Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 31

“Iweni Imara, Thabiti”

“Iweni Imara, Thabiti”

“Ndugu zangu wapendwa, iweni imara, thabiti.”—1 KOR. 15:58.

WIMBO 122 Iweni Imara, Thabiti!

MUHTASARI a

1-2. Mkristo anaweza kulinganishwaje na ghorofa refu sana? (1 Wakorintho 15:58)

 MWISHONI mwa miaka ya 1970, jengo lenye ghorofa 60 lilijengwa hatua kwa hatua huko Tokyo, Japani. Watu walijiuliza jengo hilo lingewezaje kuhimili matetemeko ya ardhi yanayotokea mara kwa mara katika jiji hilo. Siri ilikuwa nini? Mainjinia walikuwa wamebuni jengo hilo liwe imara lakini lenye uwezo wa kunyumbulika ili lihimili mitikisiko ya tetemeko la ardhi. Wakristo ni kama ghorofa hilo refu. Jinsi gani?

2 Mkristo anapaswa kudumisha usawaziko kati ya kuwa imara na kunyumbulika. Anapaswa kuwa imara na thabiti na kuazimia kuendelea kutii sheria na viwango vya Yehova. (Soma 1 Wakorintho 15:58.) Anakuwa “tayari kutii” na halegezi msimamo wake. Kwa upande mwingine, anahitaji kuwa mwenye “usawaziko,” au mwenye kunyumbulika, ikiwa hali inaruhusu au hata anapohitajika kufanya hivyo. (Yak. 3:17) Mkristo ambaye amejifunza kuwa na maoni hayo yenye usawaziko ataepuka kushikilia sana maoni yake au kuendekeza mambo yasiyofaa. Katika makala hii, tutachunguza jinsi tunavyoweza kuwa thabiti. Pia, tutachunguza njia tano ambazo Shetani hujaribu kutumia ili kudhoofisha azimio letu na tutajifunza jinsi ya kupinga jitihada zake.

TUNAWEZAJE KUWA IMARA?

3. Ni sheria gani za Mpaji-sheria Mkuu zilizo kwenye Matendo 15:28, 29?

3 Akiwa Mpaji-sheria Mkuu, sikuzote Yehova amewapa watu wake sheria zilizo wazi. (Isa. 33:22) Kwa mfano, katika karne ya kwanza, baraza linaloongoza lilitaja njia tatu ambazo Wakristo wanapaswa kuendelea kuwa imara: (1) kwa kuepuka ibada ya sanamu, na kumwabudu Yehova peke yake, (2) kwa kuheshimu utakatifu wa damu, na (3) kwa kutii viwango vya juu vya maadili vilivyo katika Biblia. (Soma Matendo 15:28, 29.) Leo, Wakristo wanawezaje kudumisha msimamo imara katika njia hizo tatu?

4. Tunawezaje kumwabudu Yehova peke yake? (Ufunuo 4:11)

4 Tunaepuka ibada ya sanamu, na kumwabudu Yehova peke yake. Yehova aliwaamuru Waisraeli wamwabudu yeye peke yake. (Kum. 5:6-10) Yesu alipojaribiwa na Ibilisi, alisema waziwazi tunapaswa kumwabudu Yehova peke yake. (Mt. 4:8-10) Kwa hiyo, hatuabudu sanamu za kidini. Pia, hatuabudu wanadamu—iwe ni viongozi wa kidini, watawala wa kisiasa, au watu maarufu katika michezo na burudani—na hatuwatendei kama miungu. Tunachukua msimamo upande wa Yehova na kumwabudu yule ‘aliyeumba vitu vyote.’​—Soma Ufunuo 4:11.

