Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 28

Uwe na Hakika Kwamba Umeipata Kweli

Uwe na Hakika Kwamba Umeipata Kweli

“Endelea kufuata mambo uliyojifunza na uliyoshawishiwa kuamini.”—2 TIM. 3:14.

WIMBO 56 Fanya Kweli Iwe Njia Yako ya Maisha

MUHTASARI *

1. Neno “kweli” linamaanisha nini?

“ULIPATAJE kweli?” “Je, ulilelewa katika kweli?” “Umekuwa katika kweli kwa muda gani?” Huenda umewahi kuulizwa maswali hayo, au huenda umewahi kuwauliza wengine. Neno “kweli” linamaanisha nini? Kwa ujumla, tunalitumia kufafanua mambo tunayoamini, njia yetu ya ibada, na njia yetu ya maisha. Mtu aliye “katika kweli” anajua mambo ambayo Biblia inafundisha, na anaishi kulingana na kanuni za Biblia. Hivyo, anawekwa huru kutokana na mafundisho ya uwongo ya kidini na anafurahia maisha bora zaidi ambayo mtu asiye mkamilifu anaweza kuwa nayo.—Yoh. 8:32.

2. Kulingana na Yohana 13:34, 35, ni jambo gani ambalo mwanzoni huenda likamvuta mtu katika kweli?

2 Ni jambo gani ambalo mwanzoni lilikuvuta katika kweli? Huenda ni mwenendo mzuri wa watu wa Yehova. (1 Pet. 2:12) Au huenda ni upendo wao kwa wengine. Watu wengi wamejionea upendo huo walipohudhuria mkutano kwa mara ya kwanza, na ndilo jambo wanalokumbuka kuliko chochote kilichosemwa jukwaani. Jambo hilo halishangazi kwa sababu Yesu alisema kwamba wanafunzi wake wangetambuliwa kwa upendo walio nao. (Soma Yohana 13:34, 35.) Lakini mengi zaidi yanahitajiwa ili mtu awe na imani yenye nguvu.

3. Ni nini kinachoweza kutokea ikiwa imani yetu kwa Mungu inategemea tu upendo wa Kikristo unaoonyeshwa na ndugu na dada zetu?

3 Imani yetu inapaswa kutegemea mengi zaidi ya upendo wa Kikristo ulio miongoni mwa watu wa Mungu. Kwa nini? Tuseme kwamba mwamini mwenzako, au hata mzee wa kutaniko au painia anafanya dhambi nzito. Au vipi ikiwa ndugu au dada anafanya jambo linalokuumiza? Au labda mtu fulani anakuwa mwasi-imani, akisisitiza kwamba sisi hatuna kweli. Hali hizo zikitokea, je, utakwazika na kuacha kumtumikia Yehova? Somo ni hili: Ikiwa utajenga imani yako kwa Mungu kwa kutegemea tu mambo ambayo watu wengine wanafanya, badala ya kuijenga kwa kutegemea uhusiano wako wa kibinafsi pamoja na Yehova, basi imani yako haitakuwa na nguvu. Unapojenga nyumba yako ya imani, hupaswi tu kujenga kwa kutumia vifaa vyepesi kama vile hisia, lakini unapaswa kutumia pia vifaa vigumu kama vile habari za uhakika na hoja zenye nguvu. Unahitaji kujithibitishia mwenyewe kwamba Biblia inafundisha kweli kumhusu Yehova.—Rom. 12:2.

4. Kulingana na Mathayo 13:3-6, 20, 21, baadhi ya watu huathirikaje imani yao inapojaribiwa?

4 Yesu alisema kwamba baadhi ya watu wangeikubali kweli “kwa shangwe,” lakini imani yao ingenyauka baada ya kujaribiwa. (Soma Mathayo 13:3-6, 20, 21.) Huenda hawakujua kwamba kuwa mfuasi wa Yesu kungehusisha changamoto na hali ngumu mbalimbali. (Mt. 16:24) Au huenda walifikiri kwamba kuwa Mkristo kungemaanisha kuishi maisha yasiyo na matatizo yoyote, maisha yaliyojaa baraka tu, yasiyo na changamoto zozote. Lakini katika ulimwengu wa leo, changamoto haziwezi kukosekana. Hali zinaweza kubadilika na kusababisha shangwe yetu ipungue kwa kipindi fulani.—Zab. 6:6; Mhu. 9:11.

