Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 29

“Nendeni Mkafanye Wanafunzi”

“Nendeni Mkafanye Wanafunzi”

“Basi, nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.”​—MT. 28:19.

WIMBO 60 Ni Uzima Kwao

MUHTASARI *

1-2. (a) Kulingana na amri ya Yesu inayopatikana kwenye Mathayo 28:18-20, kazi kuu ya kutaniko la Kikristo ni gani? (b) Tutachunguza maswali gani katika makala hii?

LAZIMA mitume walikuwa na matazamio makubwa walipokuwa wakikusanyika kando ya mlima. Baada ya kufufuliwa, Yesu alikuwa amepanga kukutana nao katika eneo hilo. (Mt. 28:16) Huenda hiyo ndiyo pindi ambayo “aliwatokea ndugu zaidi ya 500 kwa wakati mmoja.” (1 Kor. 15:6) Kwa nini Yesu alipanga kukutana na wanafunzi wake? Ili kuwapa kazi hii yenye kusisimua: “Basi, nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.”​—Soma Mathayo 28:18-20.

2 Wanafunzi waliosikia maneno hayo ya Yesu wakawa sehemu ya kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza. Kazi kuu ya kutaniko hilo ilikuwa kuwasaidia watu wengi zaidi wawe wanafunzi wa Kristo. * Leo, kuna makumi ya maelfu ya makutaniko ya Wakristo wa kweli duniani kote, na kazi kuu ya makutaniko hayo bado ni ileile. Katika makala hii, tutachunguza maswali manne: Kwa nini kazi ya kufanya wanafunzi ni muhimu sana? Inahusisha nini? Je, Wakristo wote wanapaswa kushiriki katika kazi hiyo? Na kwa nini tunahitaji kuwa na subira tunapofanya kazi hiyo?

KWA NINI KAZI YA KUFANYA WANAFUNZI NI MUHIMU SANA?

3. Kulingana na Yohana 14:6 na 17:3, kwa nini kazi ya kufanya wanafunzi ni muhimu sana?

3 Kwa nini kazi ya kufanya wanafunzi ni muhimu sana? Kwa sababu ni wanafunzi wa Kristo tu wanaoweza kuwa rafiki za Mungu. Isitoshe, wale wanaomfuata Kristo huboresha maisha yao sasa na wana tumaini la kuishi milele wakati ujao. (Soma Yohana 14:6; 17:3.) Kwa hakika, Yesu ametukabidhi jukumu muhimu, hata hivyo hatutekelezi jukumu hilo kwa uwezo wetu wenyewe. Mtume Paulo alisema hivi kujihusu na kuhusu wale alioshirikiana nao kwa ukaribu: “Sisi ni wafanyakazi wenzi wa Mungu.” (1 Kor. 3:9) Hilo ni pendeleo zuri ajabu ambalo Yehova na Kristo wamewapa wanadamu wasio wakamilifu!

4. Tunajifunza nini kutokana na jambo ambalo Ivan na Matilde walijionea?

4 Kazi ya kufanya wanafunzi inaweza kutupatia shangwe nyingi sana. Mfikirie Ivan na Matilde mke wake, wanaoishi nchini Kolombia. Walimhubiria kijana anayeitwa Davier, ambaye aliwaambia hivi: “Ninatamani kufanya mabadiliko maishani mwangu, lakini ninashindwa.” Davier alikuwa mwanandondi wa kulipwa aliyetumia dawa za kulevya, aliyekunywa pombe kupita kiasi, na aliishi na rafiki yake wa kike anayeitwa Erika. Ivan anaeleza hivi: “Tulianza kumtembelea katika kijiji cha mbali alichoishi, na ilitulazimu kuendesha baiskeli zetu kwa saa nyingi katika barabara zenye matope mengi. Baada ya Erika kutambua kwamba tabia na mtazamo wa Davier ulikuwa ukibadilika, alijiunga na Davier kujifunza Biblia.” Baada ya muda, Davier aliacha kutumia dawa za kulevya, pombe, na kupigana ndondi. Pia, alifunga ndoa na Erika. Matilde anasema hivi: “Davier na Erika walipobatizwa mwaka wa 2016, tulikumbuka maneno ambayo Davier alizoea kusema, ‘Ninataka kubadilika, lakini ninashindwa.’ Tulishindwa kuzuia machozi yetu.” Bila shaka, sisi sote hufurahi sana tunapowasaidia watu kuwa wanafunzi wa Kristo.

KAZI YA KUFANYA WANAFUNZI INAHUSISHA NINI?

