Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 32

Mwige Yehova—Uwe Mwenye Usawaziko

Mwige Yehova—Uwe Mwenye Usawaziko

“Usawaziko wenu na ujulikane kwa watu wote.”​—FLP. 4:5.

WIMBO 89 Sikiliza, Tii, Upate Baraka

MUHTASARI a

Ungependa kuwa mti gani? (Tazama fungu la 1)

1. Ni kwa njia gani Wakristo wanapaswa kuwa kama mti? (Tazama pia picha.)

 “UPEPO hauwezi kuvunja mti unaoweza kujipinda.” Methali hiyo inakazia sifa muhimu ambayo inasaidia miti fulani isitawi, yaani, uwezo wa kujipinda. Ili kusitawi kiroho, Wakristo wanapaswa kuwa na uwezo wa kunyumbulika, tayari kujipinda. Jinsi gani? Tunapaswa kuwa wenye usawaziko kwa kunyumbulika hali zetu za kibinafsi zinapobadilika na kwa kuheshimu maoni na maamuzi ya wengine.

2. Ni sifa gani zitakazotusaidia kunyumbulika hali zinapobadilika, na tutachunguza nini katika makala hii?

2 Tukiwa watumishi wa Yehova, tunapaswa kuwa wenye usawaziko. Pia, tunapaswa kuwa wanyenyekevu na wenye huruma. Katika makala hii, tutachunguza jinsi sifa hizo zilivyowasaidia baadhi ya Wakristo wanyumbulike hali zilipobadilika. Pia, tutaona jinsi sifa hizo zinavyoweza kutusaidia. Lakini kwanza, acheni tujifunze kutoka kwa Yehova na Yesu ambao ni mifano mikamilifu ya kuonyesha usawaziko.

YEHOVA NA YESU NI WENYE USAWAZIKO

3. Ni nini kinachothibitisha kwamba Yehova ni mwenye usawaziko?

3 Yehova anaitwa “Mwamba” kwa sababu yuko thabiti na imara. (Kum. 32:4) Hata hivyo, pia ni mwenye usawaziko. Mambo yanapobadilika ulimwenguni, Mungu wetu anaendelea kunyumbulika ili kufanya kusudi lake litimie. Yehova aliwaumba wanadamu kwa mfano wake wakiwa na uwezo wa kunyumbulika hali zinapobadilika. Alituandalia kanuni zilizo wazi katika Biblia ambazo zinatusaidia kufanya maamuzi yenye hekima hata tukabili changamoto gani maishani. Mfano ambao Yehova ameweka na kanuni ambazo ametupatia zinathibitisha kwamba ingawa yeye ni “Mwamba,” pia Yehova ni mwenye usawaziko.

4. Toa mfano unaothibitisha kwamba Yehova ni mwenye usawaziko. (Mambo ya Walawi 5:7, 11)

4 Njia za Yehova ni kamilifu na zenye usawaziko. Yeye hunyumbulika anaposhughulika na wanadamu. Kwa mfano, fikiria jinsi Yehova alivyowatendea Waisraeli kwa usawaziko. Hakutarajia kila mtu atoe dhabihu ileile, iwe ni tajiri au maskini. Katika visa fulani, alimruhusu kila mtu atoe dhabihu kulingana na hali zake.​—Soma Mambo ya Walawi 5:7, 11.

5. Toa mfano ambao unaonyesha Yehova ni mnyenyekevu na ana huruma.

5 Unyenyekevu na huruma ya Yehova humchochea kuwa mwenye usawaziko. Kwa mfano, Yehova alionyesha unyenyekevu kabla ya kuharibu watu waovu huko Sodoma. Kupitia malaika wake, Yehova alimwagiza Loti mwadilifu akimbilie kwenye eneo lenye milima. Loti aliogopa kwenda huko. Basi, akaomba kwamba yeye na familia yake waruhusiwe kukimbilia huko Soari, mji mdogo ambao ulipaswa kuharibiwa. Yehova angeweza kusisitiza kwamba Loti anapaswa kufuata kikamili maagizo yaliyotolewa. Badala yake, alikubali ombi la Loti, ingawa hilo lilimaanisha kwamba mji wa Soari haungeharibiwa. (Mwa. 19:18-22) Karne nyingi baadaye, Yehova aliwaonyesha huruma wakaaji wa Ninawi. Alimtuma nabii Yona atangaze kuhusu uharibifu ambao ungelipata jiji hilo na wakaaji wake waovu. Lakini Waninawi walipotubu, Yehova aliwahurumia, naye hakuharibu jiji hilo.​—Yona 3:1, 10; 4:10, 11.

