zamani, tunawaalika wengine wajiunge nasi kuadhimisha Ukumbusho kulingana na njia ambayo Yesu alifundisha.

KUWAALIKA WENGINE KWENYE UKUMBUSHO

Unaweza kufanya nini ili ushiriki kikamili katika kampeni ya kuwaalika watu kwenye Ukumbusho? (Tazama fungu la 8 hadi 10) e

8. Watu wa Yehova wamefanya nini ili kuwaalika wengine kwenye Ukumbusho? (Tazama picha.)

8 Kwa miaka mingi, watu wa Yehova wamewaalika wengine kwenye Ukumbusho. Mwaka wa 1881, ndugu na dada huko Marekani walialikwa kukutana kwenye nyumba ya mtu binafsi huko Allegheny, Pennsylvania, kwa ajili ya tukio hilo la pekee. Baadaye, kila kutaniko lilifanya Ukumbusho. Mwezi wa Machi 1940, wahubiri waliambiwa kwamba wangeweza kumwalika mtu yeyote kutoka kwenye eneo lao ambaye alionyesha kwamba anapendezwa. Mwaka wa 1960, kwa mara ya kwanza, mialiko iliyochapishwa ilitumwa kutoka Betheli kwenda kwenye makutaniko. Tangu wakati huo, mabilioni ya mialiko ya Ukumbusho imetolewa. Kwa nini tunatumia muda na jitahidi nyingi sana kuwaalika wengine?

9-10. Ni nani wanaonufaika na jitihada zetu za kuwaalika wengine kwenye Ukumbusho? (Yohana 3:16)

9 Sababu moja inayotufanya tuwaalike wengine waadhimishe Ukumbusho pamoja nasi ni kwamba tunataka wale waliohudhuria kwa mara ya kwanza wajifunze yale ambayo Yehova na Yesu wametufanyia sisi sote. (Soma Yohana 3:16.) Tunatumaini kwamba mambo wanayoona na kusikia kwenye Ukumbusho yatawachochea wajifunze mengi zaidi na kuwa watumishi wa Yehova. Lakini wengine wananufaika pia.

10 Pia, tunawaalika wale ambao wameacha kumtumikia Yehova. Tunafanya hivyo ili kuwakumbusha kwamba bado Mungu anawapenda. Wengi hukubali tunapowaalika na tunafurahi sana kuwaona. Kuhudhuria Ukumbusho huwakumbusha jinsi walivyofurahia sana kumtumikia Yehova wakati uliopita. Fikiria mfano wa Monica. c Alianza kuhubiri tena pamoja na kutaniko wakati wa janga la COVID-19. Baada ya kuhudhuria Ukumbusho mwaka wa 2021, alisema hivi: “Ukumbusho huu umekuwa wa pekee sana kwangu. Kwa mara ya kwanza baada ya miaka 20, nimeanza kuwatolea watu tena ushahidi na kuwaalika kwenye Ukumbusho. Kwa kweli, nilifanya yote niliyoweza kuwaalika wengine kwa sababu ninathamini sana mambo yote ambayo Yehova na Yesu wamenifanyia.” (Zab. 103:1-4) Iwe watu watakubali au kukataa mwaliko wetu, tunawaalika wengine kwa bidii kwenye Ukumbusho tukijua kwamba Yehova anathamini jitihada zetu.

11. Yehova amebariki jinsi gani jitihada zetu za kuwaalika watu kwenye Ukumbusho? (Hagai 2:7)

11 Yehova amebariki sana jitihada zetu za kuwaalika wengine kwenye Ukumbusho. Mwaka wa 2021, licha ya vizuizi vilivyosababishwa na janga la COVID-19, tulikuwa na kilele cha wahudhuriaji 21,367,603. Idadi hiyo ni karibu mara mbili na nusu ya idadi ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni! Hapana shaka kwamba Yehova hapendezwi tu na idadi ya watu wanaohudhuria, badala yake anapendezwa kibinafsi na kila mtu anayehudhuria. (Luka 15:7; 1 Tim. 2:3, 4) Tunasadiki kwamba Yehova anatumia kazi yetu ya kuwaalika watu ili kutusaidia kupata watu wenye mioyo minyoofu.​—Soma Hagai 2:7.

KUADHIMISHA UKUMBUSHO LICHA YA HALI NGUMU

Yehova hubariki jitihada zetu za kuadhimisha Ukumbusho (Tazama fungu la 12) f

12. Ni hali gani ambazo zinaweza kufanya iwe vigumu kwetu kuhudhuria Ukumbusho? (Tazama picha.)

12 Yesu alitabiri kwamba katika siku za mwisho tungekabiliana na kila aina ya hali ngumu​—kama vile upinzani katika familia, mateso, vita, magonjwa, na mengine mengi. (Mt. 10:36; Marko 13:9; Luka 21:10, 11) Nyakati nyingine, hali hizo hufanya iwe vigumu kwetu kuadhimisha kifo cha Yesu. Ndugu na dada zetu wamefanya nini ili kushinda changamoto hizo, na Yehova amewasaidiaje?

