Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Acha Sheria na Kanuni za Mungu Zizoeze Dhamiri Yako

Acha Sheria na Kanuni za Mungu Zizoeze Dhamiri Yako

“Ninavitafakari vikumbusho vyako.”​—ZAB. 119:99.

NYIMBO: 127, 88

1. Ni jambo gani linalowatofautisha wanadamu na wanyama?

JAMBO moja linalowatofautisha wanadamu na wanyama ni kwamba wanadamu wamepewa zawadi ya dhamiri. Na hali imekuwa hivyo tangu kuumbwa kwa wanadamu. Adamu na Hawa walijificha baada ya kuvunja sheria ya Yehova. Jambo hilo linaonyesha kwamba dhamiri yao ilikuwa ikiwasumbua.

2. Ni katika njia gani dhamiri yetu inaweza kulinganishwa na dira? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

2 Watu walio na dhamiri ambayo haijazoezwa vizuri wanaweza kulinganishwa na meli inayosafiri kwa kutegemea dira iliyo na kasoro. Kuanza safari ukitegemea dira iliyo na kasoro ni hatari. Upepo na mawimbi ya bahari yanaweza kuiondoa meli kwa urahisi kutoka kwenye njia yake. Dira yenye vipimo sahihi inaweza kumsaidia nahodha kuiongoza meli kwenye njia sahihi. Dhamiri inaweza kulinganishwa na dira inayotupatia mwongozo kuhusu maadili. Ni uwezo ulio ndani yetu wa kutofautisha kati ya lililo sawa na lisilo sawa, ambao unaweza kutuongoza kwenye njia inayofaa. Lakini ili dhamiri yetu ituongoze vizuri, ni lazima iwe na vipimo sahihi.

3. Ni nini kinachoweza kutokea ikiwa dhamiri haijazoezwa vizuri?

3 Dhamiri ambayo haijazoezwa vizuri, haiwezi kumzuia mtu asitende mambo mabaya. (1 Tim. 4:1, 2) Dhamiri kama hiyo inaweza kutufanya tusadiki kwamba “uovu ni wema.” (Isa. 5:20) Yesu aliwaonya hivi wafuasi wake: “Saa inakuja ambayo kila mtu atakayewaua atafikiri kwamba amemtolea Mungu utumishi mtakatifu.” (Yoh. 16:2) Na hivyo ndivyo watu waliomuua mwanafunzi Stefano walivyofikiri, na wengine wengi wamefanya vivyo hivyo pia. (Mdo. 6:8, 12; 7:54-60) Inashangaza kwamba wanadini wenye msimamo mkali huvunja sheria za Yule wanayedai kuwa wanamwabudu wanapotenda mambo maovu kama vile kuua! (Kut. 20:13) Ni wazi kwamba dhamiri zao haziwaongozi vizuri!

4. Tunaweza kufanya nini ili dhamiri yetu isiache kufanya kazi?

4 Tunaweza kufanya nini ili dhamiri yetu isiache kufanya kazi? Sheria na kanuni zilizo katika Neno la Mungu ni zenye “faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu.” (2 Tim. 3:16) Hivyo, ikiwa tutajifunza Biblia kwa bidii, ikiwa tutatafakari mambo hayo na kuyatumia maishani mwetu, tutaizoeza dhamiri yetu itambue na kutenda kulingana na njia ya Mungu ya kufikiri, na hivyo inaweza kutupatia mwongozo unaotegemeka. Acheni tuchunguze jinsi sheria na kanuni za Yehova zinavyoweza kutusaidia kuzoeza dhamiri yetu.

ACHA SHERIA ZA MUNGU ZIKUZOEZE

5, 6. Tunanufaikaje kwa kufuata sheria za Mungu?

5 Ili tunufaike na sheria za Mungu, tunahitaji kufanya mengi zaidi ya kuzisoma au kuzifahamu tu. Tunapaswa kujifunza kuzipenda na kuziheshimu. Neno la Mungu linasema hivi: “Chukieni maovu, pendeni yaliyo mema.” (Amo. 5:15) Lakini tunaweza kufanyaje hivyo? Siri ni kujifunza kuona mambo kama Yehova anavyoyaona. Kwa mfano: Wazia kwamba una matatizo ya kupata usingizi. Daktari wako anakupendekezea ratiba fulani utakayofuata kuhusu chakula, mazoezi, na mtindo wa maisha. Baada ya kufuata ratiba hiyo, unatambua kwamba inakusaidia! Hapana shaka utamthamini sana daktari wako kwa kukusaidia kufanya maisha yako kuwa mazuri zaidi.