6. Toa mfano unaonyesha kwamba Yesu aliiga usawaziko wa Yehova.

6 Yesu aliiga usawaziko wa Yehova. Alitumwa duniani ili awahubirie “kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli.” Lakini alikuwa mwenye usawaziko alipokuwa akitimiza mgawo huo. Pindi moja, mwanamke asiye Mwisraeli alimsihi Yesu amponye binti yake ambaye alikuwa “anasumbuliwa kikatili na roho mwovu.” Kwa huruma, Yesu alifanya jambo ambalo mwanamke huyo alimwomba na akamponya binti yake. (Mt. 15:21-28) Fikiria mfano mwingine. Mwanzoni mwa huduma yake, Yesu alisema hivi: “Yeyote anayenikana . . . , mimi pia nitamkana.” (Mt. 10:33) Lakini je, alimkana Petro alimpomkana mara tatu? Hapana. Yesu alijua kwamba Petro alitubu na alikuwa mwenye imani. Baada ya kufufuliwa, Yesu alimtokea Petro na inaelekea alimhakikishia kwamba amemsamehe na anampenda.​—Luka 24:33, 34.

7. Kulingana na Wafilipi 4:5, tungependa kuwa na sifa gani?

7 Tumeona kwamba Yehova Mungu na Yesu Kristo ni wenye usawaziko. Namna gani sisi? Yehova anatarajia tuwe wenye usawaziko. (Soma Wafilipi 4:5.) Biblia moja inatafsiri hivi mstari huo: “Mjulikane kuwa watu wenye usawaziko.” Tunaweza kujiuliza hivi: ‘Je, watu wananiona kuwa mwenye usawaziko, mwenye kukubali sababu, na kuwavumilia wengine? Au je, wanaona kwamba ninashikilia maoni yangu, ni mkali, au mwenye kichwa kigumu? Je, ninasisitiza wengine wafanye mambo kwa njia ambayo ninafikiri kwamba mambo yanapaswa kufanywa? Au je, ninawasikiliza wengine na kukubaliana na maoni yao inapofaa?’ Kadiri tunavyozidi kuwa wenye usawaziko, ndivyo tunavyoonyesha kwamba tunamwiga Yehova na Yesu. Acheni tuchunguze hali mbili ambazo tunapaswa kuwa wenye usawaziko—hali zetu za kibinafsi zinapobadilika na wengine wanapokuwa na maoni au kufanya maamuzi yaliyo tofauti na yetu.

UWE MWENYE USAWAZIKO HALI ZINAPOBADILIKA

8. Ni nini kinachoweza kutusaidia kuwa wenye usawaziko hali zinapobadilika? (Tazama pia maelezo ya chini.)

8 Usawaziko unahusisha kunyumbulika hali zetu zinapobadilika. Mabadiliko hayo yanaweza kutusababishia matatizo tusiyotarajia. Huenda ukapatwa na ugonjwa ghafla. Au mabadiliko ya ghafla ya hali ya kiuchumi au ya kisiasa yanapotokea mahali tunapoishi yanaweza kuvuruga kabisa maisha yetu. (Mhu. 9:11; 1 Kor. 7:31) Huenda hata tukakabili hali ngumu tunapopata badiliko la mgawo wa kitheokrasi. Hata tukabili changamoto gani, tunaweza kufanikiwa kunyumbulika hali zinapobadilika ikiwa tutachukua hatua nne zifuatazo: (1) kubali kwamba mambo yamebadilika, (2) fikiria kuhusu wakati ujao, (3) kazia fikira mambo yanayojenga, na (4) uwasaidie wengine. b Acheni tuchunguze mifano halisi maishani inayoonyesha jinsi hatua hizo zinavyoweza kutusaidia.

