Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 30

Endelea Kukua Katika Upendo Wako

Endelea Kukua Katika Upendo Wako

“Kupitia upendo na tuendelee kukua katika mambo yote.”​—EFE. 4:15.

WIMBO 2 Jina Lako Ni Yehova

MUHTASARI a

1. Ulipata kweli gani ulipoanza kujifunza Biblia?

 JE, UNAKUMBUKA wakati ulipoanza kujifunza Biblia? Huenda ulishangaa kujua kwamba Mungu ana jina. Labda ulifarijika kujua kwamba Mungu hatesi watu katika moto wa mateso. Na inawezekana ulisisimka kwa sababu ya tumaini la kuwaona tena wapendwa wako waliokufa na kuishi pamoja nao katika dunia paradiso.

2. Mbali na kujifunza kweli za Biblia, ulifanya maendeleo gani mengine? (Waefeso 5:1, 2)

2 Kadiri ulivyozidi kujifunza Neno la Mungu, ndivyo upendo wako kwa Yehova ulivyozidi kukua. Upendo huo ulikuchochea kutumia mambo uliyojifunza. Ulifanya maamuzi mazuri yanayotegemea kanuni za Biblia. Uliboresha mtazamo na mwenendo wako kwa sababu ulitamani kumfurahisha Mungu. Kama vile mtoto anavyomwiga mzazi mwenye upendo, ulikuwa ukimwiga Baba yako wa mbinguni.​—Soma Waefeso 5:1, 2.

3. Huenda tukajiuliza maswali gani?

3 Huenda tukajiuliza hivi: ‘Je, sasa ninampenda Yehova zaidi kuliko nilivyompenda nilipobatizwa? Tangu nilipobatizwa, je, njia yangu ya kufikiri na kutenda ni kama ya Yehova—hasa katika kuwaonyesha upendo ndugu na dada zangu?’ Ikiwa “upendo uliokuwa nao mwanzoni” umepoa kwa kadiri fulani, usivunjike moyo. Wakristo wa karne ya kwanza walipatwa na jambo kama hilo. Yesu hakuwakataa na hatatukataa sisi pia. (Ufu. 2:4, 7) Anajua kwamba tunaweza kusitawisha upendo tuliokuwa nao mwanzoni tulipojifunza kweli.

4. Tutachunguza nini katika makala hii?

4 Makala hii itazungumzia jinsi tunavyoweza kuendelea kukua katika upendo wetu kwa Yehova na kwa wengine. Kisha tutaona baraka ambazo tutapata tunapoimarisha upendo wetu.

IMARISHA UPENDO WAKO KWA YEHOVA

5-6. Mtume Paulo alikabili changamoto gani katika huduma yake, lakini ni nini kilichomchochea aendelee kumtumikia Yehova?

5 Mtume Paulo alikuwa na maisha yenye kuridhisha katika utumishi wa Yehova, lakini alikabiliana na changamoto nyingi. Mara kwa mara Paulo alisafiri kwa mwendo mrefu, na siku hizo haikuwa rahisi kusafiri. Katika safari zake, wakati mwingine Paulo alikabili “hatari za kutokana na mito” na “hatari za kutokana na wezi.” Pindi nyingine hata alipigwa na wapinzani wake. (2 Kor. 11:23-27) Na wakati mwingine Wakristo wenzake hawakuthamini jitihada za Paulo za unyoofu za kuwasaidia.​—2 Kor. 10:10; Flp. 4:15.

6 Ni nini kilichomsaidia Paulo aendelee kumtumikia Yehova? Paulo alijifunza mengi kuhusu utu wa Yehova kutokana na Maandiko na kupitia mambo yaliyompata. Paulo alisadiki kwamba Yehova Mungu anampenda. (Rom. 8:38, 39; Efe. 2:4, 5) Naye akampenda Yehova sana. Paulo alionyesha upendo wake kwa Yehova “kwa kuhudumu na kuendelea kuwahudumia watakatifu.”​—Ebr. 6:10.

