Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 27

Iga Uvumilivu wa Yehova

Iga Uvumilivu wa Yehova

“Mkivumilia mtauokoa uhai wenu.”​—LUKA 21:19.

WIMBO 114 “Iweni na Subira”

MUHTASARI *

1-2. Maneno ya Yehova yanayopatikana kwenye Isaya 65:16, 17 yanatusaidiaje tusife moyo?

“USIFE MOYO!” Hicho kilikuwa kichwa chenye kusisimua cha programu ya kusanyiko la eneo la mwaka wa 2017. Programu hiyo ilituonyesha jinsi tunavyoweza kuvumilia tunapokuwa chini ya majaribu mbalimbali. Miaka minne imepita tangu wakati huo na bado tunaendelea kuvumilia maisha ya mfumo huu wa mambo.

2 Umekabili matatizo gani hivi karibuni? Kifo cha mtu wa familia au rafiki mpendwa? Ugonjwa unaohatarisha uhai? Matatizo yanayosababishwa na kusonga kwa umri? Janga la asili, ukatili, au minyanyaso? Au athari zinazotokana na magonjwa, kama vile janga la COVID-19? Tunatazamia kwa hamu siku ambayo matatizo hayo hayatakuwapo—yatasahauliwa na hayatatukia tena kamwe!—Soma Isaya 65:16, 17.

3. Lazima tufanye nini sasa, na kwa nini?

3 Maisha katika mfumo huu ni magumu, na huenda tukakabili changamoto ngumu hata zaidi wakati ujao. (Mt. 24:21) Ni wazi kwamba tunahitaji kuendelea kuimarisha uvumilivu wetu. Kwa nini? Kwa sababu Yesu alisema hivi: “Mkivumilia mtauokoa uhai wenu.” (Luka 21:19) Kutafakari kuhusu jinsi wengine wanavyovumilia majaribu yanayofanana na yetu kwa mafanikio kunaweza kuimarisha uvumilivu wetu.

4. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Yehova ni mfano bora wa uvumilivu?

4 Ni nani aliye mfano bora wa uvumilivu? Yehova Mungu. Je, unashangazwa na jibu hilo? Huenda ukashangazwa. Lakini fikira jambo hili. Ulimwengu huu unatawaliwa na Ibilisi na umejaa matatizo. Yehova ana nguvu za kuharibu ulimwengu huu mara moja, lakini anasubiri siku hususa ya kufanya hivyo wakati ujao. (Rom. 9:22) Kwa sasa, Mungu wetu anaendelea kuvumilia hadi wakati huo utakapofika. Acheni tuchunguze mambo tisa ambayo Yehova amechagua kuyavumilia.

YEHOVA AMECHAGUA KUVUMILIA NINI?

5. Jina la Mungu limechafuliwaje, nawe unahisije kuhusu hilo?

5 Kuchafuliwa kwa jina lake. Yehova analipenda jina lake na anataka kila mtu aliheshimu. (Isa. 42:8) Lakini kwa miaka 6000 hivi, jina lake zuri limechafuliwa. (Zab. 74:10, 18, 23) Jina lake lilianza kuchafuliwa katika bustani ya Edeni, Ibilisi (jina linalomaanisha “Mchongezi”) alipomshutumu Mungu kwamba alikuwa amewanyima Adamu na Hawa kitu fulani walichohitaji ili wawe na furaha. (Mwa. 3:1-5) Tangu wakati huo, Yehova amekuwa akishtakiwa kwa uwongo kwamba anawanyima wanadamu mambo ambayo kwa kweli wanahitaji. Yesu alihangaishwa na kuchafuliwa kwa jina la Baba yake. Kwa sababu hiyo, aliwafundisha wanafunzi wake wasali hivi: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe.”—Mt. 6:9.

6. Kwa nini Yehova ameruhusu muda wa kutosha upite kabla ya kusuluhisha suala la enzi kuu?

6 Kupingwa kwa enzi yake kuu. Yehova pekee ndiye aliye na haki ya kutawala mbingu na dunia, na njia yake ya kutawala ndiyo bora kabisa. (Ufu. 4:11) Lakini Ibilisi amejaribu kuwapotosha malaika na wanadamu wafikiri kwamba Mungu hana haki hiyo. Suala kuhusu haki ya Yehova ya kutawala halingeweza kusuluhishwa ndani ya siku moja. Kwa hekima, Mungu ameruhusu muda wa kutosha upite ili watu waone kwamba wanadamu wanapojaribu kujitawala wenyewe bila kumtegemea Muumba, hawawezi kufanikiwa. (Yer. 10:23) Kwa sababu ya subira ya Yehova, suala hilo litasuluhishwa mara moja kwa wakati wote. Enzi yake kuu itatetewa atakapothibitisha kwamba Ufalme wake pekee ndio unaweza kuleta amani na usalama wa kweli duniani.

