Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kweli Yesu Alikufa kwa Ajili Yangu?

Je, Kweli Yesu Alikufa kwa Ajili Yangu?

BIBLIA imejaa maelezo mengi ya kutoka moyoni ya watu waliokuwa na “hisia kama zetu.” (Yak. 5:17) Kwa mfano, ni rahisi kwetu kuelewa hisia za Paulo ambaye alikiri hivi waziwazi kwenye Waroma 7:21-24: “Ninapotaka kufanya yaliyo sawa, yaliyo mabaya yapo pamoja nami. . . . Maskini mimi!” Hisia hizo za kutoka moyoni zinatufariji tunapopambana na udhaifu wetu wenyewe.

Pia, Paulo alizungumzia hisia nyingine alizokuwa nazo. Kwenye Wagalatia 2:20, alieleza kuhusu usadikisho aliokuwa nao kwamba Yesu ‘alimpenda na kujitoa mwenyewe kwa ajili yake’ binafsi! Je, hivyo ndivyo unavyohisi? Huenda usihisi hivyo nyakati zote.

Ikiwa tunapambana na hisia za kujiona hatufai kwa sababu ya dhambi tulizofanya zamani, huenda nyakati nyingine isiwe rahisi kukubali kwamba Yehova anatupenda na ametusamehe, na inaweza kuwa vigumu hata zaidi kuiona dhabihu ya fidia ya Yesu kuwa zawadi tuliyopewa sisi binafsi. Je, kweli Yesu anataka tuione fidia kama zawadi aliyotupatia sisi binafsi? Ikiwa ndivyo, ni nini kitakachotusaidia tuione kwa njia hiyo? Acheni tuchunguze maswali hayo mawili.

MAONI YA YESU KUHUSU DHABIHU YAKE

Ndiyo, Yesu anataka tuione dhabihu yake kama zawadi aliyotupatia sisi binafsi. Tuna uhakika gani? Wazia akilini tukio linalopatikana kwenye Luka 23:39-43. Mwanamume ametundikwa kwenye mti wa mateso karibu na Yesu. Anakiri kwamba alikuwa amefanya kosa fulani. Ni lazima kosa hilo lilikuwa zito sana kwa sababu adhabu ya kikatili aliyokuwa amepewa ilitolewa kwa wahalifu waliokuwa wamefanya makosa mabaya sana. Akiwa na mkazo mkubwa sana, mwanamume huyo anamwambia hivi Yesu: “Unikumbuke utakapoingia katika Ufalme wako.”

Yesu anaitikiaje? Wazia Yesu akigeuza kichwa chake kwa maumivu makali ili amtazame usoni. Ingawa Yesu ana maumivu makali, anatabasamu na kumfariji mwanamume huyo hivi: “Kwa kweli ninakuambia leo, utakuwa pamoja nami katika Paradiso.” Yesu angeweza tu kumkumbusha mwanamume huyo kwamba “Mwana wa binadamu [alikuja] . . . kutoa uhai wake uwe fidia badala ya wengi.” (Mt. 20:28) Lakini je, uliona jinsi Yesu alivyozungumza kwa fadhili na mwanamume huyo na kukazia kwamba dhabihu yake ilimhusu yeye binafsi? Yesu alikuwa mwenye urafiki na alitumia maneno “utakuwa” na “nami.” Na alimwambia yeye binafsi kwamba ataishi katika dunia paradiso.

Bila shaka, Yesu alitaka mwanamume huyo aione dhabihu ambayo angetoa kuwa zawadi inayomhusu yeye binafsi. Ikiwa Yesu alihisi hivyo kumhusu mhalifu ambaye hakuwa hata amepata fursa ya kumtumikia Mungu, kwa kweli Yesu angehisi vivyo hivyo kumhusu Mkristo aliyebatizwa anayemtumikia Mungu. Hivyo, ni nini kinachoweza kutusaidia tusitawishe hisia zinazofaa kujihusu licha ya dhambi tulizofanya zamani?

