Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 29

Je, Uko Tayari kwa Ajili ya Dhiki Kuu?

Je, Uko Tayari kwa Ajili ya Dhiki Kuu?

“Iweni tayari.”​—MT. 24:44.

WIMBO 150 Mtafute Mungu Upate Ukombozi

MUHTASARI a

1. Kwa nini ni jambo la hekima kujitayarisha kwa ajili ya misiba?

 KUJITAYARISHA kunaweza kuokoa uhai wetu. Kwa mfano, msiba unapotokea ni rahisi kwa watu waliojitayarisha kwa ajili ya msiba huo kuokoka na kuwasaidia wengine. Shirika moja la kutoa msaada huko Ulaya linasema hivi: “Matayarisho mazuri yanaweza kuokoa uhai.”

2. Kwa nini tunapaswa kujitayarisha kwa ajili ya dhiki kuu? (Mathayo 24:44)

2 “Dhiki kuu” itaanza ghafla. (Mt. 24:21) Hata hivyo, tofauti na misiba mingine mingi, tunatarajia kwamba dhiki kuu itatokea. Miaka 2,000 hivi iliyopita, Yesu aliwaonya wafuasi wake wajitayarishe kwa ajili ya siku hiyo. (Soma Mathayo 24:44.) Ikiwa tumejitayarisha, itakuwa rahisi zaidi kwetu kuvumilia kipindi hicho kigumu na kuwasaidia wengine wafanye hivyo pia.​—Luka 21:36.

3. Sifa ya uvumilivu, huruma, na upendo zitatusaidiaje kujitayarisha kwa ajili ya dhiki kuu?

3 Fikiria sifa tatu ambazo zinaweza kutusaidia kujitayarisha kwa ajili ya dhiki kuu. Tutatendaje ikiwa tutaambiwa tuhubiri ujumbe mkali wa hukumu na kupingwa na watu wasioamini? (Ufu. 16:21) Tutahitaji sifa ya uvumilivu ili kumtii Yehova, tukitumaini kwamba atatulinda. Tutafanya nini ikiwa ndugu zetu watapoteza baadhi ya mali zao au mali zao zote? (Hab. 3:17, 18) Tutahitaji sifa ya huruma ili tuchochewe kuwasaidia. Tutatendaje ikiwa baada ya kushambuliwa na muungano wa mataifa, tutalazimika kuishi na ndugu na dada zetu kwa muda fulani katika nyumba moja? (Eze. 38:10-12) Tutahitaji kuwaonyesha upendo wenye nguvu ili tufaulu kukabiliana na kipindi hicho kigumu.

4. Biblia inaonyeshaje kwamba tunapaswa kuendelea kusitawisha sifa ya uvumilivu, huruma, na upendo?

4 Neno la Mungu linatutia moyo tuendelee kusitawisha sifa ya uvumilivu, huruma, na upendo. Andiko la Luka 21:19 linasema: “Mkivumilia, mtauokoa uhai wenu.” Andiko la Wakolosai 3:12 linasema: “Jivikeni . . . huruma.” Andiko la 1 Wathesalonike 4:9, 10 linasema: “Ninyi wenyewe mmefundishwa na Mungu kupendana. . . . Hata hivyo, tunawahimiza, akina ndugu, endeleeni kufanya hivyo kwa ukamili zaidi.” Mistari hiyo yote iliandikwa kwa ajili ya wanafunzi ambao tayari walikuwa wameonyesha sifa ya uvumilivu, huruma, na upendo. Hata hivyo, walipaswa kuendelea kusitawisha sifa hizo. Ni lazima tufanye hivyo pia. Ili kutusaidia kufanya hivyo, tutachunguza jinsi ambavyo Wakristo wa karne ya kwanza walionyesha kila moja kati ya sifa hizo. Kisha tutaona jinsi tunavyoweza kuwaiga wanafunzi hao, na hivyo kuthibitisha kwamba tuko tayari kwa ajili ya dhiki kuu.