7. Ni nani waliomwasi Yehova, naye atawafanya nini?

7 Kuasi kwa baadhi ya watoto wake. Yehova aliwaumba watoto wake wa kiroho na wa kibinadamu wakiwa wakamilifu, bila kasoro yoyote. Lakini baadaye mwana wake wa kiroho aliyeasi, Shetani, (jina linalomaanisha “Mpinzani”) aliwafanya wanadamu wakamilifu Adamu na Hawa wamwasi Yehova. Malaika na wanadamu wengine walijiunga katika uasi huo. (Yuda 6) Baadaye, hata watu katika taifa la Israeli, watu waliochaguliwa na Mungu, walimkataa na kuanza kuabudu miungu ya uwongo. (Isa. 63:8, 10) Yehova alikuwa na haki ya kuhisi amesalitiwa. Hata hivyo, alivumilia na ataendelea kuvumilia hadi wakati utakapofika wa kuwaangamiza waasi wote. Jambo hilo litawaletea kitulizo washikamanifu wake ambao kama yeye, wanavumilia uovu katika mfumo huu wa mambo!

8-9. Ni uwongo gani unaosemwa kumhusu Yehova, nasi tunaitikiaje?

8 Uwongo wenye kuendelea wa Ibilisi. Shetani alimshutumu mtumishi mnyoofu wa Yehova, Ayubu, na pia waabudu wote waaminifu wa Yehova kwamba wanamtumikia Mungu kwa sababu za kibinafsi. (Ayu. 1:8-11; 2:3-5) Ibilisi ameendelea kuwashutumu wanadamu hadi leo hii. (Ufu. 12:10) Tunaweza kufanya sehemu yetu ili kuthibitisha kwamba Shetani ni mwongo kwa kuvumilia majaribu na kuendelea kuwa washikamanifu kwa Yehova kwa sababu tunampenda. Kama ilivyokuwa kwa Ayubu, tutabarikiwa kwa sababu ya uvumilivu wetu.—Yak. 5:11.

9 Shetani anatumia viongozi wa dini ya uwongo kusema kwamba Yehova ni mkatili na ndiye anayesababisha mateso ya wanadamu. Baadhi yao hata husema kwamba watoto wanapokufa, Mungu amewachukua kwa sababu anahitaji malaika zaidi mbinguni. Kwa kweli watu hao wanakufuru! Lakini sisi tunajua kwamba Yehova ni Baba mwenye upendo. Tunapopata ugonjwa hatari au kufiwa na mtu tunayempenda, kamwe hatumlaumu Mungu wetu. Badala yake, tuna imani kwamba, siku moja atarekebisha hali. Tunaweza kumwambia kila mtu aliye tayari kutusikiliza kwamba Yehova ni Mungu mwenye upendo. Kisha Yehova anaweza kumjibu yule anayemdhihaki.—Met. 27:11.

10. Zaburi 22:23, 24 inafunua nini kumhusu Yehova?

10 Kuteseka kwa watumishi wake wapendwa. Yehova ni Mungu mwenye huruma. Anachukia anapoona tunateseka, iwe ni kwa sababu ya minyanyaso, magonjwa, au kutokamilika kwetu. (Soma Zaburi 22:23, 24.) Yehova anaelewa maumivu yetu; anataka kuyaondoa, na atayaondoa. (Linganisha Kutoka 3:7, 8; Isaya 63:9.) Siku inakuja ambapo “atafuta kila chozi kutoka katika macho [yetu], na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.”—Ufu. 21:4.