6 Vivyo hivyo, Muumba wetu ametupatia sheria zinazotulinda kutokana na matokeo mabaya ya dhambi na hivyo kufanya maisha yetu yawe mazuri zaidi. Fikiria jinsi tunavyonufaika tunapofuata sheria za Biblia zinazokataza kusema uwongo, kutunga hila, kuiba, kufanya uasherati, ukatili, na kuwasiliana na roho waovu. (Soma Methali 6:16-19; Ufu. 21:8) Tunapojionea thawabu nyingi tunazopata kwa kufanya mambo kulingana na mapenzi ya Yehova, upendo wetu kwake utazidi kuongezeka na tutazidi kuthamini sheria zake.

7. Kusoma na kutafakari kuhusu masimulizi halisi ya Biblia kunaweza kutusaidia kufanya nini?

7 Tunafurahi kwamba si lazima tupatwe na matokeo mabaya yanayosababishwa na kuvunja sheria za Mungu ili tujifunze masomo muhimu. Tunaweza kujifunza kutokana na makosa ya watu wengine ambayo yameandikwa katika Neno la Mungu. Andiko la Methali 1:5 linasema: “Mtu mwenye hekima husikiliza na kujifunza zaidi.” Kwa kweli, tunapokea mafundisho bora zaidi kutoka kwa Mungu, kama inavyokuwa wakati tunaposoma na kutafakari kuhusu masimulizi halisi katika Biblia. Kwa mfano, wazia maumivu ambayo Mfalme Daudi alipata baada ya kuvunja sheria ya Yehova kwa kufanya uzinzi na Bath-sheba. (2 Sam. 12:7-14) Tunaposoma na kutafakari simulizi hilo, huenda tukajiuliza hivi: ‘Mfalme Daudi angefanya nini ili aepuke kufanya uzinzi na Bath-sheba, jambo ambalo lilimsababishia maumivu ya moyo? Ikiwa ningekabili kishawishi kama chake, je, ningekuwa na nguvu za kukipinga? Je, ningekimbia kama Yosefu, au ningejiruhusu ninaswe kama Daudi?’ (Mwa. 39:11-15) Tunapotafakari matokeo mabaya ya dhambi, tunaufanya moyo wetu uwe na nguvu ya ‘kuchukia maovu.’

8, 9. (a) Dhamiri yetu hutimiza kusudi gani? (b) Kanuni za Yehova na dhamiri yetu hufanyaje kazi pamoja?

8 Huenda tukaepuka mazoea ambayo Mungu anachukia. Hata hivyo, kuna mambo mengine au hali ambazo Maandiko hayatoi sheria fulani hususa kuzihusu. Katika hali kama hizo, tunawezaje kujua mambo yanayokubalika na yanayompendeza Mungu? Hapo ndipo dhamiri yetu iliyozoezwa na Biblia inapohusika.

9 Yehova amechochewa na upendo kutupatia kanuni tunazoweza kutumia pamoja na dhamiri yetu iliyozoezwa na Biblia. Yeye mwenyewe anasema hivi: “Mimi, Yehova, ni Mungu wako, Ninayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe, Ninayekuongoza katika njia unayopaswa kutembea.” (Isa. 48:17, 18) Tunapotumia akili na moyo wetu kuchanganua kanuni za Biblia, tunarekebisha, kuongoza, na kufinyanga dhamiri yetu. Kisha, kufanya hivyo hutusaidia kufanya maamuzi kwa hekima.

ACHA KANUNI ZA MUNGU ZIKUONGOZE

10. Kanuni ni nini, na Yesu alizitumiaje kwa njia yenye matokeo mazuri?

10 Kanuni ni kweli ya msingi au fundisho linalotumiwa kuwa msingi wa kufikiri au kutenda kwa njia fulani. Kuelewa kanuni kunahusisha kuelewa njia ya kufikiri ya Mpaji-sheria wetu na sababu zilizomfanya atunge sheria fulani. Katika kipindi chote cha huduma yake, Yesu alifundisha kweli za msingi ili kuwasaidia wanafunzi wake watambue matokeo ya mitazamo au matendo fulani. Kwa mfano, alifundisha kwamba kinyongo kinaweza kumfanya mtu atende kwa ukatili, na tamaa inaweza kumwongoza mtu afanye uzinzi. (Mt. 5:21, 22, 27, 28) Ili tuwe na dhamiri iliyozoezwa vizuri, tunapaswa kuruhusu kanuni za Mungu zituongoze, na hivyo kumletea Mungu utukufu.​—1 Kor. 10:31.

