Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Mashahidi wa Yehova wanapaswa kuzionaje tovuti za kutafuta wenzi wa ndoa?

Bila shaka, Yehova anataka watu wawili waliofunga ndoa wawe na furaha na wafurahie uhusiano wa karibu unaodumu. (Mt. 19:4-6) Ikiwa unatamani kufunga ndoa, unaweza kupataje mwenzi wa ndoa anayefaa? Muumba wetu, Yehova, anajua mambo yanayoweza kufanya uchumba na ndoa ifanikiwe. Hivyo, ikiwa utatumia kanuni ambazo ametupatia, utafanikiwa. Fikiria baadhi ya kanuni hizo.

Kwanza, tunahitaji kujua jambo hili kujihusu: “Moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari.” (Yer. 17:9) Mtu anapojaribu kutafuta na kumvutia mtu anayetaka kufunga naye ndoa, anaweza kusitawisha haraka hisia kali na kushindwa kufanya maamuzi kwa hekima. Watu wanapofanya uamuzi wa kufunga ndoa kwa msingi wa hisia tu, wanaishia kuvunjika moyo. (Met. 28:26) Hiyo ndiyo sababu si jambo la hekima kuanza kuonyeshana hisia za mahaba mwanzoni mwa uhusiano au kufanya makubaliano kabla ya kufahamiana vizuri.

Methali 22:3 inasema hivi: “Mtu mwerevu huona hatari na kujificha, lakini wajinga husonga mbele na kupata madhara.” Kwa nini inaweza kuwa hatari kutumia tovuti za kutafuta wenzi wa ndoa? Inasikitisha kwamba baadhi ya watu walikuja kutambua kwa uchungu mwingi kwamba watu waliokuwa wakiwasiliana nao mtandaoni walikuwa wakiwalaghai. Pia, watu wasio wanyoofu wamefungua akaunti za uwongo ili kuwaibia pesa watu wanaodanganyika kwa urahisi. Nyakati nyingine, watu wanaofanya udanganyifu huo mbaya sana wanadai kwamba wao ni Mashahidi.

Fikiria hatari nyingine. Baadhi ya tovuti hizo zina programu zinazofanya hesabu ili kujua ni watu gani wanaofaana. Hata hivyo, hakuna uthibitisho wowote unaoonyesha kwamba mbinu hizo zinafanya kazi. Je, litakuwa jambo la hekima kuzitumaini programu hizo za wanadamu kufanya maamuzi kuhusu jambo muhimu kama vile kuchagua mwenzi wa ndoa anayefaa? Programu za kompyuta haziwezi kamwe kutegemeka kama kanuni za Biblia.—Met. 1:7; 3:5-7.

Kanuni inayopatikana kwenye Methali 14:15 inasema hivi: “Mjinga huamini kila neno, lakini mwerevu hutafakari kila hatua.” Kabla ya kumfikiria mtu fulani kuwa mwenzi wa ndoa anayefaa, unahitaji kumfahamu vizuri. Lakini itakuwa vigumu kufahamiana vizuri ikiwa mlikutana kwenye mtandao. Hata ikiwa mnapeana habari zinazowahusu na kutumia muda mwingi kuandikiana ujumbe, je, kweli unaweza kusema unamjua vizuri mtu huyo? Baadhi ya watu waliofikiri kwamba wamepata mtu anayewafaa, walishtuka walipoonana na mtu huyo ana kwa ana.

Mtunga zaburi alisema hivi: “Sishirikiani na watu wadanganyifu, nami huwaepuka wale wanaoficha jinsi walivyo.” (Zab. 26:4) Watu wengi wanafikiri kwamba ni jambo la kawaida kudanganya kuhusu habari za kibinafsi ili kuwavutia zaidi watu wengine. Huenda wakaficha jinsi walivyo kikweli au wasijionyeshe jinsi walivyo wanapowasiliana na wengine mtandaoni. Ingawa huenda baadhi ya watu wakajitambulisha kuwa Mashahidi wa Yehova, je, kweli ni Wakristo waliobatizwa? Je, wamekomaa kiroho? Je, wana uhusiano wa kibinafsi na Yehova? Je, wanaheshimika katika kutaniko lao? Au huenda wao ni mfano mbaya na ni ‘watu wabaya kushirikiana nao’? (1 Kor. 15:33; 2 Tim. 2:20, 21) Je, wako huru Kimaandiko kufunga ndoa? Unahitaji kujua mambo hayo, lakini ni vigumu kuyajua bila msaada wa Mashahidi wengine wanaomjua mtu huyo vizuri. (Met. 15:22) Na bila shaka, mtumishi mshikamanifu wa Yehova hawezi kamwe kufikiria ‘kufungwa nira isivyo sawa’ pamoja na mtu asiye mwamini.—2 Kor. 6:14; 1 Kor. 7:39.

Kama tulivyoona, kuna hatari zinazojitokeza tunapotumia mitandao kutafuta mwenzi wa ndoa, hata hiyo, kuna njia bora tunazoweza kutumia kutafuta mwenzi na kusitawisha uhusiano unaoweza kuongoza kwenye ndoa inayoheshimika. Unaweza kukutana wapi na mtu anayeweza kuwa mwenzi wa ndoa anayefaa? Ikiwa inaruhusiwa kukusanyika pamoja, Mashahidi wa Yehova wanaweza kufahamiana ana kwa ana wanapohudhuria mikutano ya kutaniko, makusanyiko, na vikusanyiko vingine.

Kadiri mnavyotumia wakati pamoja, ndivyo mtakavyoona ikiwa malengo na viwango vyenu vinafanana

Ikiwa haiwezekani kukusanyika pamoja, kama vile wakati wa janga la COVID-19, tunatumia vifaa vya kielektroni kuhudhuria mikutano ya kutaniko na tunaweza kufahamiana na Mashahidi wengine waseja. Unaweza kuona jinsi wanavyoshiriki mikutano na kusikia wanavyodhihirisha imani yao kupitia maelezo yao. (1 Tim. 6:11, 12) Pia, baada ya mkutano mnaweza kuzungumza mkiwa kwenye vikundi vya watu wachache-wachache kwenye breakout room za Zoom. Kupitia vikusanyiko vya vikundi vya Mashahidi kwa njia ya video, unaweza kuona jinsi mtu unayevutiwa naye anavyoshughulika na wengine na hilo linaweza kufunua utu wake halisi. (1 Pet. 3:4) Baada ya muda, kadiri mnavyofahamiana zaidi, unaweza kujua ikiwa malengo na viwango vyenu vinafanana na ikiwa mnafaana.

Wakristo waseja wanapotafuta mwenzi wa ndoa anayefaa kwa njia inayopatana na kanuni za Biblia, kuna uwezekano mkubwa watajionea ukweli wa methali inayosema hivi: “Anayepata mke mwema [au mume] amepata kitu chema, naye hupata kibali cha Yehova.”—Met. 18:22.