Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

Upendezi wa Kibinafsi Huleta Baraka Maishani

Upendezi wa Kibinafsi Huleta Baraka Maishani

Nikiwa pamoja na mama yangu na dada yangu, Pat, 1948

“KANISA la Anglikana halifundishi ukweli. Eendelea kuutafuta.” Baada ya nyanya (bibi) yangu ambaye alikuwa mfuasi wa Kanisa la Anglikana kusema hivyo, mama yangu alianza kutafuta dini ya kweli. Hata hivyo, aliwapuuza Mashahidi wa Yehova na aliniambia nijifiche walipofika nyumbani kwetu jijini Toronto, Kanada. Lakini mdogo wake wa kike alipoanza kujifunza na Mashahidi mwaka wa 1950, mama yangu alijiunga naye. Walijifunza katika nyumba ya shangazi yangu na baadaye wakabatizwa.

Baba yangu alikuwa mzee katika kanisa la United Church of Canada, hivyo, kila Jumapili alituagiza mimi na dada yangu twende katika mafundisho ya kidini ya watoto, na baada ya hapo tulijiunga naye kwenye misa ya saa tano asubuhi. Alasiri tulienda na mama kwenye Jumba la Ufalme. Tulijionea wazi tofauti kati ya dini hizo mbili.

Nikiwa pamoja na familia ya Hutcheson wakati wa Kusanyiko la Kimataifa la Mapenzi ya Mungu, 1958

Mama aliwaeleza imani yake mpya rafiki zake wa karibu Bob na Marion Hutcheson, ambao pia walikubali kweli na kuwa Mashahidi wa Yehova. Mwaka wa 1958, ndugu na dada Hutcheson walinialika niende pamoja nao na wana wao watatu kwenye Kusanyiko la Kimataifa la Mapenzi ya Mungu huko New York City. Ninapokumbuka wakati huo, sasa ninatambua jitihada nyingi zilizohusika katika kunialika mimi pia, lakini kusanyiko hilo lilikuwa mojawapo ya pindi bora zaidi maishani mwangu.

UPENDEZI WA KIBINAFSI ULINISAIDIA KUFANYA MAAMUZI MAZURI

Nilipokuwa kijana, tuliishi katika shamba ambapo nilifurahia kuwatunza wanyama. Nilifikiria kuhusu kuwa daktari wa wanyama. Mama yangu alimwambia mzee wa kutaniko kuhusu jambo hilo. Kwa fadhili, mzee huyo alinikumbusha kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” na akaniambia nifikirie jinsi kuhudhuria chuo kikuu kwa miaka kadhaa kutakavyoathiri uhusiano wangu pamoja na Yehova. (2 Tim. 3:1) Matokeo ni kwamba niliamua sitaenda chuo kikuu.

Bado nilijiuliza nitafanya nini baada ya kumaliza shule ya sekondari. Ingawa nilishiriki katika utumishi wa shambani kila mwisho juma, sikufurahia huduma na sikuwazia ninaweza kuwa painia. Wakati huohuo, baba na mjomba wangu ambao hawakuwa Mashahidi walinitia moyo nifanye kazi ya wakati wote katika kampuni kubwa ya bima jijini Toronto. Mjomba wangu alikuwa na cheo kikubwa huko, hivyo nilikubali kazi hiyo.

Jijini Toronto, mara nyingi nilifanya kazi muda wa ziada na nilishirikiana na watu ambao hawakuwa Mashahidi, hivyo sikuhudhuria mikutano na sikuhubiri kwa ukawaida. Mwanzoni niliishi na babu yangu ambaye hakuwa Shahidi lakini baada ya kifo chake, nilihitaji kutafuta mahali pengine pa kuishi.

Ndugu na dada Hutcheson ambao niliandamana nao katika kusanyiko la mwaka wa 1958, walikuwa kama wazazi kwangu. Walinialika niishi nyumbani kwao na walinisaidia kukua kiroho. Nilibatizwa mwaka wa 1960, pamoja na John, mwana wao. John alianza upainia na hilo lilinichochea kuongeza bidii katika utumishi wa shambani. Akina ndugu kutanikoni walitambua maendeleo yangu ya kiroho, na hatimaye niliwekwa rasmi kuwa mtumishi wa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. a

MWANDAMANI MARIDADI NA KUANZA UPAINIA

Siku ya harusi yetu, 1966

Mwaka wa 1966, nilifunga ndoa na Randi Berge, painia mwenye bidii ambaye alikuwa tayari kutumikia kwenye eneo lenye uhitaji mkubwa. Mwangalizi wetu wa mzunguko alituonyesha upendezi wa kibinafsi, na akatutia moyo tusaidie kutaniko huko Orillia, Ontario. Hivyo tulifungasha mizigo yetu na kuhama.