7. Ni njia gani moja ambayo tunaweza kuimarisha upendo wetu kwa Yehova?

7 Tunaweza kuimarisha upendo wetu kwa Mungu kwa kujifunza Neno lake kwa bidii. Unaposoma Biblia jaribu kutambua jambo ambalo kila simulizi linafunua kumhusu Yehova. Jiulize hivi: ‘Simulizi hili linaonyeshaje kwamba Yehova ananipenda? Linanipatia sababu gani za kumpenda Yehova?’

8. Sala inaweza kutusaidiaje kuimarisha upendo wetu kwa Mungu?

8 Njia nyingine ambayo tunaweza kuimarisha upendo wetu kwa Yehova ni kwa kumfunulia moyo wetu kwa ukawaida katika sala. (Zab. 25:4, 5) Naye Yehova atajibu sala zetu. (1 Yoh. 3:21, 22) Khanh, dada anayeishi huko Asia, anasema hivi: “Mwanzoni upendo wangu kwa Yehova ulitegemea ujuzi, lakini upendo huo uliimarika zaidi nilipoona jinsi anavyojibu sala zangu. Hilo lilinichochea kufanya mambo yanayomfurahisha.” b

IMARISHA UPENDO WAKO KWA WENGINE

9. Timotheo alionyeshaje kwamba alikuwa akifanya maendeleo katika kuonyesha upendo?

9 Miaka kadhaa baada ya kuwa Mkristo, Paulo alikutana na kijana aliyeitwa Timotheo. Timotheo alimpenda Yehova, na pia aliwapenda watu. Paulo aliwaambia hivi Wafilipi: “Sina mtu mwingine aliye na mwelekeo kama [wa Timotheo] atakayejali kwa unyoofu mahangaiko yenu.” (Flp. 2:20) Hapa Paulo hakuwa akizungumzia uwezo wa Timotheo wa kupanga mambo au kuzungumza hadharani, lakini ni wazi kwamba Paulo alifurahishwa na jinsi Timotheo alivyowapenda ndugu na dada. Bila shaka, makutaniko ambayo Timotheo alitumikia yalitazamia kwa hamu awatembelee.​—1 Kor. 4:17.

10. Anna na mume wake waliwaonyeshaje upendo akina ndugu na dada?

10 Sisi pia tunatafuta njia za kuwasaidia ndugu na dada zetu Wakristo. (Ebr. 13:16) Fikiria kisa cha Anna, aliyetajwa katika makala iliyotangulia. Baada ya kimbunga kikali kutokea, yeye na mume wake walitembelea familia moja ya Mashahidi nyumbani kwao na wakatambua kwamba paa la nyumba yao lilikuwa limeharibiwa. Matokeo ni kwamba familia hiyo haikuwa na nguo safi. Anna anasema hivi: “Tulichukua nguo zao, tukazifua na tukawarudishia zikiwa zimepigwa pasi na kukunjwa vizuri. Tuliona hilo kuwa jambo dogo, lakini lilitokeza urafiki wa karibu ambao umeendelea mpaka leo.” Upendo wa Anna na mume wake kuelekea akina ndugu na dada uliwachochea kuwasaidia kwa njia hususa.​—1 Yoh. 3:17, 18.

11. (a) Huenda wengine wakahisije tunapowaonyesha upendo? (b) Kulingana na Methali 19:17, Yehova anatendaje tunapoonyesha upendo?

11 Tunapowatendea wengine kwa upendo na fadhili, mara nyingi wao hutambua kwamba tunajitahidi kuiga jinsi Yehova anavyofikiri na kutenda. Na huenda wakathamini matendo yako ya fadhili kwa njia ambayo hukuwazia. Dada Khanh aliyetajwa awali, anakumbuka jinsi wengine walivyomsaidia. Anasema hivi: “Ninathamini msaada wa dada wapendwa walioenda pamoja nami katika huduma. Walikuja kunichukua, wakanikaribisha chakula cha mchana, na kuhakikisha nimerudi nyumbani salama. Sasa ninatambua kwamba walifanya jitihada nyingi. Na walifanya hivyo kwa upendo.” Bila shaka, si kila mtu atatushukuru kwa mambo tunayowafanyia wengine. Dada Khanh anasema hivi kuhusu wale waliomsaidia: “Ninatamani kuwalipa kwa ajili ya matendo yao mengi ya fadhili, lakini sijui wanaishi wapi. Hata hivyo, Yehova anajua waliko, naye atawalipa kwa niaba yangu.” Dada Khanh anasema ukweli. Yehova anatambua hata matendo madogo ya fadhili tunayowatendea wengine. Anaona matendo hayo kuwa dhabihu yenye thamani na kama deni ambalo atalipa.​—Soma Methali 19:17.