JAMBO LILILOMSAIDIA PAULO

Huduma ambayo Paulo alipewa na Yesu ilimsaidia kuelewa kwamba Yesu alikufa kwa ajili yake. Jinsi gani? Alieleza hivi: “Ninamshukuru Kristo Yesu Bwana wetu, aliyenitia nguvu, kwa sababu aliniona kuwa mwaminifu kwa kunipa huduma, ingawa zamani nilikuwa mkufuru na mtesaji na mtu mwenye dharau.” (1 Tim. 1:12-14) Mgawo ambao Paulo alipewa ulimsadikisha kwamba Yesu alikuwa amemwonyesha rehema, alimpenda, na alimtumaini yeye binafsi. Sawa na Paulo, Yesu ametukabidhi sisi binafsi huduma. (Mt. 28:19, 20) Je, huduma yetu inaweza kutusaidia kuelewa kwamba Yesu alikufa kwa ajili yetu pia?

Albert, ambaye hivi karibuni alimrudia Yehova baada ya kutengwa na ushirika kwa miaka 34 hivi, anaeleza: “Dhambi zangu ziko mbele yangu daima. Lakini ninapokuwa katika huduma mimi huhisi kama mtume Paulo kwamba mimi binafsi nimepewa huduma hii na Yesu. Jambo hilo huniimarisha na kunifanya niwe na hisia zinazofaa kujihusu, kuhusu maisha yangu, na wakati wangu ujao.”​—Zab. 51:3.

Unapojifunza Biblia na watu wa namna zote, wahakikishie kwamba Yesu ni mwenye rehema kuwaelekea na anawapenda

Allan, ambaye aliishi maisha ya uhalifu na jeuri kabla ya kujifunza kweli, anakiri hivi: “Bado ninakumbuka mambo yote mabaya niliyowatendea watu. Nyakati nyingine jambo hilo hufanya nishuke moyo. Lakini ninamshukuru Yehova kwa sababu anaruhusu mtenda dhambi kama mimi awapelekee wengine habari njema. Ninapoona jinsi watu wanavyoitikia habari njema, hilo hunikumbusha jinsi Yehova alivyo mwema na mwenye upendo sana. Ninahisi kwamba ananitumia mimi kuwasaidia wengine wanaopambana na hisia kama zangu kwa sababu ya mambo waliyofanya zamani.”

Huduma yetu hutusaidia kutumia nguvu zetu kutenda matendo mazuri na kuwa na mawazo mazuri. Huduma yetu hutuhakikishia kwamba Yesu ni mwenye rehema kutuelekea, anatupenda, na anatutumaini.

YEHOVA NI MKUU KULIKO MIOYO YETU

Huenda mioyo yetu ikaendelea kutuhukumu kwa sababu ya makosa yetu ya zamani hadi mfumo mwovu wa Shetani utakapoondolewa. Ni nini kitakachotusaidia kupambana na hisia hizo?

Jean, dada ambaye mara kwa mara amekuwa akipambana na hisia za hatia kwa sababu ya maisha ya kinafiki aliyoishi alipokuwa kijana, anasema hivi: “Mimi hufurahi kujua kwamba ‘Mungu ni mkuu kuliko mioyo yetu.’” (1 Yoh. 3:19, 20) Sisi pia tunafarijika kujua kwamba Yehova na Yesu wanaelewa vizuri zaidi hali yetu ya dhambi kuliko sisi wenyewe. Kumbuka, walichochewa na upendo kutoa fidia, si kwa ajili ya wanadamu wakamilifu, bali kwa ajili ya watenda dhambi wanaotubu.​—1 Tim. 1:15.

Tunaisadikishia mioyo yetu ukweli huo muhimu tunaposali na kutafakari kuhusu jinsi Yesu alivyowatendea wanadamu wasio wakamilifu na tunapofanya yote tuwezayo kutimiza huduma aliyotupatia. Ukifanya hivyo, kama Paulo, utasema hivi: Yesu “[alinipenda] na kujitoa mwenyewe kwa ajili yangu.”