Mara tu tulipofika Orillia, nilijiunga na Randi na kuwa painia wa kawaida. Tayari shauku yake ilikuwa imenichochea! Nilipoongeza bidii katika utumishi wa upainia, nilijionea shangwe ya kutumia Biblia na kuwaona watu wakiielewa kweli. Ilikuwa baraka kubwa kuwasaidia wenzi fulani wazuri wa ndoa walioishi huko Orillia kufanya mabadiliko maishani mwao na kuwa watumishi wa Yehova.

KUJIFUNZA LUGHA NA NJIA MPYA YA KUFIKIRI

Pindi moja nilipotembelea jiji la Toronto, nilikutana na Arnold MacNamara, ambaye alikuwa kati ya ndugu waliosimamia kazi Betheli. Aliniuliza ikiwa tungependa kuwa mapainia wa pekee. Mara moja nilimjibu hivi: “Bila shaka! Tutaenda sehemu yoyote isipokuwa Quebec!” Nilikuwa nimeathiriwa na maoni yasiyofaa ya watu wa Kanada waliozungumza Kiingereza, kuhusu misukosuko ya kijamii katika jimbo la Quebec lenye watu waliozungumza Kifaransa. Wakati huo, chama fulani cha kisiasa huko Quebec kilitaka jimbo hilo lijitenge na sehemu nyingine za Kanada.

Arnold alijibu hivi: “Kwa wakati huu, Quebec ndio mahali pekee ambapo ofisi ya tawi inawatuma mapainia wa pekee.” Mara moja nilikubali kwenda. Tayari nilijua kwamba Randi alitamani kutumikia huko. Baadaye, nilitambua huo ulikuwa moja kati ya uamuzi bora zaidi maishani mwetu!

Baada ya kujifunza Kifaransa kwa wiki tano, mimi na Randi pamoja na wenzi wengine wa ndoa tulienda huko Rimouski, kilomita 540 hivi kaskazini mashariki ya jiji la Montreal. Bado tulikuwa na mengi ya kujifunza, jambo hilo lilionekana wazi katika mkutano niliposoma baadhi ya matangazo. Nilisema kwamba katika kusanyiko linalofuata tutakuwa na “wajumbe wengi wa ndege anayeitwa mbuni” badala ya kusema “wajumbe kutoka Austria.”

Nyumba tuliyoiita “White House,” huko Rimouski

Huko Rimouski, sisi wanne tuliungwa mkono na dada wanne waseja wenye bidii na pia ndugu na dada Huberdeau na binti zao wawili. Ndugu na dada Huberdeau walikodi nyumba yenye vyumba saba vya kulala na mapainia wote walioishi humo walichangia kulipa kodi. Tuliita White House (Nyumba Nyeupe), kwa sababu sehemu ya mbele ya nyumba hiyo ilikuwa nyeupe. Kwa kawaida, kati ya watu 12 na 14 waliishi humo. Tukiwa mapainia wa pekee, mimi na Randi tulienda kuhubiri asubuhi, mchana, na jioni, na hivyo tulithamini kwamba sikuzote kulikuwa na mtu wa kuandamana nasi katika huduma—hata jioni ya majira ya baridi kali.

Tulikuwa na uhusiano wa karibu sana pamoja na mapainia hao waaminifu hivi kwamba wakawa kama familia yetu. Nyakati nyingine tuliketi pamoja na kuota moto au tulikuwa na siku ambayo sisi sote tulipika pamoja. Ndugu mmoja alikuwa mwanamuziki, hivyo, mara nyingi Jumamosi usiku tuliimba na kucheza dansi.

Eneo la kuhubiri la Rimouski lilizaa matunda! Katika kipindi cha miaka mitano, tulikuwa na shangwe ya kuona wanafunzi kadhaa wa Biblia wakifanya maendeleo na kubatizwa. Idadi ya wahubiri iliongezeka na kufikia wahubiri 35 hivi.

Huko Quebec, tulipata mazoezi bora ya kuwa waeneza injili. Tuliona jinsi Yehova alivyotusaidia katika huduma na alivyotosheleza mahitaji yetu ya kimwili. Pia, tulijifunza kuwapenda watu waliozungumza Kifaransa, lugha yao, na utamaduni wao—jambo lililotusaidia kupenda tamaduni nyingine pia.​—2 Kor. 6:13.