Mtu anapofanya maendeleo ya kiroho, anatafuta njia za kuwasaidia wengine (Tazama fungu la 12)

12. Akina ndugu wanaweza kuonyeshaje upendo wao katika kutaniko? (Tazama pia picha.)

12 Ikiwa wewe ni ndugu, unawezaje kuwaonyesha wengine upendo na kujitahidi kuwasaidia? Ndugu kijana anayeitwa Jordan alimwuliza mzee wa kutaniko jinsi ambavyo angeweza kufanya mengi zaidi ili kusaidia kutanikoni. Mzee huyo alimpongeza kwa maendeleo ambayo tayari alikuwa amefanya, kisha akampa ushauri kuhusu jinsi ambavyo angeweza kufanya mengi zaidi. Kwa mfano, alipendekeza Jordan ajitahidi kufika mapema katika Jumba la Ufalme na kuwasalimia wengine, atoe maelezo kwenye mikutano, ahubiri kwa ukawaida pamoja na kikundi chao cha utumishi, na kutafuta njia hususa za kuwasaidia wengine. Jordan alipofuata ushauri huo, hakuwa akijifunza tu ustadi mpya, bali pia alikuwa akiimarisha upendo wake kwa ndugu na dada zake. Jordan alijifunza kwamba ndugu anapokuwa mtumishi wa huduma, haanzi kuwasaidia wengine wakati huo; badala yake, anaendelea kuwasaidia.​—1 Tim. 3:8-10, 13.

13. Upendo ulimchocheaje ndugu anayeitwa Christian astahili tena kuwa mzee wa kutaniko?

13 Namna gani ikiwa zamani ulitumikia ukiwa mtumishi wa huduma au mzee? Yehova anakumbuka kazi uliyofanya wakati uliopita na upendo uliokuchochea kufanya hivyo. (1 Kor. 15:58) Pia, anaona upendo unaoendelea kuonyesha. Ndugu anayeitwa Christian alivunjika moyo alipoondolewa kuwa mzee. Ingawa hivyo, anasema hivi: “Niliamua kufanya yote ambayo ningeweza ili kumtumikia Yehova kwa kuchochewa na upendo—iwe nina mapendeleo au sina mapendeleo.” Baada ya muda, aliwekwa rasmi tena kuwa mzee. Christian anakiri hivi: “Nilikuwa na wasiwasi kuhusu kutumikia tena. Lakini niliamua kwamba ikiwa Yehova, kupitia rehema zake, alitaka nitumikie tena nikiwa mzee, ningefanya hivyo kwa sababu ya upendo wangu kwake na kwa ndugu na dada zangu.”

14. Unajifunza nini kutokana na maelezo ya dada anayeishi nchini Georgia?

14 Watumishi wa Yehova pia wanawaonyesha upendo jirani zao. (Mt. 22:37-39) Kwa mfano, Elena, dada anayeishi nchini Georgia, anasema hivi: “Mwanzoni, jambo pekee lililonichochea kuhubiri ni upendo wangu kwa Yehova. Lakini upendo wangu kwa Baba yangu wa mbinguni ulivyozidi kuongezeka, upendo wangu kuelekea watu uliongezeka pia. Nilijaribu kuwazia matatizo ambayo walikabili na mambo ambayo wangependa kuzungumzia. Kadiri nilivyowafikiria kwa njia hiyo, ndivyo nilivyotamani kuwasaidia.”​—Rom. 10:13-15.

