Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 28

Epuka Kuchochea Mashindano—Endeleza Amani

Epuka Kuchochea Mashindano—Endeleza Amani

“Tusiwe tunajisifu, tusichochee mashindano juu yetu, wala tusioneane wivu.”​—GAL. 5:26.

WIMBO 101 Kufanya Kazi Pamoja kwa Umoja

MUHTASARI *

1. Roho ya mashindano inaweza kuwaathirije watu?

KATIKA ulimwengu wa leo, watu wengi wana ubinafsi unaochochewa na roho ya mashindano. Mfanyabiashara anaweza kutumia mbinu zinazoweza kuwaumiza wengine ili ajinufaishe. Mwanariadha anaweza kumuumiza kimakusudi mwanariadha wa timu nyingine ili ashinde. Mwanafunzi anaweza kufanya udanganyifu kwenye mtihani ili afaulu na kwenda kusoma kwenye chuo mashuhuri. Tukiwa Wakristo, tunatambua kwamba matendo hayo ni dhambi; ni sehemu ya “matendo ya mwili.” (Gal. 5:19-21) Hata hivyo, je, inawezekana kwamba huenda baadhi ya watumishi wa Yehova wakawa wanachochea roho ya mashindano kutanikoni bila hata kutambua? Ni muhimu kujiuliza swali hilo kwa sababu roho ya mashindano inaweza kuathiri umoja wa undugu wetu.

2. Tutazungumzia nini katika makala hii?

2 Katika makala hii, tutazungumzia sifa mbaya zinazoweza kutufanya tuchochee roho ya mashindano kati yetu. Pia, tutachunguza mifano ya wanaume na wanawake waaminifu katika nyakati za Biblia ambao hawakuruhusu roho ya mashindano iwatawale. Kwanza, acheni tuzungumzie jinsi tunavyoweza kuchunguza nia yetu.

CHUNGUZA NIA YAKO

3. Tunapaswa kujiuliza maswali gani?

3 Ni vizuri kuchunguza nia yetu mara kwa mara. Tunaweza kujiuliza hivi: ‘Je, ninapima thamani yangu kwa kujilinganisha na wengine? Je, ninachochewa na tamaa ya kujiona kuwa bora kuliko wengine katika kila jambo ninalofanya, au kwamba ninafanya vizuri zaidi kuliko ndugu au dada fulani hususa? Au je, ninajitahidi kufanya yote ninayoweza ili kumpa Yehova kilicho bora?’ Kwa nini tunapaswa kujiuliza maswali hayo? Ona yale ambayo Neno la Mungu linasema.

4. Kwa nini tunapaswa kuepuka kujilinganisha na wengine kama inavyotajwa kwenye Wagalatia 6:3, 4?

4 Biblia inatuhimiza tuepuke kujilinganisha na wengine. (Soma Wagalatia 6:3, 4.) Kwa nini? Kwa upande mmoja, ikiwa tunafikiri kwamba tunafanya vizuri kuliko ndugu zetu, huenda tukawa na kiburi. Kwa upande mwingine, ikiwa tutajilinganisha na wengine kwa njia isiyofaa, huenda tukavunjika moyo. Vyovyote vile, ikiwa tutakuwa tukifikiria kwa njia hizo, hatutakuwa tukionyesha utimamu wa akili. (Rom. 12:3) Katerina, * dada anayeishi nchini Ugiriki alisema hivi: “Nilizoea kujilinganisha na wengine walioonekana kuwa warembo kuliko mimi, wenye matokeo zaidi katika huduma, na wenye uwezo mkubwa zaidi wa kuanzisha urafiki. Matokeo ni kwamba nilijihisi sina thamani.” Tunapaswa kukumbuka kwamba Yehova alituvuta kwake, si kwa sababu sisi ni warembo, tuna ufasaha wa kuzungumza, au tunapendwa na watu wengi, bali kwa sababu tunampenda Yehova na kumsikiliza Mwana wake.—Yoh. 6:44; 1 Kor. 1:26-31.

5. Unajifunza nini kutokana na kisa cha Ndugu Hyun?

5 Swali lingine tunaloweza kujiuliza ni; ‘Je, ninajulikana kuwa mfanya amani, au mara nyingi ninajikuta sielewani na watu?’ Fikiria kisa cha Ndugu Hyun, anayeishi nchini Korea Kusini. Wakati fulani aliwaona baadhi ya wale waliokuwa na mapendeleo ya utumishi kuwa washindani wake. Anasema hivi: “Niliwachambua ndugu hao na mara nyingi sikukubaliana na mambo waliyosema.” Matokeo yalikuwaje? Anakiri hivi: “Mtazamo wangu ulisababisha mgawanyiko kutanikoni.” Baadhi ya marafiki wa Hyun walimsaidia kutambua tatizo lake. Hyun alifanya mabadiliko yaliyohitajika na sasa anatumikia akiwa mzee aliye mfano mzuri. Tukitambua kwamba tuna mwelekeo wa kuchochea mashindano badala ya kuendeleza amani, ni lazima tuchukue hatua.