Bila kutarajia, ofisi ya tawi ilituomba tuhamie katika mji wa Tracadie, kwenye pwani ya mashariki ya New Brunswick. Jambo hilo lilitokeza changamoto kwa sababu tulikuwa tumetoka tu kutia sahihi mkataba wa kodi ya nyumba na nilikuwa na mkataba wa kufanya kazi ya kufundisha ya muda kwenye shule. Isitoshe, baadhi ya wanafunzi wetu wa Biblia walikuwa wametoka tu kuwekwa rasmi kuwa wahubiri na tulikuwa katikati ya ujenzi wa Jumba la Ufalme.

Tulisali mwisho juma wote kuhusu badiliko hilo na tukatembelea mji wa Tracadie, ambao ulikuwa tofauti sana na jiji la Rimouski. Lakini tulifikia mkataa kwamba kwa kuwa Yehova anataka twende huko, tutaenda huko. Tulimjaribu Yehova na tuliona jinsi alivyoondoa kila kipingamizi. (Mal. 3:10) Kama kawaida, sikuzote hali nzuri ya kiroho ya Randi, roho yake ya kujidhabihu, na ucheshi wake ulifanya changamoto ya kuhama iwe rahisi zaidi.

Mzee pekee katika kutaniko letu jipya alikuwa Robert Ross. Yeye pamoja na Linda mke wake, walikuwa wamefanya upainia huko na waliamua kubaki baada ya mtoto wao wa kwanza kuzaliwa. Ingawa walikuwa wakimtunza mvulana wao mdogo, walitutia sana moyo mimi na Randi kwa kutukaribisha kwa uchangamfu, na kwa bidii yao katika huduma ya shambani.

BARAKA ZA KUTUMIKIA MAHALI POPOTE UNAPOHITAJIKA

Majira ya baridi kali katika mzunguko wetu wa kwanza

Baada ya kufanya upainia katika mji wa Tracadie kwa miaka miwili, tulipata mgawo mwingine ambao hatukutarajia—mwaliko wa kutumikia katika kazi ya kuzungukia makutaniko. Tulitumikia kwenye mizunguko ya lugha ya Kiingereza kwa miaka saba na baadaye tulihamia kwenye mzunguko wa lugha ya Kifaransa huko Quebec. Léonce Crépeault, mwangalizi wetu wa wilaya huko Quebec alikuwa akinipongeza nilipotoa hotuba. Lakini sikuzote baadaye angeniuliza, “Unawezaje kufanya hotuba zako ziwafae zaidi wasikilizaji wako?” b Upendezi wa kibinafsi alionionyesha ulinisaidia nikazie fikira kufanya ufundishaji wangu uwe rahisi zaidi kueleweka na kutaja mambo hususa.

Kati ya migawo niliyofurahia zaidi ni ule niliokuwa nao mwaka wa 1978 kwenye Kusanyiko la Kimataifa la “Imani Ishindayo” jijini Montreal. Nilifanya kazi katika Idara ya Chakula. Tulikuwa tunatarajia wahudhuriaji 80,000, na kulikuwa na mpango mpya wa kuandaa chakula. Kila kitu kilikuwa kipya kabisa: vifaa, menyu, na njia ya kutayarisha chakula. Tulikuwa na trela kubwa 20 zilizotumika kama friji, na wakati mwingine ziliharibika. Kabla ya siku ya kwanza ya kusanyiko, hatukuweza kuingia kwenye uwanja wa kusanyiko ili kufanya maandalizi hadi saa sita usiku kwa sababu ya tukio la michezo lililokuwa limepangwa mapema. Na tulipaswa kuanza kuwasha majiko kabla ya mapambazuko ili kuandaa kiamsha kinywa! Tulikuwa tumechoka lakini nilijifunza mambo mengi kutokana na bidii, ukomavu, na ucheshi wa wajitoleaji wenzangu. Tulijenga uhusiano wa karibu ambao umedumu hadi leo. Ilikuwa shangwe kubwa kuhudhuria kusanyiko hilo la kihistoria huko Quebec, jimbo lilelile ambako ndugu na dada zetu waliteswa vikali wakati wa miaka ya 1940 na 1950.