5. Kwa nini tunatii sheria ya Yehova kuhusu utakatifu wa uhai na damu?

5 Tunatii sheria ya Yehova kuhusu utakatifu wa uhai na damu. Kwa nini? Kwa sababu Yehova anasema kwamba damu inawakilisha uhai, ambao ni zawadi yenye thamani kutoka kwake. (Law. 17:14) Kwa mara ya kwanza Yehova alipowaruhusu wanadamu wale nyama, aliwaamuru wasile damu. (Mwa. 9:4) Alitaja tena amri hiyo alipowapatia Waisraeli Sheria ya Musa. (Law. 17:10) Na aliliongoza baraza linaloongoza la karne ya kwanza litoe agizo kwamba Wakristo wote waendelee “kujiepusha . . . na damu.” (Mdo. 15:28, 29) Tunatii amri hiyo kwa uthabiti tunapofanya uamuzi kuhusu matibabu. b

6. Tunafanya jitihada gani ili kutii viwango vya juu vya maadili kutoka kwa Yehova?

6 Tunafuata kabisa viwango vya juu vya maadili kutoka kwa Yehova. (Ebr. 13:4) Akitumia lugha ya mfano, mtume Paulo anatushauri ‘tuviue’ viungo vya mwili wetu, yaani, tufanye yote tunayoweza ili kuondoa tamaa zisizofaa za mwili. Tunaepuka kutazama au kufanya jambo lolote ambalo linaweza kutuongoza tufanye uasherati. (Kol. 3:5; Ayu. 31:1) Tunaposhawishiwa, tunakataa mara moja wazo au tendo lolote ambalo linaweza kuharibu urafiki wetu pamoja na Mungu.

7. Tunapaswa kuazimia kufanya nini, na kwa nini?

7 Yehova anatarajia tuwe “watiifu kutoka moyoni.” (Rom. 6:17) Sikuzote mwongozo wake unatunufaisha, na hatuwezi kubadili sheria zake. (Isa. 48:17, 18; 1 Kor. 6:9, 10) Tunajitahidi kumfurahisha Yehova na kuonyesha mtazamo kama wa mtunga zaburi aliyesema hivi: “Nimeazimia kuyatii masharti yako nyakati zote, mpaka mwisho.” (Zab. 119:112) Hata hivyo, Shetani atajaribu kudhoofisha azimio letu. Anatumia mbinu gani?

SHETANI ANAJARIBU JINSI GANI KUDHOOFISHA AZIMIO LETU?

8. Shetani anatumiaje mateso kujaribu kudhoofisha azimio letu?

8 Mateso. Ibilisi anatumia mashambulizi ya kimwili na kihisia ili kujaribu kudhoofisha azimio letu. Lengo lake ni ‘kutumeza,’ anataka kuharibu uhusiano wetu pamoja na Yehova. (1 Pet. 5:8) Wakristo wa karne ya kwanza walitishwa, walipigwa, na kuuawa kwa sababu ya azimio lao la kusimama imara. (Mdo. 5:27, 28, 40; 7:54-60) Leo, Shetani anaendelea kutumia mateso. Hilo linaonekana wazi kupitia jinsi ndugu na dada zetu wanavyotendewa kikatili huko Urusi na katika nchi nyingine, na kupitia mashambulizi ya kibinafsi kutoka kwa wapinzani.

9. Toa mfano unaoonyesha kwamba tunapaswa kujihadhari tunaposhinikizwa kwa njia isiyo ya wazi.

9 Kushinikizwa kwa njia isiyo ya wazi. Mbali na kutumia mashambulizi ya moja kwa moja, pia Shetani anatumia “matendo yenye hila.” (Efe. 6:11) Kwa mfano, mfikirie ndugu anayeitwa Bob, aliyelazwa hospitalini ili afanyiwe upasuaji mkubwa. Aliwajulisha madaktari kwamba hangekubali kamwe kutiwa damu mwilini. Daktari wa upasuaji alikubali kuheshimu uamuzi wake. Hata hivyo, usiku kabla ya kufanyiwa upasuaji, daktari wa nusu-kaputi alimtembelea Bob baada ya watu wa familia yake kwenda nyumbani. Alimwambia Bob inawezekana kwamba hawatatumia damu lakini watakuwa nayo hapo karibu ikiwa itahitajika. Labda daktari huyo alifikiri kwamba Bob angebadili maoni yake bila watu wa familia yake kuwepo. Lakini Bob aliendelea kuwa thabiti, akasema kwamba hangekubali kutiwa damu katika hali yoyote ile.