EPUKA KUJISIFU NA KUWA MWENYE WIVU

6. Kulingana na Wagalatia 5:26, ni sifa gani mbaya zinazochochea roho ya mashindano?

6 Soma Wagalatia 5:26. Ni sifa gani mbaya zinazoweza kuchochea roho ya mashindano? Sifa moja ni kujisifu. Mtu anayejisifu ana kiburi na ni mbinafsi. Sifa nyingine mbaya ni wivu. Mtu mwenye wivu si kwamba tu anataka kitu ambacho mtu mwingine anacho, bali anataka pia kumnyang’anya kitu hicho. Kwa kweli, wivu ni aina ya chuki. Bila shaka, tunataka kuziepuka sifa hizo mbaya kama ukoma!

7. Tunaweza kutumia mfano gani kuonyesha athari zinazosababishwa na kujisifu na wivu?

7 Kujisifu na wivu ni sifa mbaya zinazoweza kulinganishwa na mchwa wanaokula paa la nyumba. Hata kama nyumba inaonekana ni nzuri kadiri gani, ikiwa inaendelea kuliwa na mchwa hatimaye itaanguka. Vivyo hivyo, mtu anaweza kuendelea kumtumikia Yehova kwa muda fulani. Lakini ikiwa ana mwelekeo wa kujisifu na wivu, ataanguka kwa kishindo! (Met. 16:18) Ataacha kumtumikia Yehova na atajiumiza yeye mwenyewe na wengine. Hata hivyo, tunaweza kujilindaje dhidi ya kujisifu na kuwa wenye wivu?

8. Tunaweza kushindaje mwelekeo wa kujisifu?

8 Tunaweza kushinda sifa mbaya ya kujisifu kwa kuendelea kukumbuka shauri la mtume Paulo kwa Wafilipi: “Msifanye jambo lolote kwa ugomvi au kwa kujisifu, bali kwa unyenyekevu mwaone wengine kuwa bora kuliko ninyi.” (Flp. 2:3) Ikiwa tutawaona wengine kuwa bora kuliko sisi, hatutashindana na wale ambao huenda wana vipawa au uwezo mkubwa kuliko sisi. Badala yake, tutafurahi pamoja nao, hasa ikiwa wanatumia uwezo wao kwenye utumishi wa Yehova ili kumsifu. Na ikiwa ndugu na dada zetu walio na vipawa wanafuata ushauri wa mtume Paulo, wataweza kuona sifa nzuri tulizo nazo. Matokeo ni kwamba, sisi sote tutaendeleza amani na umoja kutanikoni.

9. Tunaweza kushindaje mwelekeo tulio nao wa kuwa na wivu?

9 Tunaweza kushinda mwelekeo tulio nao wa kuwa na wivu kwa kusitawisha kiasi, yaani, kwa kutambua mipaka yetu. Ikiwa tuna sifa ya kiasi, hatutajaribu kuthibitisha kwamba tuna vipawa au uwezo zaidi kuliko wengine. Badala yake, tutajitahidi kujifunza kutoka kwa wale walio na uwezo kuliko sisi. Kwa mfano, tuseme ndugu ni msemaji mzuri wa hotuba za watu wote. Tunaweza kumuuliza jinsi anavyotayarisha hotuba zake. Ikiwa dada ni mpishi mzuri, tunaweza kumwomba mapendekezo yatakayotusaidia kuboresha upishi wetu. Ikiwa kijana Mkristo hafaulu kuanzisha urafiki kwa urahisi, anaweza kuomba msaada kwa mtu mwingine ambaye ana uwezo wa kuanzisha urafiki kwa urahisi. Ikiwa tutafanya hivyo, tutaepuka kuwa na wivu na tutaboresha uwezo wetu wenyewe.