IMARISHA UVUMILIVU WAKO

5. Wakristo wa karne ya kwanza walivumiliaje majaribu yao?

5 Wakristo wa karne ya kwanza walihitaji kuvumilia. (Ebr. 10:36) Licha ya kushughulika na matatizo ambayo huwapata watu wote, pia walikabili majaribu mengine ya ziada. Wengi wao waliteswa, si tu na viongozi wa kidini Wayahudi na maofisa wa serikali Waroma, bali pia na watu wa familia zao wenyewe. (Mt. 10:21) Na wakati mwingine katika kutaniko walihitaji kukabiliana na uvutano wa waasi-imani na mafundisho yao yaliyosababisha mgawanyiko. (Mdo. 20:29, 30) Ingawa hivyo, Wakristo hao walivumilia. (Ufu. 2:3) Walifanya hivyo jinsi gani? Walitafakari mifano ya watu wanaotajwa katika Maandiko ambao walivumilia, kama vile Ayubu. (Yak. 5:10, 11) Walisali ili wapate nguvu. (Mdo. 4:29-31) Na walikazia fikira matokeo mazuri ambayo wangepata kwa kuvumilia.​—Mdo. 5:41.

6. Unajifunza nini kutokana na jambo ambalo Merita alifanya ili kuvumilia upinzani?

6 Sisi pia tunaweza kuvumilia ikiwa tutajifunza kwa ukawaida mifano ya watu waliovumilia iliyo katika Neno la Mungu na pia katika machapisho yetu, na kutafakari kuwahusu. Hivyo ndivyo alivyofanya Merita, dada anayeishi nchini Albania, na akafaulu kuvumilia upinzani mkali kutoka kwa familia yake. Anasema hivi: “Nilitiwa moyo sana nilipojifunza simulizi la Ayubu katika Biblia. Ayubu aliteseka sana—hakujua yule aliyesababisha majaribu yake—ingawa hivyo alisema hivi: “Mpaka nitakapokufa, sitaukana utimilifu wangu!” (Ayu. 27:5) Nilifikiria jinsi majaribu yangu yalivyo madogo sana kwa kulinganisha na majaribu ya Ayubu. Tofauti naye, nilijua yule aliyesababisha majaribu hayo.”

7. Hata ikiwa sasa hatukabiliani na jaribu kali, tunapaswa kujifunza kufanya nini?

7 Sisi pia tunaweza kusitawisha sifa ya uvumilivu kwa kuzungumza na Yehova kwa ukawaida kuhusu mambo yanayotuhangaisha. (Flp. 4:6; 1 The. 5:17) Labda sasa hukabiliani na jaribu kali. Hata hivyo, je, wewe hutafuta mwongozo wa Yehova kila mara unapokasirika, unapochanganyikiwa, au kulemewa na hisia? Ikiwa sasa unamwomba Mungu msaada kwa ukawaida unapokabiliana na changamoto za kila siku, hutasita kufanya hivyo utakapokabili changamoto kubwa zaidi wakati ujao. Utakuwa na uhakika kwamba Yehova anajua kihususa wakati na jinsi ya kukusaidia.​—Zab. 27:1, 3.

UVUMILIVU

Kila jaribu tunalovumilia linaweza kutusaidia kuvumilia jaribu linalofuata (Tazama fungu la 8)

8. Mfano wa Mira unaonyeshaje kwamba kuvumilia majaribu sasa kunaweza kutusaidia kuvumilia majaribu wakati ujao? (Yakobo 1:2-4) (Tazama pia picha.)

8 Itakuwa rahisi zaidi kwetu kuvumilia dhiki kuu wakati ujao ikiwa sasa tunavumilia majaribu. (Rom. 5:3) Kwa nini tunasema hivyo? Ndugu wengi wametambua kwamba kila jaribu la imani walilovumilia liliwasaidia kuvumilia jaribu lililofuata. Uvumilivu uliwasaidia kuimarisha imani yao kwamba Yehova yuko tayari na anataka kuwasaidia. Kisha imani yao iliwasaidia kuvumilia jaribu lililofuata. (Soma Yakobo 1:2-4.) Mira, painia anayeishi nchini Albania, ametambua kwamba mambo ambayo alivumilia zamani yanamsaidia kuendelea kuvumilia. Anasema wakati mwingine anahisi kwamba yeye tu ndiye anayepatwa na matatizo mengi sana. Lakini anakumbuka mambo ambayo Yehova amefanya ili kumsaidia katika kipindi cha miaka 20 iliyopita, kisha anajiambia hivi: ‘Endelea kuwa mwaminifu. Usiache kumtumikia Yehova sasa, tayari amekusaidia kuvumilia mambo mengi magumu.’ Wewe pia unaweza kutafakari jinsi ambavyo tayari Yehova amekusaidia kuvumilia. Uwe na uhakika kwamba anatambua kila mara unapovumilia jaribu naye atakuthawabisha. (Mt. 5:10-12) Kisha dhiki kuu itakapoanza, tayari utakuwa umejifunza jinsi ya kuvumilia na utaazimia kuendelea kuvumilia.