10. Kwa nini njia ya kufikiri ya wanadamu ni mtego? (1 Wakorintho 3:19, 20)

10 Njia ya kufikiri ya wanadamu. Ikiwa tutaona mambo kulingana na maoni ya wanadamu, huenda tukampuuza Yehova na viwango vyake. (Soma 1 Wakorintho 3:19, 20.) Mara nyingi, “hekima ya ulimwengu huu” huchochea tamaa za mwili. Baadhi ya Wakristo huko Pergamamu na Thiatira waliwaiga watu waliowazunguka ambao walikuwa na maadili mapotovu na waliabudu sanamu. Yesu aliyapatia makutaniko hayo mawili shauri kali kwa sababu ya kuvumilia uasherati. (Ufu. 2:14, 20) Leo, tunashawishiwa kukubali maoni yasiyofaa. Huenda watu wa familia yetu na marafiki wakajaribu kutusadikisha kwamba tuna msimamo mkali sana na kwamba hatupaswi kufuata sheria za Yehova. Kwa mfano, huenda wakadai kwamba si jambo muhimu kuendelea kuwa safi kiadili na viwango vya maadili vya Biblia vimepitwa na wakati.

11. Tunaposimama imara, tunapaswa kuepuka nini?

11 Nyakati nyingine, huenda tukafikiri kwamba mwongozo ambao Yehova anatupatia hautoshi. Hata huenda tukashawishiwa ‘kupita mambo yaliyoandikwa.’ (1 Kor. 4:6) Viongozi wa kidini katika siku za Yesu walikuwa na hatia ya dhambi hiyo, waliongeza sheria zao kwenye Sheria waliyopewa na Mungu, na hivyo kufanya iwe vigumu kwa watu wa kawaida kuifuata Sheria. (Mt. 23:4) Yehova anatupatia mwongozo ulio wazi kupitia Neno lake na tengenezo lake. Hatupaswi kuongeza sheria zetu kwenye maagizo anayotupatia. (Met. 3:5-7) Kwa hiyo, hatupiti mambo yaliyoandikwa katika Biblia au kuwawekea sheria waabudu wenzetu kuhusu mambo ya kibinafsi.

12. Shetani anaendelezaje “udanganyifu mtupu”?

12 Udanganyifu. Shetani anatumia “udanganyifu mtupu” na “mambo ya msingi ya ulimwengu” huu ili kuwapotosha watu na kusababisha migawanyiko. (Kol. 2:8) Katika karne ya kwanza, mambo hayo yalitia ndani falsafa zilizotegemea mawazo ya wanadamu, mafundisho ya Wayahudi yasiyotegemea Maandiko, na fundisho la kwamba Wakristo wanapaswa kufuata Sheria ya Musa. Huo ulikuwa udanganyifu kwa sababu ulifanya watu waache kumkazia fikira yule aliye Chanzo cha hekima ya kweli, Yehova. Leo, Shetani anatumia vyombo vya habari na mitandao ya kijamii ili kusambaza uvumi usio na msingi na habari za uwongo zinazoenezwa na viongozi wa kisiasa. Tulijionea jambo hilo wakati wa janga la COVID-19. c Mashahidi wa Yehova waliosikiliza mwongozo kutoka kwenye tengenezo letu, waliepuka mahangaiko ambayo yaliwapata wale waliosikiliza habari za uwongo.​—Mt. 24:45.

13. Kwa nini tunapaswa kujilinda dhidi ya mambo yanayokengeusha fikira?

13 Mambo yanayokengeusha fikira. Tunapaswa kuendelea kukazia fikira “mambo muhimu zaidi.” (Flp. 1:9, 10) Mambo yanayokengeusha fikira yanaweza kuchukua muda na nguvu zetu nyingi na hivyo tushindwe kufanya mambo yanayofaa. Mambo ya kawaida maishani—kama vile kula, kunywa, burudani, na kazi ya kimwili—yanaweza kutukengeusha fikira ikiwa tutayaona kuwa mambo muhimu zaidi maishani. (Luka 21:34, 35) Isitoshe, kila siku tunasikia habari kuhusu mizozo katika jamii na mijadala ya kisiasa. Hatupaswi kuruhusu mambo hayo yatukengeushe fikira. La sivyo, huenda tukaanza kuunga mkono upande fulani katika akili na moyo wetu. Shetani anatumia mbinu hizo zote zilizotajwa akiwa na lengo la kudhoofisha azimio letu la kufanya mambo yanayofaa. Acheni tuone jinsi tunavyoweza kupinga jitihada zake na kubaki imara.