Mkristo mkomavu hujali dhamiri za wengine (Tazama fungu la 11 na 12)

11. Dhamiri zinaweza kutofautianaje?

11 Huenda Wakristo wawili ambao dhamiri zao zimezoezwa na Biblia wakawa na maoni yanayotofautiana kabisa kuhusu mambo fulani. Fikiria kuhusu matumizi ya pombe. Biblia haishutumu kunywa pombe kwa kiasi. Hata hivyo, inaonya dhidi ya kunywa pombe kupita kiasi, na vilevile ulevi. (Met. 20:1; 1 Tim. 3:8) Je, hilo linamaanisha kwamba hakuna mambo mengine ambayo Mkristo anapaswa kufikiria maadamu yeye anakunywa pombe kwa kiasi? Sivyo, hata kidogo. Ingawa ameridhika kwamba dhamiri yake haimsumbui, Mkristo huyo anapaswa kufikiria dhamiri za wengine.

12. Andiko la Waroma 14:21 linaweza kutuchocheaje kuheshimu dhamiri za wengine?

12 Paulo aliandika hivi kuhusu uhitaji wa Wakristo kujali dhamiri za wengine: “Ni vema kutokula nyama au kunywa divai au kufanya jambo lolote ambalo litamkwaza ndugu yako.” (Rom. 14:21) Je, utakuwa tayari kuepuka kufanya mambo ambayo una haki ya kuyafanya ili usimkwaze ndugu ambaye dhamiri yake inatofautiana na dhamiri yako? Bila shaka utakuwa tayari kufanya hivyo. Kabla ya kupata ujuzi wa kweli, baadhi ya ndugu zetu walikunywa pombe kupita kiasi, lakini sasa wameazimia kwamba hawatainywa. Kwa hakika, hakuna yeyote kati yetu ambaye angependa kufanya jambo linaloweza kumfanya ndugu arudie mwenendo unaoweza kumsababishia madhara makubwa! (1 Kor. 6:9, 10) Hivyo, si tendo la upendo kwa Mkristo aliyewakaribisha wageni kumshinikiza ndugu anywe pombe ikiwa ndugu huyo anakataa kufanya hivyo.

13. Timotheo aliweka mfano gani mzuri wa kutanguliza masilahi ya Ufalme?

13 Huenda kijana Timotheo alikuwa na umri wa kati ya miaka 17 hadi 23 hivi alipokubali kupitia maumivu ya kutahiriwa ili aepuke kuwakwaza Wayahudi ambao angewahubiria. Alikuwa na mtazamo kama wa mtume Paulo. (Mdo. 16:3; 1 Kor. 9:19-23) Kama Timotheo, je, wewe uko tayari kudhabihu mambo ya kibinafsi kwa ajili ya hali njema ya wengine?

‘SONGA MBELE KUELEKEA UKOMAVU’

14, 15. (a) Kusonga mbele kuelekea ukomavu kunahusisha nini? (b) Ni katika njia gani kuwaonyesha wengine upendo kunahusiana na ukomavu wa Kikristo?

14 Wakristo wote wanapaswa “[kuliacha] nyuma fundisho la msingi kumhusu Kristo” na “[kusonga] mbele kuelekea ukomavu.” (Ebr. 6:1) Hilo halijitokezi tu. Tunahitaji ‘kusonga mbele,’ yaani, kuendelea kujitahidi kufikia ukomavu. Kufikia ukomavu kunahusisha kujitahidi kuongeza na kufikia kiwango cha juu cha ujuzi na ufahamu. Hiyo ndiyo sababu tumetiwa moyo mara kwa mara tusome sehemu fulani ya Biblia kila siku. (Zab. 1:1-3) Je, umejiwekea lengo la kusoma sehemu fulani ya Biblia kila siku? Kufanya hivyo kutakusaidia kufahamu vizuri zaidi sheria na kanuni za Yehova na kuelewa kwa kina Neno la Mungu.