ONYESHA HURUMA

9. Kutaniko la Antiokia ya Siria lilionyeshaje huruma?

9 Fikiria jambo lililotokea Wakristo huko Yudea walipokabili njaa kali. Kutaniko la Antiokia ya Siria liliposikia kuhusu njaa hiyo, bila shaka walihisi huruma kuelekea ndugu zao huko Yudea. Basi wakaonyesha huruma yao kwa matendo. “Wakaamua kila mmoja kulingana na uwezo wake, watume msaada kwa akina ndugu walioishi Yudea.” (Mdo. 11:27-30) Ingawa akina ndugu waliokabili njaa waliishi eneo la mbali, Wakristo huko Antiokia waliazimia kuwasaidia.​—1 Yoh. 3:17, 18.

HURUMA

Misiba ya asili inaweza kutupatia nafasi ya kuonyesha huruma (Tazama fungu la 10)

10. Tunaweza kuonyesha huruma kwa njia gani waabudu wenzetu wanapopatwa na msiba? (Tazama pia picha.)

10 Leo, sisi pia tunaweza kuonyesha huruma tunapopata habari kwamba waabudu wenzetu wamepatwa na msiba. Tunaitikia upesi—labda kwa kuwauliza wazee ikiwa tunaweza kusaidia katika kazi ya kutoa msaada, kwa kutoa mchango kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote, au kwa kusali kwa ajili ya wale walioathiriwa na msiba. b (Met. 17:17) Kwa mfano, mwaka wa 2020, zaidi ya Halmashauri 950 za Kutoa Msaada ziliundwa ulimwenguni pote ili kuwasaidia wale walioathiriwa na janga la COVID-19. Tunathamini sana kazi iliyofanywa na Halmashauri za Kutoa Msaada. Wakichochewa na huruma kwa ajili ya ndugu na dada zao, wamesambaza vifaa vya msaada, wameandaa msaada wa kiroho, na katika visa vingine wamerekebisha au kujenga upya nyumba za akina ndugu na sehemu za ibada.​—Linganisha 2 Wakorintho 8:1-4.

11. Ni kwa njia gani matendo ya huruma yanamletea utukufu Baba yetu wa mbinguni?

11 Tunapoonyesha huruma wakati wa msiba, wengine wanaona jinsi tunavyojidhabihu. Kwa mfano, mwaka wa 2019, Kimbunga Dorian kiliharibu Jumba la Ufalme huko Bahamas. Ndugu zetu walipokuwa wakijenga upya jumba hilo, walimwomba mwanakandarasi ambaye si Shahidi awape gharama ya kazi ambayo ilihitaji kufanywa. Aliwaambia hivi: “Ningependa kutoa mchango . . . wa mashine, wafanyakazi, na vifaa vya ujenzi. . . . Ningependa kufanya hivyo kwa ajili ya tengenezo lenu. Nimeguswa moyo na jinsi mnavyowatendea rafiki zenu.” Watu wengi ulimwenguni hawamjui Yehova. Lakini wengi wao wanaona matendo ya Mashahidi wa Yehova. Ni pendeleo kujua kwamba matendo yetu ya huruma yanaweza kuwachochea watu watamani kujifunza kumhusu Yehova ambaye ni “tajiri katika rehema”!—Efe. 2:4.

