Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Ufalme Wangu Si Sehemu ya Ulimwengu Huu”

“Ufalme Wangu Si Sehemu ya Ulimwengu Huu”

“Nimezaliwa kwa ajili ya hili, na kwa ajili ya hili nimekuja ulimwenguni, ili nitoe ushahidi kuhusu kweli.”—YOH. 18:37.

NYIMBO: 15, 74

1, 2. (a) Ulimwengu unazidi kugawanyika katika njia gani? (b) Tutajibu maswali gani katika makala hii?

AKIZUNGUMZIA kuhusu wakati uliopita, dada mmoja kutoka kusini mwa Ulaya anasema hivi: “Tangu nilipokuwa na umri mdogo, nilijionea tu ukosefu wa haki. Hivyo niliupinga mfumo wa kisiasa wa nchi yangu na kuunga mkono maoni yenye msimamo mkali. Isitoshe, kwa miaka mingi nilikuwa mpenzi wa mwanamume aliyekuwa gaidi.” Pia, mwanamume mmoja kutoka kusini mwa Afrika ambaye sasa ni ndugu yetu aliunga mkono matendo ya kikatili hapo awali. Anasema hivi: “Niliamini kwamba kabila langu lilikuwa bora kuliko makabila mengine, nami nikajiunga na chama fulani cha kisiasa. Tulifundishwa kuwaua maadui wetu kwa mikuki, kutia ndani watu wa kabila letu waliounga mkono vyama vingine vya kisiasa.” Dada mmoja anayeishi Ulaya ya kati anakiri hivi: “Nilikuwa mwenye ubaguzi, na nilimchukia mtu yeyote kutoka nchi nyingine au mtu wa dini tofauti na yangu.”

2 Leo, mtazamo ambao ndugu na dada hao walikuwa nao unazidi kuenea ulimwenguni. Vikundi vya kikatili vinavyopigania uhuru vinazidi kusitawi, migawanyiko ya kisiasa inazidi kushamiri, na katika nchi nyingi wenyeji wanazidi kuwachukia wageni wanaohamia. Kama Biblia ilivyotabiri, katika siku hizi za mwisho watu wa namna zote watakuwa “wasiotaka makubaliano yoyote.” (2 Tim. 3:1, 3) Ingawa ulimwengu unazidi kugawanyika, Wakristo wanaweza kulindaje umoja wao? Tunaweza kujifunza mambo mengi kutokana na jinsi Yesu alivyoshughulikia hali fulani katika karne ya kwanza, wakati ambapo vurugu za kisiasa zilisababisha migawanyiko. Acheni tuchunguze mambo matatu muhimu: Kwa nini Yesu alikataa kujihusisha kwa vyovyote na harakati za kupigania mabadiliko? Alionyeshaje umuhimu wa watumishi wa Mungu kuepuka kuunga mkono upande wowote katika mambo ya kisiasa? Na Yesu alitufundisha mambo gani yanayotusaidia kujua kwamba ni kosa kuwatendea wengine kwa ukatili hata hali iweje?

MTAZAMO WA YESU KUHUSU HARAKATI ZA KUPIGANIA UHURU

3, 4. (a) Wayahudi katika siku za Yesu walikuwa na matumaini gani ya kisiasa? (b) Hisia hizo ziliwafanya wanafunzi wa Yesu wawe na maoni gani?

3 Wayahudi wengi ambao Yesu aliwahubiria walitamani sana kuwa huru kutokana na utawala wa Roma. Wazeloti, yaani, Wayahudi wazalendo walichochea hisia hizo miongoni mwa watu. Wengi wa watu hao wenye misimamo mikali walifuata sera za Yuda Mgalilaya. Alikuwa masihi wa uwongo aliyewapotosha watu wengi katika karne ya kwanza. Mwanahistoria Myahudi Yosefo alisema kwamba Yuda “aliwachochea wananchi wenzake kuasi, na kuwaita waoga wale waliokubali kuwalipa Waroma ushuru.” Mwishowe, Waroma walimuua Yuda. (Mdo. 5:37) Baadhi ya Wazeloti walitenda kwa ukatili ili kufikia malengo yao.