JIFUNZE KUTOKANA NA MIFANO ILIYO KWENYE BIBLIA

Kwa sababu alikuwa mnyenyekevu, Gideoni alidumisha amani pamoja na watu wa Efraimu (Tazama fungu la 10 hadi 12)

10. Gideoni alikabili changamoto gani?

10 Fikiria tukio lililomhusisha Gideoni, aliyekuwa wa kabila la Manase, na watu wa kabila la Efraimu. Gideoni na wanaume wake 300 walikuwa wamepata ushindi mkubwa kwa msaada wa Yehova, jambo ambalo wangeweza kujivunia sana. Watu wa Efraimu walikutana na Gideoni, si kwa sababu walitaka kumpongeza, bali kumshutumu. Inaelekea walikuwa wamekasirika kwa sababu Gideoni hakuwaita tangu mwanzo wajiunge naye katika vita dhidi ya maadui wa Mungu. Wanaume hao walikazia fikira zaidi kulinda heshima ya kabila lao, hivi kwamba walikosa kukazia fikira jambo kuu—Gideoni alikuwa ametoka tu kusaidia kulitukuza jina la Yehova na kuwalinda watu Wake.—Amu. 8:1.

11. Gideoni alishughulikaje na watu wa Efraimu?

11 Kwa unyenyekevu, Gideoni aliwaambia hivi watu wa Efraimu: “Mimi nimefanya nini nikilinganishwa nanyi?” Kisha akawapa mfano hususa wa jinsi Yehova alivyokuwa amewabariki. Matokeo ni kwamba “hasira yao ikapoa.” (Amu. 8:2, 3) Gideoni alikuwa tayari kujinyenyekeza ili kudumisha amani miongoni mwa watu wa Mungu.

12. Tunajifunza nini kutokana na mfano wa Waefraimu na Gideoni?

12 Tunaweza kujifunza nini kutokana na simulizi hilo? Kutokana na mfano wa Waefraimu, tunajifunza kwamba hatupaswi kukazia sana fikira kulinda heshima yetu kuliko kumtukuza Yehova. Tukiwa vichwa vya familia na wazee kutanikoni, tunaweza kujifunza jambo fulani kutoka kwa Gideoni. Ikiwa mtu fulani atakasirika kwa sababu ya jambo fulani tulilofanya, tunaweza kujitahidi kuelewa kwa nini mtu huyo alikasirika. Pia, tunaweza kumpongeza kwa mambo mazuri aliyofanya. Ili kufanya hivyo, tunahitaji kuwa wanyenyekevu hasa ikiwa ni wazi kwamba mtu huyo ndiye aliyekosea. Ni muhimu zaidi kurudisha amani kuliko kujitetea kwamba hatuna makosa.

Kwa sababu alimtumaini Yehova arekebishe mambo, Hana alipata tena amani ya moyoni (Tazama fungu la 13 na 14)

13. Hana alikabili changamoto gani, naye aliishindaje?

13 Fikiria pia mfano wa Hana. Alikuwa ameolewa na Mlawi aliyeitwa Elkana ambaye alimpenda sana. Elkana alikuwa na mke mwingine aliyeitwa Penina. Elkana alimpenda Hana zaidi kuliko Penina; hata hivyo, “Penina alikuwa na watoto, lakini Hana hakuwa na watoto.” Kwa sababu hiyo, Penina alimdhihaki “daima Hana ili kumkasirisha.” Hana alitendaje? Hana aliumia sana. “Alilia na kushindwa kula.” (1 Sam. 1:2, 6, 7) Hata hivyo, Biblia haisemi popote kwamba Hana alijaribu kulipiza kisasi. Badala yake, alimmiminia Yehova moyo wake na kutumaini kwamba Yehova angerekebisha mambo. Je, mtazamo wa Penina kumwelekea Hana ulibadilika? Biblia haisemi. Lakini tunajua kwamba, Hana alipata tena amani ya moyoni na kuidumisha. “Uso wake haukuwa na huzuni tena.”—1 Sam. 1:10, 18.

14. Tunajifunza nini kutokana na mfano wa Hana?

14 Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano Hana? Ikiwa mtu fulani anajaribu kushindana na wewe kwa njia fulani, kumbuka kwamba unaweza kudhibiti hali hiyo. Usijiruhusu uvutwe na kuingia kwenye mashindano. Badala ya kulipa uovu kwa uovu, jitahidi kufanya amani na mtu huyo. (Rom. 12:17-21) Hata ikiwa hataitikia vizuri, utadumisha amani yako ya moyoni.

Kwa sababu walitambua kwamba Yehova alikuwa akibariki kazi yao, Apolo na Paulo hawakushindana (Tazama fungu la 15 hadi 18)

15. Apolo na Paulo walifanana katika mambo gani?

15 Mwishowe, fikiria mambo tunayoweza kujifunza kutokana na mfano wa mwanafunzi Apolo na mtume Paulo. Wote wawili walikuwa wanayajua vizuri sana Maandiko, wote wawili walikuwa walimu bora na walijulikana sana. Wote wawili walikuwa wamewasaidia watu wengi kuwa wanafunzi. Lakini hakuna aliyemwonea wivu mwenzake.