TUNAWEZAJE KUENDELEA KUBAKI IMARA?

Ili usimame imara, tafakari kuhusu wakfu na ubatizo wako, jifunze Neno la Mungu na kulitafakari, sitawisha moyo imara, na umtumaini Yehova (Tazama fungu la 14 hadi 18)

14. Ni jambo gani moja ambalo linaweza kutusaidia kubaki imara upande wa Yehova?

14 Fikiria kuhusu wakfu na ubatizo wako. Ulichukua hatua hizo kwa sababu ulitaka kusimama upande wa Yehova. Kumbuka mambo ambayo yalikusaidia kusadiki kwamba umepata kweli. Ulipata ujuzi sahihi kumhusu Yehova na ukaanza kumheshimu na kumpenda akiwa Baba yako wa mbinguni. Ulisitawisha imani na ukachochewa kutubu. Moyo wako ulikuchochea kuacha mazoea yasiyofaa na kuishi kulingana na mapenzi ya Mungu. Ulifarijika ulipotambua kwamba Mungu amekusamehe. (Zab. 32:1, 2) Ulihudhuria mikutano ya Kikristo na ukaanza kuwaambia wengine kuhusu mambo mazuri uliyokuwa unajifunza. Sasa ukiwa Mkristo aliyejiweka wakfu na kubatizwa, unatembea kwenye barabara ya uzima ukiwa umeazimia kuendelea kutembea katika barabara hiyo.​—Mt. 7:13, 14.

15. Kwa nini kujifunza na kutafakari kunatunufaisha?

15 Jifunze Neno la Mungu na kulitafakari. Kama vile mti unavyoweza kuwa imara kwa sababu ya mizizi yenye kina, tunaweza kubaki imara ikiwa imani yetu imetia mizizi kabisa katika Neno la Mungu. Mti unapozidi kukua, mizizi yake huzidi kupenya ardhini na kusambaa. Tunapojifunza na kutafakari, tunaimarisha imani yetu na kusadiki hata zaidi kwamba njia za Mungu zinafaa kabisa. (Kol. 2:6, 7) Tafakari jinsi maagizo, mwongozo, na ulinzi wa Yehova ulivyowasaidia watumishi wake nyakati za kale. Kwa mfano, Ezekieli alimkazia uangalifu malaika alipokuwa akipima kwa makini vipimo vya hekalu kwenye maono. Maono hayo yalimwimarisha Ezekieli na yanatupatia masomo hususa kuhusu jinsi tunavyoweza kuunga mkono viwango vya Yehova vya ibada safi. d (Eze. 40:1-4; 43:10-12) Sisi pia tunanufaika tunapotenga wakati ili kujifunza na kutafakari mambo mazito zaidi ya Neno la Mungu.

16. Moyo imara ulimlindaje Bob? (Zaburi 112:7)

16 Sitawisha moyo imara. Mfalme Daudi alitangaza kwamba angeendelea kumpenda Yehova alipoimba hivi: “Moyo wangu uko imara, Ee Mungu.” (Zab. 57:7) Sisi pia tunaweza kuwa na moyo imara kwa kumtegemea kabisa Yehova. (Soma Zaburi 112:7.) Fikiria jinsi hilo lilivyomsaidia Bob, aliyetajwa awali. Alipojulishwa kwamba damu ingekuwa hapo karibu ikiwa ingehitajika, mara moja alijibu kwamba ikiwa kuna uwezekano wowote wa kutiwa damu angeondoka kwenye hospitali hiyo mara moja. Baadaye, Bob alisema hivi: “Sikuwa na shaka wala wasiwasi kuhusu jambo ambalo lingenipata.”