4 Mbali na watu hao wenye misimamo mikali, Wayahudi wa kawaida walikuwa wakisubiri kwa hamu sana kuja kwa Masihi ambaye angeleta mabadiliko ya kisiasa. Walitarajia kwamba Masihi atakapokuja, angeliletea taifa lao utukufu na kuwaweka huru kutokana na ukandamizaji wa Waroma. (Luka 2:38; 3:15) Wengi waliamini kwamba Masihi angesimamisha ufalme hapa duniani katika nchi ya Israeli. Ikiwa jambo hilo lingetokea, mamilioni ya Wayahudi waliotawanyika katika nchi nyingine wangerudi katika nchi yao. Kumbuka kwamba pindi moja Yohana Mbatizaji alimuuliza Yesu hivi: “Je, wewe ndiye Yule Anayekuja, au tumtarajie mwingine?” (Mt. 11:2, 3) Huenda Yohana alitaka kujua ikiwa kulikuwa na mtu mwingine ambaye angetimiza matumaini yote ya Wayahudi. Pia, wanafunzi wawili waliokutana na Yesu walipokuwa njiani kwenda Emau, baada ya Yesu kufufuliwa, walikuwa na matumaini ambayo hayakuwa yametimia kumhusu Masihi. (Soma Luka 24:21.) Punde baadaye, mitume wa Yesu walimuuliza hivi: “Bwana, je, unaurudisha ufalme kwa Israeli wakati huu?”—Mdo. 1:6.

5. (a) Kwa nini watu wa Galilaya walitaka Yesu awe mfalme wao? (b) Yesu alirekebishaje maoni yao?

5 Hapana shaka kwamba watu wa Galilaya walitaka kumfanya Yesu awe mfalme wao kwa sababu ya matumaini waliyokuwa nayo kumhusu Masihi. Si vigumu kuelewa kwa nini walifikiri kwamba Yesu angekuwa kiongozi bora: Alikuwa msemaji mzuri; alikuwa na uwezo wa kuwaponya wagonjwa; hata alikuwa na uwezo wa kuwalisha wenye njaa. Baada ya kuwalisha wanaume 5,000 hivi, Yesu alitambua mawazo yao. Biblia inasema hivi: “Yesu akijua walitaka kuja kumkamata wamfanye awe mfalme, akaondoka tena akaenda mlimani akiwa peke yake.” (Yoh. 6:10-15) Siku iliyofuata, huenda hisia hizo zilikuwa zimetulia kwa kiasi fulani ng’ambo ile nyingine ya Bahari ya Galilaya. Hivyo, Yesu akaueleza umati kusudi hasa la kazi yake. Alikuwa amekuja kuwaletea manufaa ya kiroho, si ya kimwili. Aliwaambia hivi: “Msifanye kazi kwa ajili ya chakula kinachoharibika, bali kwa ajili ya chakula kinachodumu kufikia uzima wa milele.”—Yoh. 6:25-27.

6. Yesu alionyeshaje wazi kwamba hakutaka kujitafutia mamlaka ya kisiasa hapa duniani? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

6 Muda mfupi kabla ya kifo chake, Yesu alitambua kwamba baadhi ya wafuasi wake walitarajia asimamishe ufalme hapa duniani katika jiji la Yerusalemu. Alirekebisha maoni hayo alipotoa mfano wa mina. Mfano huo ulionyesha kwamba “mtu fulani wa familia mashuhuri,” yaani Yesu, angelazimika kusafiri na angerudi baada ya muda mrefu. (Luka 19:11-13, 15) Pia, Yesu aliwaambia waziwazi viongozi wa Roma kuhusu msimamo wake wa kutounga mkono upande wowote katika mambo ya kisiasa. Pontio Pilato alimuuliza Yesu hivi: “Je, wewe ndiye Mfalme wa Wayahudi?” (Yoh. 18:33) Huenda gavana huyo alihofia kwamba Yesu angesababisha vurugu za kisiasa, jambo ambalo lilimhangaisha muda wote wa utawala wake. Yesu alijibu hivi: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu.” (Yoh. 18:36) Hangejihusisha na siasa kwa kuwa Ufalme wake ungekuwa wa mbinguni. Alimwambia Pilato kwamba kazi yake hapa duniani ilikuwa “[kutoa] ushahidi kuhusu kweli.”—Soma Yohana 18:37.