BARAKA ZINAZOTOKANA NA KUWAONYESHA WENGINE UPENDO

Tendo moja la upendo linaweza kuwaletea baraka watu wengine wengi (Tazama fungu la 15 na 16)

15-16. Kama inavyoonyeshwa kwenye picha, ni baraka gani zinazotokana na kuwaonyesha wengine upendo?

15 Tunapowaonyesha upendo ndugu zetu, si wao tu wanaonufaika. Baada ya janga la COVID-19 kuanza, ndugu anayeitwa Paolo na mke wake waliwasaidia dada wengi wenye umri mkubwa wajifunze jinsi ya kuhubiri kwa kutumia vifaa vya kielektroni. Dada mmoja ambaye mwanzoni hakuweza kutumia kifaa chake mwishowe alifaulu. Alitumia kifaa chake kuwakaribisha watu wake wa ukoo kwenye Ukumbusho. Watu 60 kati yao walihudhuria kupitia video mtandaoni! Dada huyo na watu wake wa ukoo walinufaika kutokana na jitihada za Paolo na mke wake. Baadaye, dada huyo alimwandikia hivi ndugu Paolo: “Asante sana kwa kutufundisha sisi wenye umri mkubwa. Sitasahau kamwe jinsi Yehova anavyotujali na jitihada zako nyingi.”

16 Paolo alijifunza somo muhimu kutokana na jambo hilo. Lilimkumbusha kwamba upendo ni muhimu kuliko ujuzi au uwezo wetu wa kiasili. Anakumbuka hivi: “Zamani nilitumikia nikiwa mwangalizi wa mzunguko. Leo, ninatambua kwamba ingawa huenda ndugu na dada wamesahau hotuba nilizotoa, bado wanakumbuka jinsi nilivyowasaidia kwa njia hususa.”

17. Ni nani mwingine atakayenufaika tunapoonyesha upendo?

17 Tunapowaonyesha wengine upendo, sisi wenyewe tunanufaika kwa njia tusizotarajia. Jonathan, anayeishi nchini New Zealand, anathibitisha ukweli wa jambo hilo. Jumamosi moja alasiri, alimwona painia fulani akihubiri barabarani. Jonathan aliamua kuhubiri pamoja na painia huyo kila Jumamosi alasiri. Wakati huo, hakutambua jinsi ambavyo yeye mwenyewe angenufaika kutokana na tendo hilo la fadhili. Jonathan anakiri hivi: “Wakati huo, sikufurahia utumishi wa shambani. Lakini niliposikiliza jinsi painia huyo alivyofundisha na kuona jinsi alivyopata matokeo katika huduma, hilo lilinichochea kupenda sana kuhubiri. Pia, nilipata rafiki mzuri ambaye alinisaidia kukua kiroho, kufurahia huduma, na kumkaribia zaidi Yehova.”

18. Yehova angependa tufanye nini?

18 Yehova angependa sisi sote tuimarishe upendo wetu kwake na kwa wengine. Kama tulivyojifunza, tunaweza kuimarisha upendo wetu kwa Yehova kwa kusoma Neno lake na kulitafakari, na kwa kuzungumza naye kwa ukawaida katika sala. Tunaweza kuimarisha upendo wetu kwa ndugu na dada zetu kwa kuwasaidia kwa njia hususa. Upendo wetu unapozidi kukua, tutazidi kumkaribia Yehova na ndugu na dada zetu. Na tutafurahia urafiki huo milele!

WIMBO 109 Pendaneni Sana Kutoka Moyoni

a Iwe tumejifunza kweli hivi karibuni au tumekuwa tukimtumikia Yehova kwa miaka mingi, sisi sote tunaweza kufanya maendeleo. Makala hii itazungumzia njia muhimu tunayoweza kufanya hivyo: kwa kukua katika upendo wetu kwa Yehova na kwa wengine. Unapotafakari habari hii chunguza maendeleo ambayo tayari umefanya na jinsi unavyoweza kufanya maendeleo zaidi.

b Baadhi ya majina yamebadilishwa.