11. Yehova anahisije kuhusu watumishi wake washikamanifu waliokufa?

11 Kutenganishwa na marafiki wake waliokufa. Yehova anahisije kuhusu wanaume na wanawake waaminifu ambao wamekufa? Anatamani kuwaona tena! (Ayu. 14:15) Je, unaweza kuwazia jinsi ambavyo Yehova anamkosa rafiki yake Abrahamu? (Yak. 2:23) Au Musa ambaye alizungumza naye “uso kwa uso”? (Kut. 33:11) Na kwa kweli atakuwa anatamani sana kumsikia Daudi na watunga Zaburi wengine wakiimba nyimbo zao nzuri za sifa! (Zab. 104:33) Ingawa marafiki hao wa Mungu wamelala katika kifo, Yehova hajawasahau. (Isa. 49:15) Anakumbuka kila kitu kuhusu utu wao. Biblia inasema “kwa maoni yake, wote wako hai.” (Luka 20:38, maelezo ya chini) Siku moja, atawafufua ili waishi tena, naye atasikia tena sala zao za kutoka moyoni na kukubali ibada yao. Ikiwa umempoteza mpendwa wako katika kifo, maneno hayo na yakubembeleze na kukufariji.

12. Ni jambo gani hasa linalomtaabisha Yehova katika siku hizi za mwisho zenye uovu?

12 Wanadamu waovu wanaowakandamiza wanadamu wenzao. Uasi ulipoanza Edeni, Yehova alijua kwamba hali zingekuwa mbaya sana kabla hazijawa nzuri. Yehova anachukia uovu, ukosefu wa haki, na ukatili ulio katika ulimwengu wa leo. Sikuzote amewaonyesha huruma hasa wanyonge, yaani, walio dhaifu na wasio na mtetezi, mayatima, na pia wajane. (Zek. 7:9, 10) Kihususa, Yehova hutaabika anapoona watumishi wake waaminifu wakikandamizwa na kufungwa gerezani. Muwe na hakika kwamba anawapenda ninyi nyote mnaovumilia pamoja naye.

13. Ni mwenendo gani wenye kudhalilisha ambao Mungu anaona miongoni mwa wanadamu, naye atafanya nini kuhusu hilo?

13 Kuzorota kwa maadili katika ngono. Wanadamu waliumbwa kwa mfano wa Mungu. Lakini Shetani anawafanya wajishushie heshima kwa kujihusisha katika matendo mapotovu kiadili yenye kudhalilisha. Alipoona kwamba “uovu wa mwanadamu ulikuwa mkubwa” katika siku za Noa, “Yehova akaghairi kwamba aliwaumba wanadamu duniani, naye akaumia moyoni mwake.” (Mwa. 6:5, 6, maelezo ya chini, 11) Je, hali zimekuwa nzuri zaidi tangu wakati huo? La hasha! Ni lazima Ibilisi awe anafurahi sana anapoona jinsi ukosefu wa maadili katika ngono ulivyoongezeka sana, kutia ndani vitendo vya upotovu wa kimaadili kati ya watu wa jinsi tofauti na pia kati ya watu wa jinsia moja! (Efe. 4:18, 19) Shetani anafurahi hasa anapofaulu kusababisha waabudu wa kweli waanguke katika dhambi. Subira ya Yehova itakapofikia mwisho wake, ataonyesha jinsi anavyochukia upotovu wote wa maadili.

14. Wanadamu wanauathirije uumbaji wa Mungu?

14 Kuharibiwa kwa uumbaji wake. Mwanadamu ‘hamtawali tu mwanadamu mwenzake kwa kumuumiza,’ bali pia haitunzi vizuri dunia na wanyama ambao Yehova alimkabidhi awatunze. (Mhu. 8:9; Mwa. 1:28) Baadhi ya wataalamu wanaonya kwamba ndani ya miaka michache ijayo, shughuli za wanadamu zinaweza kuangamiza aina milioni moja zaidi ya viumbe hai. Hivyo, haishangazi kusikia wanasema kwamba mazingira yako hatarini! Tunashukuru kwamba Yehova ameahidi “kuwaharibu wale wanaoiharibu dunia” na kuibadili sayari yetu kuwa paradiso.—Ufu. 11:18; Isa. 35:1.

MAMBO TUNAYOJIFUNZA KUTOKANA NA UVUMILIVU WA YEHOVA

15-16. Ni jambo gani linalopaswa kutuchochea kuvumilia pamoja na Yehova? Toa mfano.