Je, unakazia fikira matatizo ya ulimwengu au Ufalme wa Mungu? (Tazama fungu la 7)

7. Kwa nini huenda ikawa vigumu kuepuka kuunga mkono kimoyomoyo harakati za kisiasa za kupigania uhuru?

7 Tunapoelewa kazi yetu vizuri kama Yesu alivyoelewa kazi yake, tutaepuka kuunga mkono hata kimoyomoyo au kimyakimya harakati za kisiasa za kupigania uhuru. Huenda isiwe rahisi kuepuka kufanya hivyo. Mwangalizi mmoja wa mzunguko anasema hivi: “Maoni yenye msimamo mkali yanazidi kuongezeka miongoni mwa watu katika eneo letu. Watu wametekwa na roho ya uzalendo, na wengi wanaamini kwamba uhuru wa kisiasa utaboresha maisha yao. Tunafurahi kwamba akina ndugu wamelinda umoja wao wa Kikristo kwa kukazia fikira kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme. Wanamtegemea Mungu asuluhishe ukosefu wa haki na matatizo mengine tunayokabili.”

YESU ALISHUGHULIKAJE NA MASUALA YA KISIASA YALIYOSABABISHA MIGAWANYIKO?

8. Toa mfano wa mambo yaliyowalemea Wayahudi wa karne ya kwanza.

8 Mara nyingi ukosefu wa haki huwachochea watu wajiingize katika mambo ya kisiasa. Suala la kulipa kodi liliibua hisia kali katika siku za Yesu. Kwa kweli, uasi wa Yuda Mgalilaya aliyetajwa awali, ulizuka serikali ya Roma ilipowataka watu wajiandikishe ili kuhakikisha kwamba wanalipa ushuru. Raia wa Roma, kutia ndani watu waliomsikiliza Yesu walipaswa kulipia kodi vitu vingi, kama vile kodi ya bidhaa mbalimbali, kodi ya ardhi, na kodi ya nyumba. Pia, wakusanya kodi walikuwa wafisadi sana, jambo lililowafanya watu wahisi wamelemewa hata zaidi. Wakusanya kodi wangenunua cheo fulani kwenye mnada kilichowapa mamlaka ya kukusanya kodi kisha wangejinufaisha na pesa zilizokusanywa. Zakayo, mkuu wa wakusanya kodi katika mji wa Yeriko, alipata utajiri wake kwa kuwapunja watu pesa. (Luka 19:2, 8) Inaonekana wakusanya kodi wengi walifanya vivyo hivyo.

9, 10. (a) Maadui wa Yesu walijaribu jinsi gani kumhusisha katika suala fulani la kisiasa? (b) Tunajifunza nini kutokana na jibu la Yesu? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

9 Maadui wa Yesu walijaribu kumnasa wakitaka aunge mkono upande mmoja katika suala la kodi. Walikuwa wakizungumzia “kodi ya kichwa,” kodi ya dinari moja ambayo kila raia katika utawala wa Roma alipaswa kulipa. (Soma Mathayo 22:16-18.) Wayahudi hasa walichukizwa na kodi hiyo. Kodi hiyo iliwakumbusha kwamba walikuwa chini ya utawala wa serikali ya Roma. “Wafuasi wa chama cha Herode” waliokuwa wamezusha suala hilo, walitumaini kwamba ikiwa Yesu angeshutumu kodi hiyo, basi angeshtakiwa kwa kosa la uchochezi. Na ikiwa angesema ilikuwa lazima kulipa kodi hiyo, huenda wafuasi wake wangeacha kumsikiliza.

10 Yesu alikuwa mwangalifu ili asiunge mkono upande wowote katika suala hilo la kodi. Alisema hivi: “Mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, na Mungu vitu vya Mungu.” (Mt. 22:21) Bila shaka, Yesu alijua kwamba ufisadi ulikuwa jambo la kawaida miongoni mwa wakusanya kodi. Hata hivyo, Yesu hakutaka kukengeushwa kutoka katika suala muhimu zaidi. Suala hilo muhimu lilikuwa Ufalme wa Mungu ambao ungekuwa suluhisho la kweli. Kwa kufanya hivyo, aliwawekea mfano mzuri wafuasi wake wote. Wanapaswa kuepuka kujihusisha katika masuala ya kisiasa, hata iwe masuala hayo yanaonekana kuwa sawa au ya haki kadiri gani. Wakristo hufuatia Ufalme wa Mungu na uadilifu Wake. Wanafanya hivyo badala ya kusitawisha maoni ya kishupavu kuelekea matendo fulani ya ukosefu wa haki au kuyashutumu.​—Mt. 6:33.