15 Sheria iliyo muhimu zaidi kwa Wakristo ni sheria ya upendo. Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu—mkiwa na upendo miongoni mwenu.” (Yoh. 13:35) Yakobo, ndugu nusu ya Yesu aliuita upendo “sheria ya kifalme.” (Yak. 2:8) Paulo alisema: “Upendo ndio utimizo wa sheria.” (Rom. 13:10) Hatushangai kwamba upendo unasisitizwa sana kwa kuwa Biblia inatuambia kwamba “Mungu ni upendo.” (1 Yoh. 4:8) Upendo wa Mungu hauonyeshwi tu kupitia hisia. Yohana aliandika hivi: “Hivi ndivyo upendo wa Mungu ulivyofunuliwa kwetu, kwamba Mungu alimtuma Mwana wake mzaliwa-pekee ulimwenguni ili tupate uzima kupitia yeye.” (1 Yoh. 4:9) Naam, upendo wa Mungu ulimchochea kutenda. Kiwango cha upendo tunaomwonyesha Yehova, Mwana wake, ndugu zetu Wakristo, na vilevile wanadamu wengine ni uthibitisho wa ukomavu wetu wa Kikristo.​—Mt. 22:37-39.

Tunapotumia kanuni za Biblia, dhamiri yetu itazidi kutupatia mwongozo wenye kutegemeka (Tazama fungu la 16)

16. Tunapofanya maendeleo kuelekea ukomavu wa kiroho, kwa nini tutathamini zaidi kutumia kanuni?

16 Unaposonga mbele kuelekea ukomavu wa Kikristo, utathamini zaidi kutumia kanuni za Biblia. Hiyo ni kwa sababu sheria hutumika katika hali fulani hususa, ilhali kanuni huwa na matumizi mapana. Kwa mfano, mtoto mdogo hawezi kuelewa hatari ya kushirikiana na marafiki wasiofaa, hivyo mzazi mwenye utambuzi atamwekea sheria za kumlinda. (1 Kor. 15:33) Lakini kadiri mtoto huyo anavyoendelea kukomaa, uwezo wake wa kufikiri unakua, na sasa anaweza kutumia kanuni za Biblia. Hivyo, uwezo wake wa kufanya maamuzi ya hekima anapochagua marafiki utazidi kuongezeka. (Soma 1 Wakorintho 13:11; 14:20.) Tunapofanya maamuzi kwa kutumia kanuni za Biblia, dhamiri yetu itazidi kutupatia mwongozo wenye kutegemeka, nayo itapatanishwa na njia ya Mungu ya kufikiri.

17. Kwa nini tunaweza kusema kwamba tuna vifaa tunavyohitaji ili kufanya maamuzi kwa hekima?

17 Je, tuna kila kitu tunachohitaji ili tufanye maamuzi yatakayompendeza Yehova? Ndiyo. Tunapotumia kwa ustadi sheria na kanuni zilizo katika Neno la Mungu, tutakuwa na “uwezo kamili, [tukiwa] na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.” (2 Tim. 3:16, 17) Hivyo, tafuta kanuni za Biblia ili ‘uyafahamu mapenzi ya Yehova.’ (Efe. 5:17) Tumia vizuri vifaa vya kujifunzia vilivyoandaliwa kupitia kutaniko la Kikristo kama vile Fahirisi, Mwongozo wa Utafiti wa Mashahidi wa Yehova, Watchtower Library, Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO, na programu ya JW Library. Vifaa hivyo vimetayarishwa kwa njia ambayo itatusaidia kunufaika kikamili na funzo letu la kibinafsi au la familia.

DHAMIRI ILIYOZOEZWA NA BIBLIA HULETA BARAKA

18. Tunapata baraka gani tunapotenda kulingana na sheria na kanuni za Yehova?

18 Tunapata baraka kwa kushika sheria na kanuni za Yehova, kama tunavyosoma katika andiko la Zaburi 119:97-100: “Jinsi ninavyoipenda sana sheria yako! Ninaitafakari mchana kutwa. Amri yako hunifanya niwe na hekima kuliko maadui wangu, kwa sababu ninayo milele. Nina ufahamu mwingi kuliko walimu wangu wote, kwa sababu ninavitafakari vikumbusho vyako. Ninatenda kwa uelewaji mwingi kuliko wanaume wazee, kwa sababu ninayatii maagizo yako.” Uwezo wetu wa kutenda kwa hekima, ufahamu, na uelewaji utazidi kuongezeka ikiwa tutatumia wakati ‘kutafakari’ sheria na kanuni za Mungu. Tukijitahidi kwelikweli “[tutafikia] kiwango cha kimo kamili cha Kristo” tunapoendelea kuruhusu sheria na kanuni za Mungu zizoeze dhamiri yetu.​—Efe. 4:13.