5. Ndugu na dada zetu wengi wanaonyeshaje kuwa wana uhakika kwamba wana kweli?

5 Ndugu na dada zetu wengi wameonyesha kuwa wana uhakika kwamba wana kweli. Jinsi gani? Imani yao haiyumbi hata mwamini mwenzao anapowaumiza kihisia au kujihusisha na mwenendo usio wa Kikristo. (Zab. 119:165) Kila mara wanapokabili jaribu, imani yao huzidi kuimarika, badala ya kudhoofika. (Yak. 1:2-4) Unaweza kujengaje imani kama hiyo yenye nguvu?

JIPATIE “UJUZI SAHIHI WA MUNGU”

6. Wanafunzi wa karne ya kwanza walijenga imani yao juu ya nini?

6 Wanafunzi wa karne ya kwanza walijenga imani yao kwa kutegemea ujuzi wa Maandiko na mafundisho ya Yesu Kristo, yaani, “kweli ya habari njema.” (Gal. 2:5) Kweli hiyo ni mafundisho yote ya Kikristo, kutia ndani habari za uhakika kuhusu dhabihu ya fidia ya Yesu na ufufuo wake. Mtume Paulo alikuwa na uhakika kwamba mafundisho hayo yalikuwa ya kweli. Kwa nini? Kwa sababu alitumia Maandiko kuthibitisha “kwa marejeo kwamba ilikuwa lazima Kristo ateseke na kufufuliwa kutoka kwa wafu.” (Mdo. 17:2, 3) Wanafunzi wa karne ya kwanza waliyakubali mafundisho hayo na walitegemea roho takatifu iwasaidie kulielewa Neno la Mungu. Walijisadikishia wenyewe kwamba mafundisho hayo yalitegemea Maandiko. (Mdo. 17:11, 12; Ebr. 5:14) Hawakujenga imani yao kwa kutegemea tu hisia, na hawakumtumikia Yehova eti kwa sababu tu walifurahia kushirikiana na waamini wenzao. Badala yake, walijenga imani yao juu ya msingi wa “ujuzi sahihi wa Mungu.”—Kol. 1:9, 10.

7. Imani yetu katika kweli za Biblia itatusaidiaje?

7 Kweli za Neno la Mungu hazibadiliki. (Zab. 119:160) Kwa mfano, hazibadiliki mwamini mwenzetu anapotukosea au anapofanya dhambi nzito. Na hazibadiliki tunapokumbwa na matatizo. Hivyo, tunahitaji kuyajua vizuri mafundisho ya Biblia na kusadiki kabisa kwamba ni ya kweli. Imani yetu thabiti iliyojengwa kwa kutegemea kweli za Biblia itatusaidia tusitetereke wakati wa majaribu, kama tu ambavyo nanga inaweza kuifanya mashua isipoteze mwelekeo wakati wa dhoruba kali. Unaweza kuimarishaje usadikisho wako kwamba una kweli?

‘SHAWISHIWA KUAMINI’

8. Kulingana na 2 Timotheo 3:14, 15, ni nini kilichomsaidia Timotheo awe na uhakika kwamba alikuwa ameipata kweli?

8 Timotheo alikuwa na uhakika kwamba alikuwa na kweli. Kwa nini alikuwa na uhakika huo? (Soma 2 Timotheo 3:14, 15.) Mama na nyanya yake ndio waliokuwa wa kwanza kumfundisha “maandishi matakatifu.” Lakini hapana shaka kwamba yeye mwenyewe pia alitumia wakati na nguvu kujifunza maandishi hayo. Kwa sababu hiyo, ‘alishawishiwa kuamini’ kwamba yalikuwa na kweli. Baadaye, Timotheo, mama yake, na nyanya yake walijifunza mafundisho ya Kikristo. Hapana shaka kwamba Timotheo alipendezwa na upendo ulioonyeshwa na wafuasi wa Yesu, na alitamani sana kushirikiana na ndugu na dada zake wa kiroho na kuwasaidia. (Flp. 2:19, 20) Hata hivyo, imani yake haikujengwa kwa kutegemea jinsi alivyohisi kuelekea wanadamu wenzake, bali ilitegemea habari hakika zilizomfanya azidi kumkaribia Yehova. Ni lazima wewe pia ujisadikishie mwenyewe mambo unayojifunza kumhusu Yehova katika usomaji wako wa Biblia.