16. Unaweza kumfafanuaje Apolo?

16 Apolo alikuwa “mzaliwa wa Aleksandria,” jiji lililokuwa kitovu cha elimu katika karne ya kwanza. Inaonekana kwamba alikuwa msemaji mzuri na alikuwa na “ujuzi mwingi wa Maandiko.” (Mdo. 18:24) Apolo alipokuwa kwenye jiji la Korintho, baadhi ya watu kutanikoni walionyesha wazi kwamba walimpendelea zaidi kuliko ndugu wengine, kutia ndani Paulo. (1 Kor. 1:12, 13) Je, Apolo alichochea mtazamo huo ambao ungewagawanya watu? Hatuwezi kumwazia akifanya hivyo. Isitoshe, muda fulani baada ya Apolo kuondoka Korintho, Paulo alimhimiza arudi tena huko. (1 Kor. 16:12) Paulo asingefanya hivyo ikiwa angehisi kwamba Apolo alikuwa analigawa kutaniko. Ni wazi kwamba Apolo alitumia vipawa vyake kwa njia nzuri, yaani, kutangaza habari njema na kuwaimarisha ndugu zake. Pia, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Apolo alikuwa mtu mnyenyekevu. Kwa mfano, Biblia haionyeshi popote kwamba Apolo alikasirika Akila na Prisila ‘walipomfafanulia kwa usahihi zaidi njia ya Mungu.’—Mdo. 18:24-28.

17. Paulo aliendelezaje amani?

17 Mtume Paulo alikuwa anajua kuhusu kazi nzuri iliyofanywa na Apolo. Lakini Paulo hakuhofia kwamba watu wangemwona Apolo kuwa bora kuliko yeye. Unyenyekevu, kiasi, na usawaziko wa Paulo unaonekana kupitia shauri ambalo alilipatia kutaniko la Korintho. Hakufurahia watu waliposema, “Mimi ni wa Paulo,” badala yake, alielekeza sifa zote kwa Yehova Mungu na Yesu Kristo.—1 Kor. 3:3-6.

18. Kulingana na 1 Wakorintho 4:6, 7, tunajifunza nini kutokana na mfano wa Apolo na Paulo?

18 Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Apolo na Paulo? Huenda tukafanya kazi kwa bidii kwa ajili ya Yehova, na huenda tukawasaidia wengi kufikia hatua ya ubatizo. Lakini tunatambua kwamba mafanikio yote tuliyo nayo ni kwa sababu ya baraka za Yehova. Mfano wa Apolo na Paulo unatufundisha somo lingine—kadiri tunavyokuwa na majukumu mengi zaidi kutanikoni, ndivyo tunavyokuwa na fursa kubwa zaidi ya kuendeleza amani. Tunathamini sana wakati wanaume waliowekwa rasmi wanapoendeleza amani na umoja kwa kutumia Neno la Mungu kama msingi wa ushauri wanaotoa, na kwa kutojikazia uangalifu wao wenyewe, bali kielelezo chetu, Kristo Yesu!—Soma 1 Wakorintho 4:6, 7.

19. Kila mmoja wetu anaweza kufanya nini? (Tazama pia sanduku, “ Epuka Kuchochea Mashindano.”)

19 Kila mmoja wetu ana uwezo au kipawa fulani alichopewa na Mungu. Tunaweza kutumia zawadi hiyo “kuhudumiana.” (1 Pet. 4:10) Huenda tukahisi kwamba tunatimiza sehemu ndogo tu. Lakini matendo hayo madogo yanayoendeleza umoja ni kama mishono midogo-midogo inayounganisha vazi. Acheni tujitahidi kuondoa moyoni mwetu mwelekeo wowote wa kuwa na roho ya mashindano. Na tuazimie kufanya yote tunayoweza ili kuendeleza amani na umoja kutanikoni.—Efe. 4:3.

WIMBO 80 “Onjeni Mwone Kwamba Yehova Ni Mwema”

^ fu. 5 Kama tu ambavyo ufa mdogo unaweza kudhoofisha chombo cha udongo, roho ya mashindano inaweza kudhoofisha kutaniko. Ikiwa kutaniko haliko imara na halina umoja, haliwezi kuwa mahali penye amani pa kumwabudu Mungu. Makala hii itazungumzia kwa nini tunapaswa kuepuka kusitawisha roho ya mashindano, na mambo tunayoweza kufanya ili kuchochea amani kutanikoni.

^ fu. 4 Baadhi ya majina yamebadilishwa.