15 Fikiria matatizo yote ambayo Baba yetu wa mbinguni amekuwa akivumilia kwa maelfu ya miaka. (Tazama sanduku “ Mambo Ambayo Yehova Anavumilia.”) Yehova angeweza kukomesha mfumo huu mwovu wa mambo wakati wowote. Lakini subira yake imethibitika kuwa baraka kwetu! Fikiria mfano huu. Tuseme mwanamume fulani na mke wake wanaambiwa kwamba mtoto wao ambaye hajazaliwa ana matatizo makubwa ya afya na kwamba atakuwa na maisha magumu na atakufa akiwa na umri mdogo. Hata hivyo, wazazi hao wanafurahi mtoto huyo anapozaliwa, hata ingawa haitakuwa rahisi kumtunza. Upendo wao kwa mtoto huyo unawachochea kuvumilia hali yoyote ngumu ili wamtunze kwa njia bora kabisa.

16 Vivyo hivyo, wazao wote wa Adamu na Hawa wanazaliwa wakiwa na dhambi. Hata hivyo, Yehova anawapenda na kuwatunza. (1 Yoh. 4:19) Na tofauti na wazazi wa kibinadamu katika mfano wetu, Yehova anaweza kurekebisha hali yetu. Ameweka siku ambayo ataondoa matatizo yote yanayowahangaisha wanadamu. (Mt. 24:36) Je, upendo wa Yehova haupaswi kutuchochea sisi pia kuvumilia pamoja naye kwa muda wote tunaohitaji kuvumilia?

17. Maneno yanayomhusu Yesu kwenye Waebrania 12:2, 3, yanatutiaje moyo tuendelee kuvumilia?

17 Yehova ni kielelezo kikamilifu cha uvumilivu. Yesu alifaulu kuiga uvumilivu wa Baba yake. Akiwa mwanadamu, Yesu alivumilia maneno makali, aibu, na mti wa mateso kwa ajili yetu. (Soma Waebrania 12:2, 3.) Bila shaka, mfano wa Yehova wa uvumilivu ulimpa Yesu nguvu za kuvumilia. Unaweza kutuimarisha sisi pia.

18. Andiko la 2 Petro 3:9 linatusaidiaje kuelewa kile kinachotimizwa na subira ya Yehova?

18 Soma 2 Petro 3:9. Yehova anajua wakati bora wa kuuharibu ulimwengu huu mwovu. Subira yake imewezesha kukusanywa kwa umati mkubwa wenye idadi ya mamilioni ya watu, wanaomwabudu na kumsifu. Wote wanashukuru kwamba Yehova amevumilia kwa muda mrefu hivi kwamba wakazaliwa, wakajifunza kumpenda, na kujiweka wakfu kwake. Mamilioni ya watu watakapovumilia hadi mwisho, itakuwa wazi kabisa kwamba Yehova alifanya uamuzi sahihi alipoamua kuonyesha subira.

19. Tunapaswa kuazimia kufanya nini, na tutapata thawabu gani?

19 Tunajifunza kutoka kwa Yehova jinsi ya kuvumilia kwa shangwe. Licha ya huzuni na mateso yote yaliyosababishwa na Shetani, Yehova ameendelea kuwa “Mungu mwenye furaha.” (1 Tim. 1:11) Sisi pia tunaweza kuendelea kuwa wenye shangwe tunapongojea kwa subira Yehova alitakase jina lake, atetee enzi yake kuu, akomeshe uovu wote, na kuondoa matatizo yote tunayokabili sasa. Acheni tuazimie kuvumilia na tufarijike kwa kujua kwamba Baba yetu wa mbinguni anavumilia pia. Tukifanya hivyo, maneno haya yatathibitika kuwa kweli kwa kila mmoja wetu: “Mwenye furaha ni yule anayeendelea kuvumilia jaribu, kwa sababu atakapokubaliwa atapokea taji la uzima, ambalo Yehova aliwaahidi wale wanaoendelea kumpenda.”—Yak. 1:12.

WIMBO 139 Wazia Wakati Vitu Vyote Vitakuwa Vipya

^ fu. 5 Sote tunakabili matatizo ya aina moja au nyingine. Kwa sasa, mengi kati ya matatizo hayo hayana suluhisho; kwa ufupi tunahitaji tu kuyavumilia. Hata hivyo hatuko peke yetu. Yehova pia anavumilia mambo mengi. Katika makala hii, tutachunguza mambo tisa ambayo anavumilia. Pia, tutaona mambo ambayo uvumilivu wa Yehova umetimiza na jinsi tunavyoweza kunufaika kutokana na mfano wake.