11. Tunaweza kufanya nini ili kupambana na ukosefu wa haki kwa njia nzuri zaidi?

11 Wengi ambao sasa ni Mashahidi wa Yehova na ambao awali walikuwa na misimamo mikali ya kisiasa wamefaulu kubadili maoni hayo. Dada mmoja kutoka Uingereza anasema hivi: “Baada ya kujifunza somo kuhusu mambo ya kijamii katika chuo kikuu nilisitawisha maoni yenye msimamo mkali. Nilitaka kutetea haki za watu weusi, kwa kuwa tuliteseka sana kwa sababu ya ukosefu mwingi wa haki. Ingawa nilishinda katika mijadala mingi, bado nilivunjika moyo. Sikutambua kwamba ni lazima mambo yanayosababisha ubaguzi wa rangi yang’olewe kutoka katika mioyo ya watu. Hata hivyo, nilipoanza kujifunza Biblia nilitambua kwamba nilipaswa kuyang’oa kwanza kutoka katika moyo wangu mwenyewe. Na dada mweupe ndiye aliyenisaidia kwa subira kuchukua hatua hiyo. Sasa ninatumikia nikiwa painia wa kawaida katika kutaniko la lugha ya ishara, na ninajifunza kuwahubiria watu wa namna zote.”

“RUDISHA UPANGA WAKO MAHALI PAKE”

12. Yesu aliwaambia wanafunzi wake waepuke “chachu” gani?

12 Katika siku za Yesu ilikuwa kawaida kwa watu kuchanganya dini na mambo ya siasa. Kitabu kimoja (Daily Life in Palestine at the Time of Christ) kinasema kwamba “Wayahudi waligawanyika katika madhehebu ya kidini ambayo leo yanaweza kulinganishwa na vyama vya kisiasa.” Hivyo, Yesu aliwaonya wanafunzi wake hivi: “Endeleeni kuwa macho; jihadharini na chachu ya Mafarisayo na ya Herode.” (Marko 8:15) Inaonekana Yesu alipomtaja Herode, alikuwa akiwarejelea wafuasi wa chama cha Herode. Katika mambo ya kisiasa, Mafarisayo waliunga mkono jitihada za kuwaweka huru Wayahudi. Simulizi la Mathayo linafunua kwamba Yesu aliwataja pia Masadukayo katika mazungumzo hayo. Masadukayo walitaka Waroma waendelee kuwatawala Wayahudi. Wengi wao hawakutaka hali ibadilike kwa sababu walifurahia vyeo vya kisiasa katika utawala wa Roma. Yesu aliwaonya wanafunzi wake kwa msisitizo kwamba waepuke mafundisho, au chachu, ambayo vikundi hivyo vitatu viliendeleza. (Mt. 16:6, 12) Jambo lenye kutokeza ni kwamba mazungumzo hayo yalitokea muda mfupi tu baada ya watu kutaka kumfanya Yesu kuwa mfalme.

13, 14. (a) Masuala ya kisiasa na ya kidini yalisababishaje ukatili na ukosefu wa haki? (b) Kwa nini si sawa kuwatendea wengine kwa ukatili hata ikiwa tumetendewa isivyo haki? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

13 Dini inapochanganywa na mambo ya kisiasa, vurugu na matendo ya kikatili yanaweza kutokea kwa urahisi. Yesu aliwafundisha wanafunzi wake kwamba wanapaswa kuepuka kuunga mkono upande wowote katika mambo hayo. Kwa sababu ya kuchanganya dini na mambo ya kisiasa, wakuu wa makuhani na Mafarisayo walipanga kumuua Yesu. Walimwona kuwa mpinzani wa kisiasa na wa kidini ambaye angefanya wapoteze mamlaka yao. Walisema hivi: “Tukimwacha aendelee, watu wote watamwamini, nao Waroma watakuja na kuchukua mahali petu na taifa letu.” (Yoh. 11:48) Hivyo, Kuhani Mkuu Kayafa akawa mstari wa mbele kupanga njama ya kumuua Yesu.—Yoh. 11:49-53; 18:14.