9. Wenzi wa ndoa wamishonari walikabilianaje na majaribu yasiyotarajiwa?

9 Kubali kwamba mambo yamebadilika. Emanuele na Francesca walipewa mgawo wa umishonari katika nchi ya kigeni. Walipokuwa wanaanza kujifunza lugha na kufahamiana na akina ndugu kutanikoni, janga la COVID-19 lilitokea na wakalazimika kujitenga mbali na watu wengine. Kisha, mama ya Francesca akafa ghafla. Francesca alitamani sana kuwa na watu wa familia yake, lakini hangeweza kusafiri kwa sababu ya janga hilo. Alifauluje kukabiliana na mambo hayo yenye kuvunja moyo? Kwanza, Emanuele na Francesca walisali ili wapate hekima ya kushughulika na hali za kila siku. Yehova alijibu sala zao kwa kuwaandalia msaada wa kiroho wakati unaofaa. Kwa mfano, walitiwa moyo na ndugu mmoja aliyesema hivi katika mahojiano kwenye video: “Kadiri tunavyokawia kukubaliana na hali tunayokabili, shangwe yetu pia inakawia kurudi na hilo huathiri uwezo wetu wa kutumia fursa za kumtumikia Yehova mahali tulipo.” c Pili, walichochewa kuboresha ustadi wao wa kuhubiri kwa simu na hata walianzisha funzo la Biblia. Tatu, walikubali msaada na utegemezo kutoka kwa akina ndugu na dada wenyeji. Dada mmoja mwenye ufikirio, aliwatumia ujumbe mfupi kila siku wenye mstari wa Biblia kwa mwaka mmoja. Ikiwa tutakubali kwamba hali zimebadilika, tutapata shangwe katika mambo tunayoweza kufanya.

10. Dada mmoja alinyumbulika jinsi gani alipopatwa na mabadiliko makubwa maishani?

10 Fikiria kuhusu wakati ujao, na ukazie fikira mambo yanayojenga. Christina, dada mmoja kutoka Romania anayeishi nchini Japani, alivunjika moyo kutaniko la Kiingereza alilohudhuria lilipovunjwa. Hata hivyo, hakuendelea kufikiria wakati uliopita. Badala yake, alijitahidi kufanya yote aliyoweza katika kutaniko la Kijapani na akahubiri kwa bidii katika Kijapani. Alimwomba mwanamke ambaye walikuwa wakifanya kazi pamoja zamani amfundishe kuzungumza Kijapani vizuri zaidi. Mwanamke huyo alikubali kutumia Biblia na broshua Furahia Maisha Milele! kumfundisha Christina Kijapani. Christina hakuboresha tu uwezo wake wa kuzungumza Kijapani, bali pia mwanamke huyo alianza kupendezwa na kweli. Tunapokazia fikira wakati ujao na kuwa na mtazamo unaofaa, mabadiliko yasiyotarajiwa yanaweza kuleta baraka zisizotarajiwa.

11. Wenzi fulani wa ndoa walikabilianaje na matatizo ya kiuchumi?

11 Wasaidie wengine. Wenzi wa ndoa wanaoishi katika nchi ambayo kazi yetu imepigwa marufuku walikabili matatizo ya kifedha hali ya kiuchumi ilipoporomoka katika nchi yao. Walikabilianaje na hali hiyo? Kwanza, walirahisisha maisha yao. Kisha, badala ya kukazia fikira matatizo yao wenyewe, waliamua kukazia fikira jinsi ya kuwasaidia wengine kwa kushiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri. (Mdo. 20:35) Mume alisema hivi: “Kujishughulisha sana na huduma, kulitusaidia kutotumia muda mwingi kufikiria mambo yanayovunja moyo na tukapata muda mwingi wa kukazia fikira kufanya mapenzi ya Mungu.” Hali zetu zinapobadilika, tunapaswa kukumbuka kwamba ni jambo muhimu kuendelea kuwasaidia wengine, hasa kupitia huduma yetu ya Kikristo.