5. Taja hatua ya kwanza tunayohitaji kuchukua ili kufanya wanafunzi.

5 Hatua ya kwanza tunayohitaji kuchukua ili kufanya wanafunzi ni ‘kuwatafuta’ wale wenye mioyo inayofaa. (Mt. 10:11) Tunathibitisha kwamba sisi kwa kweli ni Mashahidi wa Yehova tunapowahubiria wote tunaokutana nao. Tunathibitisha kwamba sisi ni Wakristo wa kweli tunapotii amri ya Yesu ya kuhubiri.

6. Ni nini kinachoweza kutusaidia tufanikiwe katika huduma yetu?

6 Baadhi ya watu wanatamani kujifunza kweli za Biblia, lakini watu wengi tunaokutana nao huenda mwanzoni wakaonekana kuwa hawapendezwi. Huenda tukahitaji kuwachochea wavutiwe na kweli za Biblia. Ili tupate mafanikio katika huduma yetu, tunahitaji kujitayarisha vizuri. Chagua habari hususa zinazoweza kuwavutia wale utakaokutana nao. Kisha fikiria jinsi utakavyozungumzia habari hizo.

7. Unaweza kuanzishaje mazungumzo pamoja na mtu, na kwa nini unafikiri ni muhimu kumsikiliza na kumwonyesha heshima?

7 Kwa mfano, unaweza kumwambia hivi mwenye nyumba: “Ningependa kujua maoni yako kuhusu jambo fulani. Matatizo mengi tunayokabili leo yanawaathiri watu ulimwenguni pote. Je, unafikiri tunahitaji serikali moja tu itakayotawala dunia yote ili kuondoa matatizo yaliyopo duniani leo?” Kisha unaweza kuzungumzia Danieli 2:44. Au unaweza kumwambia jirani yako hivi: “Unafikiri siri ya kuwalea watoto wenye nidhamu ni nini? Ningependa kusikia maoni yako.” Kisha zungumzia Kumbukumbu la Torati 6:6, 7. Hata iwe utachagua kuzungumzia habari gani, wafikirie watu watakaokusikiliza. Wazia jinsi watakavyonufaika kwa kujifunza yale ambayo Biblia inafundisha hasa. Unapozungumza nao, ni muhimu kuwasikiliza na kuheshimu maoni yao. Kwa njia hiyo, utawaelewa vizuri zaidi, na itakuwa rahisi zaidi kwao kukusikiliza.

8. Kwa nini tunahitaji kujitahidi kuwarudia bila kuchoka watu wanaopendezwa na kweli za Biblia?

8 Kabla ya mtu kuamua kujifunza Biblia, huenda ukahitaji kutumia wakati na jitihada nyingi ili kumrudia tena na tena. Kwa nini? Kwa sababu huenda watu wasipatikane nyumbani tunapowarudia tena. Pia, huenda ukahitaji kurudi mara kadhaa kabla ya mwenye nyumba kuwa tayari kukubali kujifunza Biblia rasmi. Kumbuka, ni rahisi zaidi kwa mmea kukua unapomwagiliwa maji kwa ukawaida. Vivyo hivyo, ni rahisi kwa mtu anayependezwa na kweli za Biblia kumpenda Yehova na Kristo zaidi na zaidi kadiri tunavyozungumzia kwa ukawaida Neno la Mungu pamoja naye.

JE, WAKRISTO WOTE WANAPASWA KUSHIRIKI KATIKA KAZI HIYO?

Mashahidi ulimwenguni pote wanahusika katika kuwatafuta wanaostahili (Tazama fungu la 9 na 10) *

9-10. Kwa nini tunaweza kusema kwamba kila mhudumu Mkristo anahusika katika kuwatafuta wale wenye mioyo minyoofu?

9 Kila mhudumu Mkristo anahusika katika kuwatafuta watu wenye mioyo minyoofu. Tunaweza kulinganisha kazi hiyo na kutafuta mtoto aliyepotea. Jinsi gani? Fikiria mfano halisi wa mtoto mwenye umri wa miaka mitatu ambaye alipotea. Watu 500 hivi walifanya kazi ya kumtafuta. Mwishowe, saa 20 hivi baada ya mtoto huyo kupotea, mtu mmoja alimpata katika shamba la mahindi. Mtu huyo hakutaka kusifiwa kwa kumpata mtoto huyo. Alisema hivi: “Mamia ya watu walihusika kumtafuta.”