9. Unahitaji kujithibitishia kweli gani tatu za msingi?

9 Unahitaji kujithibitishia mwenyewe angalau kweli hizi tatu za msingi. Kwanza, unahitaji kusadiki kwamba Yehova ni Muumba wa vitu vyote. (Kut. 3:14, 15; Ebr. 3:4; Ufu. 4:11) Pili, ni lazima ujithibitishie mwenyewe kwamba Biblia ni ujumbe wa Mungu kwa wanadamu. (2 Tim. 3:16, 17) Na tatu, unahitaji kuwa na uhakika kwamba Yehova ana kikundi cha watu waliopangwa ambao wanamwabudu chini ya uongozi wa Kristo na kwamba kikundi hicho ni Mashahidi wa Yehova. (Isa. 43:10-12; Yoh. 14:6; Mdo. 15:14) Huhitaji kujua kila kitu katika Biblia ili ujithibitishie kweli hizo za msingi. Lengo lako linapaswa kuwa kutumia ‘nguvu zako za kufikiri’ ili kuimarisha usadikisho wako kwamba una kweli.—Rom. 12:1.

UWE TAYARI KUWASADIKISHA WENGINE

10. Zaidi ya kuijua kweli, tunahitaji kuwa na uwezo wa kufanya nini?

10 Baada ya kujithibitishia kweli hizo tatu za msingi kumhusu Mungu, Biblia, na watu wa Mungu, unahitaji kuwa na uwezo wa kutumia Maandiko ili kuwathibitishia wengine kweli hizo. Kwa nini? Kwa sababu tukiwa Wakristo, tuna jukumu la kuwafundisha wale wanaotusikiliza kweli ambazo tumejifunza. * (1 Tim. 4:16) Na tunapojitahidi kuwasadikisha wengine kuhusu kweli za Biblia, tunaimarisha uhakika wetu katika kweli hizo.

11. Mtume Paulo alituwekea mfano gani akiwa mwalimu?

11 Mtume Paulo alipokuwa akiwafundisha watu, ‘aliwashawishi kumhusu Yesu kwa kutumia Sheria ya Musa na pia Manabii.’ (Mdo. 28:23) Tunaweza kumwigaje Paulo tunapowafundisha wengine kweli? Ni lazima tufanye mengi zaidi ya kutaja tu habari fulani. Ni lazima tuwasaidie wanafunzi wetu wa Biblia wajifunze na kutafakari kwa makini mambo wanayosoma katika Maandiko wanapoendelea kumkaribia Yehova. Tunataka waikubali kweli, si kwa sababu wanatupenda au kutuheshimu, bali kwa sababu wamejihakikishia wenyewe kwamba mambo wanayojifunza ni mambo ya kweli kumhusu Mungu wetu mwenye upendo.

Wazazi, wasaidieni watoto wenu wasitawishe imani kwa kuwafundisha “mambo mazito ya Mungu” (Tazama fungu la 12 na 13) *

12-13. Wazazi wanaweza kuwasaidiaje watoto wao waendelee kubaki katika kweli?

12 Wazazi, bila shaka mnataka watoto wenu waendelee kubaki katika kweli. Huenda ukahisi kwamba ikiwa wanashirikiana na marafiki wazuri kutanikoni, basi watafanya maendeleo mazuri ya kiroho. Hata hivyo, ikiwa unataka watoto wako wawe na uhakika kwamba wana kweli, wanahitaji mengi zaidi ya kuwa tu na marafiki wazuri. Wanahitaji kuwa na uhusiano wa kibinafsi pamoja na Mungu na kusadiki kwamba mambo ambayo Biblia inafundisha ni ya kweli.