12. Mfano wa Mtume Paulo unawezaje kutusaidia kunyumbulika hali zinapobadilika katika huduma yetu?

12 Katika huduma yetu, tunahitaji kunyumbulika. Tunakutana na watu wenye imani na mitazamo mbalimbali na wanaotoka katika malezi mbalimbali. Mtume Paulo alibadilikana kulingana na hali na tunaweza kuiga mfano wake. Yesu alimweka rasmi Paulo kuwa “mtume kwa mataifa.” (Rom. 11:13) Akiwa na jukumu hilo, Paulo aliwahubiria Wayahudi, Wagiriki, watu wenye elimu, wakulima, watu walioheshimiwa, na wafalme. Ili kugusa mioyo ya watu hao mbalimbali, Paulo alikuwa “mambo yote kwa watu wa namna zote.” (1 Kor. 9:19-23) Alizingatia utamaduni, malezi, na imani ya wasikilizaji wake, na kubadilisha njia yake ya kuhubiri ili iwafae. Sisi pia tunaweza kupata matokeo mazuri katika huduma ikiwa tutakuwa tayari kubadili mazungumzo yetu ili yalingane na mahitaji ya wasikilizaji wetu.

HESHIMU MAONI YA WENGINE

Ikiwa tuna usawaziko, tutaheshimu maoni ya wengine (Tazama fungu la 13)

13. Tutaepuka hatari gani inayotajwa kwenye 1 Wakorintho 8:9 ikiwa tutaheshimu maoni ya wengine?

13 Usawaziko unatusaidia pia kuheshimu maoni ya wengine. Kwa mfano, kuna akina dada ambao wanapenda kujipamba usoni, na kuna wengine ambao hawapendi. Baadhi ya Wakristo hufurahia kunywa kileo kwa kiasi, lakini wengine huamua kwamba hawatakunywa. Wakristo wote wanatamani kuwa na afya nzuri, lakini wanachagua aina mbalimbali ya matibabu. Ikiwa tunafikiri kwamba sikuzote sisi tuko sahihi, huenda tukajaribu kuwashawishi wengine wafuate maoni yetu, jambo ambalo linaweza kuwakwaza wengine na kusababisha migawanyiko. Hatungependa kamwe kufanya hivyo! (Soma 1 Wakorintho 8:9; 10:23, 24) Acheni tuchunguze mifano miwili inayoonyesha jinsi kufuata kanuni za Kimaandiko kunavyoweza kutusaidia kuwa wenye usawaziko na kudumisha amani.

Ikiwa tuna usawaziko, tutaheshimu maoni ya wengine (Tazama fungu la 14)

14. Tunapaswa kukumbuka kanuni gani za Biblia kuhusu kuvaa na kujipamba?

14 Kuvaa na kujipamba. Badala ya kutupatia sheria kali kuhusu jinsi tunavyopaswa kuvaa, Yehova anatupatia kanuni. Tunapaswa kuvaa kwa njia ambayo inamfaa mtumishi wa Mungu, inayoonyesha usawaziko, kiasi, na “utimamu wa akili.” (1 Tim. 2:9, 10; 1 Pet. 3:3) Kwa hiyo, hatujielekezei fikira wenyewe kupitia jinsi tunavyovaa. Kanuni za Biblia pia zitawasaidia wazee wa kutaniko waepuke kuweka sheria zao wenyewe kuhusu mavazi na mitindo ya nywele. Kwa mfano, wazee katika kutaniko moja walitaka kuwasaidia baadhi ya ndugu vijana ambao waliiga mtindo fulani wa nywele fupi ambazo hazikuchanwa. Wazee wangewezaje kuwasaidia bila kuweka sheria? Mwangalizi wa mzunguko aliwashauri wazee wawaambie hivi ndugu hao: “Ikiwa uko jukwaani na wasikilizaji wanakazia fikira zaidi jinsi unavyoonekana badala ya mambo unayosema, basi kuna tatizo katika njia ambayo umevalia na kujipamba.” Maelezo hayo rahisi yalisuluhisha tatizo hilo bila kuwa na uhitaji wa kuweka sheria. d

Ikiwa tuna usawaziko, tutaheshimu maoni ya wengine (Tazama fungu la 15)