10 Watu wengi ni kama mtoto huyo. Wamepotea. Hawana tumaini lolote, hivyo wanahitaji msaada. (Efe. 2:12) Zaidi ya watu milioni nane wanashirikiana pamoja kuwatafuta watu hao wenye kustahili. Huenda wewe binafsi usipate mtu anayetaka kujifunza Biblia. Hata hivyo, huenda wahubiri wengine tunaohubiri pamoja nao katika eneo lilelile wakapata mtu anayetaka kujifunza kweli inayopatikana katika Neno la Mungu. Ndugu au dada anapopata mtu ambaye hatimaye anakuwa mwanafunzi wa Kristo, kila mtu aliyeshiriki kufanya kazi ya kutafuta ana sababu nzuri ya kushangilia.

11. Hata ikiwa huna mtu unayemfundisha Biblia, ni katika njia gani nyingine unaweza kushiriki katika kazi hiyo?

11 Hata ikiwa kwa sasa huna mtu unayemfundisha Biblia, unaweza kushiriki kufanya kazi hiyo katika njia nyingine. Kwa mfano, unaweza kuwakaribisha wapya kwa uchangamfu na kuwasaidia wanapokuja kwenye Jumba la Ufalme. Kwa njia hiyo, unaweza kuwafanya wasadiki kwamba upendo ndiyo sifa inayotutambulisha kuwa Wakristo wa kweli. (Yoh. 13:34, 35) Maelezo unayotoa mikutanoni, ingawa huenda yakawa mafupi, yanaweza kuwafundisha wapya kuzungumza kuhusu imani yao kwa unyoofu na heshima. Pia, unaweza kuhubiri pamoja na mhubiri mpya na kumsaidia kutumia Maandiko kuwafundisha watu. Ukifanya hivyo, utamfundisha kumwiga Kristo.​—Luka 10:25-28.

12. Je, tunahitaji kuwa na uwezo wa pekee ili kufanya wanafunzi? Eleza.

12 Hakuna yeyote miongoni mwetu anayepaswa kufikiri kwamba anahitaji kuwa na uwezo wa pekee ili kuwafundisha wengine kuwa wanafunzi wa Yesu. Kwa nini? Mfikirie Faustina, anayeishi nchini Bolivia. Hakujua kusoma alipoanza kushirikiana na Mashahidi wa Yehova. Lakini tangu wakati huo, amejifunza kusoma kwa kiwango fulani. Sasa amebatizwa, naye anapenda kuwafundisha wengine Biblia. Kwa kawaida, yeye hujifunza Biblia pamoja na watu watano kila juma. Ingawa Faustina hawezi kusoma vizuri kama wengi wa wanafunzi wake, amefanikiwa kuwasaidia watu sita kufikia hatua ya ubatizo.​—Luka 10:21.

13. Hata ikiwa tuna shughuli nyingi sana, ni zipi baadhi ya baraka tunazoweza kupata tunapofanya kazi ya kuwafundisha wengine Biblia?

13 Wakristo wengi wana shughuli nyingi sana wakijitahidi kushughulikia majukumu muhimu. Lakini bado wao hutenga wakati wa kuwafundisha watu Biblia, nao hupata shangwe nyingi kwa kufanya hivyo. Mfikirie Melanie. Hakuwa na mume, na alikuwa akimlea binti yake mwenye umri wa miaka minane huko Alaska. Pia, alifanya kazi ya wakati wote na alimtunza mzazi wake aliyekuwa na kansa. Melanie alikuwa ndiye Shahidi pekee katika mji wa mbali alioishi. Alizoea kusali ili apate nguvu za kukabiliana na baridi na kwenda kuhubiri kwa sababu alitamani sana kupata mtu ambaye alikuwa na hamu ya kujifunza Biblia. Hatimaye alikutana na Sara, ambaye alisisimka kujifunza kwamba Mungu ana jina la kibinafsi. Baada ya muda, Sara alikubali kujifunza Biblia. Melanie anasema hivi: “Kila Ijumaa jioni, nilihisi uchovu mwingi, lakini mimi na binti yangu tulinufaika tulipoenda kumfundisha Sara Biblia. Tulifurahia kufanya utafiti wa maswali ambayo Sara alituuliza, na tulifurahi sana alipoamua kuwa rafiki ya Yehova.” Sara alikabiliana na upinzani kwa ujasiri, akaacha kushirikiana na kanisa lake, na akabatizwa.

KWA NINI TUNAHITAJI KUWA NA SUBIRA TUNAPOFANYA WANAFUNZI?

14. (a) Kufanya wanafunzi ni kama kazi ya uvuvi jinsi gani? (b) Maneno ya Paulo yaliyo kwenye 2 Timotheo 4:1, 2 yanakuchocheaje?