12. Kusitawisha huruma leo kunatusaidiaje kujitayarisha kwa ajili ya dhiki kuu? (Ufunuo 13:16, 17)

12 Kwa nini tutahitaji kuonyesha huruma wakati wa dhiki kuu? Biblia inaonyesha kwamba wale ambao hawaungi mkono serikali za ulimwengu huu watakabili changamoto—iwe ni sasa au wakati wa dhiki kuu. (Soma Ufunuo 13:16, 17.) Huenda ndugu na dada zetu wakahitaji msaada ili kupata mahitaji ya msingi. Mfalme wetu, Kristo Yesu, atakapokuja kutekeleza hukumu, tungependa atupate tukionyesha huruma, kisha atupatie mwaliko wa ‘kuurithi Ufalme.’​—Mt. 25:34-40.

IMARISHA UPENDO WAKO

13. Kulingana na Waroma 15:7, Wakristo wa karne ya kwanza waliimarishaje upendo kati yao?

13 Upendo ndiyo sifa iliyowatambulisha Wakristo wa karne ya kwanza. Lakini je, ilikuwa rahisi kwao kuonyesha upendo? Fikiria watu wa malezi mbalimbali waliokuwa katika kutaniko la Roma. Kati yao kulikuwa na Wayahudi ambao tangu utotoni walizoezwa kutii Sheria ya Musa, na pia kulikuwa na Watu wa Mataifa ambao walikuwa na malezi tofauti kabisa. Inaelekea kwamba baadhi ya Wakristo walikuwa watumwa na wengine walikuwa watu huru—au hata baadhi yao walimiliki watumwa. Wakristo hao wangeshindaje tofauti hizo na kuimarisha upendo wao? Mtume Paulo aliwahimiza ‘wakaribishane.’ (Soma Waroma 15:7.) Alimaanisha nini? Neno lililotafsiriwa ‘karibisha’ linamaanisha kumpokea mtu kwa fadhili, au kwa ukarimu kama vile nyumbani au katika kikundi cha marafiki. Kwa mfano, Paulo alimwambia Filemoni jinsi ya kumkaribisha Onesimo, mtumwa aliyekuwa amekimbia: “Mpokee kwa fadhili.” (Flm. 17) Na Akila na Prisila walimkaribisha Apolo ambaye hakujua mengi kuhusu Ukristo kwa ‘kumchukua’ ajiunge nao. (Mdo. 18:26) Badala ya kuruhusu watenganishwe na tofauti katika malezi yao, Wakristo hao walishinda tofauti zao na walikaribishana.

UPENDO

Tunahitaji upendo kutoka kwa ndugu na dada zetu wote (Tazama fungu la 15)

14. Anna na mume wake walionyeshaje upendo?

14 Sisi pia tunaweza kuwaonyesha upendo ndugu na dada zetu kwa kuwakaribisha wawe rafiki zetu. Wao pia watachochewa kutuonyesha upendo. (2 Kor. 6:11-13) Fikiria kisa cha Anna na mume wake. Muda mfupi baada ya kuhamia kwenye mgawo wao mpya wa umishonari magharibi mwa Afrika, janga la COVID-19 lilianza. Baada ya kuwasili, hawangeweza kukutana uso kwa uso na washiriki wa kutaniko lao. Wenzi hao wa ndoa walionyeshaje upendo wao? Walitumia video katika mtandao kuzungumza na akina ndugu na dada na wakawaambia jinsi ambavyo wanatamani kuwafahamu vizuri. Familia katika kutaniko hilo ziliguswa moyo, nao pia wakaanza kuwapigia simu kwa ukawaida na kuwaandikia ujumbe. Kwa nini wenzi hao wa ndoa walichukua hatua ya kwanza? Anna anasema hivi: “Matendo ya upendo ambayo mimi na familia yangu tumeonyeshwa katika nyakati nzuri na nyakati ngumu yamebaki katika moyo na akili yangu na yamenichochea kuonyesha upendo.”