15. Ni kanuni na sheria gani za Biblia zinazotuongoza tunapofanya maamuzi kuhusu matibabu? (Waroma 14:5)

15 Matibabu. Kila Mkristo anapaswa kuamua jinsi atakavyotunza afya yake. (Gal. 6:5) Biblia ina sheria chache hususa, kama vile amri ya kuepuka damu na kuepuka kuwasiliana na roho, ambazo zinaongoza uamuzi wa Mkristo kuhusu matibabu. (Mdo. 15:20; Gal. 5:19, 20) Mambo mengine ni maamuzi ya kibinafsi. Baadhi ya watu wanatafuta tu matibabu kutoka kwa madaktari, na wengine hupendelea aina nyingine za matibabu. Ingawa huenda tukasadiki kwamba aina fulani ya matibabu ndiyo inayofaa, tunahitaji kuheshimu haki ya ndugu na dada zetu ya kujifanyia maamuzi kuhusu matibabu. Kuhusu hilo, tunapaswa kukumbuka mambo yafuatayo: (1) Ufalme wa Mungu ndio tu utakaoleta uponyaji wa kudumu. (Isa 33:24) (2) Kila Mkristo anapaswa ‘kusadiki kikamili’ jambo linalomfaa. (Soma Waroma 14:5.) (3) Hatuwahukumu wengine au kufanya wakwazike. (Rom. 14:13) (4) Wakristo wanaona umoja wa kutaniko kuwa jambo muhimu zaidi kuliko uhuru wao wa kujifanyia maamuzi ya kibinafsi. (Rom. 14:15, 19, 20) Ikiwa tutakumbuka mambo hayo, tutadumisha uhusiano wa karibu pamoja na ndugu na dada zetu, na kuchangia amani kutanikoni.

Ikiwa tuna usawaziko, tutaheshimu maoni ya wengine (Tazama fungu la 16)

16. Mzee anawezaje kuonyesha usawaziko anaposhughulika na wazee wenzake? (Tazama pia picha.)

16 Wazee wa kutaniko wanapaswa kuweka mfano mzuri kuhusu usawaziko. (1 Tim. 3:2, 3) Kwa mfano, mzee hapaswi kutarajia kwamba sikuzote maoni yake yatakubaliwa kwa sababu tu ana umri mkubwa kuliko wazee wengine. Anatambua kwamba roho ya Yehova inaweza kumchochea mzee yeyote katika baraza la wazee atoe mapendekezo ambayo yatachangia kufanya uamuzi wenye hekima. Na ikiwa hakuna kanuni ya Biblia inayovunjwa, wazee wenye usawaziko huunga mkono kwa hiari uamuzi wa wazee wengi katika baraza, hata ingawa walikuwa na pendekezo tofauti.

MANUFAA YA KUWA NA USAWAZIKO

17. Wakristo wenye usawaziko hupata baraka gani?

17 Wakristo wanapata baraka nyingi wanapokuwa na usawaziko. Tunakuwa na uhusiano mzuri zaidi na ndugu na dada zetu, na kutaniko linafurahia amani. Tunafurahia kushirikiana na watu wenye nyutu na tamaduni mbalimbali miongoni mwa waabudu wa Yehova wenye umoja. Zaidi ya yote, tunafurahi kujua kwamba tunamwiga Yehova, Mungu wetu mwenye usawaziko.

WIMBO 90 Tianeni Moyo

a Yehova na Yesu ni wenye usawaziko, nao wanataka tusitawishe sifa hiyo. Ikiwa tuna usawaziko, itakuwa rahisi kwetu kunyumbulika hali zetu zinapobadilika. Kwa mfano, hali yetu ya afya au ya kiuchumi inapobadilika. Pia, tutachangia amani na umoja kutanikoni.

b Tazama makala “Jinsi ya Kukabiliana na Mabadiliko” katika gazeti la Amkeni! Na. 4 2016.

c Tazama video yenye kichwa Mahojiano na Ndugu Dmitriy Mikhaylov, inayoambatana na makala “Yehova Anabadili Mateso Kuwa Ushahidi” katika Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha ya Kikristo la Machi-Aprili 2021.

d Ili kupata maelezo zaidi kuhusu kuvaa na kujipamba, tazama somo la 52 katika kitabu Furahia Maisha Milele!