13 Ili wazazi wawafundishe watoto wao ukweli kumhusu Mungu, ni lazima waweke mfano mzuri kwa kuwa wanafunzi wazuri wa Biblia. Ni lazima watenge wakati wa kutafakari kuhusu mambo wanayojifunza. Kisha wataweza kuwafundisha watoto wao kufanya vivyo hivyo. Wanahitaji kuwafundisha watoto wao jinsi ya kutumia vifaa vya kujifunzia Biblia, kama tu wanavyowafundisha wanafunzi wao wa Biblia. Ikiwa watafanya hivyo, watawasaidia watoto wao wampende Yehova na kuitumaini njia anayotumia kuandaa chakula cha kiroho, yaani, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45-47) Wazazi, msiridhike tu kuwafundisha watoto wenu kweli za msingi za Biblia. Wasaidieni wasitawishe imani yenye nguvu kwa kuwafundisha kuhusu “mambo mazito ya Mungu” kwa kiwango kinacholingana na umri na uwezo wao.—1 Kor. 2:10.

JIFUNZE UNABII WA BIBLIA

14. Kwa nini tunapaswa kujifunza unabii wa Biblia? (Tazama pia sanduku “ Je, Unaweza Kufafanua Unabii Huu?”)

14 Unabii wa Biblia ni sehemu muhimu ya Neno la Mungu inayotusaidia tujenge imani yenye nguvu katika Yehova. Ni unabii gani mbalimbali ambao umeimarisha imani yako? Huenda ukataja unabii kuhusu “siku za mwisho.” (2 Tim. 3:1-5; Mt. 24:3, 7) Lakini ni unabii gani mwingine uliotimia unaoweza kuimarisha imani yako? Kwa mfano, je, unaweza kueleza jinsi unabii uliotajwa kwenye Danieli sura ya 2 au Danieli sura ya 11 ulivyotimia na unavyoendelea kutimia? * Ikiwa imani yako inategemea msingi imara wa Neno la Mungu, basi haiwezi kuvunjika. Fikiria mfano wa ndugu zetu ambao walikabili mateso makali sana nchini Ujerumani wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu. Ingawa hawakuelewa kikamili unabii kuhusu siku za mwisho, walikuwa na imani yenye nguvu katika Neno la Mungu.

Kujifunza Biblia, kutia ndani unabii uliomo, kunaweza kutupatia uhakika katika nyakati za majaribu (Tazama fungu la 15 hadi 17) *

15-17. Kujifunza Biblia kuliwaimarishaje ndugu zetu walipoteswa na Wanazi?

15 Chini ya utawala wa Nazi nchini Ujerumani, maelfu ya ndugu na dada zetu walipelekwa kwenye kambi za mateso. Hitler na ofisa mashuhuri aliyeitwa Heinrich Himmler waliwachukia Mashahidi wa Yehova. Kulingana na dada mmoja, Himmler alikiambia hivi kikundi kimoja cha dada zetu kwenye kambi fulani ya mateso: “Huenda Yehova wenu anatawala mbinguni, lakini hapa duniani ni sisi tunaotawala! Tutawaonyesha ni nani atakayeendelea kuwepo, ninyi au sisi!” Ni nini kilichowasaidia watu wa Yehova waendelee kuwa waaminifu?

16 Wanafunzi hao wa Biblia walijua kwamba Ufalme wa Mungu ulikuwa umeanza kutawala mwaka wa 1914. Hawakushangazwa na upinzani mkali waliokabili. Licha ya hayo, watu wa Yehova walisadiki kwamba hakuna serikali ya mwanadamu inayoweza kuzuia kusudi la Mungu lifanikiwe. Hitler hangeweza kufagilia mbali ibada ya kweli au kusimamisha serikali ambayo ingezidi nguvu Ufalme wa Mungu. Ndugu zetu walikuwa na uhakika kwamba kwa njia moja au nyingine, utawala wa Hitler ungefikia mwisho wake.