15. Unajifunza nini kutokana na mfano wa Vanessa kuhusu kuwapenda ndugu na dada zetu wote? (Tazama pia picha.)

15 Wengi wetu tunashirikiana na makutaniko yenye ndugu na dada kutoka katika malezi mbalimbali na wenye nyutu mbalimbali. Tunaweza kuimarisha upendo wetu kuelekea watu wote kwa kukazia fikira sifa zao nzuri. Ilikuwa vigumu kwa dada anayeitwa Vanessa, ambaye anatumikia huko New Zealand, kushirikiana na baadhi ya watu katika kutaniko lao. Lakini akaamua kutumia muda mwingi zaidi kushirikiana na wale ambao walikuwa na sifa ambazo hakupenda, badala ya kuwaepuka. Kufanya hivyo kulimsaidia kuona sifa ambazo Yehova anapenda kuwahusu. Anasema hivi: “Tangu mume wangu alipoanza kutumikia akiwa mwangalizi wa mzunguko tunashirikiana na ndugu na dada wengi zaidi walio na nyutu mbalimbali na ni rahisi zaidi kwangu kushirikiana nao. Sasa ninapenda nyutu mbalimbali. Bila shaka, Yehova pia anapenda unamna-namna huo kwa sababu ametuvuta kwenye kikundi hicho chenye watu wa malezi mbalimbali.” Tunapojifunza kuwaona wengine kama Yehova anavyowaona, tunathibitisha kwamba tunawapenda.​—2 Kor. 8:24.

Wakati wa dhiki kuu, tutapata ulinzi ambao Yehova ametuahidi ikiwa tutaendelea kuwa na umoja na waabudu wenzetu (Tazama fungu la 16)

16. Kwa nini tutahitaji kuonyesha upendo wakati wa dhiki kuu? (Tazama pia picha.)

16 Tutahitaji kuonyeshana upendo wakati wa dhiki kuu. Dhiki kuu itakapoanza tutapata wapi ulinzi? Fikiria jambo ambalo Yehova aliwaagiza watu wake wafanye Babiloni la kale liliposhambuliwa: “Nendeni, watu wangu, ingieni katika vyumba vyenu vya ndani, na mfunge milango nyuma yenu. Jificheni kwa muda mfupi mpaka ghadhabu itakapopita.” (Isa. 26:20) Inaonekana kwamba maneno hayo yanatuhusu pia sisi ambao tutakabiliana na dhiki kuu. Huenda ‘vyumba vya ndani’ vinarejelea makutaniko yetu. Wakati wa dhiki kuu, tutapata ulinzi ambao Yehova ametuahidi ikiwa tutadumisha umoja na waabudu wenzetu. Kwa hiyo, tunapaswa kujitahidi sasa, si kuwavumilia tu ndugu na dada zetu, bali kuwa na upendo mwingi kuwaelekea. Huenda wokovu wetu utategemea jambo hilo!

JITAYARISHE SASA

17. Ikiwa tutajitayarisha sasa, tutafaulu kufanya nini wakati wa dhiki kuu?

17 “Ile siku kuu ya Yehova” itawasababishia wanadamu taabu. (Sef. 1:14, 15) Watu wa Yehova pia watapatwa na mateso. Lakini ikiwa tutajitayarisha sasa tutafaulu kuendelea kuwa watulivu na kuwasaidia wengine. Tutavumilia matatizo yoyote ambayo tutakabili. Waabudu wenzetu wakiteseka, tutajitahidi kuwasaidia kwa kuwaonyesha huruma na kwa kuwaandalia mahitaji yao. Na tutakaa karibu na ndugu na dada zetu ambao tayari tumesitawisha upendo kuwaelekea. Kisha Yehova atatuthawabisha kwa kutupatia uzima wa milele katika ulimwengu ambao hautakuwa na msiba wala dhiki yoyote.​—Isa. 65:17.

WIMBO 144 Kaza Macho Kwenye Zawadi!

a Dhiki kuu itaanza hivi karibuni. Sifa ya uvumilivu, huruma, na upendo zitatusaidia tuwe tayari kwa ajili ya matukio ambayo hayajawahi kutokea kamwe. Tutaona jinsi Wakristo wa mapema walivyositawisha sifa hizo, jinsi tunavyoweza kufanya hivyo leo, na jinsi sifa hizo zitakavyotusaidia kuwa tayari kwa ajili ya dhiki kuu.

b Wale ambao wangependa kusaidia katika mradi wa kutoa msaada, kwanza wanapaswa kujaza fomu ya Ombi la Kujitolea Katika Kazi ya Usanifu na Ujenzi (DC-50) au Fomu ya Ombi la Kuwa Mjitoleaji (A-19), kisha wasubiri kualikwa kusaidia kwenye mradi.