Ikiwa tumejenga msingi imara wa kiroho, tunaweza kuendelea kuwa thabiti hata tukabili majaribu gani (Tazama fungu la 17)

17. Tunajifunza nini kutokana na kisa cha Bob? (Tazama pia picha.)

17 Bob alikuwa thabiti kwa sababu alikuwa ameazimia kuwa imara muda mrefu kabla ya kwenda hospitalini. Kwanza, alitamani kumfurahisha Yehova. Pili, alijifunza kwa makini mambo ambayo Biblia na machapisho yetu yanayotegemea Biblia yanasema kuhusu utakatifu wa uhai na damu. Tatu, alikuwa na usadikisho kwamba kufuata mwongozo wa Yehova kungemletea baraka za kudumu. Sisi pia tunaweza kuwa na moyo thabiti hata tupatwe na majaribu gani.

Baraka na wanajeshi wake wanafuatilia kwa ujasiri jeshi la Sisera (Tazama fungu la 18)

18. Mfano wa Baraka unatufundishaje kumtumaini Yehova? (Tazama picha kwenye jalada.)

18 Mtumaini Yehova. Fikiria jinsi Baraka alivyofanikiwa kwa sababu ya kutumaini mwongozo wa Yehova. Ingawa hakukuwa na ngao wala mkuki katika nchi yote, Yehova alimwagiza aende vitani dhidi ya wanajeshi wenye silaha, walioongozwa na mkuu wa jeshi Mkanaani aliyeitwa Sisera. (Amu. 5:8) Nabii wa kike Debora alimwambia Baraka ashuke kwenye eneo tambarare ili kukutana na Sisera na magari yake 900. Ingawa ingekuwa vigumu kwa Waisraeli kupigana na magari hayo yenye kasi kwenye eneo tambarare, Baraka alitii. Wanajeshi walipokuwa wakishuka kwenye Mlima Tabori, Yehova alisababisha mvua kubwa inyeshe. Magari ya Sisera yakakwama kwenye matope, na Yehova akampa Baraka ushindi. (Amu. 4:1-7, 10, 13-16) Vivyo hivyo, Yehova atatupatia ushindi ikiwa tutamtumaini yeye na mwongozo anaotupatia kupitia tengenezo lake.​—Kum. 31:6.

AZIMIA KUENDELEA KUWA THABITI

19. Kwa nini unataka kuendelea kuwa thabiti?

19 Tutaendelea kupigana ili tubaki thabiti kadiri tunavyoendelea kuishi katika mfumo huu wa mambo. (1 Tim. 6:11, 12; 2 Pet. 3:17) Acheni tuazimie kwamba hatutarushwa huku na huku na mateso, hatutakubali kushinikizwa kwa njia isiyo ya wazi, hatutapotoshwa na njia ya kufikiri ya wanadamu, udanganyifu, na mambo yanayokengeusha fikira. (Efe. 4:14) Badala yake, acheni tusimame imara na thabiti katika ujitoaji wetu kwa Yehova na sikuzote kuendelea kutii amri zake. Wakati huohuo, tunapaswa kuwa wenye usawaziko. Katika makala inayofuata, tutachunguza jinsi Yehova na Yesu walivyo mifano mikamilifu ya kuonyesha usawaziko.

WIMBO 129 Tutaendelea Kuvumilia

a Tangu siku za Adamu na Hawa, Shetani ameendeleza wazo la kwamba watu wanapaswa kujiamulia wenyewe mambo yanayofaa na mambo yasiyofaa. Anataka tuwe na mtazamo kama huo kuelekea sheria za Yehova na kuelekea mwongozo wowote wa kitheokrasi tunaopokea. Makala hii itatusaidia kujilinda dhidi ya roho ya kujitegemea iliyo katika ulimwengu wa Shetani na kuimarisha azimio letu la kusimama imara upande wa Yehova.

b Ili kupata maelezo zaidi ya jinsi Mkristo anavyoweza kutii maoni ya Mungu kuhusu damu, tazama somo la 39 katika kitabu Furahia Maisha Milele!

c Tazama makala “Jilinde Dhidi ya Habari za Uwongo” iliyo kwenye jw.org.