Mimi na Randi tukisaidia kutayarisha kusanyiko huko Montreal, 1985

Nilijifunza mengi kutoka kwa waangalizi wenzangu katika makusanyiko yetu makubwa huko Montreal. Mwaka mmoja, David Splane ambaye sasa ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza alikuwa mwangalizi wa kusanyiko. Katika kusanyiko lingine, nilipoombwa kushughulikia mgawo huo, David aliniunga mkono kabisa.

Mwaka wa 2011, baada ya kufurahia miaka 36 ya kuzungukia makutaniko, nilialikwa nitumikie kama mwalimu ya Shule ya Wazee wa Kutaniko. Kwa miaka miwili mimi na Randi tulilala katika vitanda 75 tofauti, lakini tulifurahia sana kujidhabihu kwa njia hiyo. Mwishoni wa kila juma, wazee walijawa na shukrani, kwa sababu waliona jinsi Baraza Linaloongoza linavyohangaikia hali yao ya kiroho.

Baadaye, nilifundisha Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme. Mara nyingi wanafunzi walihisi kulemewa kwa sababu ya ratiba yenye mambo mengi: waliketi darasani saa saba kwa siku, na kila jioni kwa saa tatu walijisomea chumbani, na kila juma walikuwa na migawo minne au mitano. Mimi pamoja na mwalimu mwingine tuliwaeleza kwamba hawangeweza kufaulu bila msaada wa Yehova. Sikuzote nitakumbuka jinsi wanafunzi walivyoshangaa kuona kwamba kwa kumtegemea Yehova, walifaulu kutimiza mengi kuliko walivyotarajia.

UPENDEZI WA KIBINAFSI HULETA BARAKA ZA KUDUMU

Upendezi wa kibinafsi ambao mama yangu aliwaonyesha wengine uliwasaidia wanafunzi wake wa Biblia kufanya maendeleo na hata ulimsaidia baba yangu kubadili maoni yake kuhusu kweli. Siku tatu baada ya kifo cha mama, baba alitushangaza kwa kuhudhuria hotuba ya watu wote kwenye Jumba la Ufalme, na aliendelea kuhudhuria mikutano kwa miaka 26. Ingawa baba hakubatizwa, wazee waliniambia kwamba alikuwa wa kwanza kufika kwenye mikutano kila juma.

Pia, mama aliweka kielelezo bora kwangu na kwa dada zangu. Dada zangu watatu na waume wao wanamtumikia Yehova kwa uaminifu. Dada wawili wanatumikia kwenye ofisi za tawi—mmoja nchini Ureno na mwingine nchini Haiti.

Sasa mimi na Randi tunatumikia kama mapainia wa pekee jijini Hamilton, Ontario. Tulipokuwa katika kazi ya kuzungukia makutaniko tulifurahia kuandamana na wengine kwenye marudio na mafunzo yao ya Biblia. Lakini sasa tunafurahi kuwaona wanafunzi wetu wenyewe wakifanya maendeleo ya kiroho. Na tunapositawisha uhusiano wa karibu pamoja na ndugu na dada katika kutaniko letu jipya, tunatiwa moyo kuona jinsi Yehova anavyowategemeza katika nyakati nzuri na mbaya.

Tunapokumbuka wakati uliopita, tunathamini sana upendezi wa kibinafsi ambao watu wengi walituonyesha. Na sisi pia tumejitahidi kuwahangaikia sana wengine tukiwatia moyo wamtumikie Yehova kadiri wanavyoweza. (2 Kor. 7:6, 7) Kwa mfano, katika familia moja, mke, mwana, na binti walikuwa kwenye utumishi wa wakati wote. Nilimuuliza mume ikiwa amewahi kufikiria kuhusu kufanya upainia. Alijibu kwamba alikuwa akiwategemeza mapainia watatu. Basi nikamuuliza, “Je, unaweza kuwategemeza vizuri kuliko Yehova?” Nilimtia moyo afurahie utumishi ambao walikuwa wakifurahia. Alianza upainia baada ya miezi sita.

Mimi na Randi tutaendelea ‘kukiambia kizazi kijacho’ kuhusu ‘kazi za Yehova zinazostaajabisha,’ na tunatumaini kwamba watafurahia kumtumikia Yehova kama vile ambavyo sisi tumefurahia.​—Zab. 71:17, 18.

a Sasa anaitwa mwangalizi wa Mkutano wa Huduma na Maisha.

b Tazama simulizi la maisha la Léonce Crépeault katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Februari 2020, ukurasa wa 26-30.