13. Yehova alibarikije ujasiri na azimio la Artem la kuadhimisha Ukumbusho alipokuwa gerezani?

13 Kufungwa gerezani. Ndugu zetu waliofungwa gerezani kwa sababu ya imani yao wanafanya yote wanayoweza ili kuadhimisha kifo cha Yesu. Fikiria mfano wa Artem. Wakati wa majira ya Ukumbusho ya mwaka wa 2020, alifungwa katika chumba cha jela chenye ukubwa wa mita 17 za mraba ambacho kilikuwa na wafungwa watano kwa wakati mmoja. Licha ya kufungwa gerezani, alifaulu kupata vitu fulani ambavyo angetumia kama mifano ya Ukumbusho, na akapanga kutoa hotuba ya Ukumbusho kwa ajili yake mwenyewe. Lakini wafungwa wenzake walivuta sigara na kutumia lugha chafu. Alifanya nini? Aliwaomba waache kutumia lugha chafu na wasivute sigara kwa saa moja tu. Artem alishangaa wakati wafungwa wenzake walipokubali kwamba hawatavuta sigara wala kutumia lugha chafu wakati wa Ukumbusho. Artem anasema, “Niliwauliza ikiwa wangependa kujua kuhusu Ukumbusho.” Ingawa walisema kwamba hawataki kujifunza kuhusu tukio hilo, baada ya kumwona na kumsikia Artem akiadhimisha Ukumbusho, walimuuliza maswali mengi kuhusu tukio hilo.

14. Ni jitihada gani zilizofanywa ili kuadhimisha Ukumbusho licha ya janga la COVID-19?

14 Janga la COVID-19. Janga hilo lilipotokea, watu wa Yehova hawangeweza kuhudhuria Ukumbusho ana kwa ana. Lakini hilo halikuwazuia kuadhimisha Ukumbusho. d Makutaniko yaliyoweza kupata Intaneti yalifanya Ukumbusho kupitia video iliyounganishwa kwenye mtandao. Lakini namna gani mamilioni ambao hawangeweza kupata Intaneti? Katika baadhi ya nchi, mipango ilifanywa ili kupeperusha hotuba kupitia televisheni au redio. Isitoshe, ofisi za tawi zilirekodi hotuba katika lugha zaidi ya 500, ili hata wale walio katika maeneo ya mbali waadhimishe Ukumbusho. Na ndugu waaminifu walifanya mipango ili hotuba hizo zilizorekodiwa zipelekwe kwa wale waliozihitaji.

15. Unajifunza nini kutokana na mfano wa mwanafunzi wa Biblia anayeitwa Sue?

15 Upinzani katika familia. Kwa wengine, changamoto kubwa zaidi ya kuadhimisha Ukumbusho ni upinzani katika familia. Fikiria mfano wa mwanafunzi wa Biblia anayeitwa Sue. Mwaka wa 2021, siku moja kabla ya Ukumbusho, Sue alimwambia mwalimu wake wa Biblia kwamba kwa sababu ya upinzani nyumbani hangeweza kuhudhuria Ukumbusho. Mwalimu wake wa Biblia alimsomea Luka 22:44. Kisha akamweleza kwamba tunapokabili hali ngumu, tunapaswa kuiga mfano wa Yesu kwa kusali kwa Yehova na kumtegemea kabisa. Siku iliyofuata, Sue alitayarisha mkate na divai na akatazama programu ya pekee ya Ibada ya Asubuhi kwenye jw.org. Siku hiyo jioni, akiwa peke yake chumbani, alisikiliza hotuba ya Ukumbusho kwenye simu yake. Baadaye, Sue alimwandikia hivi mwalimu wake wa Biblia: “Jana ulinitia moyo sana. Nilifanya yote niliyoweza ili kuhudhuria Ukumbusho, na Yehova akanisaidia. Maneno hayatoshi kueleza jinsi nilivyo mwenye furaha na shukrani!” Je, unafikiri Yehova anaweza kukusaidia ikiwa utakabili hali kama hiyo?

16. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atabariki jitihada zetu za kuhudhuria Ukumbusho? (Waroma 8:31, 32)

16 Yehova anathamini sana jitihada zetu za kuadhimisha kifo cha Yesu. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba atatubariki tunapoonyesha tunathamini mambo aliyotufanyia. (Soma Waroma 8:31, 32.) Basi, acheni tuazimie kuhudhuria Ukumbusho wa mwaka huu na kufanya yote tunayoweza ili kuongeza jitihada zetu katika utendaji wa kiroho wakati wa majira ya Ukumbusho.

WIMBO 18 Tunathamini Fidia

a Jumanne, Aprili 4, 2023, mamilioni ya watu ulimwenguni pote wataadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Wengi watahudhuria kwa mara ya kwanza. Wengine ambao wameacha kumtumikia Yehova watahudhuria baada ya miaka mingi. Wengine watalazimika kushinda vizuizi vikubwa ili kuhudhuria. Hata hali zako ziweje, unaweza kuwa na uhakika kuwa Yehova atafurahi kwa sababu ya jitihada ulizofanya ili kuhudhuria.

b Waabudu hao wanaamini kwamba wakati wa mwadhimisho huo, mkate na divai hubadilishwa na kuwa mwili na damu ya Kristo. Wanaamini kwamba mwili na damu ya Yesu hutolewa dhabihu kila mara mtu anaposhiriki katika mwadhimisho huo.

c Baadhi ya majina yamebadilishwa.

d Tazama pia makala zilizo kwenye jw.org zenye kichwa “2021 Mwadhimisho wa Ukumbusho.”

e MAELEZO YA PICHA: Tangu miaka ya 1960, mialiko ya Ukumbusho imekuwa ikiboreshwa na sasa inapatikana ikiwa imechapishwa au ya kielektroni.

f MAELEZO YA PICHA: Igizo​—Ndugu na dada wakiadhimisha Ukumbusho wakati wa msukosuko wa kijamii.