14 Hata ikiwa unaona kwamba hupati matokeo mazuri katika huduma yako, usikate tamaa kuwatafuta wanafunzi wapya wa Biblia. Kumbuka kwamba Yesu alilinganisha kazi ya kufanya wanafunzi na uvuvi. Huenda wavuvi wakatumia saa nyingi kabla ya kunasa samaki. Kwa kawaida, wao hufanya kazi usiku sana au alfajiri na mapema, na nyakati nyingine wanalazimika kusafiri umbali mrefu. (Luka 5:5) Kama wavuvi hao, kwa subira baadhi ya wahubiri hutumia saa nyingi “kuvua watu” nyakati na mahali tofauti-tofauti. Kwa nini? Ili wajitahidi kuwafikia watu wengi zaidi. Kwa kawaida, wahubiri wanaoongeza jitihada huthawabishwa kwa sababu wao hukutana na watu wanaofurahishwa na ujumbe wetu. Je, unaweza kujitahidi kuhubiri wakati ambao ni rahisi zaidi kupata watu, au kuhubiri mahali ambapo ni rahisi zaidi kuwapata?​—Soma 2 Timotheo 4:1, 2.

Wasaidie wanafunzi wako kwa subira kufanya maendeleo ya kiroho (Tazama fungu la 15 na 16) *

15. Kwa nini tunahitaji kuwa na subira tunapowafundisha watu Biblia?

15 Kwa nini tunahitaji kuwa na subira tunapowafundisha watu Biblia? Sababu moja ni kwamba tunahitaji kufanya mengi zaidi ya kumsaidia mwanafunzi wa Biblia kujua na kupenda mafundisho yaliyo katika Biblia. Tunahitaji kumsaidia mwanafunzi kumjua na kumpenda Yehova, Mtungaji wa Biblia. Zaidi ya kumfundisha mwanafunzi mambo ambayo Yesu anatarajia wanafunzi wake wafanye, tunahitaji kumsaidia ajue jinsi ya kuishi kama Mkristo wa kweli. Tunapaswa kumsaidia kwa subira anapojitahidi kutumia kanuni za Biblia maishani mwake. Baadhi ya wanafunzi wanaweza kubadili tabia na njia yao ya kufikiri katika kipindi cha miezi michache tu; lakini wengine huchukua muda mrefu zaidi.

16. Umejifunza nini kutokana na simulizi la Raúl?

16 Mmishonari mmoja nchini Peru alijionea jambo fulani linaloonyesha jinsi ilivyo muhimu kuwa wenye subira. Anasema hivi: “Nilikuwa nimejifunza vitabu viwili na mwanafunzi mmoja wa Biblia anayeitwa Raúl. Lakini bado alikuwa na matatizo makubwa maishani mwake. Alikuwa na matatizo makubwa sana ya ndoa, alitumia lugha chafu, na watoto wake walishindwa kumheshimu kwa sababu ya tabia zake. Alihudhuria mikutano kwa ukawaida, hivyo niliendelea kumtembelea ili kumsaidia yeye na familia yake. Zaidi ya miaka mitatu tangu nilipokutana naye kwa mara ya kwanza, alistahili kubatizwa.”

17. Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

17 Yesu alituambia ‘twende tukafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.’ Ili kutimiza utume huo, kwa kawaida tunahitaji kuzungumza na watu ambao njia yao ya kufikiri ni tofauti kabisa na yetu, kutia ndani wale ambao hawashirikiani na dini yoyote au hawaamini kwamba kuna Mungu. Katika makala inayofuata, tutazungumzia jinsi tunavyoweza kuwahubiria habari njema watu wa malezi tofauti-tofauti.

WIMBO 68 Kupanda Mbegu ya Ufalme

^ fu. 5 Kutaniko la Kikristo lina kazi moja kuu​—kuwasaidia watu kuwa wanafunzi wa Kristo. Makala hii inatoa mapendekezo yanayofaa yatakayotusaidia kutekeleza kazi hiyo tuliyopewa.

^ fu. 2 UFAFANUZI WA MANENO: Wanafunzi wa Kristo hufanya mengi zaidi ya kujifunza mambo ambayo Yesu alifundisha. Wao hutumia maishani mambo wanayojifunza. Nao hujitahidi kufuata kwa ukaribu kadiri wawezavyo hatua za Yesu, au kielelezo chake.​—1 Pet. 2:21.

^ fu. 52 MAELEZO YA PICHA: Mwanamume anayeenda likizo anakubali kuchukua machapisho kutoka kwa Mashahidi wa Yehova kwenye uwanja wa ndege. Baadaye, akiwa likizoni, anawaona Mashahidi wengine wakiwa katika mahubiri ya hadharani. Baada ya kurudi kutoka likizo, wahubiri wanamtembelea nyumbani kwake.

^ fu. 54 MAELEZO YA PICHA: Mwanamume huyo anakubali kujifunza Biblia. Hatimaye, anastahili kubatizwa.