17 Uhakika ambao ndugu na dada hao walikuwa nao haukuwa wa bure. Muda mrefu haukupita, utawala wa Nazi ulianguka, na Heinrich Himmler—yule ofisa aliyesema “hapa duniani ni sisi tunaotawala”—alikuwa akikimbia ili kuokoa uhai wake. Wakati huo alikutana na kumtambua Ndugu Lübke, ambaye alikuwa mfungwa hapo awali. Akiwa ameshuka moyo kabisa, Himmler alimuuliza hivi Ndugu Lübke: “Mwanafunzi wa Biblia, ni nini kinachofuata?” Ndugu Lübke alimweleza Himmler kwamba Mashahidi wa Yehova hawakuwa na shaka kwamba utawala wa Nazi ungeshindwa na kwamba wao wangeokolewa. Himmler—mwanamume ambaye hapo awali alikuwa na mengi ya kusema kuwahusu Mashahidi wa Yehova—hakuwa na chochote cha kusema. Muda mfupi baadaye, alijiua. Tunajifunza nini? Kujifunza Biblia, kutia ndani unabii uliomo, kunaweza kutusaidia tujenge imani katika Mungu isiyoweza kuvunjika, na kutupatia uhakika katika nyakati za majaribu.—2 Pet. 1:19-21.

18. Kama inavyoonyeshwa katika Yohana 6:67, 68, kwa nini tunahitaji “ujuzi sahihi na utambuzi kamili” ambao Paulo alizungumzia?

18 Kila mmoja wetu anapaswa kuonyesha upendo, sifa inayowatambulisha Wakristo wa kweli. Lakini pia tunahitaji “ujuzi sahihi na utambuzi kamili.” (Flp. 1:9) Vinginevyo tunaweza kuathiriwa “na kila upepo wa fundisho kwa udanganyifu wa watu,” kutia ndani waasi-imani. (Efe. 4:14) Wanafunzi wengi wa karne ya kwanza walipoacha kumfuata Yesu, mtume Petro alieleza jinsi alivyosadiki kabisa kwamba Yesu alikuwa na “maneno ya uzima wa milele.” (Soma Yohana 6:67, 68.) Hata ingawa wakati huo Petro hakuyaelewa kikamili maneno hayo, aliendelea kuwa mshikamanifu kwa sababu alikuwa ameelewa ukweli kumhusu Kristo. Wewe pia unaweza kuimarisha usadikisho wako kuhusu mambo ambayo Biblia inafundisha. Ukifanya hivyo imani yako itaendelea kuwa imara haidhuru kitakachotokea, na utawasaidia wengine pia wajenge imani yenye nguvu.—2 Yoh. 1, 2.

WIMBO 72 Kutangaza Ukweli wa Ufalme

^ fu. 5 Makala hii itatusaidia kuthamini mafundisho ya kweli ya Neno la Mungu. Pia, itazungumzia jinsi tunavyoweza kuimarisha usadikisho wetu kwamba mambo tunayoamini ni kweli.

^ fu. 10 Ili upate msaada wa jinsi ya kujadiliana na wengine kuhusu kweli za msingi za Biblia, tazama mfululizo wenye kichwa “Mazungumzo Pamoja na Jirani,” kwenye gazeti Mnara wa Mlinzi, kuanzia mwaka wa 2010 hadi 2015. Habari zinazozungumziwa ni kama vile “Je, Yesu Ni Mungu?,” “Ufalme wa Mungu Ulianza Kutawala Lini?,” na “Je, Mungu Anawaadhibu Watu Katika Moto wa Mateso?

^ fu. 14 Kwa habari zaidi kuhusu unabii huo, tazama gazeti Mnara wa Mlinzi la Juni 15, 2012, na la Mei 2020.

^ fu. 60 MAELEZO YA PICHA: Wakati wa ibada ya familia, wazazi wanajifunza na watoto wao unabii wa Biblia kuhusu dhiki kuu.

^ fu. 62 MAELEZO YA PICHA: Wakati wa dhiki kuu, familia hiyo haitashangazwa na mambo yanayotendeka.