14 Kayafa aliwatuma wanajeshi usiku wakamkamate Yesu. Yesu alijua kuhusu njama hiyo mbaya, hivyo wakati wa mlo wa mwisho pamoja na mitume wake aliwaambia wabebe panga. Panga mbili tu zingetosha kuwafundisha somo muhimu. (Luka 22:36-38) Baadaye usiku huo, Petro alitumia upanga kumshambulia mtu mmoja aliyekuwa kwenye umati uliokuja kumkamata Yesu. Hapana shaka kwamba alichukizwa sana na ukosefu wa haki uliotendeka kwa sababu walikuja kumkamata Yesu usiku. (Yoh. 18:10) Lakini Yesu alimwambia hivi Petro: “Rudisha upanga wako mahali pake, kwa maana wote wanaochukua upanga wataangamia kwa upanga.” (Mt. 26:52, 53) Somo hilo muhimu lilipatana na yale ambayo Yesu alikuwa ametaja katika sala yake mapema usiku huo, kwamba wanafunzi wake hawapaswi kuwa sehemu ya ulimwengu. (Soma Yohana 17:16.) Mungu tu ndiye aliye na haki ya kukomesha ukosefu wa haki.

15, 16. (a) Neno la Mungu limewasaidiaje watu wa Mungu kuepuka migogoro? (b) Yehova anaona tofauti gani anapotazama ulimwengu leo?

15 Dada kutoka Ulaya kusini aliyetajwa awali alijifunza somo hilohilo. Anasema hivi: “Nimejionea kwamba ukatili hauleti haki. Niliona kwamba mara nyingi wale walioona matendo ya kikatili kuwa suluhisho walipoteza uhai wao. Na wengine wengi wakawa wenye hasira na chuki. Nilifurahi sana kujifunza katika Biblia kwamba Mungu tu ndiye anayeweza kuleta haki ya kweli duniani. Nimekuwa nikihubiri ujumbe huo kwa miaka 25.” Yule ndugu kutoka kusini mwa Afrika aliyetajwa mapema, ameamua kubeba “upanga wa roho,” yaani, Neno la Mungu badala ya mkuki anapowahubiria jirani zake ujumbe wa amani, haidhuru wao ni wa kabila lipi. (Efe. 6:17) Na baada ya kuwa Shahidi wa Yehova, yule dada anayeishi Ulaya ya kati aliolewa na ndugu wa jamii ambayo mwanzoni aliichukia. Wote watatu walifanya mabadiliko hayo kwa sababu walitamani kuwa kama Kristo.

16 Mabadiliko hayo ni muhimu sana! Biblia inawalinganisha wanadamu na bahari yenye msukosuko, bahari ambayo haina utulivu kamwe. (Isa. 17:12; 57:20, 21; Ufu. 13:1) Masuala ya kisiasa yanapowavuruga watu, kuwagawanya, na kuwachochea kutenda kwa ukatili, sisi hudumisha amani na umoja. Na Yehova anapotazama ulimwengu wetu uliogawanyika, anaguswa moyo sana anapoona umoja uliopo miongoni mwa watu wake.​—Soma Sefania 3:17.

17. (a) Tunaweza kuendeleza umoja katika njia zipi tatu? (b) Tutachunguza nini katika makala inayofuata?

17 Tumeona kwamba tunaweza kuendeleza umoja wa Kikristo katika njia tatu: (1) Kwa kuweka tumaini letu katika Ufalme wa Mungu utakaoondoa ukosefu wote wa haki, (2) kwa kukataa kuunga mkono upande wowote katika masuala ya kisiasa, na (3) kwa kupinga matendo yote ya kikatili. Hata hivyo, nyakati nyingine ubaguzi unaweza kuhatarisha umoja wetu. Makala inayofuata itatusaidia kuchunguza jinsi tunavyoweza kukabiliana kwa mafanikio na changamoto hiyo, kama Wakristo wa karne ya kwanza walivyofanya.